Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 5/1 kur. 5-8
  • Jinsi Tazamio la Kikristo Lilivyofifia

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi Tazamio la Kikristo Lilivyofifia
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Jinsi Tazamio Lilivyofifia
  • Ulinzi Wakomeshwa
  • Giza la Karne ya Tano Mpaka Karne ya Kumi na Tano W.K.
  • Kupunguza Uzito wa Mambo kwa Uprotestanti
  • Matazamio ya Ukatoliki
  • Hali ya Kikristo ya Kufanya Ulinzi Haijafa
  • Wenye Furaha Ni Wale Wanaokutwa Wakilinda!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Ule Uasi-imani Mkubwa Wasitawi
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Umeenda Wapi Ulinzi wa Wakristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Endelea Kutarajia!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 5/1 kur. 5-8

Jinsi Tazamio la Kikristo Lilivyofifia

YESU aliwaambia wanafunzi wake ‘waendelee kulinda’ kwa ajili ya kuwapo kwake na kuja kwa Ufalme wake. (Marko 13:37, NW) Kuna ushahidi mwingi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kwamba Wakristo wa karne ya kwanza walifanya hivyo. Kwa kweli, wengine walikosa sana subira. (2 Wathesalonike 2:1, 2) Kwa upande mwingine, ili wazuie kudhoofika ko kote kwa tazamio la Kikristo, Paulo, Yakobo, Petro na Yohana waliandika barua ambamo katika hizo walitia moyo ndugu zao waendelee kukesha kiroho huku wakingojea kwa subira “kuwapo” kwa Kristo na “siku ya Yehova.”​—Waebrania 10:25, 37; Yakobo 5:7, 8, NW; 1 Petro 4:7, NW; 2 Petro 3:1-15, NW; 1 Yohana 2:18, 28.

Vitabu vya uchunguzi vilivyochapishwa na wanahistoria na wanatheolojia wa Jumuiya ya Wakristo vinakubali uhakika huo. Katika Supplément, yenye kuzungumza mambo kirefu, kitabu chenye mambo ya kutegemeka cha Kifaransa, Dictionnaire de la Bible ya Katoliki kinasema: “Ni kazi bure kujaribu kwa vyo vyote kukana kuwapo kwa hali ya kutazamia mwisho iliyo wazi katika mengi ya maandiko ya Agano Jipya. . . . Katika Ukristo wa kwanza . . . tazamio la Parousia [kuwapo] lina sehemu ya maana sana na linaendelea kuanzia upande mmoja wa Agano Jipya mpaka upande mwingine.”

Lakini ni kwa nini wanatheolojia wengine wa Jumuiya ya Wakristo wanajaribu “kwa vyo vyote kukana kuwapo kwa hali ya kutazamia mwisho” ambako kulikuwa wazi kati ya Wakristo wa kwanza? Bila shaka, ili kutetea hali ya usingizi iliyo wazi leo kati ya wengi wanaoitwa Wakristo ati, na pia kati ya viongozi wao wa kiroho. Badiliko hilo lilitokeaje?

Jinsi Tazamio Lilivyofifia

Kudhoofika kwa tazamio la Kikristo kulikuwa mojalapo la matokeo ya uasi wa imani yaliyokuwa yamekwisha anza kujionyesha hata kabla ya kufa kwa mitume wa Kristo. Mtume Paulo alionya kwamba uasi wa imani ulikuwa tayari ‘unatenda kazi’ ndani ya kundi la Kikristo katika siku zake. (2 Wathesalonike 2:3, 4, 7) Miaka michache baadaye, mtume Petro alitahadharisha Wakristo wenzake juu ya “waalimu wa uongo” na “wenye kudhihaki” ambao wangesema: “Iko wapi ahadi ile ya [kuwapo] kwake? Kwa maana, tangu hapo babu zetu walipolala, vitu vyote vinakaa hali iyo hiyo, tangu mwanzo wa kuumbwa.”​—2 Petro 2:1; 3:3, 4.

Kwa kupendeza, tazamio la Kikristo linalofaa lilidumishwa kwa wakati fulani na wale walioamini ukweli wa Kimaandiko kwamba “kuwapo” kwa Yesu kulikoahidiwa kutatangaza kukaribia kwa Utawala wa Miaka Elfu wake juu ya dunia. Yustini Mata (alikufa kama mwaka 165 W.K.) Aireniasi (alikufa kama mwaka 202 W.K.) na Tatuliano (alikufa baada ya mwaka 220 W.K.) wote waliamini Utawala wa Mileani wa Kristo na kupendekeza tazamio la bidii la mwisho wa mfumo mbovu wa mambo uliopo.

Kwa kadiri wakati ulivyopita na uasi wa imani ukasitawi, tumaini la mileani la dunia kubadilishwa iwe paradiso ya duniani pote chini ya Ufalme wa Kristo liliisha polepole kisha kukawa na tazamio la kuwazia ambalo msingi wake ulikuwa wazo la falsafa za Kigiriki la kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu. Tumaini la Paradiso lilihamishwa likawa la mbinguni badala ya duniani, tumaini ambalo lingetimizwa wakati wa kufa. Tazamio la Kikristo la parousia, au kuwapo kwa Kristo, na kuja kwa Ufalme wake vikadhoofika. ‘Kwa nini kuwapo kwa Kristo kutazamiwe kwa bidii,’ ndivyo walivyowaza ‘ikiwa unaweza kutumaini kujiunga na Kristo mbinguni wakati wa kufa?’

Kufifia huko kwa ulinzi wa Wakristo, kuliwasukuma Wakristo waasi-imani wajifanye tengenezo la kanisa lenye kuundwa vizuri ambalo halikukaza macho tena kwenye kuja kwa parousia, au kuwapo kwa Kristo, bali kwenye kutawala washiriki walo na, ikiwezekana, ulimwengu. Kitabu The Encyclopædia Britannica kinasema: “[Kulikoelekea kuwa] kuchelewa kwa Parousia kulitokeza kudhoofika kwa tazamio hilo lenye kukaribia katika kanisa la kwanza. Katika tukio hilo la kudhoofika kwa fundisho la mambo ya mwisho, kanisa hilo lililoundwa lilizidi kuchukua mahali pa Ufalme wa Mungu uliotazamiwa. Kufanyizwa kwa Kanisa Katoliki likiwa muundo wa kitawala kunahusiana moja kwa moja na kufifia kwa tazamio hilo lenye kukaribia.”

Ulinzi Wakomeshwa

Bila shaka “Baba,” au “mwalimu” wa kanisa aliyekomesha kukaa kwa Wakristo wakiwa wanalinda ni Augustino wa Hippo (354-430 W.K.). Katika kitabu chake kinachojulikana sana The City of God, Augustino alisema: “Kanisa sasa duniani ndilo ufalme wa Kristo na ufalme wa mbinguni.”

Kitabu The New Bible Dictionary kinaeleza matokeo ya maoni hayo juu ya theolojia ya Katoliki, kikisema: “Katika theolojia ya Katoliki ya Roma jambo lenye kutofautisha ni kule kutambulisha ufalme wa Mungu na Kanisa katika hali yake ya kidunia kuwa kitu kimoja, kitambulisho ambacho kwa sehemu kubwa kililetwa na uvutano wa Augustino. Kupitia utawala wa viongozi wa kidini Kristo anafanywa kuwa Mfalme wa ufalme wa Mungu. Eneo la ufalme huo lina mipaka ile ile na uwezo wa mamlaka ya Kanisa. Ufalme wa mbinguni unapanuliwa wakati Kanisa linapotimiza mgawo wake na kusonga mbele ulimwenguni.”

Jambo hilo liliondoa lazima yote ya ‘kuendelea kulinda’ kwa ajili ya ishara ambayo ingeonyesha kwamba Ufalme wa Mungu ulikuwa karibu. Akiandika katika kitabu The New Encyclopædia Britannica, Profesa E. W. Benz anathibitisha hilo, akisema: “Yeye [Augustino] alipunguza uzito wa tazamio hilo la awali lililokaribia kwa kutangaza kwamba Ufalme wa Mungu tayari umeanza katika ulimwengu huu wakati wa kuundwa kwa kanisa; kanisa ndilo wakili wa kihistoria wa Ufalme wa Mungu Duniani. Ufufuo wa kwanza, kulingana na Augustino, unatokea daima ndani ya kanisa kwa namna ya sakramenti ya Ubatizo, ambayo kupitia hiyo waaminifu wanaingizwa kwenye Ufalme wa Mungu.”

Augustino pia ndiye aliyefanya hatua ya mwisho ya kuacha tumaini la Kimaandiko la Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu Kristo ambao kwa huo Yeye atarudisha Paradiso duniani. (Ufunuo 20:1-3, 6; 21:1-5) Kitabu The Catholic Encyclopedia kinakubali hivi: “Mt. Augustino hatimaye alishikilia usadikisho kwamba hakutakuwako mileani. . . . Sabato ya miaka elfu moja baada ya miaka elfu sita ya historia ni uzima wa milele wote; au, kwa maneno mengine, hesabu elfu moja imekusudiwa ionyeshe ukamilifu.” Ensaiklopedia kubwa Britannica (1977) inaongeza hivi: “Kwake [Augustino] mileani, ilikuwa imekuwa hali ya kiroho ambayo katika hiyo kanisa kwa ujumla lilikuwa limeingia katika Pentekoste. . . . Hakuna kujiingiza ko kote kwa mtu mwenye nguvu zinazopita zile za kibinadamu kulikotazamiwa kuwa ni karibu katika historia.” Kwa hiyo, kwa Wakatoliki, sala “ufalme wako uje” ikawa haina maana.

Giza la Karne ya Tano Mpaka Karne ya Kumi na Tano W.K.

Fasirio la Augustino, tunaambiwa, ‘likawa kiwango cha fundisho la kidini katika karne ya tano mpaka ya kumi na tano.’ Kwa hiyo, tazamio la Kikristo, likafifia sana. Tunasoma hivi: ‘Katika Jumuiya ya Wakristo ya karne ya tano mpaka ya kumi na tano, kupunguza uzito wa mambo ya mwisho kukatiwa mahali pake katika mfumo wa mafundisho ya kidini yasiyo na msingi ambayo mategemeo yayo ya kifalsafa kwanza yalikuwa ni mwanafalsafa Mgiriki Plato na, baadaye magharibi, kwa mwanafalsafa Mgiriki Aristotle. Mawazo ya kimapokeo juu ya parousia, ufufuo na kadhalika yaliunganishwa na mawazo ya Kigiriki juu ya nafsi na kutokufa kwayo. . . . Ukristo wa karne ya tano mpaka ya kumi na tano . . . [uliacha] nafasi ndogo tamaa ya kujua ni jambo lingepata wanadamu mwishowe. Lakini tamaa hiyo iliendelea kuwapo katika madhehebu fulani zenye kushikilia imani tofauti.’​—Encyclopædia Britannica, chapa ya 1970.

Kanisa la Katoliki ya Roma, linazungumza kwa njia yenye madharau kuhusu hizo “madhehebu fulani zenye kushikilia imani tofauti,” kwa kuziita “madhehebu za mileani.” Wanahistoria wa kanisa hilo wanazungumza kwa madharau juu ya “Woga Unaohusu Mwaka wa 1000.” Lakini lilikuwa kosa la nani kwamba wengi wa watu wa kawaida waliogopa kwamba ulimwengu ungekwisha mwaka wa 1000? “Woga” huo ulikuwa matokeo ya moja kwa moja ya theolojia ya Mkatoliki “Mtakatifu” Augustino. Alidai kwamba Shetani alifungwa wakati wa kuja kwa kwanza kwa Kristo. Kwa kuwa andiko la Ufunuo 20:3, 7, 8 linasema kwamba Shetani angefungwa kwa miaka 1,000 halafu ‘atafunguliwa ili awadanganye mataifa yote,’ haishangazi kwamba watu fulani katika karne ya kumi walikuwa wakiogopa yanayoweza kutokea mwaka wa 1,000.

Kama ilivyo, Kanisa rasmi la Katoliki ya Roma lililaani “woga” huo, kama lilivyomlaani Mtawa wa Cistercia Joakimu wa Flora, aliyetabiri mwisho wa kipindi cha Kikristo ungekuwa 1260. Mwishowe, mwaka wa 1516, kwenye Baraza la Tano la Latera, Papa Leo wa Kumi alikataza kirasmi Mkatoliki yeyote kutabiri wakati Mpinga-Kristo na Hukumu ya Mwisho vingekuja. Kuvunja sheria hiyo kungemletea mtu kizuizi cha kutengwa!

Kupunguza Uzito wa Mambo kwa Uprotestanti

Badiliko kuu la kanisa katika karne ya 16, kwa dai la kuirudia Biblia ati, lingalipaswa kutokeza tena tazamio la Kikristo na kwa muda lilifanya hivyo. Lakini katika jambo hilo, kama ilivyo katika mengi mengine, Badiliko hilo halikutimiza ahadi zalo. Halikuwa alama ya kurudia Ukristo wa kweli wa Biblia. Makanisa ya Uprotestanti yaliyotokezwa na Badiliko hilo yaliacha upesi kufanya ulinzi wa Kikristo kisha yakajipatanisha na ulimwengu wa wakati huu.

Tunasoma hivi: “Hata hivyo, upesi makanisa ya wakati wa Badiliko Kuu, yakawa mashirika ya maeneo [ya kitaifa], nayo yakafunika tazamio la wakati wa mwisho, na kwa hiyo fundisho la ‘mambo ya mwisho’ likawa baki la imani zisizo na msingi.” “Katika uhuru wa kidini uliotokezwa, sana-sana kati ya Waprotestanti na Wayahudi, kuelekea mwisho wa karne ya 18 mpaka ya 19, tazamio la mambo ya mwisho lilifutiliwa mbali. Lilionwa kuwa sehemu ya masalio yasiyofaa ya dini ya kimapokeo, yasiyonyooka ya kizamani ambayo hayangekubaliwa tena katika kizazi chenye elimu. Katika visa vingi, mawazo ya mambo ya mwisho yaliachwa kabisa, na [wazo] rahisi la kutokufa kwa nafsi baada ya kifo likatokezwa kuwa ndio mwisho wa mwanadamu. Wanatheolojia wengine walifasiri upya tazamio la Ufalme wa Mungu kwa njia ya kiadili, yenye ushirikina kwa kiasi fulani au ya kijamii.”​—Encyclopædia Britannica.

Kwa hiyo, badala ya kusaidia Wakristo ‘waendelee kulinda’ kwa ajili ya kuwapo kwa Kristo na kuja kwa Ufalme wa Mungu, wanatheolojia wa Uprotestanti wamepunguza uzito wa tazamio la Kikristo la kweli. Kwa wengi wao, “ufalme wa Mungu . . . ukaja kufikiriwa zaidi na zaidi katika maana ya kibinafsi; ni kuongozwa sana na neema na amani katika mioyo ya watu.” Kwa wengine, “kuja kwa ufalme kunatia hatua ya kusonga mbele ya uadilifu wa kijamii na usitawi wa jumuiya.”​—The New Bible Dictionary (ya Kiprotestanti).

Matazamio ya Ukatoliki

Angalau, Wakatoliki wangalipaswa wawe wanalinda kwa ajili ya kuwapo kwa Kristo. Ijapokuwa theolojia ya Augustino iliyokomesha tazamio la Ufalme na tumaini la mileani kwa Wakatoliki, imani za Kanisa la Roma zingali zinatia ndani jukumu la Mkristo kuendelea kulinda kwa ajili ya kurudi kwa Kristo. Kwa mfano, Kundi la Vatikani kwa ajili ya Fundisho la Imani lilipelekea maaskofu Wakatoliki ulimwenguni pote barua, yenye idhini ya mtakatifu John Paul wa Pili na yenye tarehe Mei 17, 1979, iliyosema: “Kwa kupatana na Maandiko, Kanisa linangojea ‘kujidhihirisha kwenye utukufu kwa Bwana Yetu Yesu Kristo.’ “

Kwa maneno hilo ndilo fundisho la Kanisa la Katoliki. Lakini, kwa matendo, ni mara ngapi Mkatoliki wa kawaida anasikia kasisi wake akihubiri juu ya uhitaji wa kuendelea kulinda kwa ajili ya kuwapo kwa Kristo na kuja kwa Ufalme wa Mungu? Kwa kupendeza, kusudi lenyewe la barua iliyotajwa juu kutoka kwa Baraza la Makundi ya Roma lilikuwa ni “kutia nguvu imani ya Wakristo kuhusu mambo ambayo yametiliwa mashaka.” Lakini ni kwa nini kurudi kwa Kristo kumetiliwa shaka na waitwao ati Wakristo? Je! yaweza kuwa jibu limedokezwa katika mitajo ifuatayo kutoka The New Encyclopædia Britannica? “Kwa muda mrefu kanisa limepuuza mafundisho yalo kuhusu sehemu yote ya mambo ya mwisho.” “Tangu lile Badiliko Kuu, Kanisa la Roma limekuwa bila kuwa kabisa na vikundi vyenye kutenda vyenye kutazamia mambo ya mwisho.”

Hali ya Kikristo ya Kufanya Ulinzi Haijafa

Tazamio la Kikristo lilififia ndani ya makanisa ya Jumuiya ya Wakristo kwa sababu waliacha kweli zilizo wazi za Biblia wakachagua kufuata falsafa ya Kigiriki na theolojia ya “Mtakatifu” Augustino. Makala zifuatazo zitaonyesha kwamba watumishi wa kweli wa Mungu sikuzote wamekuwa wakitazamia kuwapo kwa Kristo, na kwamba leo kuna watu ambao wamethibitisha kuwa kwao katika hali ya kulinda ya Kikristo kwa miaka mingi na ambao wamevumbua tena tumaini zuri ajabu linaloweza kuwa lako. Tafadhali endelea kusoma, halafu umuulize mmoja wa Mashahidi wa Yehova akusaidie ‘uendelee kulinda’ uone utimizo wa tumaini hilo la Biblia.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

“Ni kazi bure . . . kukana kuwapo kwa hali ya kutazamia mwisho iliyo wazi katika mengi ya maandiko ya Agano Jipya”

[Picha katika ukurasa wa 6]

Augustino alishikilia kwamba kanisa duniani ndilo Ufalme wa Kristo

[Picha katika ukurasa wa 7]

Papa Leo wa Kumi alikataza Mkatoliki ye yote kutabiri ni wakati gani Hukumu ya Mwisho ingekuja

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki