Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 4/1 kur. 149-154
  • Vitu Ambavyo “Ufalme wa Mbinguni” Unafanana Navyo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Vitu Ambavyo “Ufalme wa Mbinguni” Unafanana Navyo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • CHACHU NA DIVAI
  • “UFALME WA MBINGUNI UMEFANANA NA” VITU MBALIMBALI
  • Kufunuliwa Wazi kwa Kimbilio la Uongo la Ufalme
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Mifano ya Ufalme
    “Ufalme Wako Uje”
  • Hujui Ni Wapi Itafanikiwa!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 4/1 kur. 149-154

Vitu Ambavyo “Ufalme wa Mbinguni” Unafanana Navyo

“Ufalme wa Mungu umefanana na nini? nami niufananishe na nini?”​—Luka 13:18.

1, 2. Kwa kutumia mifano katika kufundisha kwake, Yesu alitimiza unabii gani?

MIFANO ilikuwa sehemu kubwa ya njia ya kufundisha ya Yesu Kristo karne kumi na tisa zilizopita. Kwa njia hiyo alitimiza unabii fulani wa Biblia. Juu ya jambo hilo tunahakikishiwa katika masimulizi ya maisha ya Yesu Kristo yaliyoandikwa na mtume Mathayo Lawi. Mwandikaji huyu aliyeandika habari za maisha yake anatuambia hivi:

2 “Mambo haya yote Yesu aliwaambia makundi ya watu kwa mifano. Kwa kweli, bila mfano yeye hakusema nao; ili lipate kutimizwa lililosemwa kupitia kwa nabii aliyesema hivi: ‘Nitafungua kinywa changu kwa mifano, nitatangaza mambo yaliyofichwa tangu kuwekwa msingi [wa ulimwengu].’”​—Mt. 13:34, 35, NW; Zab, 78:2.

3. Mifano inayohusu ufalme wa Mungu inaweza kuitwa naye Yesu aliianzaje?

3 Mifano hiyo iliyohusu hasa ufalme wa Mungu wa Kimasihi inaweza kuitwa mifano ya Ufalme. Nyakati nyingine ilianzwa kwa maneno haya, “Ufalme wa mbinguni umefanana na,” au, “Tulinganishe na nini ufalme wa Mungu?” au, “Niufananishe na nini ufalme wa Mungu?”​—Mt. 13:47; Marko 4:30; Luka 13:20.

4, 5. (a) Yesu alitoa mifano mingapi, naye alitoa mfululizo gani wayo katika Mathayo, sura ya kumi na tatu? (b) Kulingana na Luka 13:17-21, ni chini ya hali gani Yesu alisimulia mifano ya punje ya haradali na chachu?

4 Yesu anasemekana kuwa alitoa mifano 30. Kulingana na sura ya kumi na tatu ya Injili ya Mathayo, wakati mmoja Yesu alitoa mfululizo wa mifano saba ya Ufalme yenye kuhusiana sana. Wa kwanza ulikuwa mfano wa mpanzi, kisha ule wa ngano na magugu, punje ya haradali, chachu iliyofichwa katika kinyunga (unga uliokandwa), lulu yenye thamani kubwa na juya (wavu wa kuvulia samaki). (Mt. 13:1-50) Mwandikaji wa Injili Luka anatoa utangulizi wa mifano ya punje ya haradali (au mastadi) na chachu kwa njia tofauti, na kusema hivi:

5 “Aliposema haya wakatahayari wote walioshindana naye; mkutano wote wakafurahi kwa sababu ya mambo matukufu yaliyotendwa na yeye. Kisha alisema, Ufalme wa Mungu umefanana na nini? nami niufananishe na nini? Umefanana na punje ya haradali aliyotwaa mtu akaitupa katika shamba lake; ikamea, ikawa mti; ndege wa angani wakakaa katika matawi yake. Akasema mara ya pili, Niufananishe na nini ufalme wa Mungu? Umefanana na chachu aliyotwaa mwanamke akaisitiri ndani ya pishi tatu za unga, hata ukachacha wote pia.”​—Luka 13:17-21.

6. Kwa kuwa Yesu aliitoa mifano hiyo watu walipokwisha kufurahia mambo aliyofanya, huenda mtu akaelekea kufikiri Yesu alitaka kuonyesha nini kwa mifano hiyo?

6 Kwa kuwa ‘mkutano wote walifurahi kwa sababu ya mambo matukufu yaliyotendwa na yeye,’ mtu huenda akaelekea kufikiri kwamba Yesu alisimulia mifano miwili ya unabii, kwa sababu ya kufurahi kwa “mkutano wote,” kuonyesha vile ufalme wa Mungu usingefanyizwa na “kundi dogo” tu, kama Yesu alivyokuwa ameonyesha mapema, katika Luka 12:32. Huenda akaelekea kufikiri kwamba, badala yake, ungekuwa mkubwa nao ulimwengu wote wa wanadamu ungekuwa kama ndege kwa kukaa katika kimbilio walilopewa na Ufalme. Pia, huenda akafikiri kwamba wanadamu wote wangejawa na mafundisho ya kweli ya Ukristo. Kwa mfano, Critical and Exegetical Handbook to the Gospel of Matthew, cha H. A. W. Meyer, Th.D., chapa ya Kiingereza ya 1884, kinasema hivi ukurasa wa 259, fungu la tatu:

Mfano wa punje ya haradali umekusudiwa kuonyesha kwamba jamii kubwa, yenye wale ambao wangeshiriki katika ufalme wa Kimasihi, yaani, watu wa kweli wa Mungu walio raia wa ufalme wa wakati ujao, ingekua kutoka mwanzo mdogo iwe umati mkubwa wa watu, na hivyo ipanuke sana sana; . . . “wakiwa kundi dogo, wakaongezeka wakawa kundi lisilohesabika.” Kwa upande mwingine, mfano wa chachu umekusudiwa kuonyesha vile maongozi ya wazi ya ufalme wa Masihi (Efe. iv.4 ff.) yanavyopenya kidogo kidogo katika raia zake wote wa wakati ujao, mpaka jamii yote iingizwe sana sana katika hali hiyo ya kiroho inayoistahilisha kukubaliwa katika ufalme.

7, 8. Luka anaandika ulizo gani zito baada yapo. na anaandika mfano gani wa Yesu wa Ufalme?

7 Walakini, hapa pana uhakika unaostahili kuangaliwa kuwa wa maana. Ndio huu: Mara tu anapokwisha kuandika mifano hiyo miwili ya Yesu na kueleza vile alivyokwenda akihubiri mahali mahali baada ya hapo, mwandikaji wa Injili Luka anatokeza ulizo la mtu fulani: “Je! Bwana, watu wanaookolewa ni wachache?” Je! jibu la Yesu lilielekea kupatana na wazo hilo? Je! lilionyesha ufalme ungekuwa wa “kundi dogo”?​—Luka 13:22, 23.

8 Sikiliza: “Jitahidini kuingia katika mlango ulio mwembamba, kwa maana nawaambia ya kwamba wengi watataka kuingia, wasiweze. Wakati mwenye nyumba atakaposimama na kuufunga mlango, nanyi mkaanza kusimama nje na kuubisha mlango, mkisema, Ee Bwana, tufungulie; yeye atajibu na kuwaambia, Siwajui mtokako; ndipo mtakapoanza kusema, Tulikula na kunywa mbele yako nawe ulifundisha katika njia zetu. Naye atasema, Nawaambia, Siwajui mtokako; ondokeni kwangu ninyi nyote mlio wafanyaji wa udhalimu. Ndipo kutakapokuwa na kilio na kusaga meno, mtakapomwona Ibrahimu na Isaka na Yakobo na manabii wote katika ufalme wa Mungu, nanyi wenyewe mmetupwa nje.” (Luka 13:23-28) Kwa hiyo, wanaoingilia katika “mlango ulio mwembamba” itawapasa ‘kujitahidi’ kwa kadiri ya hesabu yao.​—Angalia pia Luka 13:5-9.

9. Kwa kujitolea kuongeza makala kwa toleo la Watch Tower la Aprili 1881, J. H. Paton aliuelezaje mfano wa chachu?

9 Huko nyuma katika toleo la Zion’s Watch Tower la Aprili 1881, katika ukurasa wa 5, yalitokea maneno yaliyoandikwa na J. H. Paton kwa kujitolea, juu ya mfano wa chachu. Katikati ya mazungumzo yake alisema hivi:

Kazi hii ya maendeleo na usitawi mtukufu, 1 inaelekea kufananishwa na mfano wa Mwokozi, ambamo Yeye alilinganisha ufalme wa mbinguni na chachu, ambayo mwanamke niichukua akaificha katika pishi tatu za unga hata fungu lote likachachu. Mt. 13:33. Ubishi unaoelekea sana kuwa wa akili nzuri na wa maana sana juu ya matumizi haya ya mfano, unahusu uhakika wa kwamba chachu ya mkate na ya mafundisho inazungumzwa, katika Biblia kuwa kitu chenye kuchafua na kupotoa. Je! Mwokozi angefananisha ufalme wa mbinguni na kitu na njia ya kupotolea mambo? Tunafahamu hapa Mwokozi anatumia sehemu moja tu ya chachu, katika mfano Wake, nayo ndiyo uwezo wake wenye kuenea. Haukomi mpaka kazi imalizike, kwa hiyo ufalme wa Mungu hautakomesha utendaji wake mpaka laana iondolewe.

10. Toleo la Watch Tower la Mei 15, 1900, lilielezaje mfano wa chachu?

10 Walakini, Zion’s Watch Tower, la tarehe ya Mei 15, 1900, ukurasa wa 154, lilikuwa na maoni yenye kutofautiana na hayo. Chini ya kichwa kidogo “Mfano wa Chachu,” lilisema hivi: “Chachu inafananisha upotovu katika sehemu zote za Maandiko: Kila mara nyingine inapotumiwa katika Maandiko inaonyeshwa kuwa uovu, uchafu, kitu chenye kunajisi. . . . Lisingeelekea kuwa jambo la akili nzuri kufikiri kwamba Bwana wetu angetumia hapa neno chachu kwa maana nzuri kama Wakristo wanavyodhani kwa ujumla, likimaanisha neema fulani ya roho takatifu. Bali, tunaona upatano katika mafundisho yake yote, na tunaweza kuwa na hakika pia kwamba asingetumia chachu kama mfano wa haki kama vile asingetumia ukoma kama mfano wa utakatifu.”

11. The Watch Tower la Juni 15, 1910, lilielezaje mfano wa chachu?

11 The Watch Tower, la tarehe ya Juni 15, 1910, ukurasa wa 205, lilifuata wazo ilo hilo. Lilisema hivi, chini ya kichwa “Chachu Iliyofichwa katika Unga”: “Mfano wa ‘chachu’ (mstari 33) unaonyesha jinsi kanisa lingeingia katika hali mbaya, kama ilivyokuwa imekwisha semwa mapema kwa unabii. Kama vile mwanamke anavyochukua kinyunga chake cha kuokea na kutia chachu ndani kisha kinachacha, ndivyo ingekuwa kwa kanisa la Kristo; chakula cha nyumba yote kingechachishwa au kuchafuliwa. Kila kisehemu kingedhoofishwa na chachu ya mafundisho ya uongo ambayo yangeenea katika chakula chote. Hivyo leo karibu kila fundisho lililosisitizwa na Yesu na mitume wake limepotolewa au kupindwa na makosa ya vizazi ambavyo havikuwa na mwangaza wa mambo ya kiroho.”​—Tazama pia The Watch Tower la Juni 15, 1912, kurasa 198, 199, chini ya kichwa “Mfano wa Chachu.”

CHACHU NA DIVAI

12. Huenda mtu aliyetajwa mapema aliyejitolea kuandika habari katika Watch Tower akasisitizia nini kwa ubishi, na huenda akataja mfano gani wa Yesu unaohusu divai na viriba?

12 Sasa, kama J. H. Paton angalikuwa hai wakati huo kama mhariri wa Watch Tower C. T. Russell, pengine angalipinga makala hizo katika matoleo ya Watch Tower ya 1900, 1910 na 1912. Pengine angalisisitiza The Watch Tower lishikamane na ile “sehemu moja tu ya chachu, katika mfano wa [Yesu] nayo ndiyo uwezo wake wenye kuenea.” Kwa kuwa uwezo wenye kuenea umo katika kuchachishwa kwa kitu chenyewe, pengine angalibisha kwamba kuchacha ni kuchacha, jambo lenye kuonwa kuwa baya. Kwa hiyo pengine angalitaja Mathayo 9:17, ambapo Yesu anasema hivi: “Wala watu hawatii divai mpya katika viriba vikuukuu; na kama wakitia, vile viriba hupasuka, divai ikamwagika, na viriba vikaharibika; bali hutia divai mpya katika viriba vipya, vikahifadhika vyote.”​—Pia, Marko 2:22; Luka 5:37, 38.

13. (a) Basi, ni katika maana gani kuchacha kwa divai kunatumiwa? (b) Kwa sababu hiyo, ni ulizo gani linalotokea juu ya maana ya mfano ya kuchacha kunakosababishwa na chachu?

13 Kuchacha kunakoendelea kwa divai mpya kunaleta mapovu ya hewa na kupasua viriba vikuukuu visivyoweza kurudia hali yavyo ya kawaida baada ya kutumiwa. Kuchacha kwa divai ni kwenye kusudi jema, na kwa hiyo hapa kuchacha kunatumiwa kwa njia njema nako kunafananisha jambo jema. Lakini je! hiyo inatoa sababu ya kwamba kuchacha kunakosababishwa na chachu kunatumiwa kama mfano wa jambo jema katika mfano wa mwanamke aliyeficha chachu katika pishi kubwa tatu za unga mpaka unga wote ukachacha? Na kwa hiyo je! Biblia inatumia chachu mara moja au mbili kama mfano wa mabaya na maovu? Je! Biblia inatumia chachu kama mfano kwa njia mbili, kama mfano wa yaliyo mema na haki na pia kama mfano wa yaliyo mabaya na maovu?

14. Ni uhakika gani unaoonyesha kwamba Biblia haichukui kuchacha kwa divai sawa na kuchacha kunakosababishwa na chachu inayoongezwa kwa fungu la unga?

14 Kwa haki inawezaje kubishwa kwamba Biblia inatumia chachu ya kinyunga kwa njia mbili hivyo, na hali katika mwadhimisho wa sikukuu ya Kupitwa na sikukuu ya siku saba iliyofuata, divai iliruhusiwa kunywewa ijapokuwa chachu yote ya mkate ilikatazwa, ikapigwa marufuku, hata mwenye kuvunja sheria hiyo angeuawa? (Law. 23:5-13; Luka 22:7-20) Kwa hiyo, je! Biblia inachukua chachu zote na uwezo wazo wenye kuenea kwa njia ile ile moja? Je! Biblia inachukua uwezo wenye kuenea kama jambo la peke yake linalopaswa kufikiriwa, bila kujali kinachochachisha? Jibu la Maandiko ni Sivyo! Ama sivyo, tusingefahamu sababu gani kunaelekea kuwa na tofauti katika mwadhimisho wa sikukuu ya Kupitwa na sikukuu ya juma moja ya mkate usiotiwa chachu iliyofuata sikukuu ya Kupitwa.

15. Kwa habari ya kuchacha, ni jambo gani lenye kuamua, na kwa hiyo je! mfano wa chachu unaonyesha jambo jema au baya?

15 Kwa hiyo, kuchacha pamoja na uwezo wake wa kuchachisha silo jambo linaloamua kama maana yake ya mfano ni njema au mbaya. Bali, kitu kinachoongezwa kuendeleza kuchacha ndicho kinachoamua. Katika Maandiko Matakatifu, kuchacha (kama jambo) hakutenganishwi na kinachokusababisha kuchacha kwenyewe. Kwa hiyo, kuchacha kunakotokezwa kwa vyepesi katika divai inayotengenezwa hakupangwi kuwa sawa na kuchacha kunakoendelezwa na kikolezo katika kinyunga, yaani chachu au kinyunga kikali (cha zamani).a Kwa hiyo mtu ye yote akitaja kuchachishwa kwa divai mpya inayotiwa katika viriba vipya ndiyo aonyeshe kwamba chachu (kinyunga kikali) inayoongezwa katika mkate unaokandwa ni mfano wa yaliyo mema na haki anakosea. Hoja yake haina msingi wa Biblia. Kwa sababu hiyo hoja iliyotumiwa na J. H. Paton katika toleo la Zion’s Watch Tower la Aprili 1881 si nzuri. Maandiko yaliyoongozwa na Mungu yawatulazimisha tutofautishe chachu (kinyunga kikali) kinapokuwa mfano. Kwa hiyo, mfano wa chachu si mfano wenye kuonyesha jambo jema; bali, unaonyesha jambo baya. Lakini tutatoa habari zaidi juu ya shauri hilo la chachu baadaye katika mazungumzo yetu.

“UFALME WA MBINGUNI UMEFANANA NA” VITU MBALIMBALI

16, 17. Kwa nini huenda wengine wakapinga yaliyotangulia kwa sababu ya vile mifano ya punje ya haradali na chachu inaanzwa? Lakini ni utangulizi aina gani unaotolewa kwa mfano wa juya, linalotumiwa kwa kazi gani?

16 Je! maelezo ya zamani yaliyokuwamo katika matoleo ya 1900, 1910 na 1912 ya The Watch Tower juu ya mfano wa chachu yangali mazuri leo, wakati ambao mifano ya Yesu inafikia upeo wa utimizo wayo? Naam, ndivyo kabisa! Huenda wanafunzi wengine wa Biblia wakaelekea kupinga, kwa maana, kama wasemavyo, “ufalme wa mbinguni” ndio unaosemekana kuwa kama chachu na kama punje ya haradali (mastadi). (Mt. 13:31-33) Naam, lakini ni kweli pia kwamba, katika mfano wa saba na ambao ndio wa mwisho wa mfululizo ulio katika Mathayo, sura ya kumi na tatu, Yesu alisema hivi:

17 “Tena ufalme wa mbinguni umefanana na juya, lililotupwa baharini, likakusanya [samaki] wa kila namna; hata lilipojaa. walilivuta pwani; wakaketi, wakakusanya walio wema vyomboni, bali walio wabaya wakawatupa. Ndivyo itakavyokuwa katika mwisho wa dunia; malaika watatokea, watawatenga waovu mbali na wenye haki, na kuwatupa katika tanuru ya moto; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno.”​—Mt. 13:47-50.

18. (a) Kwa hiyo, ni maulizo gani yanayotokezwa juu ya mfano wa juya na ule wa wanawali wenye busara na wapumbavu? (b) Kwa wazi Yesu alimaanisha nini kwa kusema “ufalme wa mbinguni umefanana na”?

18 Sasa tunajua kwamba wenye kufanyiza “ufalme wa mbinguni” au “ufalme wa Mungu” wa Kimasihi ni Mwana-Kondoo Yesu Kristo na wafuasi wake wa kiroho Kiisraeli 144,000. (Ufu. 7:4-8; 14:1-5) Kwa hiyo hapa tunalazimika kuuliza hivi, Je! Yesu alimaanisha kwamba jamii hii ya Ufalme ya watu mia arobaini na nne elfu nye watu “waovu” na “wenye haki” ndani yake lenyewe linalotumiwa na malaika wadogo kuliko Yesu Kristo? Tunakumbuka kwamba Yesu alianza mfano mwingine, akisema hivi: “Ndipo ufalme wa mbinguni utakapofanana na wanawali kumi, waliotwaa taa zao, wakatoka kwenda kumlaki bwana arusi. Watano wao walikuwa wapumbavu, na watano wenye busara.” (Mt. 25:1, 2) Je! tuelewe kwamba jamii ya Ufalme ya watu mia arobaini na nne elfu na mmoja imegawanyika katika nusu moja ya wapumbavu na nusu nyingine ya wenye busara? Isingeweza kuwa hivyo hata! Kwa wazi, basi, Yesu aliposema “ufalme wa mbinguni umefanana na” alimaanisha kwamba kuna sehemu inayofanana na hiki au kile, inayohusiana na ufalme wa mbinguni. Au, alimaanisha kwamba mambo inyohusiana na Ufalme yatakuwa kama kile na kile.

19, 20. (a) Ili tupate ufahamu unaofaa, lazima tujue nini juu ya kusudi la mfufulizo wa mifano? (b) Kulingana na maneno yake mwenyewe, kwa sababu gani Yesu alisema na watu kwa mifano?

19 Ufahamu huo juu ya maana ya maneno unaeleza sababu gani Yesu alifananisha matukio mabaya na mema pia na “ufalme wa mbinguni” au “ufalme wa Mungu” wa Kimasihi. Ili tupate ufahamu unaofaa, lazima tukumbuke kusudi la kutolewa kwa mfufulizo wa mifano. Yesu mwenyewe alitujulisha kusudi hilo. Alipokwisha kutoa hadharani mfano wa aina nne za udongo ambazo juu yazo mbegu ya mpanzi ilianguka, wanafunzi wake walimwuliza: “Kwa nini wasema nao kwa mifano?” Sasa, na tuangalie jibu hili la Yesu:

20 “Ninyi [wanafunzi] mmejaliwa kuzijua siri za ufalme wa mbinguni, bali wao hawakujaliwa. Kwa maana ye yote mwenye kitu atapewa, naye atazidishiwa tele; lakini ye yote asiye na kitu, hata kile alicho nacho atanyang’anywa. Kwa sababu hii nasema nao kwa mfano; kwa kuwa [akitaja Isaya 6:9, 10] wakitazama hawaoni, na wakisikia hawasikii, wala kuelewa. Na neno la nabii Isaya linatimia kwao, likisema, Kusikia mtasikia, wala hamtaelewa; kutazama mtatazama, wala hamtaona. Maana mioyo ya watu hawa imekuwa mizito, na kwa masikio yao hawasikii vema, na macho yao wameyafumba; wasije wakaona kwa macho yao, wakasikia kwa masikio yao, wakaelewa kwa mioyo yao, wakaongoka, nikawaponya.”​—Mt. 13:10-15.

21. (a) Yesu alipotumia mifano. Isaya 6:9, 10 ilitimizwaje kwa habari ya Israeli? (b) Mfano wa aina nne za udongo ulionyeshaje jambo ilo hilo?

21 Hilo ndilo lililokuwa kusudi la Yesu lililosemwa la kunena na Waisraeli kwa kutumia mifano, kutimiza Zaburi 78:2; na kwa kutumia mfano Yesu alionyesha kwamba unabii wa Isaya 6:9, 10 ungetimizwa, yaani, kwamba wachache kwa kulinganishwa, mabaki, wangekubali ujumbe wake wa kweli na kuwa Wakristo halisi wanaoustahili “ufalme wa mbinguni.” Kwa mfano, katika mfano wa mpanzi alizungumza juu ya aina nne za udongo, kwamba tatu kati ya nne hazikuwa na mazao. Namna nzuri tu ya udongo ndiyo iliyozaa kwa wingi, mara 30, 60, mara 100, katika kuutangaza ujumbe wa Ufalme. (Mt. 13:3-8) Hivyo katika mfano ule ule wa kwanza wa mfululizo huo jambo baya juu ya “ufalme wa mbinguni” ndilo linalotangulia.

22. Katika mfano wa Yesu wa ngano na magugu, Isaya 6:9, 10 inatimizwa juu ya jamii gani?

22 Katika ule mfano unaofuata wa ngano na magugu, adui alipanda magugu katika konde (shamba) lote, hata wakati wa mavuno ulipofika, konde lilikuwa limeharibiwa na kuwapo kwa wingi wa magugu, Yesu alieleza kwamba “mbegu njema” ni Wakristo wa kweli waliotiwa mafuta, “wana wa ufalme.” Magugu ni Wakristo wa kujifanya, yaani, “wana wa yule mwovu,” Ibilisi aliyeyapanda. Wakati wa mavuno ni “mwisho wa dunia” (mwisho wa taratibu ya mambo, NW), ambamo tumo sasa. Tunapotazama kazi ya mavuno ya kiroho ambayo imekuwa ikiendelea tangu masika ya mwaka wa 1919 W.K., twaona nini? Twaona kwamba “wana wa ufalme” wanaovunwa chini ya uongozi wa malaika ni mabaki tu, leo wakiwa karibu elfu kumi wenye kula na kunywa mifano ya mkate na divai katika mwadhimisho wa Kijio cha Bwana. Tangu mwaka wa 1948, ambapo ripoti inaonyesha walikuwa 25,395, wamekuwa wakipungua idadi. Kwa upande mwingine, “wana wa ufalme” wa kujifanya, wale ambao juu yao unabii wa Isaya 6:9, 10 unatimizwa, wana karibu washiriki milioni elfu moja wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo.​—Mt. 13:24-30, 36-43.

23. Katika mfano wa hazina iliyofichwa, ni wangapi wanaochukua hatua njema?

23 Katika mfano wa hazina iliyofichwa shambani, mtu mmoja tu ndiye aliyeigundua hazina hiyo “akauza alivyo navyo vyote, akalinunua shamba lile.” Wengine wote walielekeza maono yao ya mambo yaliyo bora upande mwingine kwa sababu macho yao yalikuwa kana kwamba ‘yametiwa kibandiko’ nao hawakukiona kitu chenye thamani kilichofichwa katika shamba hilo.​—Mt. 13:44.

24. Katika mfano wa lulu ya thamani kubwa, ni wafanya biashara wangapi wenye kusafiri waliokuwa na nia ya kulipa bei yake?

24 Katika mfano wa “lulu moja ya thamani kubwa,” “mfanya biashara” mmoja tu ndiye aliyetamani sana kuwa na lulu isiyopatikana vyepesi. Yeye peke yake ndiye ‘aliyekwenda haraka akauza alivyo navyo vyote, akainunua.’ Wafanya biashara wengine wote wenye kusafiri walikuwa wakitafuta kitu kingine walichoona kuwa chenye thamani, inaelekea kitu ambacho kisingewafanya wauze vyote walivyokuwa navyo ndio wapate pesa za kukinunua.​—Mt. 13:45, 46.

25, 26. (a) Ni wakati gani mifano ya juya na konde ngano inapofikia upeo wa utimizo wayo? (b) unabii mbalimbali unatimizwaje juu ya “wenye haki” na juu ya Wakristo wa kujifanya?

25 Katika mfano wa juya, chombo hicho kikubwa cha kuvulia samaki, kinachotumiwa na wavuvi wanaofananisha “malaika,” kinakusanya samaki “wa kila namna,” samaki waliofaa kuliwa na Wayahudi wenye kushika Torati na samaki wengine waliokatazwa na sheria ya Musa. Samaki wenye kufaa peke yao ndio waliokusanywa ndani ya vyombo, na wale wengine wakatupiliwa mbali kama chukizo.​—Mt. 13:47-50.

26 Je! hapa duniani, katika “mwisho wa taratibu ya mambo,” ambapo tupo tangu mwaka wa 1914 W.K., ndipo mfano wa konde la ngano unapofikia upeo wa utimizo wake? Kwa hiyo kazi zinapoendelea, ‘kuwatenga waovu mbali na wenye haki, chini ya uongozi usioonekana wa malaika watakatifu wa Mungu, tunaona mambo gani ya hakika juu ya jambo hilo kuhusiana na “ufalme wa mbinguni”? Je! “wenye haki” wanaoitwa kwenye ufalme wa kimbinguni ni wengi sana sana? Kwa kinyume, wao ni “mabaki” ya kiroho wachache sana, ijapokuwa wanakanisa wa Jumuiya ya Wakristo wanaotazamia kufika mbinguni wafapo wanakadiriwa kuwa mamia ya mamilioni. Unabii wa Isaya 6:9, 10 unatimizwa juu ya Wakristo hao wa kujifanya. Watatupwa katika “moto” wa “dhiki kubwa” ambayo iko karibu sana. (Mt. 13:47-50) Kwa hiyo Jumuiya ya Wakristo, mfano wa uongo wa “ufalme wa mbinguni,” sipo mahali pa kukimbiliwa na ye yote sasa.

[Maelezo ya Chini]

a “Njia ya kuchachisha vileo inataka divai bora zifanyizwe kwa uangalifu. . . . Ngozi za matunda ya mzabibu kwa kawaida zinakuwa zimefunikwa na vijidudu (bacteria), ukungu, na chachu. Chachu za mwituni kama Pichia, Kloeckera, na Torulopsis mara nyingi zinakuwa nyingi zaidi kuliko chachu ya divai inayoitwa Saccharomyces. Ingawa kwa kawaida namna namna za Saccharomyces zinaonwa kuwa za kutamanika zaidi kwa kuchachisha vileo sawasawa, inawezekana kwamba namna namna nyingine za chachu zinaweza kuongeza ladha. hasa mwanzoni mwanzoni mwa kuchachisha. Saccharomyces inapendelewa kwa sababu ina matokeo mazuri katika kugeuza sukari iwe kileo na kwa sababu haishindwi nguvu sana na vileo.”​—Encyclopædia Britannica, Volume 19, chapa ya 1974, ukurasa 879, chini ya “Kuchachisha.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki