Kuupandia Mbegu Ufalme wa Mungu
1. Msichana mmoja wa shule alimweka mfalme aliyemwuliza ulizo kwenye ufalme gani, na je! jibu lake lilikuwa jibu lisiloweza kutokeza maulizo?
MFALME mmoja wa nchi moja ya Ulaya ya Kati alikuwa akikagua mojayapo ya shule za watu wote ya raia zake. Akauliza darasa la shule hiyo maulizo kadha. Kama vile hadithi hiyo ituambiavyo, yeye aliuliza msichana mmoja mdogo maulizo juu ya “ufalme wa mimea” na “ufalme wa wanyama” naye akapendezwa na majibu ya msichana huyo. Akifuatilia jambo hilo, yeye alimwuliza msichana huyo hivi: “Mimi ni wa ufalme gani?” Akitazamia jibu, “Ule ufalme wa wanyama,” macho yake yalitoa machozi wakati msichana huyo mdogo alipojibu: “Ufalme wa Mungu.” Ijapokuwa kanisa ambalo mfalme huyo alikuwa mshiriki wake lilifikiri kwamba jibu la msichana huyo lilikuwa sahihi na vilevile la kumwogopa Mungu, je! yeye alikuwa wa ufalme wa Mungu? Je! mtawala huyo wa kisiasa wa serikali ya kilimwengu alikuwa kweli kweli ameingizwa kwenye “ufalme wa Mungu”? Hapa pana jambo la kufikiria!
2. (a) Kukubaliwa kuingia kwenye ufalme wa Mungu ni kukubaliwa kuingia kwenye serikali ya namna gani? (b) Wayahudi wa siku za Yesu walionyeshaje kwamba hawakuwa wakiupandia ufalme huo?
2 Kukubaliwa kuingia katika ufalme wa Mungu ndilo pendeleo kuu zaidi analoweza mtu kupewa hapa duniani. Ufalme wa Mungu ndiyo serikali kuu zaidi kupita serikali zote. Hii ndiyo serikali ambayo mwanzishi wa Ukristo alihubiri habari zake katika Mashariki ya Kati. Historia inasema hivi kuhusu Yesu Kristo: “Hata baada ya Yohana [Mbatizaji] kutiwa gerezani [katika mwaka 30 W.K.], Yesu akaenda Galilaya, akiihubiri Habari Njema ya Mungu, akisema, Wakati umetimia, na ufalme wa Mungu umekaribia; tubuni, na kuamini Injili.” (Masimulizi ya Marko, sura ya kwanza, mist. 14 na 15) Walakini, umati mkubwa wa Wayahudi hawakutubu na kuwa na imani. Kama jambo lenye kuchukiza sana, walimwua Yesu kwa kumsingizia kuwa adui ya mfalme wa Kirumi, Kaisari. Kwa njia ya mfano, wao hawakuupandia mbegu ufalme wa Mungu. Lakini ni akina nani miongoni mwetu wanaofanya hivyo leo. Twaweza kujuaje? Tutaona.
3. Wanafunzi wa Yesu walimwuliza maulizo juu ya mfano gani ambao Yesu alikuwa amewatolea wasikilizaji waliokuwa ufuoni mwa bahari, naye alisema nini juu ya masikio?
3 Wengi wetu leo hupenda mifano ya mambo. Yesu Kristo alipata kujulikana sana kwa kufanyiza mifano au kwa kusema mithali. Akiwa mhubiri mwenye kwenda huku na huku, aliwavuta wasikilizaji wengi. Pindi moja, akiwa ndani ya merikebu katika Bahari ya Galilaya, yeye aliwafundisha wasikilizaji waliokuwa ufuoni (pwani) mwa bahari. Alitoa mfano wa namna nne za udongo wa kilimo. Kwa faragha, wanafunzi wake waliokuwa washiriki wa karibu walimwuliza maana ya jambo hilo. Baada ya kuwaeleza na kutaja mambo zaidi, alisema hivi, hata kwa hao waliokuwa washiriki wake wa karibu: “Mtu akiwa na masikio ya kusikilia, na asikie.” (Marko 4:1-23) Hatujui ni wasikilizaji wangapi kati ya hao wasikilizaji waliokuwa ufuoni mwa bahari waliokuwa na masikio ya namna hiyo. Lakini Yesu alitazamia wanafunzi wake aliotolea maelezo ya mfano huo wawe na masikio yenye kusikia. Kwa masikio ya namna hiyo, yale waliyopata kusikia kutoka kwake yangekaa daima ndani yao na kuwapa nuru. Ni akina nani kati yetu leo walio na masikio ya namna hiyo? Yatatusaidia kuupandia mbegu ufalme wa Mungu ifaavyo.
4. Kuna sababu gani yenye maana kwamba mtu awe na ‘masikio yenye kusikia,’ na ni kwa sababu gani sisi hatutaki kuwa kama ule udongo uliokuwa kando ya njia?
4 Ikiwa hatuna “masikio ya kusikilia,” hatutasikiliza aliyofundisha Yesu. Kusikiliza ni jambo la maana, kwa kuwa mwandikaji wa Biblia Marko anaendelea kuandika hivi: “Akawaambia, Angalieni msikialo.” (Marko 4:24) Haitupasi kamwe kuwa kama namna ya kwanza ya udongo katika mfano wa Yesu. Ni ule udongo uliokuwa kando ya njia. Ulikuwa umekanyagwa ukawa mgumu sana hivi kwamba haukuruhusu mbegu ziupenye na kuingia ndani, bali uliziacha zikiwa wazi zikaliwa na ndege. (Marko 4:4, 15) Sisi hatutaki Shetani Ibilisi, kupitia kwa mawakili wake, atupokonye kweli za Kikristo kwa kutokusikiliza kwetu. Jambo hilo lingeonyesha kwamba hatuheshimu cheo alichokuwa nacho na alicho nacho sasa Mwalimu, Yesu Kristo katika mpango wa Mungu.
5. Baada ya Yesu kutoa onyo la upole juu ya kusikiliza, yeye alisema nini juu la kutoa na kupata kipimo?
5 Kanuni inayotajwa mara nyingi ni kwamba tunapata kutoka kwa jambo fulani kulingana na tunachotia ndani yake. Yesu alionyesha faida ambayo tungepata kwa kusikiliza inavyostahili yale aliyosema. Alifanya hivyo kwa kuongeza maneno haya katika onyo lake la upole juu ya kusikiliza: “Kipimo kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa, na tena mtazidishiwa. Kwa maana mwenye kitu atapewa, naye asiye na kitu, hata kile alicho nacho atanyang’anywa.”—Marko 4:24, 25.
6. Kwa habari ya kumpimia Yesu kipimo cha kupendezwa na cha kumsikiliza, je! yeye aliahidi kwamba angetoa tu kipimo kinacholingana?
6 Kwa hiyo, tukimpa Yesu kipimo kidogo katika kupendezwa na kusikiliza, hatuwezi kutazamia kupata mengi kutoka kwake, angaa kutoka kwa yale anayosema kwa ajili ya uongozi wetu, kwa faida yetu. Lakini tukionyesha kwamba tunamthamini akiwa Mwalimu wetu na kumpimia kipimo kamili katika kumsikiliza, kisha naye ataitikia na kutupatia kipimo kinacholingana cha habari na nuru. Hata hivyo, katika habari hii, yeye hahangaikii tu kusawazisha mambo. Mahali pake, kwa ukarimu wake na kulingana na uwezo wake, yeye atatupendelea na kutupatia mengi zaidi ya vile tulivyotazamia. Hivyo tunatajirishwa na kuwezeshwa kushiriki pamoja na wengine mengi tuliyo nayo, tukiwasaidia kufahamu mambo.
7, 8. Maneno hayo ya Yesu yaliyotangulia kutajwa yalitimizwaje kuhusiana na wanafunzi wake waliokuwa washiriki wake wa karibu, na kwa sababu gani?
7 Mwanafunzi aliyependelewa lazima awe na nia ya kujifunza, ndiyo, amheshimu kweli kweli Mwalimu wake na athamini mafundisho yake. Akiwa na nia ya namna hiyo, yeye atapewa mengi. Kwa mfano, baada ya hotuba ya Yesu ambayo alitoa akiwa ndani ya merikebu, wanafunzi waliokuwa washiriki wake wa karibu hawakuliachilia jambo hilo mara hiyo na kuliona kama jambo la kupendezwa nalo kwa kitambo tu. Waliuweka akilini mfano wake. Baadaye, faraghani, walimwuliza aueleze. Kwa sababu ya jitihada zao za ziada za kutaka kujua maana ya mafundisho yake, walipewa mengi zaidi ya wasikilizaji waliokuwa ufuoni mwa bahari. Wao hawakuvunjwa moyo na maneno ya mapema ya Yesu: “Hamjui mfano huu? Basi mifano yote mtaitambuaje?” (Marko 4:13) Wengi wa wasikilizaji waliokuwa ufuoni mwa bahari waliendelea kukaa katika hali hiyo. Lakini mitume wa Yesu walikuwa na tamaa ya kujifunza na kufahamu. Kwa hiyo, walijichukulia daraka la kuuliza wapewe mengi zaidi ya muhtasari tu ya mambo. Kwa hiyo walipewa mengi zaidi ya yaliyotazamiwa. Kwa habari yao, maneno ya Yesu yakatimizwa:
8 “Ninyi mmejaliwa kuijua siri ya ufalme wa Mungu, bali kwa wale walio nje yote hufanywa kwa mifano.”—Marko 4:11.
9, 10. Mambo yalikuwaje kwa habari ya wale waliokuwa nje, na kwa sababu gani?
9 Walio nje waliendelea kutosheka na muhtasari tu ya mambo yaliyotajwa katika mifano. Walikosa tamaa yenye kusukuma ya kutaka kujua mambo ya hakika yaliyofanya mifano hiyo itolewe. Kwa hiyo hawakupata kuifahamu. Wao hawakutaka kutenda kulingana na yale yaliyofundishwa na mifano hiyo. Kwa hiyo walijiepusha na daraka kubwa zaidi liletwalo na kufahamu. Kwa kuwa hawakujali kutanguliza ufalme wa Mungu, walithamini mambo ya kimwili zaidi ya mambo ya kiroho, “[ile] siri [takatifu] ya ufalme wa Mungu.”
10 Kwa sababu hawakutaka kujitwalia nafasi waliyofunguliwa na mifano ya Yesu, kwa kweli, wale wa nje, walipoteza yote. Kile walichokuwa nacho kwa habari ya kuizoelea mifano ya Yesu, kilitwaliwa kutoka kwao. Shetani Ibilisi alikitwaa kutoka kwao, kupitia kwa mawakili wake wa kibinadamu au kupitia kwa uchawi. Nuru yo yote ambayo huenda walikuwa wamekuwa nayo kupitia kwa kusikiliza mifano ya Yesu ilifunikwa na giza. Nuru ya kweli, ikisonga mbele na kuupita ufahamu wa mambo waliyoyasikia kutokana na mifano ya Yesu, iliwaacha katika giza kwa kulinganisha, wakiwa na maarifa ya juujuu tu ya mambo ya Kibiblia. Kwa hiyo walipapasa-papasa kama vipofu.
MFANO WA MTU ALIYEMWAGA MBEGU
11. Kulingana na Marko 4:26-29, Yesu alitoa mfano gani wakati huo?
11 Katika kutoa mfano juu ya jambo hilo lililotangulia kutajwa, Marko 4:26-29 anaandika hivi: “[Kwa hiyo Yesu akaendelea,] akasema, Ufalme wa Mungu, mfano wake ni kama mtu aliyemwaga mbegu juu ya nchi; akawa akilala na kuondoka, usiku na mchana, nayo mbegu ikamea na kukua, asivyojua yeye. Maana nchi huzaa yenyewe; kwanza jani, tena suke, kisha ngano pevu katika suke. Hata matunda yakiiva, mara aupeleka mundu, kwa kuwa mavuno yamefika.”a
12. Wanafunzi fulani wa Biblia wanafikiri kwamba mfano huo unafundisha nini kwa habari ya ufalme wa Mungu?
12 Katika mfano wa mapema wa Yesu alioutoa akiwa ndani ya merikebu, yeye alieleza juu ya mpanzi ambaye mbegu zake zilianguka kwenye namna nne za udongo. (Marko 4:1-9) Je! mpanzi huyo alifananisha mtu yule yule kama vile mtu huyo aliyemwaga mbegu katika mfano wake wa baadaye. Wanafunzi wengi wa Biblia wanafikiri hivyo. Wanafikiri kwamba mtu huyo aliyemwaga mbegu juu ya nchi vilevile anafananisha mtangazaji aliye mkuu zaidi wa ufalme wa Mungu, yaani, Yesu Kristo. Kwa msingi huo wanatoa sababu kwamba zile “mbegu” zinafananisha washiriki wa jamii ya Ufalme wa kimbinguni. Hivyo mfano wote unafananisha ukuzi wa jamii hiyo ya Ufalme kuanzia na wale 3,000 katika siku ya Pentekoste ya mwaka 33 W.K. kufikia hesabu kamili ya mwisho ya 144,000. (Ufu. 14:1) Kwa hiyo, lazima sasa tuwe katika “wakati wa mavuno” ya washiriki wa mwisho wa warithi wa ufalme wa Mungu. Walakini, maelezo ya namna hiyo ya mfano huo wa Yesu yanakutana na magumu kadha yasiyoshindika. Hayo yaweza kuwa magumu gani?
13. Yesu alianza kujenga kundi lake lililozaliwa kwa roho wakati gani, naye alikuwa katika hali gani wakati huo?
13 Basi, mfano huo unasema kwamba mtu huyo aliyemwaga mbegu, “akawa akilala na kuondoka, ‘usiku na mchana.” Maelezo ya namna hiyo yanalinganaje na Yesu Kristo aliyetukuzwa tangu aanze kujenga kundi lake la wanafunzi waliozaliwa kwa roho katika siku ya Pentekoste? Hayalingani naye hata kidogo! Petro wa kwanza 3:18, NW, husema juu ya Yesu kuwa “akiuawa katika mwili, lakini akifanywa hai katika roho,” hivi kwamba yeye si mwanadamu mkamilifu sasa kama vile alivyokuwa alipokuwa hapa duniani. Tangu Mungu Mwenye Nguvu Zote alipomfufua Yesu kutoka kwa wafu katika siku ya Jumapili, Nisani 16, 33 W.K., Mwana huyo wa Mungu “ni mng’ao wa utukufu wake na chapa ya nafsi yake.”—Ebr. 1:3.
14. Kwa habari ya jambo la kulala usingizi katika wakati wa usiku, ni kwa sababu gani mtu aliyemwaga mbegu juu ya nchi hangefananisha Yesu Kristo aliyetukuzwa?
14 Mambo yakiwa hivyo, vipi basi? Basi, Zaburi 121:1-4 husema hivi: “Msaada wangu u katika [Yehova], aliyezifanya mbingu na nchi. Asiuache mguu wako usogezwe; asisinzie akulindaye; naam, hatasinzia wala hatalala usingizi, yeye aliye mlinzi wa Israeli.” (Angalia pia Yeremia 1:12.) Hivyo, basi, Yesu Kristo aliyetukuzwa akiwa katika mkono wa kuume wa Mungu angeweza kulalaje kwa ukawaida wakati wa jua kutua katika Mashariki ya Kati kama mwanadamu duniani? Yeye hahitaji tena usingizi wa usiku wa kidunia ili awe katika hali ya kuweza kufanya kazi ya saa za nuru ya mchana. Kwani, miaka 1,000 kwa mwanadamu ni kama siku moja tu kwa Yesu Kristo aliye mfano wa Mungu! (Zab. 90:4; 2 Pet. 3:8) Kwa sababu hii moja peke yake yule mtu amwagaye mbegu juu ya nchi hangeweza hata kidogo kumfananisha Yesu Kristo aliyetukuzwa na asiyeweza kufa.b
15. Ni jambo gani linaloonyesha kama Mwana wa Mungu aliyekuwapo kabla ya kuwa mwanadamu alijua namna mbegu zikuavyo na namna nchi izaavyo matunda yenyewe?
15 Jambo jingine la kuangaliwa ni kwamba mfano huo wa Yesu unaendelea kusema: “Nayo mbegu ikamea na kukua, asivyojua yeye. Maana nchi huzaa [matunda polepole] yenyewe.” (Marko 4:27, 28) Ikiwa, sasa, mbegu imeayo na kukua inafananisha kundi la Kikristo katika ukuzi wake kuanzia na washiriki wake wachache mpaka kuwa na washiriki wengi, inamaanisha kwamba mpanzi hajui namna kundi hilo likuavyo kufikia washiriki 144,000 wenye nguvu. Walakini Yesu Kristo aliyekuwapo kabla ya kuwa mwanadamu alikuwa mfanya kazi pamoja na Yehova Mungu katika siku ya tatu ya kuumba, wakati ‘nchi ilipoanza kutoa majani, mche utoao mbegu kwa jinsi yake, na mti uzaao matunda, ambao mbegu zake zimo ndani yake, kwa jinsi yake.’ (Mwa. 1:12) Hivyo Mwana wa Mungu aliyekuwapo kabla ya kuwa mwanadamu alionyesha kuwa na maarifa kamili ya ukuzi wa miche na ya namna nchi inavyozaa matunda polepole yenyewe.
16. Ni maono gani katika kitabu cha mwisho cha Biblia yanayoonyesha kama Yesu Kristo aliyetukuzwa anasinzia au kulala usingizi kwa habari ya ukuzi wa makundi ya Kikristo?
16 Walakini, kwa habari ya ukuzi wa kundi, Ufunuo, kitabu cha mwisho cha Biblia, kilichoandikwa miaka 63 hivi baada ya Yesu kupaa mbinguni katika siku ya Alhamisi, Iyari 25, 33 W.K. (Mei 12, 33 W.K.), kinamfananisha Yesu kama akitembea kati ya vile vinara saba vya taa ambavyo hufananisha makundi saba katika Asia Ndogo. Macho yake yakiwa kama “mwali wa moto,” apaswa kuwa macho kabisa anapoichunguza hali ya kiroho ya hayo makundi saba yenye kujulikana sana. Lazima awe alijua namna makundi hayo yalivyokua yakawa katika hali anayoyaeleza kuwa.—Ufu, 1:14; 2:18.
17. Ni maono gani yanayoelezwa katika Ufunuo 5:6 yanayoonyesha kama Yesu Kristo aliyetukuzwa angeweza kufananishwa na yule mtu amwagaye mbegu juu ya nchi na kulala usiku?
17 Kwa habari ya kupaa kwa Yesu na kuonekana kwake mbele za Mungu huko mbinguni, yeye anafananishwa na mwana-kondoo ambaye alikuwa ndipo tu amechinjwa, na kuwa hai tena akiwa na “macho saba, ambazo ni [roho] saba za Mungu zilizotumwa katika dunia yote.” (Ufu. 5:6) Kuliko kuonyesha hali ya kusinzia au ya usingizi, uwezo kama huo wa kuona wenye nguvu mara saba wa Mwana-Kondoo wa Mungu ungeonyesha hali ya kuwa macho kabisa na kuweza kufahamu yote, wakati wote. Kwa wazi, basi, Yesu Kristo aliyetukuzwa hangeweza kufananishwa na mtu yule ambaye humwaga mbegu juu ya nchi na ambaye hulala usiku asiyejua namna alichopanda kikuavyo.
18. Hivyo, basi, kupatana na akili, huyo mtu katika ule mfano anafananisha nani?
18 Kwa hiyo, basi, mtu huyo katika mfano huo anafananisha nani? Marko mwandikaji wa Biblia anavuta fikira zetu kwa mkulima huyo mmoja baada tu ya Yesu kuwashauri wanafunzi waliokuwa washiriki wake wa karibu wasikilize wayasikayo. Kadiri fulani ya usikilizaji ingelipwa kwa mambo kadiri iyo hiyo, na hata kuongezewa mengi zaidi. Kwa hiyo, kupatana na akili, mtu huyo katika mfano huo anafananisha kila mtu mmoja mmoja anayejidai kuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo, Mhubiri aliye mkuu zaidi wa ufalme wa Mungu.
MAMBO YENYE KUONYESHA YA MFANO HUO
19, 20. Ni mambo gani mawili makuu yanayotia ndani huo mfano wote, na kwa hiyo ni jambo gani linalomaanishwa na mfano huo, kukiwa na matazamio gani, wingi au ubora?
19 Yesu aliuanza mfano huo kwa kusema hivi: “Katika njia hii [au Hivyo] ufalme wa Mungu ni kama vile tu wakati mwanamume anapotupa mbegu juu ya ardhi.”—Marko 4:26, NW; Tafsiri ya Kingdom Interlinear.
20 Tunaona mambo mawili makubwa yanayotia ndani huo mfano wote. Kwanza, kuna kule kupandwa kwa mbegu kuhusiana na ufalme wa Mungu, na, pili, kuna kule kuvuna mazao yanayotokana na mbegu zilizopandwa. Kwa hiyo maana yenyewe ni hii, kama vile kwa hakika kulivyokuwako kupanda mbegu, lazima kuvuna kutazamiwe. Lile jambo moja linafuata lile jingine bila kuepukwa. Ukweli ulio mzito ni kwamba apandacho mtu kuhusiana na ufalme wa Mungu kinaongoza kwenye atakachovuna. Mahali pa wingi, ubora wa avunacho ni jambo la maana!
21. Je! Yesu alionyesha waziwazi ni mbegu ya namna gani au ni udongo wa namna gani ilimopandwa ndani yake, na hata hivyo, ni ulizo gani linalotokea kwa habari ya mbegu hiyo?
21 Yesu hakuonyesha waziwazi namna ya mbegu au namna ya udongo unaohusika katika kupanda, Yeye alisema hivi: “Hata matunda yakiiva, mara aupeleka mundu [chombo kidogo cha mkononi], kwa kuwa mavuno yamefika.” (Marko 4:29) Wayahudi waliopewa mfano huo walikuwa na nyakati tatu za mavuno katika wakati wa mwaka wa kilimo. Mavuno ya kwanza yalikuwa baada tu ya Sikukuu ya Kupitwa ya majira ya masika, wakati ambapo suke la shayiri lilipotolewa na kuhani mkuu katika Nisani 16 katika hekalu la Yerusalemu. Siku hamsini tangu hapo, kuhani mkuu alitoa mazao ya kwanza ya mavuno ya ngano katika hekalu na baada ya hapo mavuno hayo yaliendelea. Mavuno ya tatu yalikuwa mwishoni mwa kiangazi nayo yalikumbukwa kwa sikukuu ya kukusanya, au ya vibanda, kuanzia na siku ya 15 ya mwezi wa saba, Tishri. (Kut. 23:14-17) Haikutajwa katika mfano huo ni wakati gani kati ya nyakati hizo tatu za mavuno uliomaanishwa. Lakini, hata iwe ni mbegu gani iliyopandwa, inafananisha nini?
22. Ikiwa mbegu hiyo haifananishi kundi la Kikristo, inafananisha nini, na je! ukuzi wa “mbegu” hizo waweza kurekebishwa?
22 Mfano wa Yesu unasema kwamba mbegu iliyopandwa ilimea ikakua na kutokeza nafaka iliyopevuka katika suke. Tumekwisha kuona kwamba mbegu iliyopandwa haikufananisha washiriki wa kundi la Kikristo. Kama vile makala inayofuata itakavyoonyesha, mbegu zilizomwagwa juu ya nchi hufananisha mbegu za sifa, maoni na uwezo wa kibinafsi wa mpanzi kwa ajili ya utumishi kuhusiana na ufalme wa Mungu. Ni lazima atafute chakula cha kuzilisha kana kwamba kutoka katika ardhi. Ukuzi wa sifa hizi za kibinafsi kufikia kukomaa na kupevuka ili zivunwe ni wa polepole. Hilo ni jambo la kuangaliwa na sisi, kwa kuwa si jambo lisiloweza kurekebishwa.
[Maelezo ya Chini]
a Linganisha yafuatayo na Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) wa Desemba 1, 1950, ukurasa 492, mafungu 34 na 35.
b Angalia Kitabu All the Parables of the Bible (Mifano Yote ya Biblia) cha Lockyer, ukurasa 252, fungu la 8: pia, The Pulpit Commentary (Kitabu Pulpit cha Maelezo) juu ya Marko cha Spence na Excell, Kitabu cha Kwanza, ukurasa 159 na 205.
[Picha katika ukurasa wa 8]
“Ufalme wa Mungu, mfano wake ni kama mtu aliyemwaga mbegu juu ya nchi; aawa akilala na kuondoka, usiku na mchana, nayo mbegu ikamea na kukua.”
[Picha katika ukurasa wa 10]
Kila mtu mmoja mmoja anayedai kuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo hupanda mbegu za sifa, maoni na uwezo wa kibinafsi kwa ajili ya utumishi kuhusiana na ufalme wa