Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • kc sura 11 kur. 96-104
  • Mifano ya Ufalme

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mifano ya Ufalme
  • “Ufalme Wako Uje”
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “MPANZI” MWINGINE
  • UFALME-BANDIA
  • YULE MPANZI NA “ADUI” YAKE
  • MPANGO WENYE KUFANIKIWA WA ‘KUVUA SAMAKI’
  • Kufunuliwa Wazi kwa Kimbilio la Uongo la Ufalme
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Mifano Kuhusu Ufalme
    Yesu—Njia, Kweli, na Uzima
  • Kufundisha kwa Vielezi
    Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi
  • Vitu Ambavyo “Ufalme wa Mbinguni” Unafanana Navyo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
Pata Habari Zaidi
“Ufalme Wako Uje”
kc sura 11 kur. 96-104

Sura ya 11

Mifano ya Ufalme

1 Sababu gani mifano ya Yesu inawapendeza wote wanaomtumikia Mungu?

ALIPOKUWA pamoja na wanafunzi wake, Yesu alisema mifano mingi. Mifano hiyo inaonyesha yanayohusika katika kuwa mshiriki wa ufalme wa mbinguni. Inaonyesha mwendo ambao ni lazima uchukuliwe na lile “kundi dogo” la warithi wa Ufalme, pia na wale watakaopata uzima wa milele duniani chini ya ufalme huo. Hao “kondoo wengine” pia wanashangilia kuujua unabii unaohusu Ufalme, nao kwa bidii sana wanasali “uje.”—Luka 12:32; Yohana 10:16; 1 Wathethalonike 5:16-20.

2, 3. (a) Sababu gani Yesu alitumia mifano? (b) Sababu gani wengine wasio wanafunzi wake walishindwa kufahamu? (c) Tofauti na wale wanaosimuliwa katika Mathayo 13:13-15, sababu gani sisi tumepaswa kujifunza Neno la Mungu kwa bidii?

2 Alipokuwa amekwisha kuwasimulia watu mmojawapo mifano hiyo, wanafunzi wa Yesu walimjia na kumwuliza: “Kwanini wewe unawaambia kwa kutumia mifano? Kwa kujibu Yesu alisema:

“Ni ninyi mmepewa kufahamu siri za ufalme wa mbingu, lakini watu hao hawakupewa.” (Mathayo 13:10, 11, “NW”)

Sababu gani? Ni kwasababu hawakuwa na nia ya kuchimbua sana na kupata maana yenye kina zaidi ya maneno yake, ili mioyo yao iwasukume wachukue hatua kwa ajili ya “habari njema.” Hawakuuona ule Ufalme kuwa “hazina” au “lulu yenye thamani kubwa.”—Mathayo 13:44-46, NW.

3 Yesu alitumia maneno ya unabii wa Isaya akionyesha yametimia kwa hao wasioamini, akisema: “Kwa kusikia, ninyi mtasikia lakini hamtapata kuelewa hata kidogo; na, kutazama, mtatazama lakini hamtaona hata kidogo. Maana moyo wa watu hawa umekuwa usiopokea kitu, na kwa masikio yao wamesikia bila itikio, na wamefumba macho yao; wasipate kamwe kuona kwa macho yao na kusikia kwa masikio yao na kupata kuelewa kwa mioyo yao na kugeuka nami niwaponye.” (Mathayo 13:13-15, NW) Imetupasa tutake kuepuka kuwa kama watu hao wasiothamini. Basi, na tujitahidi kujifunza Neno la Mungu.

4. (a) Ni mioyo ya aina gani inayoshindwa kufaidika na lile neno? (b) Tunaweza kufaidikaje tukijitahidi kuelewa maana ya lile neno?

4 Katika mfano wake uliotokezwa katika Mathayo 13:3-8, Yesu anajisema mwenyewe kuwa “mpanzi” wa mbegu. Yeye anapanda “neno la ufalme” katika mioyo ya aina mbalimbali. Mioyo ya watu fulani ni kama udongo kando ya barabara. Kabla ya mbegu kupata mizizi, Ibilisi anatumia wafuasi wake kama “ndege” ili wang’oe “neno mbali na mioyo yao ili wasipate kuamini na kuokolewa.” Mioyo mingine ni kama udongo wenye mawe. Kwanza, inakubali neno kwa furaha, lakini ndipo mmea mchanga unanyauka kwa jaribu au mateso. Mbegu nyingine inaanguka katika “miiba”, ambamo inasongwa na “mahangaikio na mali na anasa za maisha haya.” Ah, lakini iko pia ile “mbegu” iliyopandwa juu ya udongo wa aina nzuri!

“Hiyo ndiyo yule anayesikia neno na kupata kulielewa, anayezaa kwelikweli matunda na kufanyiza huyu mara mia, yule sitini, yule mwingine thelathini.” (Mathayo 13:18-23; Marko 4:3-9, 14-20; Luka 8:4-8, 11-15, “NW”)

Ndiyo, tutabarikiwa, na utumishi mtakatifu wetu kwa Mungu utakuwa wenye kuzaa matunda kweli kweli ikiwa tunalipokea lile neno katika mioyo yenye kuthamini na kujitumikisha kwa ajili ya ufalme wa Mungu!

“MPANZI” MWINGINE

5. (a) Sasa tunatiwa moyo tuangalie mfano gani mwingine? (b) Sababu gani “mwanamume” huyo hangeweza kuwa ni Bwana Yesu?

5 Kati ya Injili zote, masimulizi ya Marko pekee ndiyo yanayofuatia mfano huo wa ule “mpanzi” kwa kuongezea mfano unaohusu “mpanzi” tofauti. Muda mfupi kabla ya kutoa mfano huo, Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwa faragha hivi: “Angalieni kile mnachosikia.” Kisha akaunganisha mfano huo, akisema:

“Kwa njia hiyo ufalme wa Mungu ni kama wakati mwanamume anapoitupa mbegu juu ya udongo, na analala usiku na anaamka mchana, na mbegu inachipuka na kukua ikawa ndefu, hasa jinsi inavyokua yeye hajui.” (Marko 4:24-27, “NW”)

Kwa wazi, “mwanamume” huyo si yule Bwana Yesu Kristo aliyetukuzwa, kwa sababu yeye hahitaji usingizi wa usiku hapa duniani. Wala haingekuwa sahihi kusema kwamba yule Mwana wa Mungu, aliyefanya kazi pamoja na Baba yake katika kuumba vitu vyote, “hajui” jinsi ukuzi unavyotukia. (Wakolosai 1:16) Hivyo katika maneno yanayozunguka tunaweza kufahamu kwamba yule “mwanamume” anamaanisha Mkristo mmoja mmoja ambaye imempasa awe ‘akiangalia’ mambo yanayohusiana na “ufalme wa Mungu.”

6. Ni mambo gani mawili ambayo kila “mpanzi” amepaswa kuangalia, na kwa sababu gani?

6 Kila “mpanzi” amepaswa atazame tabia za utu ambazo anatumia katika kupanda, na pia mazingira ambamo anapanda. Pasipo sisi kujua, huenda usitawi wa utu wetu ukavutwa uwe mzuri au mbaya, kulingana na ule “udongo” au aina ya watu tunaoshirikia nao tunapotaka kusitawisha sifa za Kikristo—iwe ni ndani au nje ya kundi. (Linganisha 1 Wakorintho 15:33, NW.) Hatimaye, “punje iliyo kamili” itaonekana katika kichwa, na tutavuna sawasawa na ilivyo. (Marko 4:28, 29, NW) Ni jambo la maana kama nini kwamba wale wa lile “kundi dogo,” na wote wanaojitahidi kuufikia uzima wa milele katika mpango wa Ufalme wa Mungu, waangalie wanachopanda na mahali wanapopanda kuhusiana na usitawishaji wa nyutu zilizo kama utu wa Kristo!—Waefeso 4:17-24; Wagalatia 6:7-9.

UFALME-BANDIA

7. Ile mifano mbalimbali inatusaidia kuuonaje ule Ufalme?

7 Masimulizi ya Marko yanaeleza Yesu akiendelea kusema:

“Tutafananisha ufalme wa Mungu na nini, au tutausimulia kwa mfano gani?” (Marko 4:30, “NW”)

Ndipo anatukaribisha tuutazame ule Ufalme katika hali tofauti. Kweli kweli, mifano hiyo inatusaidia tuutazame ule Ufalme kwa maoni mbalimbali, kama vile tunavyoweza kuchunguza jengo fulani upande wa nje na upande wa ndani, na tukiwa kwenye pembe mbalimbali.

8. (a) Sababu gani ule ukuzi mkubwa ajabu kutokana na punje ya haradali haungeweza kumaanisha wale warithi wa Ufalme? (b) Sababu gani maana ya ukuzi huo inafaa kutumiwa kuhusu “ufalme” wa Jumuiya ya Wakristo? (c) Masimulio ya Mungu juu ya Israeli kafiri yanaungaje mkono maoni hayo?

8 Hivyo imetupasa tuufananishe ufalme wa Mungu na nini? Yesu anajibu:

“Kama punje ya haradali, ambayo wakati ilipopandwa katika udongo ilikuwa ndiyo ndogo kuliko mbegu zote zilizo juu ya dunia—lakini wakati imekwisha kupandwa, inatokea na inakuwa kubwa zaidi ya mboga nyingine zote na inafanyiza matawi makubwa, hata ndege wa mbinguni wanaweza kupata makao chini ya uvuli wayo.” (Marko 4:30-32, “NW”)

Huo ni ukuzi mkubwa ajabu—na bila shaka ni wa jambo fulani lenye mpanuko mkubwa zaidi ya lile “kundi dogo” la warithi wa Ufalme 144,000, ambao ‘Baba ametoa kibali ya kuwapa ufalme’! (Luka 12:32 NW; Ufunuo 14:1, 3) Ni ukuzi wa ule “mti”-bandia mkubwa wa Jumuiya ya Wakristo iliyopotoka ikaliacha kundi ambalo Yesu alikuwa amepanda. (Luka 13:18, 19) Ni kubwa mno! Inajivunia kuwa na washiriki zaidi ya 900,000,000 ulimwenguni pote, ambao inadai ati watakwenda mbinguni. Ufalme huo kafiri ulifananishwa zamani na taifa kafiri la Israeli, ambalo Yehova alisema habari zake hivi: “Nalikuwa nimekupanda, mzabibu mwema sana, mbegu nzuri kabisa; umegeukaje, basi, kuwa mche usiofaa wa mzabibu-mwitu machoni pangu?”—Yeremia 2:21-23; ona pia Hosea 10:1-4.

9. (a) “Ndege” na yale matawi ya ule “mti” ni nani? (b) Kulingana na maneno yaliyo katika 2 Wathesalonike 1 na Mathayo 7, sababu gani imetupasa tuondoke kabisa karibu na “mti” huo?

9 Kulingana na masimulio ya Mathayo ya “mti” huo, “ndege wa mbinguni wanakuja na kupata makao kati ya matawi yayo.” Kwa wazi, hao ni “ndege” wale wale wa ule mfano uliotangulia kutolewa wanaomeza kwa pupa lile “neno la ufalme” linaloanguka kando ya barabara. (Mathayo 13:4, 19, 31, 32, NW) “Ndege” hao wanatua katika yale mamia ya matawi ya kimadhehebu ya ule “mti.” Wanafananisha yule “mtu wa kuhalifu,” wale makasisi wa Jumuiya ya Wakristo. Watapoteza kituo chao cha ulinzi wakati Mungu atakapoukata na kuuangusha “mti” huo, pamoja na dini ile nyingine yote ya uongo. Jihadhari, sasa! Kwa maana kuanguka kwa “mti” huo kuko karibu sana!—Linganisha 2 Wathesalonike 1:6-9, UV; 2:3, NW; Mathayo 7:19-23, UV.

10, 11. (a) Mathayo na Luka wanasimulia mfano wa ile “punje ya haradali” kulingana na hali gani, na sababu gani hiyo inafaa? (b) Ule mfano wa Ufalme juu ya chachu unatupatia shauri pole na onyo gani?

10 Kwa kufaa, Luka anasimulia mfano huo wa “punje ya haradali” kufuatia lawama kali ambalo Yesu alitolea wanadini makafiri wa siku zake. Kisha Mathayo na Luka wanamwonyesha Yesu kuwa akitoa ule mfano wa “chachu” kama kwamba wanataka kukazia jambo hilo. (Mathayo 13:32, 33; Luka 13:10-21) Nyakati zote chachu ina maana isiyo nzuri inapotumiwa kama mfano katika Biblia, kama vile wakati Yesu alipoonya wanafunzi wake ‘wajilinde na chachu ya Mafarisayo na Masadukayo,’ na wakati mtume Paulo aliposhauri Wakristo waiondolee mbali ile “chachu ya uovu na ubaya.”—Mathayo 16:6, 11, 12; 1 Wakorintho 5:6-8; Wagalatia 5:7-9.

11 Katika mfano huo, sehemu fulani kuhusiana na “ufalme wa mbingu” inasemekana kuwa inafanana na chachu ambayo mwanamke anaficha katika vipimo vitatu vya unga wa ngano. Hivyo mchanganyo wote wa unga wa ngano unachachishwa. Hiyo inafananisha kule kuchafuliwa kisiri-siri kwa kundi linalodai kuwa la Kikristo kwa mafundisho na mazoea ya Kibabuloni. Matokeo yanakuwa mwundo mkubwa mno wa ufalme-bandia wa Jumuiya ya Wakristo. Hilo limepasa liwe onyo kwetu. Wakiyatazama matokeo yenye kusikitisha ya ukafiri ulio katika Jumuiya ya Wakristo, lile “kundi dogo” la warithi wa Ufalme na wenzao leo wamepaswa kujihadhari wasiruhusu kamwe “chachu” ya mafundisho ya uongo, yenye udanganyifu ichafue kuthamini kwao kwa moyo wote usafi na kweli ya lile “neno la ufalme.”

YULE MPANZI NA “ADUI” YAKE

12, 13. (a) Katika ule mfano wa “ngano” na “magugu,” Yesu alitambulishaje wale wanaotajwa katika mfano? (b) Yale mavuno ni nini, na tunaona ushuhuda gani kuonyesha kwamba yanatukia leo?

12 Katika mfano mwingine Yesu anafananisha “ufalme wa mbingu” na “mwanamume aliyepanda mbegu nzuri katika shamba lake.” Kisha, “wakati wanaume walipokuwa wamelala, adui yake akaja, akapanda kwa wingi magugu kati ya ngano, akaondoka.” Ni matunda ya aina gani ambayo yangeweza kutazamiwa kuvunwa katika shamba hilo? Yesu aliendelea kutambulisha mpanzi huyo kuwa ni yeye mwenyewe, “Mwana wa mtu,” ambaye kupandwa kwa mbegu yake ya Ufalme kunatokeza matunda ya Wakristo walio mfano wa ngano, “wana wa ufalme.” Adui ndiye “Ibilisi,” na yale “magugu” ndio “wana wa mwovu,” yaani, “mbegu” (uzao) yake ya kidini yenye unafiki. (Linganisha Mwanzo 3:15.) Katika utimizo, Wakristo fulani wa kweli waliendelea kukua miongoni mwa jamii ya “magugu” ambayo yamekuwa alama ya ukafiri mkubwa tangu karne ya kwanza. Lakini sasa katika karne yetu ya 20, tumeufikia wakati wa kuvuna—“umalizio wa mfumo wa mambo, na wale wavunaji ni malaika”!—Mathayo 13:24-30, 36-39, NW.

13 Mwishowe, chini ya mwelekezo wa kimalaika, zile “ngano” zinatenganishwa na yale “magugu.” Tofauti iliyo wazi kati ya ngano na magugu imefanywa ionekane. Kama tutakavyoona, kuna ushuhuda mwingi unaoonyesha kwamba “Mwana wa mtu” yupo leo katika ufalme wake wa kimbingu, akikusanya Wakristo wa kweli walio mfano wa ngano kwenye utendaji wa Ufalme. Lakini namna gani Jumuiya ya Wakristo na walimu wayo wa ukafiri? Mfano wa Yesu unaendelea kusema:

“Mwana wa mtu atatuma malaika zake, nao watakusanya watoe katika ufalme wake vitu vyote vyenye kukwazisha na watu wanaotenda uhalifu.”

Kwa karne nyingi makasisi wa Jumuiya ya Wakristo wamekwaza watu wanyofu kwa mafundisho yao ya uongo na kwa wonyesho wao wa utawa wa ki-nje tu. Lakini wamekuja chini ya hukumu ya Mungu, nao ‘wanalia na kusaga meno.’ Leo wanaombolezea upungufu wa msaada kutoka kwa waamini wa kawaida na mgawanyiko katika madaraja yao wenyewe. Tofauti na hivyo, watumishi wa Yehova walio mfano wa ngano wanatoa ushuhuda kwa furaha juu ya ufalme wake. Wanang’aa “kwa mng’aro kama jua katika ufalme wa Baba yao.”—Mathayo 13:40-43; linganisha Isaya 65:13, 14, NW.

MPANGO WENYE KUFANIKIWA WA ‘KUVUA SAMAKI’

14, 15. (a) Yesu alianzishaje mpango mkubwa wa ‘kuvua samaki,’ lakini ni ‘uvuvi’ wa aina zipi nyingine ambao umeendelea tangu wakati huo, na kumekuwako ‘mvuo gani wa samaki’? (b) Kisha wale malaika wanashiriki sehemu gani, na wanawawekaje wale “samaki”? (c) Kwa hiyo imetupasa tuwe wenye shukrani kwa sababu ya nafasi gani?

14 “Tena,” asema Yesu, “ufalme wa mbingu unafanana na jarife linalotelemshwa katika bahari na kukusanya samaki wa kila aina.” (Mathayo 13:47, NW) Yesu mwenyewe ndiye alianzisha mpango huo wa ‘kuvua samaki,’ wakati ule alipoita wanafunzi wake wa kwanza waache nyavu zao ili awafanye “wavuvi wa watu.” (Mathayo 4:19) Lakini wakati wa ukafiri ule mkuu, chini ya uchunguzi mkali wa malaika, vikundi vya waaminifu wachache na dini za Jumuiya ya Wakristo vimeendelea ‘kuvua’ waongofu. Walakini, je! mamia ya mamilioni yote ya viumbe wa baharini wa mfano yamekuwa ni ‘samaki wazuri’? Kama tulivyokwisha kuona, dini za Jumuiya ya Wakristo zimetegemeza mafundisho juu ya falsafa ya Kigiriki ya Plato, na juu ya “mafumbo” ya Babuloni wa kale. Matunda yao yameonekana katika zile chuki, ugomvi na umwagaji wa damu ambazo zimetia madoa historia ya kuwako kwa Jumuiya ya Wakristo, na katika kuunga kwao mkono vile vita vya karne yetu ya 20.

15 Hatimaye, “katika umalizio wa mfumo wa mambo,” ni wakati wa wale malaika kulivuta “jarife.” Hilo linafananisha matengenezo yaliyo duniani ya wale wanaodai kuwa wafuasi wa Yesu Kristo—wa kweli na wa uongo. “Samaki” hao wanaopatikana kuwa ‘wasioufaa’ “ufalme wa mbingu” lazima watupwe mbali, watupwe katika “tanuri la moto” la uharibifu. “Huko ndiko kulia kwao na kusaga meno kutakuwa.” (Mathayo 13:48-50, NW) Tunapaswa kuwa wenye shukrani kama nini kwa kuwa na nafasi ya kuhesabiwa pamoja na hao—watu walio tofauti, waliojiweka wakf kulitukuza jina la Yehova na wanaosali kwa jinsi yenye maana ufalme wake “uje”!

16. Mfano huo wa mwisho unatokeza maulizo gani, na kwa sababu gani imetupasa tupendezwe na kupata majibu?

16 Walakini, ni nini “umalizio wa mfumo wa mambo” ambao Yesu anasema kwa mkazo katika mfano wake wa mwisho? “Siku za mwisho” ambazo juu yazo wanafunzi kadha wa Yesu waliandika, ni nini? Je! sasa tunaishi katika siku hizo? Ikiwa ndivyo, zina maana gani kwetu, na kwa wanadamu wote?

[Sanduku katika ukurasa wa 104]

TII MIFANO YA YESU YA UFALME

• Hiyo inaeleza ule Ufalme kuwa wenye kutamanika, kama vile “hazina” au “lulu.” Wale wanaoutafuta wanafananishwa na “udongo wa aina nzuri,” “ngano,” “samaki wazuri.”

• Ule ufalme-bandia unafananishwa na “mti” wa haradali wenye matawi mengi, mchanganyo wa unga wa ngano uliochachishwa. Wenye kuuunga mkono ndio wale “ndege,” yale “magugu,” wale ‘samaki wasiofaa.’

• Kwa kuutazama ule usitawi wa Ufalme tukiwa kwenye pembe mbalimbali, tunaweza kufahamu vizuri zaidi lile suala kuu lililo mbele ya wanadamu leo, na tunatiwa moyo tuutetee ule Ufalme kwa uthabiti na kwa ushikamanifu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki