Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • kc sura 10 kur. 87-95
  • Ufalme Bandia Watokea

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ufalme Bandia Watokea
  • “Ufalme Wako Uje”
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ULE UKAFIRI (UASI-IMANI) MKUBWA
  • ASILI ZA UKATOLIKI
  • NAMNA GANI UPROTESTANTI?
  • “BABULONI MKUU”
  • Konstantino Mkubwa Je, Alikuwa Mtetezi wa Ukristo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Jinsi Jumuiya ya Wakristo Ilivyokuja Kuwa Sehemu ya Ulimwengu Huu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Konstantino
    Amkeni!—2014
  • Ule Uasi-imani Mkubwa Wasitawi
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
“Ufalme Wako Uje”
kc sura 10 kur. 87-95

Sura ya 10

Ufalme Bandia Watokea

1. Zile “habari njema” zilisitawi kwa kadiri gani katika nyakati za kwanza?

INGAWA lilikabiliwa na mateso ya ukatili kabisa, kundi changa la Kikristo likaendelea kusitawi na kupanuka. Ile kweli ya habari njema kuhusu ufalme wa Mungu kupitia Masihi ikaendelea “katika ulimwengu wote, na kuzaa matunda na kukua.” Watangazaji wa Ufalme walipopenya ndani ya maeneo mapya wapinzani wakalalamika kwamba “watu hawa wamekuwa wakivuruga dunia yote na sasa wako hapa mjini.”—Wakolosai 1:5, 6, UV; Matendo 17:6, HNWW.

2. Shetani alifanya jitihada gani azuie kuenea kwa ile kweli, lakini sababu gani alishindwa?

2 Walakini, wanadamu wa vivi hivi wangeweza kufanya nini ili wazuie kweli isienee? Maandishi ya historia yanaonyesha kwamba katika karne tatu za kwanza za Wakati wa Kawaida wetu, Makaisari wa Milki ya Roma walitokeza mawimbi 10 ya mateso juu ya Wakristo wa kwanza, lakini yote hayakutimiza lo lote. Wale waliofuata hatua za Yesu, ‘wakiwa thabiti katika imani,’ walikataa kubadili msimamo wao ijapokuwa yule “simba angurumaye,” yule Ibilisi, alihakikisha kwamba wengi wao wametupwa kwenye simba halisi au sivyo wameteswa mpaka kufa.—1 Petro 5:8, 9; linganisha 1 Wakorintho 15:32; 2 Timotheo 4:17.

3. Sababu gani ni lazima uivae “suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu”?

3 Kwa kuwa kwa kawaida shambulio la uso kwa uso la mateso ya moja kwa moja lilishindwa, yule Ibilisi alitaka kutega wafuasi wa Yesu kwa werevu zaidi. Walizungukwa na ulimwengu wenye kiburi, usio na adili, wenye kupenda sana anasa, naye Shetani akautumia sana kujaribu kuwaondoa katika utumishi wa Mungu. Walihitaji ‘kusimama imara,’ kama mtume Paulo anavyorudia kusema mara tatu katika Waefeso 6:11-18, NW, akieleza kirefu zile ‘silaha za kiroho kutoka kwa Mungu’ ambazo ni lazima watumie. Je! wewe mwenyewe umevaa hiyo “suti kamiliya silaha toka kwa Mungu”? Ni lazima uivae ili uyashinde majaribu ya hizi “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5) Wakristo wa huko nyuma katika karne ya kwanza waliihitaji. Hasa ni kwa sababu gani hivyo?

4. Katika karne ya kwanza, ni kweli gani za msingi za Ufalme ambazo Wakristo walifahamu?

4 Imani yao ilikuwa na isiyochafuliwa. Wakati huo, wote walikuwa Wakristo wapakwa mafuta kwa roho na waliotazamia kufufuliwa wakati ujao waingie “katika ule ufalme wa milele wa Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo.” (2 Petro 1:11, NW; 1 Wakorintho 15:50) Angalau tangu wapata mwaka wa 96 W.K. wakati yule mtume mzee Yohana alipopokea Ufunuo kwa uongozi wa kimungu, walifahamu kwamba hesabu yao, wakiwa “kundi dogo,” ingekuwa 144,000. Wakiwa ‘wafalme na makuhani’ washirika wa Kristo mbinguni, wangetawala dunia kwa miaka 1,000. Yohana alionyeshwa kwamba “baada ya” kukusanywa kwa wale 144,000 wa Israeli wa kiroho, “mkutano mkubwa” usio na hesabu wa waume na wanawake washikamanifu, kutoka “watu wa kila taifa, na kabila, na janaa, na lugha,” ungetambuliwa. Wakiwa jamii wangeiokoka “dhiki ile iliyo kuu” iliyo ya mwisho duniani, wawe kiini cha jamii ya kibinadamu itakayofurahia baraka za miaka elfu chini ya utawala wa ule Ufalme.—Luka 12:32: Ufunuo 7:4, 9-17; 20:1-6; 21:1-5.

ULE UKAFIRI (UASI-IMANI) MKUBWA

5, 6, (a) Ni maandiko gani yanayoonyesha kwamba, hata wakati huo, yule Ibilisi alikuwa akitumia mtindo wa werevu zaldi wa kushambulia? (b) Kwa kifupi, ulikuwa nini?

5 Basi, Ibilisi alitumia mtindo gani wa werevu wa kushambulia? Akielekeza nyuma kwenye Israeli wasio na imani, mtume Petro alikuwa ameonya hivi: “Wakawako pia manabii wa uongo miongoni mwa watu hao, kama watakavyokuwako pia walimu wa uongo miongoni mwenu ninyi. Watu wenyewe hao wataingiza kisiri-siri madhehebu zenye kuharibu . . . Pia, kwa tamaa watawatumieni ninyi kwa faida yao kwa kutumia maneno ya bandia.” (2 Petro 2:1, 3, NW) Walimu hao wa kimadhehebu, wakiwa na mafundisho yao ya kidini ya bandia, tayari walikuwa wameanza kutokea karibu na mwisho wa ile karne ya kwanza, maana ilikuwa karibu mwaka wa 98 W.K. mtume Yohana alipoandika hivi: “Kama ambavyo mmesikia kwamba mpinga-Kristo anakuja, hata sasa wametokea wapinga-Kristo wengi . . . Walitoka kwetu, lakini hawakuwa wa aina yetu.”—1 Yohana 2:18, 19, NW.

6 Katika ile inayoonekana kuwa ndiyo barua yake ya pili iliyo halali, mtume Paulo alikuwa ameonya mapema sana mwaka wa 51 W.K. kuhusu mafundisho ya uongo juu ya ile “siku ya Yehova.” Aliandika hivi: “Msiache mtu ye yote awashawishe kwa jinsi yo yote, kwa sababu haitakuja isipokuwa ule ukafiri uje kwanza na mtu wa kuhalifu apate kufunuliwa, mwana wa uharibifu.” “Mtu wa kuhalifu” huyo angeweza kuwa nani? Lazima awe ni viongozi wa kidini makafiri (waasi-imani) ambao ni wahalifu kwa sababu, wajapodai kuwa Wakristo, ‘hawamjui Mungu’ na ‘hawazitii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu.’ (2 Wathesalonike 1:6-8; 2:1-3, NW) Jamii hiyo iliyo kafiri inge-wezaje kutokea katika kundi la Kikristo?

7. Baadhi ya wafuasi wa Yesu walinaswa namna gani, kwa matokeo gani?

7 Mitume wa Yesu Kristo walipokuwa hai bado, walikuwa kizuizi ili mafundisho ya uongo yasiingizwe, lakini “fumbo la uhalifu huo” lilikuwa limeanza kutenda kazi, “kulingana na utendaji wa Shetani,” nalo lilijitokeza mbele katika karne ya pili. Ijapokuwa Yesu alikuwa amewaambia wafuasi wake, “nyote ni ndugu,” tamaa ya ukubwa wa kibinafsi ilifanya watu fulani wanaswe na yule Ibilisi. Sasa walifanyiza tofauti kati ya viongozi wa kidini na waamini wa kawaida tu. Polepole hali ile iliyotabiriwa na mtume Paulo ikatokea: “Utakuja wakati ambapo watu hawatasikiliza mafundisho ya kweli, ila watafuata tamaa zao wenyewe na kujikusanyia walimu tele watakaowaambia mambo yale tu ambayo masikio yao yako tayari kusikia. Watakataa kuusikia ukweli.”—2 Timotheo 4:3, 4, HNWW; 2 Wathesalonike 2:6-10, NW; Mathayo 23:8.

8. (a) Ni vyanzo gani viwili vya mafundisho ya uongo vilivyokuwa vikubwa? (b) Ensaiklopedia zinasimuliaje kuchafuliwa kwa Ukristo?

8 Basi, waligeuzia wapi masikio yao? Kwenye mafundisho yaliyotokana na mahali ambapo ndicho chanzo cha dini ya uongo katika Babuloni wa kale, na kwenye falsafa za Wagiriki, zilizopendwa sana na wengi katika ulimwengu wa Roma wa wakati huo. Kama kitabu M’Clintock and Strong’s Cyclopaedia kinavyoeleza: “Ule usafi wa Injili ulichafuliwa; kawaida na sherehe kubwa-kubwa ziliingizwa; walimu wa Ukristo walipewa heshima na faida za mapato, na ule ufalme wa Kristo ukageuzwa kwa kadiri kubwa kuwa ufalme wa ulimwengu huu.” Na kuhusu hilo kitabu Encyclopaedia Britannica kinaongezea haya: “Labda hakuna jambo ambalo limeelekea sana sana kuchafua Ukristo kuliko kule kuingizwa ndani yao mambo ya ushirikina ambayo yenyewe ni ya kipagani kweli kweli, au yamedokezwa na mazoea ya kipagani. Baada ya kushindwa kuupinga Ukristo, upagani umefanya mengi ili kuuchafua, nao umeshambulia usafi wa Ukristo kwa njia zisizo na hesabu.”

9. (a) Ni imani gani za watu wengi zinazotokana na lile fundisho la kwamba nafsi ya binadamu haifi? (b) Biblia inakanushaje mafundisho hayo?

9 Ni yapi mengine kati ya mambo hayo ya ushirikina na mazoea ya kipagani? Lenye kutokeza ni lile fundisho la Plato mwanafalsafa Mgiriki, la kwamba nafsi ya binadamu haifi. Imani kama hiyo ni ya kwamba lazima nafsi iende mahali fulani wakati wa kufa, kwenye mbingu ya furaha nyingi sana, toharani ili ipate kusafishwa au motoni ili ipate mateso ya milele. Wazo hilo linapingana na maandiko yaliyo katika Biblia kama vile Zaburi 146:4; Mhubiri 9:5, 10; Mathayo 10:28 na Warumi 6:23.

ASILI ZA UKATOLIKI

10, 11. (a) Kardinali Newman anakubali nini juu ya mafundisho mengi ya Kanisa lake? (b) Kwa kuwa anasema kwamba mazoea na mafundisho ya Kanisa “yametokana na upagani,” je! kweli yanaweza kuonwa kuwa matakatifu?

10 Katika kitabu chake Essays and Sketches, John Henry Newman, kardinali Mkatoliki wa karne ya 19, anadokezea asili ya mafundisho mengi ya Kanisa lake, akisema: “Lile jambo lililokubaliwa kila mahali ni hili:—Katika sehemu zalo za msingi au sehemu zalo mbalimbali, lile fungu kubwa la inayokubaliwa na watu wengi kuwa kweli ya Kikristo limetokana na falsafa na dini za kipagani. Kwa mfano, lile fundisho la Utatu lapatikana katika nchi za mashariki na za magharibi; ndivyo ilivyo ile sherehe ya kuosha; ndivyo ilivyo ile kawaida ya sadaka. Lile fundisho la Neno-Mungu ni la Plato; lile fundisho la Kugeuka kuwa Mtu ni la Kihindi.” Ndipo, akijibu mchambuzi anayebisha kwa kusema “Mambo hayo yamo katika upagani, kwa hiyo si mambo ya Kikristo,” kardinali huyo anasema: “Kwa kinyume, sisi tunapendelea kusema, ‘mambo hayo yamo katika Ukristo, kwa hiyo si mambo ya upagani.’ ” Lakini chanzo cha mambo hayo ni mafundisho yale ya Kibabuloni na ya Kigiriki yaliyokuwako karne nyingi kabla ya kutokea Ukatoliki wa Roma. Isitoshe, hayawezi kupatikana katika Neno la Mungu, Biblia.

11 Kwamba ule ukafiri mkubwa ulirudi kwenye dini ya kipagani ili upate huko mafundisho na sherehe zake inathibitishwa na maelezo ya Kardinali Newman katika kitabu chake The Development of Christian Doctrine, ambamo anaandika hivi: “Ili apendekeze ile dini mpya [ya Roma Katoliki] kwa wapagani, Konstantino aliingiza ndani yale mapambo ya nje waliyokuwa wamezoelea katika dini yao.” Ndipo, akiisha kuorodhesha mengi ya mazoea ya kanisa lake, kardinali huyo anakubali kwamba hayo “yote yametokana na upagani, na yametakaswa baada ya kukubaliwa kwayo katika Kanisa.” Lakini, je, fundisho la uongo laweza ‘kutakaswa,’ au lifanywe takatifu?

12, 13. (a) Konstantino alipendezwa na dini ya Roma Katoliki chini ya hali gani na kwa madhumuni gani? (b) Ni nini kinachoonyesha kama Konstantino alikuwa amekuwa Mkristo kwa moyo?

12 Hapa kardinali huyo anamtaja Konstantino Mkuu, mtawala wa Roma wa karne ya nne. Konstantino alitaka nini katika dini? Miaka kadha baada ya kuvamia Roma mwaka wa 312 W.K., Konstantino alijulisha kwamba, katika usiku wa kuamkia ushindi wake, aliiona njozi ya msalaba wa mwali wa moto, ukiwa na maneno haya yenye kusema, “Kwa Huu Shinda.” Maneno hayo akayaandika katika bendera yake. Akaikubali ile misingi ya dini ya Roma Katoliki, kwa wazi akitaka watu wa kumwunga mkono aendeleze makusudi yake mwenyewe ya kisiasa, kisha akazichukua zile imani za kipagani alizokuwa angali anazifuata sana kwa moyo na kuzichanganya na ule mfumo wa kidini “wa Kikristo.”

13 Kitabu Encyclopaedia Britannica kinasema hivi juu ya Konstantino: “Ni lazima iwe kwamba upagani ulikuwa bado ni imani yenye kutenda kazi kwa mtu huyo ambaye, kufikia karibu na mwisho wa maisha yake, aliendeleza ushirikina mwingi sana wa kipagani. . . . Konstantino alikuwa na haki ya kuitwa Mkuu kwa sababu ya matendo yake, si kwa utu wake. Akichunguzwa tabia, kwa kweli anakuwa kati ya walio wadogo zaidi ya wale wote ambao katika nyakati za kale au za kisasa jina hilo la sifa [“Mkuu”] limetumiwa kuwahusu.” Hiyo inaonyeshwa na jinsi alivyofikia hata kiasi cha kuua washiriki kadha wa jamaa yake mwenyewe. Jina lake la cheo la kipagani, “Pontifex Maximus” (Askofu Mkuu), baadaye lilipelekwa na kutumiwa na mapapa wa Kanisa la Roma Katoliki.

14. Je! kweli wale mapapa wa Roma waliuwakilisha ufalme wa Mungu, na unajibu hivyo kwa sababu gani?

14 Mpaka zile zamani za giza na zamani za kati ya karne ya sita na karne ya kumi na sita, wale mapapa wa Roma walitawala sana kama wafalme duniani. Hawakungojea Kristo asimamishe utawala wake wa miaka elfu kutoka mbinguni. Walitaka “ufalme” wakati huo, kwa faida yao ya kichoyo. Kitabu Encyclopaedia Britannica kinausimulia kwa maneno haya: “Mojayapo zile sababu za kwanza kabisa za kuchafuliwa kwa Ukristo ilikuwa ile jitihada ya kugeuza ule ufalme wa Kikristo wa Mungu uwe ufalme unaoonekana ambao katika huo watakatifu walirithi dunia kwa njia halisi.” Si ajabu kwamba watu wanyofu walitaka kupinga namna hiyo ya “kuchafuliwa kwa Ukristo”! Walakini, zile Baraza zenye ukatili za kuhukumu wazushi wa dini, ambazo kwa kuchoma watu kwenye mti pekee zilimaliza maisha za watu 30,000, zilizuia walioitwa wazushi wa dini kwa muda mrefu. Lakini si kwa wakati wote!

NAMNA GANI UPROTESTANTI?

15. (a) Hasa yale Mapinduzi ya Kidini ya Uprotestanti yalipata kuwa nini? (b) Uprotestanti umo utumwani mpaka wakati wetu kwa njia gani?

15 Wakati wa adhuhuri, Oktoba 31, 1517, Martin Lutheri, padri Mkatoliki, alipigilia misumari hoja 95 za kupinga Ukatoliki kwenye mlango wa kanisa katika Wittenberg, Ujeremani. Yale Mapinduzi ya Kidini ya Uprotestanti yakaanza. Walakini, badala ya kuleta hali ya kurudia fundisho safi la Kikristo na utumishi mtakatifu kwa Mungu, hayo Mapinduzi ya Kidini yakawa hasa ya kisiasa. Kujipatia nchi za kutawala kulifuatwa kwa kupigana vita vya kidini, kama Ile Vita ya Miaka 30 ya kuanzia mwaka wa 1618-1648 katika Ulaya, ambamo mamilioni ya watu walikufa. Nchi nyingi zilianzisha dini zao za serikali, na hizo zikaanza kufundisha mafundisho makuu ya Ukatoliki, kama vile kutokufa kwa nafsi, mahali penye moto wa mateso, ule Utatu, ubatizo wa watoto na mengine mengi. Wanaendelea kuwa katika utumwa wa mafundisho hayo ya ule ukafiri mkubwa mpaka leo hii..

“BABULONI MKUU”

16, 17. (a) Andiko la Yeremia 51:6 lina maana gani kwetu leo? (b) Dini ya Babuloni ilipataje ukubwa wenye kuenea katika mataifa yote?

16 Wanaozoea dini ya uongo si wale tu wanaodai kuwa Wakristo. Nabii Yeremia anatuonya hivi:

“Kimbiani mtoke kati ya Babulon, killa mtu naiponye nafusi yakwe.” (Jeremiah 51:6, The Old Testament in Swahili, Mombasa, chapa ya 1949)

Hilo lina maana kwetu leo. Hata katika wakati wa Yeremia, Babuloni ulikuwa mji mbaya sana kwa sababu ya desturi zenye sifa mbaya za kidini na wingi wa miungu. Lakini ukubwa wa Babuloni wa siku hizi unaenea mataifa yote. Hiyo ilitokeaje?

17 Baada ya gharika ya siku za Noa, ni katika Babuloni ambako Nimrodi mwovu, “mwindaji mwenye nguvu katika kupingana na Yehova,” alianza kujenga mji-ufalme na inaelekea hata ule mnara wa kidini wenye kufika katika mbingu. Yehova alizuia mipango hiyo kwa kuleta mchuko wa lugha za wanadamu na kuwatawanya “kote kote katika uso wa dunia.” Lakini walienda na dini yao ya uongo. Lilikuwa ndilo shina ambalo kutoka hilo dini nyingi sana za ulimwengu zimesitawi.—Mwanzo 10:8-10; 11:1-9, NW.

18. Ni lazima tuukimbie ufalme-bandia gani, na tukimbilie wapi?

18 Kama tulivyokwisha kujua, Konstantino alichanganya dini hiyo ya uongo na mafundisho ya Kikristo wakati alipoiweka misingi ya dini ya Roma Katoliki. Hiyo nayo ikawa ndicho chanzo cha mafundisho mengi ya Uprotestanti. Hata dini zisizo “za Kikristo” za dunia zina mashina yazo katika Babuloni wa kale. Zote pamoja, zile dini za Ukristo wa uongo na dini zisizo “za Kikristo” ni milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. Ni ufalme-bandia ambao mtume Yohana alitaja kuwa “Babuloni mkuu . . . ule mji mkuu unaowatawala [kidini] wafalme wa dunia.” (Ufunuo 17:5, 18, HNWW) Kwa hiyo ili ‘kila mtu aiponye nafsi yake,’ tunashauriwa vya kufaa tuukimbie ufalme-bandia wa Kibabuloni, ndiyo, tukimbilie ufalme wa Mungu!

[Sanduku katika ukurasa wa 95]

SHETANI ANASHAMBULIA WATUMISHI WA UFALME WA MUNGU KWA—

• Shambulio la uso kwa uso na moja kwa moja la mateso—kupitia watu wa ukoo wenye kuarifiwa vibaya, serikali, wanadini

• Kuwashawishi kufanya yasiyo ya adili katika jamii ya leo yenye kuendekeza

• Kusitawisha kiburi cha cheo, mali, kabila, taifa

• Kujaribu kuwafanya wapende anasa kuliko kupenda Mungu—wajishughulishe na tafrija

• Kuendeleza mafundisho ya kutosadiki kuwako kwa Mungu, ya mageuzi

• Kusingizia Ukristo wa kweli kwa kutumia ufalme-bandia wenye ukafiri wa Jumuiya ya Wakristo

• Kutokeza walimu wa uongo ili kupanda mashaka kati ya Wakristo wa kweli na kuwavunja moyo kwa werevu

TUNAWEZA KUSHINDA ULIMWENGU WA SHETANI KWA IMANI YETU

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki