Kuvuna Matunda Yanayoufaa Ufalme wa Mungu
1. Katika Yeremia 4:3, 4, Yehova alivuta fikira kwenye jambo gani?
KATIKA Yeremia 4:3, 4, Yehova asema hivi: “Ulimeni udongo katika konde zenu, wala msipande mbegu kati ya miiba. Jitahirini kwa [Yehova], mkaziondoe govi za mioyo yenu, enyi watu wa Yuda na wenyeji wa Yerusalemu; ghadhabu yangu isije ikatoka kama moto, ikawaka hata mtu asiweze kuizima, kwa sababu ya uovu wa matendo yenu.” Yehova alivuta fikira kwenye hali mbaya ya mioyo ya watu wake wa agano.
2. Mfano wa mbegu zilizoanguka katika udongo wenye miiba unaonyeshaje kwamba inatupasa kuwa waangalifu kuhusu mazingira ambayo katika hayo sisi tunapanda kiroho?
2 Vivyo hivyo, katika mfano mmoja Yesu Kristo alionyesha matokeo yenye kukatisha tamaa yanayotokana na kupanda mbegu kati ya miiba. Katika Mathayo 13:1-9 na vilevile katika Marko 4:1-9 alionyesha namna mbegu fulani zilizomwagwa na mkono wa mpanzi zilivyoanguka kwenye sehemu zilizokuwa na mbegu za miiba. Katika sehemu hizo yeye hakupata matokeo yo yote, kwa kuwa miiba ilimea ikasonga miche ya nafaka, na kwa hiyo hakuna mazao ya nafaka ambayo yangeweza kuvunwa. (Luka 8:4-8) Jambo hilo laonyesha kwamba lazima tuwe waangalifu kuhusu mazingira ambayo katika hayo tunafanya upandaji wetu wa kiroho.
3. Katika mfano wa Marko 4:26-29, mbegu inafananisha nini, nao Wakristo lazima wasitawishe nini kuhusiana na utu wao leo kama vile ilivyokuwa kwa Wakristo wa karne ya kwanza?
3 Katika mfano wa mpanzi na mbegu, kama vile unavyosimuliwa katika Marko 4:26-29, mbegu hiyo inafananisha sifa za utu. Yesu aliwaambia hivi Wayahudi wale waliokataa ule mfano wa mpanzi pamoja na mifano mingine: “Ufalme wa Mungu utaondolewa kwenu, nao watapewa [taifa] lingine lenye kuzaa matunda yake.” (Mt. 21:43, 45, 46) Kulingana na andiko hilo, kuna “matunda” ya ufalme wa Mungu. (Luka 3:8) Pamoja na matunda hayo ya Ufalme kuna lile linaloitwa “tunda la roho,” yaani, “upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujiweza.” (Gal. 5:22, 23, NW) Huko nyuma katika karne ya kwanza, Wakristo walioandikiwa na mtume Paulo walipaswa kupanda mbegu za sifa za Kikristo zilizohitaji kulishwa, kama vile Wakristo leo wanavyopaswa kufanya kuhusiana na ufalme wa Mungu. Sifa hizo za kibinafsi lazima zisitawishwe kufikia kukomaa kabisa, kukamilika.—Zek. 8:12; Yak. 3:18.
4. “Mbegu” ya sifa za Kikristo za kibinafsi yahitaji nini ili isitawi?
4 Wakati wa kupevuka kabisa ndio unaokuwa wakati wa kuzivuna. Lakini mpanzi Mkristo wa hizo “mbegu” apaswa achague kuzipanda wapi akiwa na tumaini la mwishowe kuvuna mavuno yanayotamaniwa? Yeye ataka mazao yake yawe na kibali ya Mungu, ili ahesabiwe kuwa astahili kukubaliwa kuhusiana na ufalme wa Mungu. Kama vile mbegu halisi inavyohitaji udongo, vivyo hivyo mbegu za utu wa kibinafsi wa Kikristo, lile “tunda la roho,” zahitaji mazingira.—Mit. 18:1.
5. Ili kuvuna mavuno yanayotazamiwa, lazima uangalifu utumiwe kuhusiana na jambo gani, kama vile inavyokaziwa katika Luka 8:14?
5 Ebu kumbuka ule mfano wa Yesu kuhusiana na zile namna nne za udongo ambapo mbegu za yule mpanzi zilianguka. (Marko 4:3-20; Luka 8:5-15) Mfano huo unaonyesha namna uangalifu pamoja na uchaguzi unaofaa yalivyo mambo yanayopaswa kuangaliwa kuhusiana na mazingira ya mbegu ikiwa mavuno yanayotazamiwa yatapata kuvunjwa. Kama vile Yesu alivyoeleza kuhusiana na mazingira ya mbegu yaliyokuwa na miiba: “Na [kwa habari ya zile] zilizoanguka penye miiba ni wale waliosikia, na katika kuenenda kwao husongwa na shughuli na mali, na anasa za maisha haya, wasiivishe lo lote.”—Luka 8:14.
6. Katika Wagalatia 5:7-9, Paulo alivutaje fikira kwenye matokeo mabaya ya mazingira mabaya?
6 Kupatana na jambo hilo, mtume Paulo alitaja jambo fulani kuhusiana na Wakristo waliokuwako Galatia alioandikia juu ya lile “tunda la roho,” ili kuwaonya kwamba walikuwa wakipatwa na matokeo mabaya kwa sababu ya mazingira mabaya. Yeye alisema hivi: “Mlikuwa mkipiga mbio vizuri; ni nani aliyewazuia msiitii kweli? Kushawishi huku hakukutoka kwake yeye anayewaita ninyi. Chachu kidogo huchachua donge zima.” (Gal. 5:7-9; Mt. 13:33) Wakristo hao Wagalatia walikuwa wakiongozwa vibaya na waendelezaji hao wa dini ya Wayahudi ambao mioyo yao haikuwa ikikubali kabisa kabisa Ukristo, na masikio yao hayakuitikia na macho yao yalikuwa yamefumbwa yasipate kuona. (Mt. 13:14, 15; Gal. 5:10) Lazima mashirika ya namna hiyo yenye kuzuia maendeleo yaepukwe.
7. Paulo alionyeshaje kuhangaika kama huko juu ya matokeo ya mazingira mabaya juu ya Wakristo waliokuwako Korintho?
7 Vilevile mtume Paulo aliogopa kwamba huenda kundi la Korintho likawa halikuwa likisitawisha lile “tunda la roho,” kwa kuwa aliliandikia akawaambia hivi: “Maana nachelea [naogopa], nisije nikawakuta si kama vile nitakavyo kuwakuta, nikaonekana kwenu si kama vile nitakavyo; nisije nikakuta labda fitina, na wivu, na ghadhabu, na ugomvi, na masingizio, na manong’onezo, na majivuno, na ghasia.” (2 Kor. 12:20) Baada ya kutaja maneno ya wale waliokuwa wakisema, “Tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa,” Paulo, akiwa na sababu nzuri, angeweza kutoa onyo hili: “Msidanganyike! Urafiki mbaya huharibu tabia njema.” —1 Kor. 15:32, 33, HNWW.
8. Ni kwa sababu gani sifa za utu zitaendelea kukua Mkristo ajapolala, na sababu gani yeye hawezi kuwa na hakika anapoamua kulingana na kile kinachomea mwanzoni?
8 Kama vile udongo ambamo ndani yake mbegu huanguka na ambao una uwezo uliopewa na Mungu wa kulisha ama ngano ama miiba, mazingira ambayo katika hayo Mkristo anachagua kusitawisha sifa za utu yatakuwa na matokeo kwake ama mema ama mabaya. Hata akilala akiwa katika mazingira ya namna hiyo, sheria ya uvutano wa mazingira itatenda kazi juu yake pasipo kushindwa mpaka kile kilichopandwa na ambacho kimekua kiruhusu mundu utumiwe kwa kuwa wakati wa mavuno ya kibinafsi umefika. Kwa habari hii, Yesu alisema hivi: “Maana nchi huzaa yenyewe; kwanza jani, tena suke, kisha ngano pevu katika suke.” (Marko 4:28) Kwa mpanzi, ukuzi huo unakaribia sana kutofahamika na akili zake nao unafanyizwa na nguvu ambazo yeye hawezi kuzifahamu. Ukuzi huo utaendelea polepole katika upande mmoja au mwingine, kwanza kama jani, kisha kama suke, na mwishowe kama nafaka iliyopevuka katika suke.
9. Ule mfano wa ngano na magugu unaonyeshaje namna mtu asivyoweza kuwa na hakika kuhusu matokeo ya mwisho kutokana na kupanda katika mazingira ya namna fulani?
9 Wakati mbegu imeapo kwanza na kutokeza jani, huenda mpanzi asiwe na hakika atavuna kitu gani, akiamua kulingana na namna mambo yanavyoonekana. Katika kipindi hicho cha mwanzoni cha ukuzi huenda asiwe na hakika kabisa ni kitu gani kinachokua; yeye anakumbuka tu namna ya mbegu aliyopanda. Kutoa mfano: Katika mfano wa Yesu wa ngano na magugu, katika Mathayo 13:26-30, yeye alisema hivi:
Baadaye majani ya ngano yalipomea na kuzaa, yakaonekana na magugu. Watumwa wa mwenye nyumba wakaenda wakamwambia, Bwana, hukupanda mbegu njema katika konde lako? limepata wapi basi magugu? Akawaambia, Adui ndiye aliyetenda hivi. Watumwa wakamwambia, Basi, wataka twende tukayakusanye? Akasema, La; msije mkakusanya magugu, na kuzing’oa ngano pamoja nayo. Viacheni vyote vikue hata wakati wa mavuno; na wakati wa mavuno nitawaambia wavunao, Yakusanyeni kwanza magugu, myafunge matita matita mkayachome; bali ngano ikusanyeni ghalani mwangu.
10. Ni wakati gani tutakapoona pasipo kukosea matokeo ya kupanda katika mazingira yo yote yale?
10 Kwa hiyo, baada ya kupanda mbegu za sifa zetu za utu, kile kinachomea kikiwa kama jani la nyasi huenda kwanza kisitambulikane (kisijulikane) kuwa ni kitu gani ambacho nchi imezaa. Ni baadaye tu, wakati kimekua na kuzaa matunda, ndipo mpanzi hatakosa kujua ni kitu gani ambacho nchi imemzalia.
11. Licha ya hali inayoonekana ya udongo, ni jambo gani jingine lililo la maana katika kuamua ubora wa kile kinachokuzwa katika udongo wa namna hiyo?
11 Udongo ni wa maana katika kuamua juu ya namna ya matunda yanayopatikana mwishowe. Yesu alisema hivi: “Maana nchi [si Mungu] huzaa yenyewe; kwanza jani, tena suke, kisha ngano pevu katika suke. (Marko 4:28) Katika ule mfano wa zile namna nne za udongo, Yesu alieleza tu juu ya hali zenye kuonekana za namna hizo za udongo. Lakini vilevile dawa (madini) zilizofanyiza udongo huo ni za maana katika kuamua ubora wa matunda, kama vile wakati udongo unapokuwa na chachu, magadi, au chumvi, au unapotiwa mbolea ya dawa au isiyo ya dawa, ya majani.
12. Kwa hiyo, basi, nchi au udongo hufananisha nini?
12 Kwa kuwa nchi, au udongo, inakuwa sehemu ya maana sana hivyo kwa habari ya ukuzi na ubora wa mazao, hufananisha mazingira ya kijamii, kiadili na kidini ambayo katika hayo tunasitawisha mbegu za sifa zetu za kibinafsi, na bila shaka, watua wanahusika. Hilo ni jambo linalotupasa tuwe wenye kuchagua.
MAZINGIRA AMBAYO KATIKA HAYO TUNASITAWISHA SIFA
13. Hata katika kundi la Kikristo, je! kunaweza kuwako mazingira yasiyofaa ukuzi unaofaa wa Kikristo?
13 Hata ndani ya kundi la Kikristo huenda kukawako mazingira au mashirika ambayo hayasaidii sana kiroho. Wengine ambao wametoka katika ulimwengu hivi karibuni wakaonyesha wakf wao kwa Mungu kwa kubatizwa katika maji huenda wakawa na maelekeo ya kuleta katika kundi jambo fulani ambalo bado wanashikamana nalo—kadiri fulani ya uulimwengu. Ebu na tukumbuke kwamba ni kundi la Kikristo ambalo mtume Paulo aliandikia hivi: “Naliwaandikia katika waraka wangu [uliotangulia], kwamba msichangamane na wazinzi. . . . Lakini, [sasa nawaandikia] kwamba msichangamane na mtu aitwaye ndugu, ikiwa ni mzinzi au mwenye kutamani au mwenye kuabudu sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang’anyi; mtu wa namna hii msikubali hata kula naye.”—1 Kor. 5:9-11.
14. Katika Wagalatia 6:7, 8, Paulo anawaonyaje Wakristo juu ya kupanda katika upande usiofaa?
14 Vilevile, mtume uyo huyo aliyaandikia hivi makundi yaliyokuwako katika jimbo la Kirumi la Galatia katika Asia Ndogo: “Msidanganyike, Mungu hadhihakiwi; kwa kuwa cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna. Maana yeye apandaye kwa mwili wake, katika mwili wake atavuna uharibifu; bali yeye apandaye kwa [roho], katika [roho] atavuna uzima wa milele.” (Gal. 6:7, 8) Mtu anayedai kuwa Mkristo aweza kuwa akipandia mwili wake usiokamilika mbegu kwa kutafuta kusitawisha sifa zake za kibinafsi katika mazingira ya kilimwengu yanayoufurahisha mwili wake usiokamilika.
15. Kwa hiyo, ni maulizo gani yanayotokea, kwa habari ya kutafuta mazingira yetu katika kundi la Kikristo?
15 Leo, katika kundi, je! sisi tunashirikiana sana na wale ambao kidogo wangali na maelekeo ya uulimwengu. Wao kwa kawaida wanajitia sana katika huo nao wanataka wengine washirikiane nao ili wajione kuwa na haki katika kujifurahisha mara nyingi hivyo katika uulimwengu huo. Je! sisi tunaruhusu mazingira au mashirika yetu ya kirafiki katika kundi yatuzuie tusipige mbio vizuri katika mbio za uzima wa milele? Je! sisi tunaruhusu wale washiriki wa kundi ambao wangali na maelekeo ya uulimwengu watushawishi tuelekee upande ule ule wanaoelekea, kwa sababu unafurahisha mwili wetu usiokamilika?
16. Ili tuweze kuielekea kwa kufaulu ile siku ya majaribu, ni jambo gani tunalopaswa kufikiria kuhusu mazingira yetu?
16 Huenda mwanzo matokeo ya mwendo wetu wa kujifurahisha anasa nyingi mno yasionyeshe waziwazi mwishowe tutakuwa watu wanaodai kuwa Wakristo wa namna gani. Inakuwa hivyo kwa sababu “nchi” au mazingira ambayo katika hayo tunachagua kushirikiana nayo yatazaa matunda polepole. “Jani” la nyasi laonekana kutokuwa na hatia na wale wanaoliona, si lenye hatari yenye kudhuru. Twalala usiku na kuamka mchana, nao ukuzi wa sifa zetu za kibinafsi wasonga mbele bila kushindwa, namna ukuzi huo unavyoendelea sisi hatujui. Kuendelea kwetu katika mwendo huo wa uhuru na wa rahisi kutatuongoza kwenye matokeo yasiyoepukika, yaani, ukuzi uliokomaa wa sifa zetu za kibinafsi kwa sababu ya mazingira ambayo ni kama udongo, ambayo katika hayo tumejiruhusu sisi wenyewe tusitawi. Je! yale tutakayovuna kwa kutumia mundu yatatustahilisha tuelekeane kwa kufaulu na majaribu ya siku ya kutoa hesabu?
17. Ni jambo gani tusilopaswa kusahau kuhusu mazingira ambayo katika hayo tunapanda mbegu ya sifa za utu wetu?
17 Na tusisahau kwamba, kama vile “nchi,” au udongo, mazingira ambayo katika hayo mbegu za sifa zetu za kibinafsi zimepandwa na kusitawishwa yatakuwa na matokeo katika ukuzi wetu. Yaweza kutufanya tuwe aina isiyo nzuri sana ya kile kitu halisi, kile kitu kilichokusudiwa kutokezwa wakati tulipoanza kupanda.
18. Ni mfano gani wa mashirika mabaya tunaopewa katika Hesabu 11:4-34?
18 Mfano wa kweli wa matokeo ya mashirika mabaya hata kati ya watu wa Yehova ulitolewa katika jangwa la Sinai katika siku za Musa. Twalikumbuka lile “kundi kubwa la watu waliochangamana” ambalo lilitoka Misri pamoja na Waisraeli wakaivuka Bahari ya Shamu. (Kut. 12:38) Kwa habari ya sehemu hii ya watu isiyokuwa ya Kiisraeli, nabii Musa hutuambia hivi:
Katika mkutano wa wafuasi waliokuwa kati yao [Waisraeli], wakashikwa na tamaa; wana wa Israeli nao wakalia tena, wakasema, N’nani atakayetupa nyama tule? Twakumbuka samaki tuliokula huko Misri bure; na yale matango, na matikiti, na mboga, na vitunguu, na vitunguu saumu; lakini sasa roho zetu zimekauka; hapana kitu cho chote; hatuna kitu cha kutumaini isipokuwa hii mana tu. . . . Jina la mahali pale likaitwa Kibroth-hataava; [maana yake Mahali pa Mazishi ya Tamaa ya Kichoyo].—Hesabu 11:4-34; angalia pia 1 Wakorintho 10:1-6, 10, 11.
19. Jambo lililowapata Waisraeli pamoja na “kundi kubwa la watu waliochangamana” nao jangwani laonyeshaje kwamba hatuwezi kumlaumu Mungu kwa sababu ya matokeo mabaya yanayotupata kutokana na mazingira tuliyojichagulia sisi wenyewe?
19 Hivyo hilo “kundi kubwa la watu waliochangamana” lilianzisha jambo hilo kati ya Waisraeli. Kwa sababu ya kutoridhika na riziki ya Yehova ya mkate ulioshuka kutoka mbinguni, waliigeuza mioyo yao ikaielekea Misri kwa sababu ya kutamani kwa choyo vitu walivyojifurahisha hapo kwanza katika nchi hiyo yenye kuabudu sanamu. (Zab. 105:40) Walifanya matumbo yao kuwa miungu yao, kwa sababu walikuja pamoja na tamaa ya kichoyo ya mambo ya kimwili anasa ya Misri iliyotawalwa na mashetani. (Flp. 3:19) Kwa hiyo waliwaambukiza Waisraeli tamaa ya namna hiyo. Mfano huo wa kweli ni onyo zuri kwetu leo. Hatuwezi kumlaumu Mungu kwa sababu ya matokeo mabaya tunayovuna kutokana na mazingira mabaya tuliyochagua.
20. Mahali pa Mungu kulaumika kwa sababu ya matokeo yanayotupata kutokana na mwendo tuliouchagua, ni jambo gani linalolaumika?
20 Ikiwa hatuwezi kumtia Mungu katika habari ya mifano ya zile namna nne za udongo na ngano na magugu, je! ni jambo linalopatana na akili, jambo lenye kupatana, kumtia Mungu katika utimizo wa Marko 4:26-29? Kwa ujumla, “nchi [yenyewe hutoa] machipuko yake,” na “bustani [yenyewe huotesha] vitu vilivyopandwa ndani yake.” (Isa. 61:11) Hivyo, basi, (“jani” la) marijuana, bangi, tumbako pamoja na mimea mingine inayokuzwa kwa ajili ya kutengeneza kasumba, zaweza kukua katika udongo uliolimwa kama vile nafaka zinavyokuwa. Kwa wazi, basi, mazao yanayovunwa yanategemea anachopanda mpanzi pamoja na namna ya udongo ambamo ndani yake anapanda mbegu.
21. Ni mfano gani kutoka katika nchi ya Uholanzi unaoonyesha kwamba mazingira ambayo katika hayo mbegu inapandwa huwa na matokeo juu ya mambo?
21 Mazingira ambayo katika hayo mbegu inajikuta yanakuwa na matokeo juu ya mambo. Ebu na tukumbuke kwamba namna mbalimbali za udongo huwa na dawa (madini) zinazotofautiana. Namna moja ina chachu au magadi, nyingine ina chumvi, na vivyo hivyo. Hivyo wakati wenyeji wa nchi ya Uholanzi walipotaka kutumia sehemu fulani ya nchi yenye maji ya bahari kwa ukulima, walijenga mahandaki wakayakusanya maji hayo katika maboma. Kisha wakayaondoa maji hayo kwa mabomba, na kuiacha sehemu ya nchi iliyo kama bonde. Walakini sehemu hiyo ya nchi iliyopatikana ilikuwa inajaa chumvi ya baharini. Haikuwa inafaa mara hiyo kukuza nafaka zinazoweza kuliwa. Kwa hiyo kwanza walilazimika kuutayarisha udongo huo kwa kupanda nyasi ya namna ya mafunjo iliyositawi vizuri sana katika udongo wenye chumvi. Kufanya hivyo kuliusafisha udongo. Ndipo wangeweza kukuza nafaka na kupata mavuno mazuri.
22. Kwa kawaida. sisi tunapanda wapi mbegu za sifa za utu wetu, nalo ni jambo gani lililo la hakika kuhusu matokeo ya jambo hilo?
22 Ndivyo ilivyo kwa habari ya mbegu za sifa za utu wetu: tuna lazima ya kuzipanda mahali fulani, kwa kawaida katika mazingira tunayochagua sisi wenyewe. Itatulazimu kukutana na wakati wa mavuno. Je! kile tutakachovuna kitafaa kwa ajili ya uhusiano wenye kukubalika kwa ajili ya ufalme wa Mungu? Mazingira au mashirika tunayokuwa nayo kwa ukawaida yatalihusu sana jambo hilo. Hata ndani ya kundi la Kikristo huenda tukatafuta ushirika wa kirafiki wa watu waliobatizwa ambao wangali wanashikilia mambo ya kilimwengu, na ambao hawashtakiwi na dhamiri zao kwa habari ya kuyaingiza kwa siri katika kundi la Kikristo. Utu wetu wa Kikristo pamoja na mwenendo bila shaka vitapatwa na matokeo mabaya ya mambo hayo yenye kuambukiza.
23. Kuliko vile mambo yanavyoonekana kuwa mwanzoni, ni nini kitakachoamua kama mwishowe tutapata furaha?
23 Ukuzi wa Mkristo aliyeambukizwa kuuelekea ulimwengu utakuwa wa polepole, hali ya kutoka kwenye njia ya Kikristo kwanza inakuwa ndogo sana hata haifahamiki. Ni kama vile “jani” litokavyo katika mbegu. Walakini, bila kukosea wakati wa mavuno utaonyesha tumesitawi tukawa kitu gani, kwa kuwa kutakuwako malipo kama matokeo. Wakati ambapo Ukristo wa kweli peke yake ndio utakaoweza kuelekeana na jaribu, kila mtu mmoja mmoja akilazimika kutumia mundu wake na kukusanya alichokua akawa. Je! kile atakachovuna kitamwacha katika hali ya kukata tamaa, akifunuliwa wazi kuwa madai yake ya Kikristo ni ya uongo? Mwenye furaha ni Mkristo ambaye ana sababu za Kimaandiko za kuwa mwenye kuridhika na kile kinachovunwa na mundu wake.—Linganisha Zaburi 126:5,-6.
24. Je! utakatifu wetu wa kibinafsi utazuia matokeo ya mazingira tunayoshirikiana nayo sikuzote?
24 Polepole sisi tunakua kuelekea njia moja ama nyingine, katika njia ya kilimwengu au ya kiroho. Ole wetu ikiwa tunajidanganya au kuruhusu wengine wa-tudanganye tufikiri kwamba tunaweza kuwa na mashirika mabaya pasipo kuharibu mazoea yetu mazuri ya Kikristo. (1 Kor. 15:33, NW) Hatuwezi kumdhihaki Mungu kwa kujaribu kuibadili sheria yake isiyobadilika kwamba, kama vile kulivyo kupanda, vivyo hivyo lazima kuweko mavuno na kwamba mahali tunapopanda panahusu sana kile tunachovuna. Yeye anatuonya kwamba utakatifu wetu wa kibinafsi hautatoka kwetu na mara hiyo kuwafanya wengine kuwa watakatifu, Badala yake, tukiendelea sikuzote kushirikiana na walimwengu wachafu bila kujilinda matokeo yatakuwa kwamba sisi vilevile tutakuwa wachafu.—Hag. 2:10-14.
25. Kulingana na Wagalatia 5:19-24, ni nini kitakachotuweka katika uhusiano unaoufaa ufalme wa Mungu?
25 Kwa kutangulia kufikiria mambo kimbele kwa msaada wa Maandiko tunaweza kuamua namna matokeo ya mwendo wetu yatakavyokuwa. Je! sisi mradi wetu ni kuendelea kuwa na uhusiano wenye amani na ufalme wa Mungu? “Matendo ya mwili” hayatatufikisha kwenye mradi huo! Kwa upande mwingine, kuna lile ‘tunda la roho,’ na tukilisitawisha hatutashindwa na tamaa na matendo ya mwili. Kwa kufuatia mwendo huo wa uangalifu tutaridhika kwa kuwa na matokeo ya kuvuna matunda yanayoufaa ufalme wa Mungu kupitia kwa Kristo.—Gal. 5:19-24.
26. Ni mwendo gani utakaotuthawabisha na mavuno ya sifa za utu unaokubalika?
26 Ufalme wa Mungu, ambao kwa muda mrefu sana wanafunzi wa Kristo wameomba uje, unakaribia sana kuja na kuondoa serikali zote ambazo ni adui na kuitetea enzi Yake kuu ya ulimwengu wote. Pamoja na hayo wakati wa mavuno kwa kila mtu binafsi uko mbele ya kila mmoja wetu kuhusiana na ufalme huo. Uangalifu ulio mkubwa zaidi wapaswa kutumiwa kwa habari ya mazingira yaliyo kama nchi ambamo ndani yake tunaweka mbegu za sifa za utu wetu. Ushirika wetu wa kirafiki, kitafrija, kiadili na kidini wapaswa sikuzote kuwa pamoja na wale wanaoupenda ufalme wa Mungu kupitia kwa Kristo. Kwa kufikiria kwa uzito sana kimbele juu ya kile tunachopanda, na mahali tunapokipanda, sikuzote tukiupandia mbegu ufalme wa Mungu tutathawabishwa kwa kupata mavuno mengi sana ya utu kama wa Kristo uliokomaa na wenye kutenda. Yehova Mungu atapendezwa kama nini na jambo hilo! Yeye atatupa pendeleo la kutukubali pamoja na baraka zote zinazotokana na kukubaliwa huko.
27. Ni kitu gani kitakachotutokezea utimizo wenye kibali wa mfano katika Marko 4:26-29?
27 Kwa hiyo, tukiwa chini ya uharaka wa nyakati wenye kuendelea, tutafanya vizuri tukitii onyo hili la wakati wake: “Tukaangaliane sisi kwa sisi na kuhimizana katika upendo na kazi nzuri; wala tusiache kukusanyika pamoja, kama ilivyo desturi ya wengine;. bali tuonyane; na kuzidi kufanya hivyo, kwa kadiri mwonavyo siku ile kuwa inakaribia.” (Ebr. 10:24, 25) Kufanya hivyo kutatutokezea utimizo wenye kibali wa mfano mfupi lakini wenye nguvu wa mpanzi na mbegu, wa Marko 4:26-29. Wakati huo tutapata kuona “furaha ya wakati wa mavuno.” Tukiwa na furaha kubwa sana tutapata kuthamini kabisa kwamba “yeye apandaye kwa [roho] katika [roho] atavuna uzima wa milele.”—Gal. 6:8; Isa. 9:3. —Kutoka The Watchtower June 15, 1980.
[Maelezo ya Chini]
a Hiyo inafanana na vile alivyosema Yesu katika mfano wake wa ngano na magugu, kwamba “shamba” lilikuwa ulimwengu wa watu. (Mt. 13:38) Ila hapa, katika Marko 4:26-29, “nchi” ambayo ndani yake mbegu zinapandwa, badala ya kuwa ulimwenguni pote, inahusu tu watu ambao mtu mmoja mmoja anakutana nao na kushirikiana nao. “Nchi” haifananishi “moyo” wa watu mmoja mmoja, kama vile katika Mathayo 13:19 na Luka 8:12, 15.
[Picha katika ukurasa wa 15]
Kama vile nchi ambayo juu yake mbegu huanguka, mazingira ambayo katika hayo Mkristo anachagua kusitawisha sifa za utu yatakuwa na matokeo ama mema ama mabaya kwake.