Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • jv sura 4 kur. 33-41
  • Ule Uasi-imani Mkubwa Wasitawi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ule Uasi-imani Mkubwa Wasitawi
  • Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Watakuwako Walimu Wasio wa Kweli Miongoni Mwenu”
  • ‘Hivi Sasa Inatenda Kazi’
  • Makasisi na Watu wa Kawaida
  • Mafundisho ya Kipagani Yapenyeza Ndani
  • Tumaini la Ufalme Lafifia
  • Yale Mapinduzi Makubwa ya Kidini—Je, Ni Kurudia Ibada ya Kweli?
  • Jitihada za Kukaa Macho
  • Enzi ya “Kuangaziwa Nuru ya Elimu” na ya Ukuzi wa Viwanda
  • Jinsi Tazamio la Kikristo Lilivyofifia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Uasi-Imani—Njia ya Kwenda Kwa Mungu Yazibwa
    Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu
  • Ufalme Bandia Watokea
    “Ufalme Wako Uje”
  • Je, Mababa wa Kanisa Walikuwa Watetezi wa Kweli ya Biblia?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
Pata Habari Zaidi
Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
jv sura 4 kur. 33-41

Sura ya 4

Ule Uasi-imani Mkubwa Wasitawi

“BWANA mmoja, imani moja.” (Efe. 4:5, NW) Mtume Paulo alipoandika maneno hayo chini ya upulizio wa roho (kama 60-61 W.K.), kulikuwa imani moja tu ya Kikristo. Hata hivyo, leo twaona wingi wa madhehebu, mafarakano ya kidini, na viibada ambavyo hudai kuwa vya Kikristo, ingawa hufundisha mafundisho yanayohitilafiana na kushika viwango tofauti vya mwenendo. Lo, ni tofauti kubwa kama nini na lile kutaniko moja la Kikristo lenye muungamano lililoanza siku ya Pentekoste 33 W.K.! Migawanyiko hiyo ilitokeaje? Ili kupata jibu, ni lazima turudi nyuma kwenye karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida wetu.

Tangu palepale mwanzoni, Mpinzani, Shetani, alijaribu kunyamazisha ushuhuda wa mashahidi wa Kikristo wa Yehova kwa kuleta mnyanyaso juu yao kutoka kwa wale walio nje ya kutaniko. (1 Pet. 5:8) Kwanza ulikuja kutoka kwa Wayahudi halafu kutoka kwa Milki ya Roma ya Wasio-Wayahudi. Wakristo wa mapema walifanikiwa kuvumilia namna zote za upinzani. (Linganisha Ufunuo 1:9; 2:3, 19.) Lakini Mpinzani huyo hakukubali kushindwa. Ikiwa hangeweza kuwanyamazisha kwa mkazo kutoka kwa wale walio nje, mbona asiwafisidi kutoka ndani? Kutaniko la Kikristo lilipokuwa lingali changa, kuwapo kwalo kwenyewe kulitishwa na adui wa kindani—uasi-imani.a

Hata hivyo, uasi-imani haukupenya ndani ya kutaniko bila onyo la mapema. Akiwa Kichwa cha kutaniko, Kristo alihakikisha kwamba wafuasi wake walionywa mapema.—Kol. 1:18.

“Watakuwako Walimu Wasio wa Kweli Miongoni Mwenu”

“Iweni wenye kulinda,” Yesu akatahadharisha, “kuhusu manabii wasio wa kweli ambao huja kwenu katika mavazi ya kondoo.” (Mt. 7:15, NW) Yesu alijua kwamba Shetani angejaribu kugawanya na kufisidi wafuasi Wake. Hivyo kuanzia mapema katika huduma yake, aliwaonya juu ya walimu bandia.

Walimu bandia hao wangetoka wapi? “Kutoka miongoni mwenu nyinyi wenyewe,” akasema mtume Paulo kama 56 W.K., alipokuwa akisema kwa waangalizi wa Efeso. Ndiyo, kutoka ndani ya kutaniko, wanaume ‘wangeinuka na kusema mambo yaliyopotoka, ili kuvuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.’ (Mdo. 20:29, 30, NW) Waasi-Imani hao wenye kujitafutia faida zao wenyewe hawangetosheka kufanya wanafunzi wao wenyewe; wangejitahidi ‘kuwavuta hao wanafunzi,’ yaani, wanafunzi wa Kristo.

Mtume Petro (kama 64 W.K.) alitabiri pia ufisadi wa kindani na hata akaeleza njia ambayo waasi-imani hao wangeendesha shughuli: ‘Watakuwako walimu wasio wa kweli miongoni mwenu. Hawahawa wataleta ndani kimya-kimya mafarakano yenye kuangamiza. Kwa tamaa watawatumia nyinyi kujifaidi kwa maneno bandia.’ (2 Pet. 2:1, 3, NW) Kama wajasusi au wasaliti katika kambi ya adui, walimu hao wasio wa kweli, wajapotoka ndani ya kutaniko, wangepenyeza maoni yao yanayofisidi kwa njia ya siri au iliyojificha.

Maonyo hayo ya Yesu na mitume wake hayakuwa ya bure. Upinzani wa kindani ulikuwa na mianzo midogo, lakini ulichomoza mapema katika kutaniko la Kikristo.

‘Hivi Sasa Inatenda Kazi’

Miaka inayopungua 20 baada ya kifo cha Yesu, mtume Paulo alionyesha kwamba jitihada za Shetani kusababisha mgawanyiko na kugeuza wanadamu mbali kutoka kwenye imani ya kweli zilikuwa ‘tayari zafanya kazi.’ (2 The. 2:7) Mapema sana kama 49 W.K., katika barua moja iliyopelekwa kwa makutaniko, baraza lenye kuongoza liliandika hivi: “Tumesikia kwamba baadhi ya waliotoka miongoni mwetu wamesababishia nyinyi taabu kwa maneno mengi, wakijaribu kupindua nafsi zenu ijapokuwa sisi hatukuwapa maagizo yoyote.” (Mdo. 15:24) Hivyo basi watu fulani ndani ya kutaniko walikuwa na sauti kubwa juu ya maoni yao yenye kupinga—katika kisa hiki ikiwa kwa wazi ni juu ya suala la kama Wakristo Wasio-Wayahudi walihitaji kutahiriwa na kushika Sheria ya Musa.—Mdo. 15:1, 5.

Kadiri karne ya kwanza ilivyosonga mbele, fikira ya mgawanyiko ilienea kama donda ndugu. (Linganisha 2 Timotheo 2:17.) Karibu 51 W.K., watu fulani katika Thesalonike walikuwa wakitabiri kimakosa kwamba “kuwapo” kwa Bwana Yesu kulikuwa karibu sana. (2 The. 2:1, 2, NW) Kufikia kama 55 W.K., watu fulani katika Korintho walikuwa wamekataa fundisho la Kikristo la wazi kuhusu ufufuo wa wafu. (1 Kor. 15:12) Karibu 65 W.K., wengine walisema kwamba tayari ufufuo ulikuwa umetukia, ukiwa ni wa aina ya ufananisho ambayo Wakristo wenye kuishi hupata.—2 Tim. 2:16-18.

Hakuna maandishi yoyote yaliyopuliziwa ambayo huonyesha yaliyotukia ndani ya kutaniko la Kikristo wakati wa miaka 30 iliyofuata. Lakini kufikia wakati ambapo mtume Yohana aliandika barua zake (kama 98 W.K.), kulikuwa na “wapinga-Kristo wengi”—watu waliokana kwamba “Yesu ndiye Kristo” na kwamba Yesu ndiye Mwana wa Mungu aliyekuja “akiwa mwili.”—1 Yoh. 2:18, 22; 4:2, 3.

Kwa miaka zaidi ya 60, mitume walikuwa ‘wametenda wakiwa kizuizi,’ wakijitahidi kuzuia lile wimbi la uasi-imani. (2 The. 2:7, NW; linganisha 2 Yohana 9, 10.) Lakini kutaniko la Kikristo lilipokuwa karibu kuingia katika karne ya pili, mtume wa mwisho kuwa hai, Yohana, alikufa kama 100 W.K. Uasi-imani uliokuwa umeanza kupenya polepole ndani ya kutaniko sasa ulikuwa tayari kuzuka bila kuzuiwa, ukiwa na matokeo yenye kuharibu sana kitengenezo na kimafundisho.

Makasisi na Watu wa Kawaida

“Nyinyi nyote ni akina ndugu,” Yesu alikuwa amewaambia wanafunzi wake. “Kiongozi wenu ni mmoja, Kristo.” (Mt. 23:8, 10) Hivyo basi hakukuwako jamii ya makasisi ndani ya makutaniko ya Kikristo ya karne ya kwanza. Wakiwa ndugu wa Kristo watiwa-mafuta kwa roho, Wakristo wote wa mapema walikuwa na tazamio la kuwa makuhani wa kimbingu pamoja na Kristo. (1 Pet. 1:3, 4; 2:5, 9) Kwa habari ya tengenezo, kila kutaniko lilisimamiwa na baraza la waangalizi, au wazee wa kiroho.b Wazee wote walikuwa na mamlaka sawa, na hakuna yeyote wao aliyepewa mamlaka ya ‘kupiga ubwana’ juu ya kundi lililo katika utunzaji wao. (Mdo. 20:17; Flp. 1:1; 1 Pet. 5:2, 3) Hata hivyo, kadiri uasi-imani ulivyofunuka wazi, mambo yalianza kubadilika—kwa haraka.

Miongoni mwa mikengeuko ya mapema kabisa kulikuwa na kutenganishwa kwa maneno “mwangalizi” (Kigiriki, e·piʹsko·pos) na “mwanamume mzee,” au “mzee” (Kigiriki, pre·sbyʹte·ros), hivi kwamba maneno hayo hayakutumiwa tena kurejezea cheo kilekile kimoja cha daraka. Mwongo mmoja hivi baada ya kifo cha mtume Yohana, Ignatius, “askofu” wa Antiokia, katika barua yake kwa Wasmirna, aliandika hivi: “Hakikisheni kwamba mwamfuata askofu [mwangalizi], kama Yesu Kristo amfuatavyo Baba, na presbiteri [baraza la wanaume wazee] kama kwamba mnafuata wale Mitume.” Hivyo Ignatius alitetea maoni ya kwamba kila kutaniko lapasa kusimamiwa na askofu mmoja,c au mwangalizi, ambaye alipaswa kutambuliwa kuwa tofauti, na mwenye mamlaka kubwa kuliko, wapresbiteri, au wanaume wazee.

Ingawa hivyo, kutenganishwa huko kulitokeaje? Augustus Neander katika kitabu chake, The History of the Christian Religion and Church, During the Three First Centuries, aeleza wazi lililotukia: “Katika karne ya pili . . . , ni lazima iwe ndipo cheo cha sasa cha msimamizi mkuu wa kuchaguliwa wa wapresbiteri kilipofanyizwa, ambaye, kwa sababu ndiye hasa aliyekuwa na uangalizi wa kila kitu, alipewa lile jina la [e·piʹsko·pos], na hapo akatofautishwa na wale wapresbiteri wengine wote.”

Hivyo msingi uliwekwa ili jamii ya makasisi iibuke hatua kwa hatua. Karibu karne moja baadaye, Cyprian, “askofu” wa Carthage, Afrika Kaskazini, alikuwa mtetezi imara wa mamlaka ya maaskofu—kuwa kikundi tofauti na wapresbiteri (ambao baadaye walijulikana kuwa makuhani au mapadrid), na mashemasi, na watu wa kawaida. Lakini yeye hakupendelea umashuhuri wa askofu mmoja juu ya wengine.e

Kwa kadiri maaskofu na wapresbiteri walivyopanda daraja la vyeo vya jamii ya makasisi, waliwaacha chini ya daraja hilo wale waamini wengine wote katika kutaniko. Hiyo ilitokeza mtengano kati ya makasisi (wale wenye kuongoza) na watu wa kawaida (jamii ya waamini wenye kujikalia kitako tu). Chaeleza hivi Cyclopedia ya McClintock na Strong: “Kuanzia wakati wa Cyprian [aliyekufa kama 258 W.K.], yule baba wa mfumo wa jamii ya makasisi, daraja tofauti la makasisi na watu wa kawaida lilipata kuwa wazi, na upesi sana likakubaliwa na wote. Kwa kweli, kuanzia karne ya tatu na kuendelea, neno clerus . . . ni kama lilitumiwa kabisakabisa kuhusu wahudumu ili kuwatofautisha na watu wa kawaida. Kwa kadiri jamii ya makasisi ya Kiroma ilivyositawishwa, makasisi walikuja kuwa si daraja tofauti tu . . . bali pia walitambuliwa kuwa ndio ukuhani au upadri pekee.”

Hivyo, katika muda wa miaka 150 hivi tangu kifo cha aliye wa mwisho kati ya mitume, mabadiliko mawili makubwa ya kitengenezo yalipenya ndani ya kutaniko: Kwanza, kutenganishwa kwa askofu na wapresbiteri, huku askofu akikalia cheo cha juu cha lile daraja la jamii ya makasisi; pili, kutenganishwa kwa makasisi na watu wa kawaida. Badala ya waamini wote waliozaliwa kwa roho kujumlika kuwa “ukuhani wa kifalme,” sasa makasisi “walitambuliwa kuwa ndio ukuhani au upadri pekee.”f—1 Pet. 2:9.

Mabadiliko ya jinsi hiyo yalionyesha kuacha kwa njia ya Kimaandiko ya kusimamia makutaniko katika siku za mitume. Ingawa hivyo, si mabadiliko ya kitengenezo tu yaliyokuwa matokeo ya uasi-imani.

Mafundisho ya Kipagani Yapenyeza Ndani

Mafundisho safi ya Kristo yamo katika maandishi—yamehifadhiwa katika Maandiko Matakatifu. Kwa kielelezo, Yesu alifundisha wazi kwamba Yehova ndiye “Mungu pekee wa kweli” na kwamba nafsi ya kibinadamu yaweza kufa. (Yn. 17:3; Mt. 10:28, NW) Hata hivyo, mitume walipokufa na muundo wa kitengenezo ukadhoofika, mafundisho hayo yaliyo wazi yalifisidiwa kwa kadiri mafundisho ya kipagani yalivyopenyeza ndani ya Ukristo. Jambo kama hilo lingeweza kutokeaje?

Sababu moja kuu ilikuwa ule uvutano wenye hila wa falsafa ya Kigiriki. Chaeleza hivi The New Encyclopædia Britannica: “Kuanzia katikati ya karne ya 2 WK Wakristo waliokuwa na mazoezi fulani katika falsafa ya Kigiriki walianza kuhisi uhitaji wa kueleza imani yao kulingana na mitajo ya falsafa hiyo, ili kutosheleza akili zao wenyewe na pia ili kuongoa wapagani walioelimishwa.” Mara watu wenye mawazo ya kufuata falsafa walipokuja kuwa Wakristo, haikuchukua muda mrefu kabla ya falsafa ya Kigiriki na ule uitwao eti “Ukristo” kuungana kwa njia isiyotenganika.

Tokeo la muungano huo ni kwamba, mafundisho ya kipagani kama vile Utatu na kutokufa kwa nafsi yalipenyeza polepole yakaingia katika Ukristo uliochafuliwa. Hata hivyo, mafundisho hayo yarudi nyuma mbali sana kupita wanafalsafa Wagiriki. Kwa kweli Wagiriki waliyapata kutokana na tamaduni za zamani zaidi, kwa maana kuna uthibitisho wa kwamba mafundisho hayo yalikuwa katika dini za kale za Kimisri na Kibabiloni.

Kwa kadiri mafundisho ya kipagani yalivyoendelea kupenyeza ndani ya Ukristo, mafundisho mengine ya Kimaandiko yalipotoshwa pia au yakaachiliwa mbali.

Tumaini la Ufalme Lafifia

Wanafunzi wa Yesu walijua sana kwamba ilikuwa lazima wakae macho wakitazamia “kuwapo” kwa Yesu kulikoahidiwa na kuja kwa Ufalme wake. Baada ya muda ilifahamiwa kwamba Ufalme huo utatawala juu ya dunia kwa miaka elfu na kuigeuza iwe paradiso. (Mt. 24:3; 2 Tim. 4:18; Ufu. 20:4, 6, NW) Waandikaji wa Biblia Wakristo waliwasihi mashahidi wa karne ya kwanza waendelee kuwa macho kiroho na kuendelea kujitenga na ulimwengu. (Yak. 1:27; 4:4; 5:7, 8; 1 Pet. 4:7) Lakini mara mitume walipokufa, taraja la Kikristo la kuwapo kwa Kristo na kuja kwa Ufalme wake lilififia. Kwa nini?

Sababu moja ilikuwa kuchafuliwa kiroho kulikosababishwa na fundisho la Kigiriki la kutokufa kwa nafsi. Kwa kadiri lilivyotia mizizi miongoni mwa Wakristo, tumaini la mileani liliachiliwa hatua kwa hatua. Kwa nini? The New International Dictionary of New Testament Theology chaeleza hivi: “Fundisho la kutokufa kwa nafsi liliingia kuchukua mahali pa eskatolojia [fundisho juu ya “Mambo ya Mwisho”] ya AJ [Agano Jipya] pamoja na tumaini layo la ufufuo wa wafu na uumbaji upya (Ufu. 21 mistari inayofuata), hivi kwamba nafsi hupokea hukumu baada ya kifo na hufikia paradiso ambayo sasa hufikiriwa kuwa ya ulimwengu mwingine.” Yaani, Wakristo waasi-imani walifikiri kwamba nafsi iliendelea kuwa hai baada ya mwili kufa na kwamba kwa hiyo baraka za Utawala wa Mileani wa Kristo lazima ziwe zahusiana na makao ya roho. Hivyo walihamisha Paradiso kutoka duniani hadi mbinguni, ambako, wao waliamini, ndiko nafsi iliyookolewa huenda wakati wa kufa. Basi, hakukuwa na uhitaji wa kuwa macho kutazamia kuwapo kwa Kristo na kuja kwa Ufalme wake, kwa kuwa wakati wa kufa wote walitumaini kujiunga na Kristo mbinguni.g

Ingawa hivyo, kwa kweli sababu nyingine ilifanya ionekane kuwa ni kazi bure kukaa macho kutazamia kuja kwa Ufalme wa Kristo. The New Encyclopædia Britannica yaeleza hivi: “Ule [uonekanao kuwa] ukawivu wa Parousia ulitokeza kudhoofika kwa taraja lililokaribia sana [utimizo] la kanisa la mapema. Katika utaratibu huo wa ‘kuondoa eskatolojia’ [kudhoofisha lile fundisho juu ya “Mambo ya Mwisho”], kanisa lililopangwa kitengenezo lilizidi kuchukua mahali pa Ufalme wa Mungu uliotarajiwa. Kufanyizwa kwa Kanisa Katoliki kuwa mpango wa jamii ya makasisi kwahusiana moja kwa moja na kuzorota kwa lile taraja linalokaribia sana [utimizo].” (Italiki ni zetu.) Hivyo basi, si kwamba tu baraka za mileani zilihamishwa kutoka duniani hadi mbinguni bali pia Ufalme ulihamishwa kutoka mbinguni hadi duniani. “Uhamisho” huo ulikamilishwa na Augustine wa Hippo (354-430 W.K.). Katika kitabu chake maarufu The City of God (Jiji la Mungu), yeye alitaarifu hivi: “Kanisa hata sasa ndilo ufalme wa Kristo, na ndilo ufalme wa mbinguni.”

Kwa sasa, katika kama 313 W.K., wakati wa utawala wa Maliki Mroma Konstantino, Ukristo ambao kufikia hapo ulikuwa umekuwa na fikira ya uasi-imani kwa kadiri kubwa, ulipewa utambuzi wa kisheria. Viongozi wa kidini walikuwa tayari kuingizwa katika utumishi wa Taifa, na hapo kwanza Taifa ndilo lililodhibiti mambo ya kidini. (Muda si muda, dini ingedhibiti mambo ya Taifa.) Hivyo ndivyo Jumuiya ya Wakristoh ilivyoanza, sehemu yayo (dini ya Katoliki) baadaye ikija kuwa ndiyo dini rasmi ya Taifa ya Roma. Sasa, ule “ufalme” haukuwa katika ulimwengu tu bali pia ulikuwa sehemu ya ulimwengu. Lo! ni tofauti kubwa kama nini na Ufalme ambao Kristo alihubiri!—Yn. 18:36.

Yale Mapinduzi Makubwa ya Kidini—Je, Ni Kurudia Ibada ya Kweli?

Kama magugu yenye kusitawi miongoni mwa ngano iliyosongwa, Kanisa la Roma, likiwa chini ya mtawala walo wa kipapa, lilitawala mambo ya kilimwengu kwa karne nyingi. (Mt. 13:24-30, 37-43) Kadiri lilivyozidi kuwa sehemu ya ulimwengu, ndivyo kanisa lilivyozidi kuondoka mbali na Ukristo wa karne ya kwanza. Muda wa karne hizo, mafarakano yaitwayo eti “ya uzushi” yaliitisha marekebisho ndani ya kanisa, lakini kanisa likaendelea kutumia vibaya mamlaka na kujikusanyia utajiri mwingi. Halafu, katika karne ya 16, Mapinduzi Makubwa ya Kidini ya Protestanti, yaliyokuwa uasi wa kidini, yalifyatuka kwa nguvu nyingi.

Wanamapinduzi kama vile Martin Luther (1483-1546), Ulrich Zwingli (1484-1531), na John Calvin (1509-1564) walishambulia kanisa juu ya masuala mbalimbali: Luther kuhusu kuuzwa kwa hati za rehema, Zwingli kuhusu useja wa makasisi na ibada ya Mariamu, na Calvin kuhusu uhitaji wa kanisa kurudia zile kanuni za awali za Ukristo. Jitihada hizo zilitimiza nini?

Kwa kweli, yale Mapinduzi Makubwa ya Kidini yalitimiza mema fulani, hasa kutafsiriwa kwa Biblia katika lugha za watu wa kawaida. Roho isiyozuiwa ya yale Mapinduzi Makubwa ya Kidini iliongoza kwenye utafiti ulio halisi zaidi wa Biblia na uelewevu ulioongezeka wa lugha za Biblia. Hata hivyo, yale Mapinduzi Makubwa ya Kidini hayakuwa ishara ya kurudia ibada na fundisho la kweli.i Kwa nini sivyo?

Matokeo ya uasi-imani yalikuwa yamepenya sana, hadi misingi yenyewe ya Jumuiya ya Wakristo. Hivyo, ingawa vikundi mbalimbali vya Protestanti vilijitenga vikawa huru na mamlaka ya kipapa ya Roma, vilichukua baadhi ya kasoro za msingi za Kanisa la Katoliki la Roma, mambo yaliyotokana na kuachilia mbali Ukristo wa kweli. Kwa kielelezo, ingawa hali ya kusimamia makanisa ya Protestanti ilitofautiana kidogo, mgawanyiko wa msingi wa kanisa katika jamii ya makasisi wenye kutawala na watu wa kawaida wenye kutiishwa ulidumishwa. Yaliyodumishwa pia yalikuwa mafundisho yasiyo ya Kimaandiko kama vile Utatu, nafsi isiyoweza kufa, na mateso ya milele baada ya kifo. Na kama vile Kanisa la Kiroma, makanisa ya Protestanti yaliendelea kuwa sehemu ya ulimwengu, yakijihusisha sana na mifumo ya kisiasa na jamii za walio mashuhuri wenye kutawala.

Kwa wakati huohuo, namna gani juu ya taraja la Kikristo—kuwa macho kutazamia kuwapo kwa Yesu na kuja kwa Ufalme wake? Kwa karne kadhaa baada ya yale Mapinduzi makubwa ya Kidini, makanisa—ya Katoliki na ya Protestanti pia—yalijitia sana katika mamlaka ya kilimwengu nayo yakaelekea kuahirisha mataraja ya kuja kwa Ufalme wa Kristo.

Jitihada za Kukaa Macho

Ingawa hivyo, katika karne ya 19 hali-hewa ya kidini iliongoza kwenye jitihada za kukaa macho kwa Kikristo. Kama tokeo la utafiti wa Biblia kwa upande wa makasisi fulani na wasomi wa Biblia, mafundisho kama vile nafsi isiyoweza kufa, mateso ya milele baada ya kifo, kuamulia watu kimbele mwisho wao, na Utatu yalichunguzwa upya. Kwa kuongezea, wanafunzi fulani wa Biblia walikuwa wakichunguza sana unabii mbalimbali wa Biblia unaohusu siku za mwisho. Kwa hiyo, vikundi mbalimbali vya watu vilianza kufikiri kwa uzito juu ya kurudi kulikoahidiwa kwa Bwana.—Mt. 24:3.

Katika Marekani, William Miller alitabiri kurudi kwa Kristo katika umbo lenye kuonekana katika 1843 au 1844. Msomi wa kidini Mjerumani J. A. Bengel aliiweka tarehe hiyo kuwa 1836; wafuasi wa Irving katika Uingereza walitazamia 1835 kwanza, halafu 1838, 1864, na 1866. Kulikuwa na kikundi cha Wamennoni katika Urusi ambacho kwanza kilitazamia 1889, halafu 1891.

Jitihada hizo za kuendelea kukaa macho zilitumika kuamsha wengi kwenye tazamio la kurudi kwa Bwana wetu. Hata hivyo, jitihada hizo za kukaa macho kwa Kikristo ziliishia katika kukata tamaa. Kwa nini? Sanasana, ni kwa sababu vikundi hivyo vilitegemea mno wanadamu badala ya Maandiko kwa kadiri ya kutosha. Baada ya miongo michache, vingi vya vikundi hivyo vilififia vikatokomea.

Kwa sasa, wakati wa kipindi hiki matukio mengine yalikuwa na matokeo mazito juu ya matumaini na mataraja ya kibinadamu.

Enzi ya “Kuangaziwa Nuru ya Elimu” na ya Ukuzi wa Viwanda

Katika 1848, Karl Marx na Friedrich Engels walitangaza The Communist Manifesto. Badala ya kuendeleza dini, ambayo Marx aliiita “kasumba ya watu,” waliendeleza imani ya kutokuwako kwa Mungu. Ingawa kijuujuu walionekana kuwa wapinzani dhidi ya dini yote, kwa kweli waliiendeleza dini, au ibada, ya Taifa na viongozi walo.

Karibu mwongo mmoja baadaye, katika 1859, kitabu cha Charles Darwin Origin of Species kilitangazwa; kiliongoza sana fikira ya wakati huo ya kisayansi na ya kidini. Nadharia za mageuzi ziliongoza kwenye kupinga ukweli wa masimulizi ya Biblia juu ya uumbaji na juu ya kuingia kwa dhambi kupitia kutotii kwa wanadamu wa kwanza wawili. (Mwa., sura ya 1-3) Tokeo ni kwamba, imani ya wengi katika Biblia ilidhoofishwa.

Kwa sasa, vuvumko kubwa la viwanda lilikuwa linaendelea na kutia fora. Mkazo uliacha kutiwa kwenye kilimo ukawa kwenye ukuzi wa viwanda na utengenezaji wa mashine. Kutokezwa kwa garimoshi la mvuke (mapema karne ya 19) kulikuwa kukiongoza kwenye mpanuko wa reli za kotekote nchini. Nusu ya pili ya karne ya 19 iliona kuvumbuliwa kwa simu ya mdomo (1876), gramafoni (kinanda) (1877), taa ya umeme (1878-1879), pamoja na matumizi ya Linotaipu katika kutokeza mistari ya herufi-chapa kwa ajili ya kupiga chapa (1884).

Wanadamu walikuwa wakiingia katika kipindi cha usitawi ulio mkubwa zaidi wa usafiri na uwasiliano wa haraka sana katika historia. Ingawa manufaa hizo zingetumiwa kusogeza mbele makusudi ya kibiashara na ya kisiasa, zingekuwapo pia kwa matumizi ya mambo ya kidini. Hivyo msingi ukawekwa ili uanzilishi mdogo ufanywe na kikundi kidogo cha wanafunzi wa Biblia ambao ungekuwa na matokeo ulimwenguni pote.

[Maelezo ya Chini]

a Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, nomino “uasi-imani” (Kigiriki, a·po·sta·siʹa) ina maana ya “kuondoka katika, kuachilia mbali au uasi.” (Mdo. 21:21, NW, kielezi-chini) Hapo hasa linarejezea kuacha njia kidini; kujiondoa kutoka kwenye ibada ya kweli au kuiachilia mbali.

b Katika Maandiko maneno “mwangalizi” na “mwanamume mzee,” au “mzee,” hurejezea cheo kilekile kimoja. (Mdo. 20:17, 28, NW; Tito 1:5, 7, NW) “Mwanamume mzee” huonyesha sifa za ukomavu za yule ambaye huwekwa rasmi hivyo, na “mwangalizi” huonyesha daraka lililo asili ya kuwekwa rasmi huko—kuangalia masilahi za watu wale waliokabidhiwa kwenye utunzaji wake.

c Neno la Kiingereza “bishop” (askofu) hutokana na neno la Kigiriki e·piʹsko·pos (“mwangalizi”) kama ifuatavyo: kutokana na neno bisshop la Kiingereza cha Enzi ya Katikati, lililotokana na neno bisceop la Kiingereza cha Zamani, lililotokana na neno biscopus, la Kilatini cha watu wa kawaida, ambalo ni namna tofauti ya neno episcopus la Kilatini cha Baadaye, lililotokana na neno la Kigiriki e·piʹsko·pos.

d Neno la Kiingereza “priest” (kuhani au padri) latokana na pre·sbyʹte·ros (“mwanamume mzee,” au “mzee”) kama ifuatavyo: kutokana na neno pre(e)st la Kiingereza cha Enzi ya Katikati, lililotokana na neno prēost la Kiingereza cha Zamani, lililotokana na neno prester la Kilatini cha watu wa kawaida, lililofupishwa kutokana na neno presbyter la Kilatini cha Baadaye, lililotokana na pre·sbyʹte·ros la Kigiriki.

e Baada ya muda askofu wa Roma, ambaye alidai kuwa mwandamizi wa Petro, alifikiriwa kuwa ndiye askofu mkuu zaidi na papa.—Ona Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu, kilichotangazwa (katika Kiingereza) na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., 1990, kurasa 270-272.

f Kwa kupendeza, Dakt. Neander aonelea hivi: “Mkataa bandia ulifikiwa, kwamba kwa kuwa katika Agano la Kale mlikuwa mmekuwamo ukuhani wenye kuonekana uliohusishwa na utendaji wa jamii hususa ya wanaume, ni lazima pia uwemo katika lile [Agano] Jipya . . . Ule ulinganisho bandia wa ukuhani au upadri ule wa Kikristo na ukuhani wa Kiyahudi uliendeleza tena mwinuko wa uepiskopo juu ya cheo cha wapresbiteri.”—The History of the Christian Religion and Church, kilichotafsiriwa na Henry John Rose, Chapa ya Pili, New York, 1848, uku. 111.

g Maoni hayo hudhania kimakosa kwamba wakati wa kifo Wakristo wote huenda mbinguni. Hata hivyo, Biblia hufundisha kwamba watu 144,000 tu ndio huitwa wakatawale pamoja na Kristo mbinguni. (Ufu. 7:4-8; 20:4-6) Wengine wasio na hesabu wanaweza kuwa na tumaini la uhai wa milele katika dunia paradiso chini ya Ufalme wa Kristo.—Mt. 6:10; Ufu. 7:9, 15.

h Kama ulivyotumiwa katika kichapo hiki, mtajo “Jumuiya ya Wakristo” hurejezea Ukristo wa kujidai tu, tofauti na ule Ukristo wa kweli wa Biblia.

i Kwa mazungumzo kamili zaidi juu ya Mapinduzi Makubwa ya Kidini na yale yaliyotimizwa, ona sura ya 13, “Yale Mapinduzi Makubwa ya Kidini—Jitihada ya Kutafuta Ilichukua Mgeuko Mpya,” katika kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu.

[Blabu katika ukurasa wa 33]

Wakati kutaniko la Kikristo lilipokuwa lingali changa, lilitishwa na uasi-imani

[Blabu katika ukurasa wa 34]

Upinzani wa kindani ulikuwa na mianzo midogo

[Blabu katika ukurasa wa 37]

Si kwamba tu waasi-imani walihamisha baraka za mileani kutoka duniani hadi mbinguni bali walihamisha Ufalme pia kutoka mbinguni hadi duniani

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 36]

Plato na “Ukristo”

Mwanafalsafa Mgiriki Plato (aliyezaliwa kama 428 K.W.K.) hakuwa na njia ya kujua kwamba hatimaye mafundisho yake yangepata njia ya kuingia ndani ya Ukristo ulioasi imani. Mambo makuu ambayo Plato aliuchangia “Ukristo” yalihusu mafundisho ya Utatu na kutokufa kwa nafsi.

Mawazo ya Plato juu ya Mungu na asili yalikuwa na uvutano juu ya fundisho la Utatu la Jumuiya ya Wakristo. Chaeleza hivi “Nouveau Dictionnaire Universel”: “Utatu wa Kiplato, wenyewe ukiwa ni mpango mpya tu wa utatu-utatu mwingi wa kale zaidi wenye kurudi nyuma kwenye watu wa mapema kabisa, huonekana kuwa ni utatu wa maelezo ya akili ya kifalsafa ya sifa zilizozaa nyutu tatu au watu wa kimungu wanaofundishwa na makanisa ya Kikristo. . . . Wazo hili la mwanafalsafa Mgiriki la utatu wa kimungu . . . laweza kupatikana katika dini zote za kale [za kipagani].”—Buku la 2, ukurasa 1467.

Kuhusu fundisho la nafsi isiyoweza kufa, “New Catholic Encyclopedia” yasema: “Dhana ya Kikristo ya nafsi ya kiroho iliyoumbwa na Mungu na kutiwa katika mwili wakati wa mtungo wa mimba ili kufanyiza mwanadamu kuwa kitu kizima kilicho hai ni tunda la usitawi wa muda mrefu wa falsafa ya Kikristo. Ni kupitia Origen tu [aliyekufa kama 254 W.K.] katika Mashariki na Mt. Augustine [aliyekufa 430 W.K.] katika Magharibi kwamba nafsi ikathibitishwa kuwa namna ya kiroho na dhana ya kifalsafa iliyofanyizwa kutoka asili yayo. . . . Fundisho lake [la Augustine] . . . lilikuwa na mambo mengi (kutia na makosa fulanifulani) kutokana na mawazo mapya ya Plato.”—Buku la 13, kurasa 452, 454.

[Picha katika ukurasa wa 35]

Cyprian, aliyekuwa “askofu” wa Carthage, aliwaona maaskofu kuwa jamii iliyotengana na wapresbiteri, mashemasi, na watu wa kawaida

[Picha katika ukurasa wa 38]

“Kanisa hata sasa ndilo ufalme wa Kristo, na ndilo ufalme wa mbinguni” (Augustine wa Hippo)

[Picha katika ukurasa wa 39]

Wanamapinduzi walioshambulia kanisa juu ya masuala mbalimbali

Martin Luther

John Calvin

Ulrich Zwingli

[Picha katika ukurasa wa 40]

“Communist Manifesto” ya Karl Marx kwa kweli iliendeleza ibada ya Taifa. Kitabu cha Charles Darwin “Origin of Species” kiliongoza sana fikira ya wakati huo ya kisayansi na ya kidini

[Picha katika ukurasa wa 41]

Garimoshi la mvuke

[Picha katika ukurasa wa 41]

Taa ya umeme

[Picha katika ukurasa wa 41]

Simu ya kwanza

[Picha katika ukurasa wa 41]

Linotaipu ya zamani

[Picha katika ukurasa wa 41]

Gramafoni (kinanda)

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki