Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 5/1 kur. 9-14
  • Wenye Furaha Ni Wale Wanaokutwa Wakilinda!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wenye Furaha Ni Wale Wanaokutwa Wakilinda!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Baki la Kiyahudi Lenye Kulinda
  • Kulinda kwa Wakristo wa Kwanza
  • Tazamio la Kikristo Baada ya 70 W.K.
  • ‘Wenye Furaha Ni Wale Wanaokutwa Wakilinda’
  • Endeleeni Kuwa Tayari!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Jinsi Tazamio la Kikristo Lilivyofifia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Endelea Kutarajia!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Umeenda Wapi Ulinzi wa Wakristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 5/1 kur. 9-14

Wenye Furaha Ni Wale Wanaokutwa Wakilinda!

“Wenye furaha ni watumwa wale ambao bwana anapofika anawakuta wakilinda!”​—LUKA 12:37, New World Translation.

1. Ni kwa sababu gani sikuzote watumishi wa Yehova ‘wameendelea kumtazamia yeye,’ lakini ni swali gani linaloweza kuulizwa juu ya makanisa ya Jumuiya ya Wakristo?

“YEHOVA ni Mungu wa hukumu. Wenye furaha ni wote wale wanaoendelea kumtazamia.” (Isaya 30:18, NW) Tangu Yehova alipotangaza kushindwa hatimaye kwa Nyoka na ukombozi kupitia Uzao Ulioahidiwa, watumishi wake waaminifu wameishi wakitazamia utimizo wa ahadi hiyo. (Mwanzo 3:15) Lakini je, wanatheolojia wa Jumuiya ya Wakristo wanasaidia washiriki wa makanisa yao waendelee kulinda ili waone ukombozi huo wa mwisho wa kuwekwa huru kutoka kwa Shetani na uzao wake?

2. Ni kwa sababu gani “mataifa” yanapasa yatazamie “Shilo”?

2 Katika unabii alioutoa akifa, Yakobo alitabiri kwamba Uzao wa ahadi ungekuja kupitia kabila la Yuda. Akimpa Uzao huo jina la mfano Shilo, Yakobo alisema kwamba “watu watamtii.” Kulingana na Septuagint Version ya Kigiriki, Shilo “atakuwa tazamio la mataifa.” (Mwanzo 49:10, NW) “Mataifa” yanapaswa kuwa yakiangalia sana yamwone Shilo kwa sababu Yehova alimwambia babu ya Yakobo, Abrahamu hivi: “Katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia.” (Mwanzo 22:18) Lakini kwanza Uzao huo, Shilo, au Masihi, alipaswa aje duniani kati ya wazao wa Abrahamu azaliwe katika kabila la Yuda.

Baki la Kiyahudi Lenye Kulinda

3. Luka anasema nini juu ya tazamio la Wayahudi mwaka wa 29 W.K., na je, historia inathibitishaje hilo?

3 Mwanahistoria Myahudi Luka anasema kwamba “mwaka wa kumi na tano wa kutawala kwake Kaisari Tiberio [29 W.K.],” “watu walipokuwa wakingoja yatakayotokea, wote wakiwaza-waza mioyoni mwao habari za Yohana [Mbatizaji], kama labda yeye ndiye Kristo [Kiebrania, Ma·shiʹach, Masihi].” (Luka 3:1, 15) Je! historia ya kilimwengu inathibitisha usemi huo wa Luka? Chapa mpya ya Kiingereza ya kitabu History of the Jewish People in the Age of Jesus Christ cha Emil Schurer inauliza hivi: “Je! tumaini hilo [tazamio la Kimasihi] lilibaki daima likiwa hai kati ya watu?” Kwa kujibu kinasema: “Katika karne za mwisho zilizotangulia Ukristo, na sana-sana katika karne ya kwanza A.D., kwa mara nyingine lilikuwa lenye uhai sana kama inavyoonyeshwa bila shaka na vitabu vya ufunuo wa Kiyahudi, maandishi ya jumuiya ya Bahari ya Chumvi, Yosefo na Injili. . . . Njozi za kitabu cha Danieli . . . zilikuwa na uvutano mkubwa juu ya kufanyizwa kwa wazo la kimasihi.”

4, 5. (a) Ni kwa sababu gani Wayahudi walikuwa wakimtazamia Masihi wakati huo, na jambo hilo linathibitishwaje? (b) Wayahudi wengi walikuwa wakitazamia Masihi wa aina gani, lakini Yehova alifunulia nani kuja kwa Masihi wa kweli?

4 Akitoa maelezo juu ya Mathayo 2:2, msomi mmoja aliandika hivi: “Kulikuwako, wakati huo, tazamio lililoenea sana kwamba mtu fulani mwenye kutokeza angetokea katika Yudea. Wayahudi walitazamia sana kuja kwa Masihi. Kwa kufanya hesabu ya wakati unaotajwa na Danieli (sura ya 9:25-27), walijua kwamba kipindi kilikuwa kinakaribia ambapo Masihi angetokea.” Inaweza kusemwa pia kwamba wanahistoria Waroma Suetonio na Takito, na pia wanahistoria Wayahudi Yosefo na Filo, wanataja hali hiyo ya kutazamia. Kitabu cha Kifaransa Manuel Biblique, cha Bacuez na Vigouroux (Buku la 3, ukurasa 191), kinathibitisha hilo, na kusema: “Watu walijua kwamba majuma sabini ya miaka yaliyotajwa wazi na Danieli yalikuwa yanakaribia ukomo; hakuna mtu aliyeshangaa kusikia Yohana Mbatizaji akitangaza kwamba ufalme wa Mungu ulikuwa umekaribia.”

5 Kwa hiyo, kuna ushuhuda wa kihistoria kwamba Wayahudi walikuwa wanatazamia kuja kwa Masihi, au Uzao Ulioahidiwa, na kwamba tazamio hilo lilikuwa kwa sababu ya wao kulinda waone utimizo wa unabii wa wakati.a (Danieli 9:24-27) Ni kweli kwamba Wayahudi walio wengi wa karne ya kwanza waliokuwa washiriki wa madhehebu mbali-mbali za dini ya Kiyahudi walikuwa wakitumainia Masihi wa kisiasa ambaye, kama inavyotajwa katika kitabu The Concise Jewish Encyclopedia, “angeharibu maadui wa Israeli na kusimamisha kipindi kamili cha amani na ukamilifu.” Lakini baki la Wayahudi lilikuwa likilinda kwa makini lione Masihi wa kweli. Kati yao walikuwa Zekaria na Elisabeti, wazazi wa Yohana Mbatizaji, na pia Simeoni, Ana, Yosefu na Mariamu. (Mathayo 1:18-21; Luka 1:5-17, 30, 31, 46, 54, 55; 2:25, 26, 36-38) Ni kwa hao, wala si kwa viongozi wa dini ya Kiyahudi, Yehova alithibitisha ambayo unabii wa wakati wa Danieli ulikuwa umewawezesha walinde waone, yaani, kuja kwa Uzao Ulioahidiwa, au Masihi, “ulipowadia utimilifu wa wakati.”​—Wagalatia 4:4.

Kulinda kwa Wakristo wa Kwanza

6. Wayahudi wachanga walilelewaje, na hilo lilisaidia wengine jinsi gani ili wawe wanafunzi wa Yesu?

6 Yosefu na Mariamu walijua kwamba mtoto Yesu waliyekuwa wakilea angekuja kuwa Masihi. Kikizungumza juu ya kulelewa kwake, kitabu The New Encyclopædia Britannica kinasema hivi: “Inaelekea sana Yesu alilelewa katika utawa uliositawishwa nyumbani na katika sinagogi (kutia funzo la Biblia, kutii Torati, sala, na tazamio la kuja kwa mwisho kwa Masihi).” Vijana wengine waliolelewa katika nyumba za baki aminifu la Kiyahudi walitiwa tumaini la Kimasihi, na tazamio hilo lenye kufaa liliwezesha angalau wengine wao watii mara moja mwito wa kuwa wanafunzi wa Yesu.​—Marko 1:17-20; Yohana 1:35-37, 43, 49.

7. (a) Je! Yesu alifundisha kwamba Ufalme umo ndani ya Mkristo binafsi? (b) Wakristo walipaswa kuendelea kulinda waone nini?

7 Kuelekea mwisho wa huduma yake ya kidunia, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake waendelee kulinda kwa ajili ya “kuwapo” kwake kwa wakati ujao na kuja kwa Ufalme wake. Kitabu Britannica kinasema: “Mawazo hayo ya kawaida ya mwisho wa ulimwengu, Hukumu ya Mwisho, na ulimwengu mpya wa Mungu hayakosekani katika semi za Yesu zilizohifadhiwa katika mapokeo ya Injili. Kwa hiyo, kwa vyo vyote Yesu hajageuza Ufalme wa Mbingu ukawa jambo tu la kidini linaloonwa na nafsi moja moja ya kibinadamu wala kulipa tazamio la Kiyahudi la mambo ya mwisho maana ya kuwa tukio la kimageuzi linalorithiwa katika ulimwengu wala kuwa mradi unaofikiwa kwa jitihada ya kibinadamu. . . . Yeye hakushiriki wala kutia moyo tumaini la kuwa na masihi wa kitaifa . . . wala hakuunga mkono jitihada za Wayahudi Wenye Bidii ya Kuleta Mabadiliko ili kuharakisha kuja kwa Ufalme wa Mungu.” La, aliwapa Wakristo ishara yenye sehemu nyingi ambayo kwayo kwanza wangeweza kutambua kukaribia kwa uharibifu wa Yerusalemu, halafu, baadaye sana, watambue ‘ishara ya kuwapo kwake na umalizio wa mfumo wa mambo’ (NW).​—Mathayo 24:3 mpaka 25:46; Luka 21:20-22.

8. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu hakuamini angekuja kwenye Ufalme wake baada ya muda mfupi sana, kwa hiyo ni shauri gani alilowapa wafuasi wake?

8 Watu wenye kutegemea kufikiria kwao na hata baadhi ya wanatheolojia wa Jumuiya ya Wakristo wanadai kwamba Wakristo wa kwanza waliamini kwamba parousia, au kuwapo kwa Kristo, kungetokea katika siku zao. Wengine hata wanadokeza kwamba Yesu mwenyewe aliamini angeingia kwenye Ufalme wake karibuni sana. Lakini katika mifano yake ya talanta na mina, Yesu alionyesha kwamba angerudi tu “baada ya siku nyingi” katika uwezo wake wa kifalme na kutoza hesabu watumwa wake aliokuwa amewapa amana vitu vyake. (Mathayo 25:14, 19; Luka 19:11, 12, 15) Na katika unabii wake juu ya ‘ishara ya kuwapo kwake na ya umalizio wa mfumo wa mambo’ (NW), alikubali kwamba “hata malaika walio mbinguni, wala Mwana, ila Baba peke yake” ndiye aliyejua “siku ile na saa ile” (UV) ya kuja kwa mwisho. Aliongeza hivi: “Basi, endeleeni kulinda, kwa sababu hamjui ni siku gani Bwana yenu anakuja.”​—Mathayo 24:3, 14, 36, 42, NW.

9. Je! mtume Paulo alitoa wazo la kwamba alidhani kuwapo kwa Kristo kungetokea katika siku zake? Eleza.

9 Kwa habari ya imani ya Wakristo wa kwanza juu ya kukaribia kwa kuwapo kwa Kristo, kitabu cha usomib kinasema hivi: “Kisa cha kuwaza kwamba Paulo alitazamia parousia upesi katika 1 The. kinatilika mashaka sana. Mapema katika 1 The. 5:10 Paulo alitambua uwezekano wa kwamba huenda akafa. Uwezekano hauwezi kukataliwa kwamba kwa kusema ‘sisi’ katika 1 The. 4:15 na 17 Paulo alikuwa akijihusisha na kizazi cha mwisho kwa lazima bila kudhania kwamba yeye mwenyewe angekuwa wa [kizazi] hicho.” Katika barua yake ya pili aliyomwandikia Timotheo, Paulo alitaja wazi kwamba yeye hakutumaini kupokea zawadi yake mpaka “siku ile,” siku ya “kufunuliwa” kwa Kristo katika Ufalme wake, wakati ‘Atahukumu walio hai na waliokufa.’​—2 Timotheo 4:1, 8.

10. Kuwa katika hali ya Kikristo ya kulinda inavyofaa kuliokoaje maisha za Wakristo Wayudea wa karne ya kwanza?

10 Katika kungojea kuwapo kwa Yesu Kristo na kuja kwa Ufalme wake, Wakristo walipaswa kubaki wakilinda. Kuwa macho kwa njia ya Kikristo inayofaa kuliwezesha Wakristo Wayudea watambue ishara aliyokuwa ametoa Yesu ya uharibifu wa Yerusalemu uliokuwa umekaribia. (Luka 21:20-24) Wakati Sestio Galo aliposhambulia Yerusalemu mwaka wa 66 W.K., Wakristo waliokuwa macho walitumia kwa faida kuondoka kwake kwa ghafula kusikoelekezeka wakakimbia kutoka mji huo na pia kutoka eneo jirani la Yudea. Kulingana na wanahistoria wa kanisa la kwanza Hegesipo, Eusebio na Epifanio, Wakristo, Wayudea walikimbilia ng’ambo nyingine ya Yordani mahali paitwapo Pela. Kwa wao kuwa chonjo kiroho waliokoka kifo na utumwa wakati majeshi ya Kiroma yaliporudi mwaka wa 70 W.K. chini ya Jemadari Tito wakaharibu Yerusalemu. Bila shaka Wakristo hao walifurahi sana kwa vile walivyokuwa wameendelea kulinda!

Tazamio la Kikristo Baada ya 70 W.K.

11, 12. Nia ya Kikristo inayofaa ingekuwa nini baada ya kuharibiwa kwa Yerusalemu mwaka 70 W.K., na hilo lingewalindaje?

11 Kwa kuwa kuwapo kwa Yesu kungetokea tu baada ya “siku nyingi,” nia inayofaa ya Wakristo baada ya kuharibiwa kwa Yerusalemu mwaka wa 70 W.K. na katika karne zote mpaka wakati wa mwisho ingekuwa nini? Je! tazamio la Kikristo lingepasa kupozwa, litiwe baridi? La! barua tatu za mtume Yohana na Ufunuo, zote ziliandikwa baada ya mwaka wa 70 W.K. Katika barua yake ya kwanza, Yohana anaonya dhidi ya “mpinga-Kristo,” na kuwaambia Wakristo wabaki katika umoja na Kristo huku wakingojea “kuwapo” Kwake na kufunuliwa Kwake. (1 Yohana 2:18, 28, NW; 3:2, NW) Katika barua zote tatu, Yohana anaonya dhidi ya waasi-imani. Kwa habari ya Ufunuo, tangu mwanzo mpaka mwisho unahusu kuja kwa Kristo katika utukufu wa Ufalme wake, usemi wake wa pili kutoka mwisho ukiwa: “Amina; na uje, Bwana Yesu.”​—Ufunuo 22:20.

12 Wakristo walipaswa kutenda kupatana na parousia. Yaani, siku baada ya siku walipaswa kuishi kwa kutazamia “kuwapo” kwa Kristo. Ernst Benz, profesa wa historia ya kanisa, anaandika hivi: “‘Mambo ya mwisho’ yalikuwa ndiyo mambo ya kwanza, kwa habari ya uharaka, kwa waaminifu wa kanisa la kwanza. Mambo makuu ya imani yao na tumaini lao yalikuwa ni kuja kwa Ufalme wa Mungu.” Hata ikiwa Ufalme haungekuja wakati wa maisha yao, nia hiyo inayofaa ya kutazamia ingewalinda Wakristo wasisinzie kiroho na kujiingiza katika shughuli za ulimwengu wa Shetani.​—1 Yohana 2:15-17.

13, 14. Ni maoni gani mawili yenye kupita kiasi yaliyokuwako kati ya Wakristo wenye kuasi imani katika karne za pili na tatu W.K.?

13 Ni jambo linalokubaliwa kwamba wakati uasi-imani ulipositawi baada ya kifo cha mitume, wengine walipata mawazo yenye kosa kuhusu kukaribia kwa kuja kwa Kristo katika Ufalme wake. Katika kitabu chake The Early Church and the World, C. J. Cadoux anasema: “Ireno [karne ya pili W.K.] na Hipolito [mwisho-mwisho wa karne ya pili, mapema karne ya tatu W.K.] wote wawili walifikiri inawezekana kupiga hesabu kwa kadiri fulani ya usahihi kuhusu ni wakati gani mwisho ungekuja.” Wengine, kwa ajili ya orodha ya tarehe yenye makosa, walifikiri kwamba miaka 6,000 ya historia ya kibinadamu ilikuwa karibu kwisha na kwamba kufika kwa mileani ya saba kulikuwa kumekaribia. Bila shaka, walikosea. Lakini angalau walikuwa wakijaribu kuendelea kuwa chonjo kiroho.

14 Kwa upande mwingine, Wakristo waasi-imani walio wengi walipoteza hisi zote za kuona uharaka wa nyakati na kutazamia Ufalme. Kitabu Theological Dictionary of the New Testament kinatueleza hivi: “Kwa kuvutwa na falsafa ya Plato na maadili ya Wastoiko, mababa wa karne ya pili na wa mapema karne ya tatu wanatumia kidogo wazo la Ufalme wa Mungu. Wanapotazamia mambo ya mwisho, [tazamio hilo] linaongozwa na wazo la ukamilifu wa Mkristo binafsi. . . . Mawazo ya Kigiriki ya nafsi isiyokufa, uzima wa milele na maarifa ni ya maana zaidi ya wazo la kibiblia la [Ufalme wa Mungu]. . . . Vivyo hivyo katika Origen [mwaka wa karibu 185 mpaka karibu wa 254 W.K.], . . . ni kama hakuna mahali kwa ajili ya ujumbe wa kibiblia wa ufalme wa Mungu.”

15. Uasi-imani ulipositawi, ni maoni gani ambayo makanisa yaliyoimarishwa yalisitawisha kuelekea fundisho la “Mambo ya Mwisho”?

15 Kwa ujumla, hayo ndiyo maoni yaliyokuwako katika karne zote kati ya yanayoitwa ati makanisa ya Kikristo. Kitabu The Encyclopædia Britannica kinafunua hivi: “Tangu wakati wa mtawala Mroma Konstantino (alikufa 337) kutambuliwa kwa kisiasa na Ukristo kumeeleweka kuwa tumaini lililotimizwa la Ufalme wa Kristo. Kutazamia mambo ya mwisho kwa wakati ujao kuliendelea kuwako katika madhehebu za kisiri zenye kugandamizwa.” “Katika kipindi cha kabla ya Badiliko la karne ya 16, madhehebu zenye kushikilia imani tofauti . . . zilishtaki Kanisa la Roma kuwa lilisaliti tazamio la kuja kwa mambo ya mwisho.”

‘Wenye Furaha Ni Wale Wanaokutwa Wakilinda’

16. Ni vikundi gani vilivyotokea katika karne ya 19, na baadhi yavyo viliamini nini?

16 Kwa kuwa “makanisa ya Kikristo yaliyoimarishwa zaidi” hayakuwa tena yakilinda tena yaone kuwapo kwa Kristo na kupokea kwake uwezo wa Ufalme, zilioachwa zikifanya hivyo ni zile ambazo makanisa hayo yaliziita “madhehebu zenye kushikilia imani tofauti.” Katika karne ya 19, vikundi kadha vilitokea mahali ambako Biblia na vifaa vya kujifunza Biblia vilipatikana kwa watu wa kawaida. Makanisa makubwa-makubwa, ambayo kwayo fundisho lo lote juu ya “Mambo ya Mwisho” lilikuwa limekuwa halina maana, yaliviita kwa dharau vikundi hivyo kuwa waamini wa kuja kwa pili au waamini wa utawala wa miaka elfu, kwa sababu vikundi hivyo vilikuwa vikilinda vione kurudi kwa pili kwa Kristo na vilisadiki kwamba Kristo angetawala kwa miaka elfu. Vingi vya vikundi hivyo vilitazamia kurudi kwa Kristo duniani kusimamishe Ufalme wake wa mileani (miaka elfu). Vingine kati yavyo vilipiga hesabu kuwa kurudi kwa pili kwa Kristo kungetokea mwaka 1835 (wafuasi wa Irving, katika Uingereza), 1836 (wafuasi wa Bengel, katika Ujeremani), 1843 (wafuasi wa Miller, katika Marekani) na 1889 (kikundi cha Menon katika Urusi).

17, 18. Makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yaliyoimarishwa yalitendaje, lakini Yesu alisema angetafuta nini ‘alipofika’?

17 Kama ilivyo, “makanisa yaliyoimarishwa zaidi” yalifurahi wakati matabiri hayo yalipoonekana kuwa yenye kosa. Kwa wazi, makanisa ya Katoliki, Orthodoksi na Makanisa ya Uprotestanti yaliyo mkubwa hayakufanya makosa hayo. Kwao, fundisho la “Mambo ya Mwisho” ‘halikuwa na maana.’ Walikuwa wameacha zamani ‘kuendelea kulinda.’​—Marko 13:37, NW.

18 Hata hivyo, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Wenye furaha ni watumwa wale ambao bwana anapofika anawakuta wakilinda! . . . Kwa kweli ni nani huyo aliye mtumishi wa nyumbani mwaminifu, mwenye akili, ambaye bwana yake ataweka juu ya baraza la watumishi wake ili aendelee kuwapa kipimo chao cha chakula kwa wakati unaofaa? Mwenye furaha ni mtumwa huyo, iwapo bwana yake anaporudi atamkuta akifanya hivyo!”​—Luka 12:37-43, NW.

19, 20. (a) Ni kikundi gani kilichotokea miaka ya kuanzia na wa 1870, na ni kwa sababu gani kilijitenga na ushirika wa vikundi vingine? (b) Ni gazeti gani lililokuwa chombo rasmi cha kikundi hicho, na gazeti hilo limesaidiaje hesabu yenye kuongezeka daima ya Wakristo wa kweli?

19 Kati ya zinazoitwa madhehebu zenye imani tofauti zilizokuwa zikilinda zione ishara ya kurudi kwa Kristo katika theluthi ya mwisho ya karne ya 19 kulikuwa darasa la kujifunza Biblia lililosimamiwa na Charles Russell katika Pittsburgh, Amerika. Russell aliandika hivi: “Tangu 1870 mpaka 1875 ulikuwa wakati wa ukuzi wenye kuendelea katika neema na maarifa na upendo wa Mungu na Neno lake. . . . Hata hivyo, wakati huo tulikuwa tunapata muhtasari tu wa mpango wa Mungu, na kuondoa makosa mengi tuliyokuwa tumeyapenda kwa muda mrefu. . . . Tulihuzunishwa sana na kosa la [wafuasi wa] Kuja kwa Pili, waliokuwa wakitazamia Kristo aje na mwili.”

20 Russell na washiriki wake upesi wakaelewa kwamba kuwapo kwa Kristo hakungeonekana. Walijitenga na ushirika wa vikundi vingine na, mwaka wa 1879, wakaanza kuchapisha chakula cha kiroho katika Mnara wa Mlinzi wa Sayuni na Mtangazaji wa Kuwapo kwa Kristo (Kiingereza). Tangu mwaka walo wa kwanza wa kuchapishwa, gazeti hilo lilielekeza mbele, kwa maelezo timamu ya Kimaandiko, kwenye tarehe 1914 kuwa tarehe yenye kuanzisha kipindi kipya katika orodha ya tarehe ya Biblia. Kwa hiyo wakati kuwapo kusikoonekana kwa Kristo kulipoanza mwaka wa 1914, wenye furaha walikuwa Wakristo hao kwa kukutwa wakilinda! Kwa zaidi ya karne moja, gazeti hili, sasa likiwa linaitwa Mnara wa Mlinzi​—Unaotangaza Ufalme wa Yehova, limesaidia hesabu yenye kuongezeka daima ya Wakristo wa kweli ili ‘waendelee kuangalia’ na ‘kukesha.’ (Marko 13:33, NW) Jinsi jambo hilo limefanywa itazungumzwa katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa mazungumzo ya kikamili ya unabii huo wa wakati, ona kitabu “Ufalme Wako Uje,” kurasa 58-66.

b The New International Dictionary of New Testament Theology, Buku la 2, ukurasa 923.

Maswali Fulani ya Kurudia

◻ Ni nini kinachothibitisha tazamio la Masihi wa Kiyahudi katika karne ya kwanza?

◻ Kuwa katika hali ya kulinda kuliwasaidiaje Wakristo Wayudea?

◻ Uasi-imani ulikuwa na matokeo gani juu ya tazamio la Kikristo?

◻ Ni kikundi gani cha Wakristo kilichokuwa kikitimiza matakwa hayo, na kwa msaada wa gazeti gani?

[Picha katika ukurasa wa 12]

Wachapishaji wa gazeti hili sikuzote wamekuwa wenye kulinda

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki