Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 4/1 kur. 155-164
  • Kufunuliwa Wazi kwa Kimbilio la Uongo la Ufalme

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kufunuliwa Wazi kwa Kimbilio la Uongo la Ufalme
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MHARADALI NI TOFAUTI NA TUNAVYOWEZA KUTAZAMIA
  • NAMNA GANI JUU YA VITU VILIVYOTIWA CHACHU VILIVYOTOLEWA KWA MUNGU KAMA DHABIHU?
  • Vitu Ambavyo “Ufalme wa Mbinguni” Unafanana Navyo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Hujui Ni Wapi Itafanikiwa!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Mifano ya Ufalme
    “Ufalme Wako Uje”
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 4/1 kur. 155-164

Kufunuliwa Wazi kwa Kimbilio la Uongo la Ufalme

1. Kusudi la Yesu lilikuwa nini katika kutoa mfano wa punje ya haradali, kupatana na unabii gani?

SASA, kusudi la mfano wa Yesu wa punje ya haradali ni nini, punje (mbegu) inayokuwa ndogo sana sana lakini inayositawi kuwa mti? Bila shaka kusudi ni kuonyesha jambo fulani kupatana na mtajo wa Yesu unaohusu hali mbaya inayoonyeshwa katika Isaya 6:9, 10. (Mt. 13:13-15) Alipokuwa akitoa mfano huu wa watatu katika mfululizo wa ile saba, Yesu alisema: “Ufalme wa mbinguni umefanana na punje ya haradali, aliyoitwaa mtu akaipanda katika shamba lake; nayo ni ndogo kuliko mbegu zote; lakini ikiisha kumea, huwa kubwa kuliko mboga zote, ikawa mti, hata nyuni wa angani huja na kukaa katika matawi yake.”​—Mt. 13:31.

2. Kwa kufananisha mti wa punje ya haradali na liitwalo kanisa kwa jina tu, Zion’s Watch Tower la Mei 15, 1900 lilionyesha kukaa kwa ndege wa angani kati ya Matawi ya mti huo kuwa na maana gani?

2 Toleo la Zion’s Watch Tower la tarehe ya Mei 15, 1900, ukurasa wa 153, lilisema hivi: “Mfano wa tatu wa ufalme unapokuwa mdogo sana sana katika usitawi unakusudiwa kuonyesha kwamba linaloitwa kanisa kwa jina tu la kizazi hiki cha Injili Lingekuwa kubwa sana kutoka mwanzo ndogo sana. . . . Lakini usitawi huo mkubwa haumaanishi kwa lazima jambo la faida wala cho chote chenye kutamanika sana, bali linakuwa jambo baya, kwa sababu ndege wa anga wanakuja na kukaa katika matawi yake, na kuunajisi. ‘Ndege wa anga’ katika mfano uliotangulia wa mpanzi walifananisha Shetani na mawakili wake, nasi twadhani hapa tuna haki ya kutumia mfano huo namna iyo hiyo, na kutafsiri hili kuwa linamaanisha kwamba kanisa lililoanzwa na Bwana Yesu lilisitawi haraka haraka na kuzidi sana, na kwamba kwa sababu ya mambo liliyotimiza, nguvu zake. n.k., Shetani alikuja kupitia kwa mawakili wake akakaa katika matawi mbalimbali ya Kanisa. Wamekuwa wakikaa katika matawi ya kanisa hili la Injili kwa karne nyingi hizi, nao wangali wamo ndani yake, wakiwa kitu chenye kunajisi.”

3. The Watch Tower la tarehe ya Juni 15, 1910, lilisema “mti” huo ukiwa umesitawi kabisa unafananisha nini. pamoja na ndege?

3 Likitoa maoni yanayofanana na hayo yaliyotajwa sasa hivi, toleo la The Watch Tower la Juni 15, 1910, ukurasa wa 204, liliendelea kusema hivi: “Kwa hiyo fundisho la mfano huu lingetufanya tukate shauri kwamba kanisa la Kristo, wakati mmoja, lilionwa kuwa lisilofaa kitu ulimwenguni hata ilikuwa aibu kuwa wa kanisa hilo, lakini kwamba mwishowe lingekuwa lenye kuheshimika na kubwa nao watumishi wa adui wangefurahia uvuli wake. Usitawi huu unaonyeshwa na Maandiko kuwa Babeli, yakitangaza kwamba, kwa ujumla, linaloitwa kanisa la Kristo kwa jina tu pamoja na matawi yake mbalimbali na madhehebu, ni la Kibabeli. Sikilizeni maneno ya Bwana: ‘Amekuwa ngome ya kila roho mchafu, na ngome ya kila ndege mchafu mwenye kuchukiza.’”​—Tazama pia The Watch Tower la Juni 15, 1912, ukurasa wa 198, chini ya kichwa “Kama Punje ya Haradali.”

4. (a) Makala mbili hizo za Watch Tower hazikusema “mti” wa mfano ulikuwa nini? (b) Kwa habari ya wakati na mahali, ni hali ya namna gani isiyoonyeshwa na mfano wa punje ya haradali?

4 Sasa tumo katika mwaka huu wa 1976, nalo ulizo kubwa ni, Mti huo uliokua wa punje ya haradali unafananisha nini? Yale matoleo mawili yaliyokwisha tajwa ya gazeti Watch Tower yanasema ni Babeli Mkuu. Hayasemi kwamba mti huo wa mboga unafananisha jamii ya Ufalme ya Wakristo 144,001 waliotawazwa katika mamlaka ya kimbinguni. Lakini sisi watu wa leo tusemeje? Kwanza, lazima tukumbuke mfano huu wa punje ya haradali hauonyeshi hali itakayokuwako wakati wa mileani, kuonyesha hesabu ya mwisho ya jamii ya Ufalme wakitawala kwa utukufu wa kimbinguni na wanadamu wote wakiwa wamekimbilia ufalme huu wa Kimasihi. Hauonyeshi hali ya kimbinguni kwa habari ya warithi wa “ufalme wa mbinguni.” Unaonyesha hali ya kidunia ya mambo katika kipindi fulani.

5. Mfano unafikia upeo wa utimizo wake katika kipindi gani cha pekee, nao utimizo huo unatukia wapi?

5 Kipindi hicho cha pekee ni kile kilichoonyeshwa na Yesu katika mifano ya ngano na magugu na juya. Katika mfano wa konde la ngano lililopandwa magugu pote, Yesu alisema hivi: “Mavuno ni mwisho wa dunia; na wale wavunao ni malaika.” Katika mfano wa juya, Yesu alisema: “Ndivyo itakavyokuwa katika mwisho wa dunia; malaika watatokea, watawatenga waovu mbali na wenye haki, na kuwatupa katika tanuru ya moto; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno.” (Mt. 13:39, 49, 50) “Mavuno” yanafanywa hapa duniani, ambapo ndipo penye “magugu” yanayopaswa kuchaguliwa na kuondolewa. Vivyo hivyo, kutenganisha “samaki” wanaofaa na wasiofaa kunafanywa hapa duniani, ambapo ndipo penye ‘maji’ ya kuvulia. “Magugu” ya mfano na “samaki” wasiofaa ni Wakristo wa kujidai ambao mioyo yao haiitikii, ambao masikio yao hayasikilizi, na ambayo macho yao yametiwa kibandiko yote pamoja hata isiwezekane Wakristo hao wa kujidai waponywe kiroho.​—Isa. 6:9, 10; Mt. 13:14. Linganisha Matendo 28:25-28. Tazama makala “Hakuna Kuponywa Mpaka Nyumba Ziwe Hazina Mwanadamu,” katika toleo la Watchtower la Desemba 15, 1966.

6. “Mti” huo wa mboga wa leo unajidai kuwa nini, na hivyo ni kwa sababu gani “mti” huo wa mfano usingeweza kuwa Babeli Mkuu?

6 Wakati wa “mwisho wa dunia” [mwisho wa taratibu ya mambo, NW] bila shaka mti wa mfano wa punje ya haradali umekua kabisa. Hali hiyo ya ukuzi ingelingana na wakati wa mavuno. Kwa kuwa mavuno ya “ngano” ya kiroho au “wana wa ufalme” yamekuwa yakiendelea tangu mwaka wa 1919 W.K., tunaweza kuuona mti wa mfano wa punje ya haradali sasa ukiwa umekua kabisa hapa duniani. Mti huu wa mboga unajidai kuwakilisha “ufalme wa mbinguni,” kwa maana Yesu alisema kwamba “ufalme wa mbinguni umefanana” nao. Kwa hiyo mti wa punje ya haradali usingeweza kufananisha Babeli Mkuu, kwa maana tengenezo hilo ndiyo milki ya ulimwengu ya dini ya uongo iliyoanzia Babeli ya kale. Babeli Mkuu kwa ujumla haijidai kuwa “ufalme wa mbinguni” wala “ufalme wa Mungu” wa Kimasihi wala haijidai kuuwakilisha. Walakini, sehemu iliyo na watu wengi zaidi na iliyo kubwa zaidi ya Babeli Mkuu inajidai kuwakilisha ufalme wa Mungu wa Kimasihi wa kimbinguni. Sehemu hiyo yenye nguvu zaidi ya Babeli Mkuu ni Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu), pamoja na matawi yake na madhehebu elfu moja au zaidi za kidini.

7. Ukuzi mkubwa zaidi katika historia wa Jumuiya ya Wakristo umesababishwa na nini, na jumuiya hiyo ilianza wakati gani hasa na kwa njia gani?

7 Jumuiya ya Wakristo inajidai ilitokana na kikundi cha kwanza cha Kikristo katika Yerusalemu wakati wa karne ya kwanza W.K. Leo makundi ya Jumuiya ya Wakristo ni mamilioni. Imefikia ukuzi wake mkubwa kupita wote! Lakini hali yake ya kilimwengu yenye aibu na ukosefu wa hali ya kiroho leo inahakikisha kwamba ukuzi wake mkubwa sana haukuletwa na sifa za kiroho wala kwa sababu ya kuwa kwake na nuru yenye kuendelea ya kweli ya Biblia. Historia ya kidini inaonyesha kwamba kwa kweli Jumuiya ya Wakristo ilianzishwa karne ya nne W.K. na mfalme wa kipagani wa Kirumi Konstantino Mkuu, aliyedai aliongolewa akaingia katika Ukristo mwaka wa 312 W.K lakini aliyekaa bila kubatizwa mpaka muda mfupi kabla ya kufa kwake Mei 22, 337 W. K. Yeye aliufanya Ukristo uliopotoshwa wa siku zake kuwa Kanisa la Serikali la Milki ya Kirumi, akatumia “maaskofu” karibu 300 wenye kuasi imani kufanya hivyo. Akiwa ndiye Askofu Mkuu wa Milki ya Kirumi, aliomba baraza ya kwanza ya Nikaea, Asia Ndogo, wakutane naye akakubali mafundisho ambayo baraza hiyo iliamuru kuwa ni mafundisho ya Kanisa.

8. Ni mafundisho na mazoea gani yameenea katika Jumuiya ya Wakristo leo, na kwa utimizo wa mfano gani?

8 Leo, ni nini kimeenea katika makanisa yote ya Jumuiya ya Wakristo? Je! ni mafundisho ya kweli ya Biblia na ufuataji wa utaratibu wake? Sivyo! Ni dini ya mchanganyiko ambayo Askofu Mkuu Konstantino aliendeleza, ambamo mafundisho ya Kibabeli na taratibu zake ndiyo mambo ya msingi badala ya mafundisho ya Neno Takatifu lililoongozwa na Mungu. Konstantino ndiye aliyemaliza ubishi juu ya utu na sifa za Yehova Mungu akiwa afisa-msimamizi wa Baraza ya Nikaea kwa kupendelea fundisho la Kibabeli la Utatu. Yesu Kristo alisema mapema kwa unabii juu ya utaratibu huu wa kupotoa fundisho na mazoea ya Kikristo kwa kutoa mfano wa chachu. Alisema: “Ufalme wa mbinguni umefanana na chachu aliyoitwaa mwanamke, akaisitiri ndani ya pishi tatu za unga, hata ukachachwa wote pia.”​—Mt. 13:33.

9. Maongozi hayo yenye kupotoa kidini yamekuwa yakiendelea katika Jumuiya ya Wakristo kwa muda gani, nao mawakili wa Ibilisi wamepata nafasi gani?

9 Kuchachwa kwa jamii nzima ya Jumuiya ya Wakristo sasa kumekuwa na karne kumi na sita. Ni nani awezaye kukana kwamba Jumuiya ya Wakristo haikutiwa chachu kabisa leo na maongozi yenye kupotoa ya mafundisho ya Kibabeli na hali ya kilimwengu na ukaidi wa kiNimrodi wa enzi kuu ya Yehova Mungu ya ulimwengu wote? Kupotolewa huko kwa jamii kubwa sana ya “wana wa ufalme” wa kujifanya wa Jumuiya ya Wakristo kumeufanya “ufalme wa Mungu” wa uongo wa kidunia uwe mahali bora pa kukimbiliwa na mawakili wa Shetani Ibilisi, kama “nyuni wa angani” wenye kukaa katikati ya matawi yaliyokua kabisa ya mti wa punje ya haradali.​—Mt. 13:31, 32.

10, 11. (a) Kwa sababu gani hakuna jambo la faida kwa wanadamu linaloonyeshwa katika mfano wa punje ya haradali? (b) Kwa hiyo, ni “ufalme” gani leo unaofananishwa na “mti” wa punje ya haradali?

10 Kukaa kwa “nyuni wa angani” hao wote wa mfano katika matawi mengi ya Jumuiya ya Wakristo hakukuletea Jumuiya ya Wakristo faida ya kiroho. Ni sawa na mti uliokua kutoka punje ya haradali aliyopanda mkulima katika shamba lake. Ndege wa angani waliokaa katika matawi yake waliweza kuzila punje (mbegu) za haradali, sawa na ndege wa mfano wa Yesu wa udongo wa aina nne waliozila kabisa mbegu zilizoanguka kutoka mkononi mwa mpanzi zikawa kando ya njia. (Mt. 13:4) Kulingana na mfano wa Yesu, mti huo haukufaidi wanadamu. Kwa mfano, mfano huo hauelezi vile mpanzi alivyokuja akawafukuza ndege hao mti ulipokua kabisa na kukusanya punje nyingi za haradali za kufanyizia mchuzi mzuri wa kukolezea vyakula fulani. Lakini, bila shaka mkulima hakuipanda punje ya haradali shambani pake ndiyo awape “nyuni wa angani” makao.

11 Mambo yote yakiisha kufikiriwa, ni wazi kwamba “mti” wa mfano wa punje ya haradali wa leo ndio “ufalme wa mbinguni” wa uongo, yaani, Jumuiya ya Wakristo, pamoja na mapadre wake wenye kupiga ubwana juu ya watu wa kawaida. “Mti” uliokua kabisa usingeweza kufananisha mabaki yaliyoko duniani leo ya Waisraeli wa kiroho waliotiwa mafuta, kwa maana wao ni kisehemu kidogo tu, si warithi kamili wa Ufalme 144,000. Kwa kweli, kwa zaidi ya miaka 27 mabaki ya kiroho wamekuwa wakipungua hesabu zao. Katika mwadhimisho wa Ukumbusho wa 1975 hesabu yao ilikuwa imeshuka kufikia 10,454.

MHARADALI NI TOFAUTI NA TUNAVYOWEZA KUTAZAMIA

12. Juu ya msingi wa sheria ya Biblia inayosema kwamba lazima mbegu izae kwa jinsi yake, huenda mtu kwa kufaa akatokeza ubishi gani juu ya maelezo ya kwamba mharadali unafananisha Jumuiya ya Wakristo?

12 Kwa kufaa sana, huenda mtu akabisha juu ya yaliyotangulia kwa kusema hivi: Katika mfano wa Yesu, mtu aliyepanda punje ya haradali alifanya hivyo akiwa na makusudi mema. Yeye alitazamia mharadali ukue kutokana na punje hiyo “kwa jinsi yake.” (Mwa. 1:11, 12) Yeye hakutazamia kitu tofauti na alichopanda. Hakufikiria mharadali wa uongo. Kwa kuwa ndivyo, tunawezaje kusema kwamba mpanzi alipata kitu icho hicho cha uongo? Kwa hiyo, tunawezaje kusema kwamba “mti” uliokua kutokana na punje ya haradali ulifananisha Jumuiya ya Wakristo, “ufalme wa mbinguni” wa uongo?a Je! hicho si kinyume cha sheria ya Mungu inayosema kwamba lazima mbegu izae kwa jinsi yake yenyewe? Sheria hiyo ya kimungu ikitumiwa kwa njia ya kiroho, isingeondoa wazo la kwamba Jumuiya ya Wakristo, kinyume cha “ufalme wa mbinguni,” ndiyo inayofananishwa na mti huo?

13, 14. (a) Kwa sababu gani kusingalikuwa na Jumuiya ya Wakristo kama Yesu Kristo asingalikuwako? (b) Ni kulingana na kanuni gani Mungu ataiona jumuiya hiyo kuwa yenye lawama Kwake, nayo ni mfano wa uongo wa nini?

13 Katika habari hii, Yesu Kristo ndiye aliyeanza mambo. Kama kusingalikuwa na Kristo, kusingaliwa na Jumuiya ya Wakristo. Huo ni usemi mwepesi, lakini ni wa kweli. Katika kame ya nne ya Wakati wetu wa Kawaida Jumuiya ya Wakristo ilijishikamanisha na Kristo wa kweli, si Kristo wa uongo, Masihi wa uongo, kufanya isiwezekane kutambuliwa kuwa ya uongo. Hata ilichukua cheo chake rasmi kwa kujiita Kristendomu (Jumuiya ya Wakristo). Imejipa mambo mbalimbali yanayohusiana na Yesu Kristo. Inafanya ubatizo katika maji, hata leo mengine ya makanisa yake yanazamisha kabisa katika maji. Inaadhimisha Kijio cha Bwana kwa kutumia mkate na mzao wa mzabibu. Inayo wazee au maaskofu na mashemasi. (Flp. 1:1, Authorized Version) Na kwa habari ya Biblia Takatifu kwa ujumla, Biblia zile zile ambazo mashahidi wa Kikristo wa Yehova wametumia mpaka mwanzo wa kuchapwa kwa New World Translation of the Holy Scriptures mwaka wa 1950 W. K. zimetujia kutoka kwa mashirika ya Biblia ambayo makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yameendesha.

14 Ni wazi kwamba Yesu Kristo anashirikishwa na kuanzishwa kwa Jumuiya ya Wakristo, ambayo mpaka sasa imejidai kuwa Kanisa lake la kweli. Tena, Yehova Mungu anaichukua Jumuiya ya Wakristo kulingana na inavyojidai kuwa. Kwa hiyo Yehova anaitaka iishi kulingana na madai yake naye anailaumu kwa kukosa kuishi kupatana na matakwa yake. Kwa sababu hiyo atailetea adhabu ya wakati wake. Katika huu “mwisho wa taratibu ya mambo” anaihukumu kuwa isiyoaminika kwa madai yake ya kidini. Hiyo ni mfano wa uongo wa Israeli wasioaminika wa nyakati za kale.

15, 16. Mfano wa Yesu wa ngano na magugu unaonyeshaje yeye anashirikishwa na ukuzi wa Jumuiya ya Wakristo mpaka sasa?

15 Unaoongeza uhakika wa Maandiko kwamba Yesu Kristo anashirikishwa na ukuzi wa Jumuiya ya Wakristo ni mfano wa ngano na magugu (kwekwe). Ni kweli, Yesu Kristo, “Mwana wa Adamu,” hakuyapanda magugu hayo katika shamba lake mwenyewe. Adui yake, Shetani Ibilisi, ndiye aliyefanya hivyo. Katika mfano, watumwa wa Mpanzi waligundua haraka kwamba magugu yalikuwamo katika shamba la ngano. Walitaka kuyang’oa machipukizi ya magugu. Lakini Mpanzi, mwenye shamba la ngano, akawakataza. Kwa saburi na ustahimilivu aliwaagiza watumwa wayaache magugu na ngano pia zikue pamoja mpaka wakati wa mavuno yaliyokuwa karibu na wakati wa Pentekoste. Ndipo kwanza angeagiza magugu, ambayo sasa yalikuwa yamekua kabisa, yatenganishwe na ngano.

16 Katika utimizo wa sehemu hii ya mfano, Yesu hakuagiza Jumuiya ya Wakristo iangamizwe mara tu ilipojitokeza. Aliiruhusu ipanuke. Katika maana hiyo yeye anahusika na ukuzi wa Jumuiya ya Wakristo kufikia ukubwa wake wa sasa, ambao ndio mkubwa zaidi katika historia. Hata wakati wa kuandika habari hii, Yesu Kristo hajaiangamiza Jumuiya ya Wakristo. Kwa ruhusa yake, ingali katika shamba la Mpanzi, “konde lake,” ‘shamba lake la kidini lenye kulimwa.’​—Mt. 13:24-27; linganisha 1 Wakorintho 3:9, NW.

17. “Juya” la mfano limetumiwa na nani, na katika mwaka wa 1891 na 1912, “juya” hilo lilisemwa kuwa linafananisha nini?

17 Unaozidi kuonyesha vile Yesu anavyoshirikishwa na ukuzi wa Jumuiya ya Wakristo ni mfano wa juya. (Mt. 13:47-50) Wavuvi wanaotumia juya hilo wanafananisha malaika wa kimbinguni wakiwa chini ya uongozi wa Yesu Kristo aliyetukuzwa. Lakini juya lenyewe linafananisha nini? Kwa sababu mfano unasema kwamba “ufalme wa mbinguni umefanana na juya,” je! juya hilo linawafananisha washiriki 144,001 wa jamii ya “ufalme wa mbinguni”? Sivyo, lisingeweza kuwafananisha wao, tunapofikiria sehemu zote za mfano pamoja. Kitabu “Thy Kingdom Come,” kilichochapwa mwaka wa 1891, kilisema katika ukurasa wa 214 kwamba juya lilifanisha “liitwalo Kanisa la Kikristo kwa jina tu.” The Watch Tower la tarehe ya Juni 15, 1912, katika ukurasa wake wa 201 na chini ya kichwa “Mfano wa Wavu wa Samaki,” liliusema kuwa “wavu wa Injili, wenye mkusanyo kamili wa kila namna.”

18. The Watchtower la tarehe ya Novemba 15. 1967 lilisema juya linafananisha nini?

18 Karibuni zaidi, katika toleo la Watchtower la Novemba 15, 1967, ilitokea makala ya funzo yenye kichwa “Mkashushe Nyavu Zenu Mvue Samaki.” Katika ukurasa 686, ukurasa wa sita unasema kwamba “juya linafananisha tengenezo la kidunia linalojidai kuwa kundi la Mungu lililomo katika agano jipya na Mungu kupitia kwa Mpatanishi Yesu Kristo. Kwa hiyo linajidai kuwa Israeli wa kiroho, taifa takatifu lililotiwa mafuta kwa roho ya Mungu litakalotawala na Yesu Kristo katika ufalme wa kimbinguni. Linatia ndani wenye kujidai kwa kweli na wenye kujidai kwa uongo au wasioaminika. Kwa kufaa linatia ndani Jumuiya ya Wakristo, pamoja na Wakristo wake wa kujidai walio mamia ya maelfu, walio wa madhehebu mamia yanayoitwa ya Kikristo.”

19, 20. (a) Uhusiano wa Yesu na punje ya haradali ya mfano umekuwa kama uhusiano gani wa Yehova, kama unavyoonyeshwa katika Yeremia 2:21-23? (b) Katika Hosea 10:1-4. Yehova alifananishaje kuharibika kwa Israeli na “mzabibu”?

19 Hivyo katika mifano ya Ufalme Yesu Kristo alionyesha kushirikishwa kwake na ukuzi wa liitwalo tengenezo la Kikristo kwa jina tu au Jumuiya ya Wakristo. Uhusiano wake na Jumuiya ya Wakristo ni kama uhusiano wa Baba yake wa kimbinguni Yehova na Israeli wa nyakati za kale wenye kuasi imani. Kusudi la Yehova katika kuanzisha taifa la Israeli huko nyuma mwaka wa 1513 K. W. K. lilikuwa jema na lenye haki. Lakini kulitukia nini kwa taifa hilo alilokuwa amelichagua na kuliweka imara katika Nchi ya Ahadi katika Palestina? Yehova mwenyewe anajibu ulizo hilo katika Yeremia 2:21-23. Humo anasema hivi: “Nami nalikuwa nimekupanda, mzabibu mwema sana, mbegu nzuri kabisa; umegeukaje, basi, kuwa mche usiofaa wa mzabibu-mwitu machoni pangu? Maana ujapojiosha kwa magadi, na kujipatia sabuni nyingi lakini uovu wako umeandikwa mbele zangu, asema Bwana [Yehova]. Wawezaje kusema, Sikutiwa unajisi, sikuwafuata Mabaali? itazame njia yako bondeni, ujue uliyoyatenda; wewe u ngamia [wa kike] mwepesi, [mwenye kukimbia-kimbia kule na huku bila kusudi katika njia zake].”

20 Pia, katika Hosea 10:1-4, Yehova anasema hivi: “Israeli ni mzabibu wenye kuharibika utoao matunda yake; kwa kadiri ya wingi wa matunda yake, kwa kadiri iyo hiyo ameongeza madhabahu zake; kwa kadiri ya wema wa nchi yake kwa kadiri iyo hiyo wamefanya nguzo nzuri. Moyo wao umegawanyika; sasa wataonekana kuwa na hatia. . . . Hunena maneno yasiyo na maana; huapa kwa uongo wafanyapo maagano; basi ndipo hukumu huchipuka kama mbaruti katika matuta ya shamba.”

21. (a) Kizazi cha Kiyahudi cha siku za Yesu kilionyeshaje kuasi kwake imani? (b) Ni mambo yaliyompata nani yanayojibu ulizo la kama Yesu angeweza kupanda punje ya haradali ya mfano kisha mmea tofauti ukue?

21 Katika siku za Yesu Kristo na mitume wake taifa la Israeli lilikuwa limeasi imani sawa na ilivyokuwa katika siku za Yeremia na Hosea. Kwa kweli, kizazi cha Israeli ndicho kilichomfisha Yesu Masihi na ndicho kilichotesa mitume wake na wanafunzi wa karne ya kwanza. Waisraeli hao hasa ndio ambao Yesu, vilevile Isaya, aliwataja kuwa wenye macho yaliyofumbwa kabisa, wenye masikio yasiyosikiliza na mioyo isiyoitikia wasiweze kuponywa kiroho. (Isa. 6:9, 10; Mt. 13:13-15; Matendo 28:24-28) Kwa hiyo kizazi hicho chenye kuasi imani kilipatwa na msiba wa taifa zima mwaka wa 70 W. K. Kwa hiyo, sasa, je! kuna ye yote anayeuliza ulizo, Yesu angewezaje kupanda punje ya mfano ya haradali akiwa ndiye Mpanzi wa mfano na bado aiache iwe mti wa jinsi tofauti, mfano mpotovu wa uongo unaoitwa Jumuiya ya Wakristo? Yaliyotukia kati ya Yehova Mungu na taifa la kale la Israeli yanatoa jibu la kimungu kwa ulizo hilo!

22. Kwa sababu gani Yesu angeweza kusimulia mfano wa punje ya haradali akifikiria kwamba “mti” uliokua kabisa ungefananisha tengenezo la uongo?

22 Yesu Kristo, akiwa na maono yake ya mbele ya kinabii, angeweza kujua matokeo ya punje ya mfano ya haradali aliyoipanda katika kame ya kwanza. Aliifahamu historia ya Israeli na aliujua unabii wote. Kwa hiyo angeweza kusimulia mfano wa punje ya haradali na kumaanisha “ufalme wa mbinguni” wa uongo, Jumuiya ya Wakristo, kwamba ndiyo iliyofananishwa na mharadali uliokua kabisa ambamo “nyuni wa angani” walikaa.​—Angalia Mathayo 13:25, 38, 39; 24:23-25.

23. (a) Haitupasi kukata shauri gani kutoka na kukosa kwa mfano kuonyesha uharibifu wa “mti” punje ya haradali? (b) Mfano wa juya hauonyeshi nini juu ya wavu huo wa kuvulia samaki?

23 Mfano wa Yesu wenyewe haukuonyesha kwamba kitu kilichofananishwa na “mti” wenye kuingiliwa na ndege kingeharibiwa. Lakini hiyo si sababu ya kuonyesha kwamba uharibifu huo hautaujia “mti” wa mfano, yaani, Jumuiya ya Wakristo. (Linganisha Luka 13:5-9.) Ndivyo inavyoweza kusemwa juu ya juya: Mfano wa Yesu hauonyeshi kwamba juya lingetoweka. Lakini mfano hata hauonyeshi kwamba juya lilitumiwa tena. Kama lingalitumiwa tena, lingalivua tena kutoka ‘baharini’ mchanganyiko ule ule wa viumbe vya baharini kama ilivyoonyeshwa katika mfano. Kwa hiyo, kwa sababu mfano hauelezi juya liliharibiwa, hiyo haimaanishi kwamba kinachofananishwa na juya hilo hakitaharibiwa katika wakati wake Mungu. Kazi zenye kuongozwa na malaika zimeendeshwa kwa kutumia juya hilo la mfano karne kumi na tisa zilizopita. Lakini, wakati kazi ya kutenganisha viumbe vya baharini vilivyonaswa na juya hilo la mfano itakapokwisha, kazi hiyo ya kuvua haitarudiwa.

24. Kwa sababu gani juya la mfano litaharibiwa mbali katika wakati wake Mungu, ingawa jambo hilo halikuonyeshwa katika mfano?

24 Kwa kuwa juya lilifananisha “liitwalo Kanisa la Kikristo kwa jina tu” au ‘tengenezo la Wakristo wa kujidai, kutia na wa kweli na wa uongo,’ kwa kweli juya la mfano litaharibiwa mbali. Chombo hicho cha kidini kinachotia ndani Jumuiya ya Wakristo kitatupiliwa mbali kisitumiwe tena. Mwishoni mwa “mwisho wa taratibu ya mambo” Yehova atakuwa amekwisha pata “samaki” wake wote wema kwa ajili ya “ufalme wa mbinguni” wa kweli. (Mt. 4:17; 13:47-50) Kwa hiyo kutoonyeshwa kwa jambo hilo katika mfano hakuhakikishi kwamba juya la mfano halitatimiza kusudi lake na kuharibiwa mbali, kuwekwa mbali, lisitumiwe tena kamwe. Hata hivyo Yesu alisema kwamba “ufalme wa mbinguni” ni kama juya hilo. Kwa hakika, basi, juya lenyewe halikufananisha jamii ya Ufalme ya washiriki 144,001.

NAMNA GANI JUU YA VITU VILIVYOTIWA CHACHU VILIVYOTOLEWA KWA MUNGU KAMA DHABIHU?

25. Ingawa liitwalo tengenezo la Kikristo kwa jina tu limechachishwa kwa mambo ya Kibabeli, huenda bado mtu akawa na ulizo gani juu ya chachu iliyofichwa katika kinyunga na mwanamke, na kwa sababu gani?

25 Hakuna shaka juu ya kama liitwalo tengenezo la Kikristo kwa jina tu, lililofananishwa na “mti” wa punje ya haradali ulioingiliwa na ndege limechafuliwa na mafundisho na mazoea ya Kibabeli. Katika mazungumzo yaliyotangulia ilionyeshwa kwamba kuchafuliwa huku kwa tengenezo la Kikristo la kujidai kulifananishwa katika mfano wa Yesu ambamo mwanamke alificha chachu kidogo katika pishi kubwa tatu za Unga, ili kuchachisha unga wote. (Mt. 13:33) Na bado huenda mtu akaona ugumu kuelewa maelezo hayo ya mfano huo. Huenda akajiuliza, Je! chachu katika mfano huo kwa kweli inafananisha kitu kibaya, chenye kuchafua dini? Je! haiwezi kuwa inafananisha uwezo unaoenea katika kundi la kweli la Kikristo la warithi wa Ufalme pamoja na haki, utakatifu? Ala! vitazame vitu vilivyotolewa kwa Yehova Mungu kama dhabihu kulingana na sheria ya Musa vilivvokuwa na chachu Naye akavikubali! Je! hiyo haionyeshi kwamba Maandiko Matakatifu yanatumia chachu kama mfano wa wema na haki? Je! haiwezi kuwa ivyo hivyo pia katika mfano wa Yesu wa chachu iliyotiwa ndani ya fungu la kinyunga?

26. Huenda mwenye kuuliza akawazaje juu ya chachushwa na mikate miwili ile ya ngano ya wakati wa Pentekoste?

26 Mfano unaojulikana sana unaoweza kutajwa, wa ambapo vitu vilivyotiwa chachu vilitolewa kwa Yehova kama dhabihu chini ya amri yake na kwa kukubaliwa naye, ni mikate miwili ile ya ngano iliyotiwa chachu ambayo kuhani mkuu wa Kiyahudi alitoa katika Sikukuu ya Juma, au Pentekoste, ambayo ilikuwa siku ya kumi na sita ya mwezi mfupi wa Sivani wa wakati wa masika. Hiyo ilikuwa siku ya 50 kutoka Nisani 16, wakati ambao kuhani mkuu alitoa malimbuko ya mavuno ya shayiri. (Law. 23:15-17; Kum. 16:9-12; Matendo 20:16; 1 Kor. 16:8) Kwa sababu ya heshima yote iliyopewa kwa mikate miwili hiyo, huenda mtu akawaza hivi: Katika sikukuu hiyo Yehova aliikubali mikate miwili ya ngano yenye chachu. Basi, je! ukubali wa Yehova wakati huo wa kitu kilichotiwa chachu hauonyeshi kwamba chachu ina maana njema? Je! hiyo haihakikishi kwamba nyakati nyingine chachu inakuwa na wema wa mfano machoni pa Mungu? Ala! tazama vile mkate uliotiwa chachu ulivyokuwa mkate wenye kupendwa zaidi na watu wa kale aliowachagua Yehova, na hali mkate usiotiwa chachu uliitwa ‘mkate wa mateso.’ (Kum. 16:1-3) Bila shaka hiyo inaonyesha chachu ni nzuri inapotumiwa kama mfano katika Biblia!

27. Tukiwaza kwa njia hiyo tunafikia azimio gani juu ya maana ya chachu iliyokuwamo katika kilichofananishwa na mikate miwili ile ya ngano ya wakati wa Pentekoste?

27 Tukiwaza kwa njia hiyo kuhusu mikate ile miwili iliyotiwa chachu iliyotolewa katika sikukuu ya Juma, tunaona nini? Hivi: Mikate miwili hiyo ya Pentekoste ilikuwa mfano, ikifananisha mambo yatakayokuja kulingana na kusudi la Mungu. Kwa hiyo katika kutolewa kwa mikate miwili iliyotiwa chachu siku ya Sivani 6, kitu kilichofananishwa na chachu katika mikate lazima kiwe kitu chema, chenye haki, safi. Kwa hiyo tunauliza, Mikate miwili hiyo ya ngano iliyotiwa chachu yafananisha nini yenyewe? Inafananisha kundi la kweli la Kikristo lenye waamini wa kibinadamu wasiokamilika lililotokea siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W. K. (Zion’s Watch Tower la Machi 1, 1898, ukurasa 68, fungu 4) Kwa hiyo sasa, ikiwa siku ya Pentekoste chachu ilifananisha kitu chema, basi kwa kupatana kundi jipya la Kikristo linaonyeshwa kama likianza likiwa na chachu iliyofananishwa ya wema ndani yake lenyewe, “neema ya roho takatifu” ya pekee. Nayo yote hayo yalikuwa kabla ya kumiminwa kwa roho takatifu!

28. Walakini, kupatana na The Watch Tower, chachu iliyokuwamo katika mikate halisi ya ngano ya wakati wa Pentekoste ilifananisha nini?

28 Walakini, je! washiriki wa kibinadamu wa kundi la Kikristo walianza wakiwa na ustahili fulani ndani yao wenyewe katika siku ya Pentekoste ilipomiminwa roho takatifu ya Mungu juu yao? Sivyo; hawakuwa na haki yao wenyewe. Kwa hiyo, chachu iliyokuwamo ndani ya toleo la malimbuko ya mavuno ya ngano imeelezwa kwa muda mrefu kuwa inamaanisha dhambi, dhambi ambayo washiriki wa kundi la Kikristo la warithi-washirika wa Ufalme walirithi kutoka kwa Adamu asiyetii. (Rum. 5:12; tazama The Watch Tower la Juni 15, 1912, ukurasa wa 198, fungu la pili chini ya kichwa “Mfano wa Chachu.”) Walakini, huko nyuma siku ya Pentekoste, 33 W. K., kwa washiriki wasiokamilika wa kundi la Kikristo ikawa kweli kwamba “damu yake Yesu, Mwana wake, yatusafisha dhambi yote.”​—1 Yohana 1:7; tazama ukurasa wa 229, fungu la 1, mpaka ukurasa wa 231 wa kitabu The Temple, cha Alfred Edersheim, chapa ya mwaka wa 1881.b

29. (a) Siku ya Pentekoste inaunganishwa na siku gani ya kutoa malimbuko, na kwa njia gani? (b)Namna gani juu ya chachu kuhusu siku hiyo iliyotangulia ya kutoa malimbuko ya mavuno?

29 Maelezo hayo juu ya chachu iliyokuwamo katika mikate miwili ile ya ngano ya Pentekoste yanaungwa mkono na uhakika mwingine. Ndio huu: Pentekoste, sikukuu ya Juma (Shabuoth), inaunganishwa pamoja na siku ya kutoa malimbuko ya mavuno ya shayiri na hesabu ya wakati. Toleo hilo lilifanywa Nisani 16, siku ya tatu kutoka sikukuu ya Kupitwa. (Law. 23:9-17) Nisani 16 wakati kuhani mkuu alipopunga-punga “mganda wa malimbuko ya mavuno” ya Israeli ya shayiri, hakuna chachu iliyotolewa pamoja nayo kama dhabihu. Sehemu mbili za kumi za efa za unga mwembamba uliochanganywa na mafuta zilitolewa pamoja na robo ya hini ya divai, lakini bila chachu. (Law. 23:13) Kwa kweli, sherehe hiyo ilitukia wakati wa sikukuu ya siku saba ya mkate usiotiwa chachu, na wakati huo wote chachu yo yote haikupaswa kuwa karibu wala kuliwa, Sasa, sababu gani chachu haikuwako katika sherehe hiyo Nisani 16 ijapokuwa chachu ilikuwako katika sikukuu ya Pentekoste iliyohusiana na hii?

30. (a) Ikiwa chachu ilikuwa mfano wa kitu chenye haki. basi kutokuwako kwayo siku ya kutoa malimbuko ya shayiri kungeonyesha nini? (b) Mganda wa malimbuko ya mavuno ya shayiri ulifananisha nini?

30 Ikiwa chachu itachukuliwa kama mfano wenye kufaa kwa sababu Mungu aliikubali siku ya Pentekoste, sababu gani haikuruhusiwa kuwamo katika matoleo yaliyotolewa pamoja na kupungwa-pungwa kwa mganda wa malimbuko ya mavuno ya shayiri? Ikiwa chachu ni mfano wa kitu chema, basi je! kutokuwako kwa chachu kusingeonyesha kwamba kitu fulani chema kilikuwa kimekosekana wakati wa tolewa kwa mganda wa shayiri na kuhani mkuu? Naam, kungeonyesha kwamba katika utimizo wa mfano huu wa unabii wema fulani au “neema ya roho takatifu” ingekuwa imekosekana. Lakini je! ndivyo ilivyo hasa? Ili tupate jibu lazima tufikirie kilichofananishwa na mganda wa malimbuko ya mavuno ya shayiri. Aliyefanalishwa si mwingine ila Bwana Yesu Kristo mwenyewe aliyefufuliwa,​—1 Kor. 15:20.

31. (a) Yesu alifufuliwa siku gani na sababu gani wakati huo? (b) Kutokuruhusiwa kwa chachu siku hiyo katika Israeli kulifananisha nini juu ya ufufuo wa Kristo?

31 Kupatana na uhakika huo, Yesu Kristo alifufuliwa kwa wafu Jumapili, Nisani 16, 33 W.K., katikati ya sikukuu ya juma moja ya mkate au keki zisizotiwa chachu. Bila shaka hakuwa amekosa kitu fulani chema wakati wa ufufuo wake mtukufu, hakuwa amekosa wema fulani wala “neema ya roho takatifu,” kama ambavyo ingeonyeshwa kama chachu iliyokosekana ingechukuliwa kama mfano wa kitu chema, inayoitwa ‘chachu ya haki.’ Kwa kinyume kabisa, kutokuwapo kwa chachu Nisani 16 wakati wa kupungwa-pungwa kwa mganda wa malimbuko ya mavuno ya shayiri kulionyesha kwamba Yesu Kristo alifufuliwa akiwa mtu mkamilifu wa kiroho, mwenye haki na asiye na dhambi. Kama 1 Timotheo 3:16 (NW) inavyosema. wakati wa ufufuo wake ‘alitangazwa kuwa haki katika roho.’ Hakukuwa na “chachu” ya mfano iliyomhusu yeye.

32. (a) Yesu alisema nini juu ya mkate alioumega aliyekuwa akianzisha Kijio cha Bwana? (b) Kwa hiyo kutokuwamo kwa chachu katika mkate huo kulifananishwa nini?

32 Uhakika huu unahusiana na hilo: Nisani 16, siku ambayo malimbuko ya mavuno ya shayiri yalitolewa kwa Yehova Mungu, ilikuwa siku ya tatu kutoka sikukuu ya Kupitwa. Baada ya Yesu Kristo kuadhimisha kijio cha Kupitwa Nisani 14, 33 W. K., alichukua mkate usiotiwa chachu akaumega akawaambia mitume wake waaminifu hivi: “Twaeni, mle; huu ndio mwili wangu.” (Mt. 26:26) Tukichukua kwamba chachu inafananisha kitu chema, kwa kuwa hakukuwa na chachu katika mkate uliotumiwa, je! hiyo inamaanisha kwamba mwili wa Yesu ulikosa kitu cha maana, ulikosa haki, ulikosa “neema ya roho takatifu”? Hata! Kutokuwamo kwa chachu katika mkate ambao Yesu alisema ulifananisha mwili wake kulionyesha kwamba mwili wa Yesu ungekuwa bila dhambi yo yote na kutokamilika.​—Ebr. 7:26.

33. Kwa hiyo, basi, Maandiko Matakatifu yanatumia mfano wa chachu kwa njia gani, nasi tuna mashahidi gani wa kuunga jambo hilo mkono?

33 Kupatana na yote yaliyotangulia, matoleo ya gazeti Watch Tower ya Mei 15, 1900, na Juni 15, 1910, yalisema kweli kwa kusema kwamba chachu au kinyunga kikali kinapokuwa mfano kinatumiwa katika Maandiko yote katika maana mbaya. Kuanzia na mtajo ule ule wa kwanza wa Biblia wa chachu au kinyunga kikali, katika Kutoka 12:15-20; 13:7, mpaka mtajo wa mwisho katika Wagalatia 5:9, Maandiko Matakatifu yametumia chachu kama mfano wa yaliyo mabaya. Ikiwa tunahitaji mashahidi wa uhakika huo, tunao mashahidi wasiopungua WAWILI wa kuhakikisha kwamba Biblia inatumia chachu bila kubadilika-badilika kufananisha kitu kibaya, uovu, kosa, dhambi. Yesu alisema juu ya chachu ya Mafarisayo na chachu ya Herode. (Mt. 16:6-12; Marko 8:15; Luka 12:1) Mtume Paulo anaonya juu ya chachu inayochachisha donge zima. Anataja sikukuu halisi ya mkate usiotiwa chachu na kueleza waziwazi chachu inafananisha nini, kwa maana anasema hivi: “Pasaka wetu amekwisha kutolewa kuwa sadaka, yaani, Kristo; basi na tuifanye karamu, si kwa chachu ya kale, wala kwa chachu ya uovu na ubaya, bali kwa yasiyochachika, ndio weupe wa moyo na kweli.”​—1 Kor. 5:6-8; tazama Kumbukumbu la Torati 17:6, 7; 19:15; 1 Timotheo 5:19; Waebrania 10:28.c

34. Kwa hiyo, mfano wa chachu unafananisha nini?

34 Kwa kulingana na hilo, Yesu hakuwa na maana tofauti alipotoa mfano wa mwanamke aliyeficha chachu kidogo katika pishi kubwa tatu za unga. Kwa upatano wa kufundisha kwake, hapo alitumia chachu kufananisha kitu kisichofaa. Kwa hiyo bila shaka mfano huo unafananisha kitu kisichofaa juu ya mambo yanayohusiana na “ufalme wa mbinguni.” Hapo kutiwa chachu katika kinyunga kunafananisha kwa unabii kuchafuliwa kwa kundi la Kikristo la kujidai kwa kosa la mafundisho na mazoea ya Kibabeli. Kunafananisha kuchachishwa kwa mfano kwa kinachofananishwa na mharadali. Basi, kwa kufaa Mathayo na Luka pia wanaambatanisha mfano wa chachu na mfano wa punje ya haradali, naye Luka anafanya hivyo mara tu baada ya wanadini wanafiki kukemewa vikali.​—Luka 13:10-21.

[Maelezo ya Chini]

a Tazama kurasa 206-209 za kitabu Man’s Salvation out of World Distress at Hand! kilichochapwa mwaka wa 1975.

b Ukurasa wa 230, mistari 12-14, unasema: “Kwa hiyo walikuwa wametiwa chachu, kwa sababu matoleo ya hadhara ya Israeli ya shukrani, hata patakatifu zaidi sana, yametiwa chachu na kutokamilika na dhambi nayo yanahitaji toleo la dhambi.”

Kulingana na yaliyotangulia, tunasoma katika kitabu Biblical Commentary on The Old Testament, kilichoandikwa na Keil na Delitzsch, (Volume II-The Pentateuch) na chini ya kichwa kidogo (ukurasa 437) kinachosema “Kutakaswa kwa Sabato na Sikukuu ya Yehova.​—Sura ya XXIII,” na katika mistari ya 16-34 ukurasa 443, yafuatayo:

“‘. . . Mst. 20. Kuhani atawapunga (wana-kondoo wawili wa matoleo ya amani), pamoja na mikate ya malimbuko, kama toleo la kupungwa mbele za pamoja na wana-kondoo wawili (wawili wale ambao wametajwa sasa hivi), hiyo (mikate) itakuwa kwa Yehova ikitolewa na kuhani.’ . . . Toleo la dhambi lilipaswa kuamsha mawazo ya ndani ya kundi la Israeli wajue ni wenye dhambi, ili wanapokula mkate wao wa kila siku wenye chachu wasitumikie chachu ya hali yao zamani, bali wamwombe na kumsihi Bwana wao Mungu awasamehe na kuwaondolea dhambi yao.”

c Katika chapa ya 1971 ya Encyclopædia Judaica, Volume 7 tunaona katika safu 1235-3237, makala yenye kichwa “Hamez . . . ‘kinyunga kilichochachishwa’.” Katika safu ya 1237, chini ya kichwa “Chachu Katika Wazo la Kiyahudi,” tunasoma yafuatayo:

“Chachu inachukuliwa kama mfano wa upotovu na uchafu. ‘Chachu katika klnyunga’ ni kimojawapo cha vitu vinavyotuzuia kufanya mapenzi ya Mungu’ (Ber. 17a). Wazo hilo lilikuzwa sana katika Kabalah. Agano Jipya linataja pia ‘chachu ya uovu na ubaya’ inayotofautishwa na ‘mkate usiotiwa chachu wa weupe wa moyo na kweli’ (1 Kor. 5:8). Vivyo hivyo neno hilo linatumiwa kwa lililochukuliwa kama fundisho potovu la Mafarisayo na Masadukayo (Mt. 16:12; Marko 8:15).

“Lilitumiwa hasa kwa mchanganyiko wa vitu vichafu katika jamaa. ‘Kinyunga’ (kilichochachishwa) kilitofautishwa katika maana hii na ‘unga safi uliochungwa. ‘

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki