Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 5/1 kur. 14-19
  • Endeleeni Kuwa Tayari!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Endeleeni Kuwa Tayari!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ‘Lindeni’​—Kwa Ajili ya Nini?
  • Ni Nani Wamejithibitisha Kuwa ‘Wenye Kulinda’?
  • Kuwa Wenye Kukesha au Wenye Uzembe?
  • Ni Nini Sababu ya ‘Kuendelea Kuwa Tayari’?
  • Wenye Furaha Ni Wale Wanaokutwa Wakilinda!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Kungoja kwa “Taraja Lenye Hamu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Endelea Kutarajia!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Umeenda Wapi Ulinzi wa Wakristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 5/1 kur. 14-19

Endeleeni Kuwa Tayari!

“Endeleeni kuwa tayari, kwa sababu katika saa msiyodhani ingeweza kuwa Mwana wa mtu anakuja.”​—LUKA 12:40, New World Translation.

1. Kristo alisema nini juu ya uhitaji wa kuendelea kulinda?

YESU Kristo alisihi wafuasi wake wawe wenye kulinda. Kwa mfano, yeye alisema: “Ninyi, basi, lindeni; nimewaambia mambo yote kimbele. . . . Na ndipo watakapoona Mwana wa mtu akija katika mawingu na uwezo mwingi na utukufu. . . . Kuhusu siku hiyo au saa hakuna ajuaye, wala malaika katika mbingu wala Mwana, bali Baba. Endeleeni kuangalia, endeleeni kukesha, kwa maana hamjui wakati uliowekwa ni lini. Ni kama mtu anayesafiri ng’ambo akaacha nyumba yake na kuwapa watumwa wake mamlaka, kila mmoja kazi yake, na kumwamuru mlinda mlango aendelee kulinda. Kwa hiyo endeleeni kulinda, kwa maana hamjui ni wakati gani bwana wa nyumba anakuja, ama usiku kucha au usiku wa manane au jogoo anapowika au mapema asubuhi; kusudi wakati afikapo ghafula, asiwakute ninyi mkilala. Lakini ninayowaambia ninawaambia wote, Endeleeni kulinda.”​—Marko 13:23-37, NW.

2. Ni kwa nini sala ya kielelezo inadokeza kuwa wenye kulinda, lakini makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yamepunguzaje umaana wa tazamio la Ufalme?

2 Makala zinazotangulia zimetoa ushuhuda mwingi kutoka vyanzo visivyoegemea upande wo wote kwamba makanisa ya Jumuiya ya Wakristo ‘hayajaendelea kulinda.’ Kulingana na The Catholic Encyclopedia, yameondoa umaana wa tazamio la Ufalme kwa kudai kwamba “ufalme wa Mungu maana yake ni . . . kutawala kwa Mungu katika mioyo yetu,” na kwa hiyo wakaondoa maana yote kutoka kwa sala ya kielelezo, au Sala ya Bwana. Hata hivyo The New Encyclopædia Britannica kinasema: “Maombi ya Sala ya Bwana yanadokeza hali yenye kuhuzunisha sana kwamba jina la Mungu na mapenzi yanatukanwa, kwamba Ufalme wake ungali haujaja.” Ndiyo, sala ya kielelezo inadokeza hali ya kuwa wenye kulinda, Ni kwa ajili ya mambo gani hasa ambayo Wakristo wangebaki wakiwa wanalinda?

‘Lindeni’​—Kwa Ajili ya Nini?

3. Ni kwa nini Wakristo hawapaswi kupuuza wakati?

3 Uchunguzi wa uangalifu wa unabii mbalimbali wa Biblia juu ya “Mambo ya Mwisho” unafunua mambo yenyewe ambayo Wakristo wangepaswa ‘kuendelea kulinda.’ Kwanza, hawangepaswa kuacha kuuona wakati, kwa maana Yesu Kristo alizungumza juu ya “wakati uliowekwa” anaoujua Baba peke yake. (Marko 13:32, 33, NW) Kuongezea hilo, Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba Yerusalemu ungekanyagwa “na mataifa, mpaka nyakati zilizowekwa za mataifa zitakapotimizwa.” (Luka 21:24, NW) Kwa wazi, Yesu aliwapa wafuasi wake habari hiyo ili awasaidie watambue wakati wa mwisho, kwa maana hiyo ni sehemu ya jibu lake kwa ulizo hili: “Mwalimu, mambo hayo yatakuwa lini? nayo ni nini ishara ya kuwa mambo hayo ya karibu kutukia?”​—Luka 21:7.

4. Wakristo walipaswa walinde ili waone “ishara” gani?

4 Kuongezea kuelekeza kwao fikira kwenye wakati, Wakristo walipaswa kulinda waone “ishara” waliyoomba, ambayo inatajwa pia katika Mathayo 24:3 na Marko 13:4. Ishara hiyo yenye sehemu nyingi​—kutia vita vya kimataifa, njaa, matetemeko ya ardhi, magonjwa ya kuambukia na kuteswa kwa Wakristo wa kweli​—ingekamatana na utimizo wa unabii mbalimbali wa wakati ili kutambulisha “kizazi” ambacho ‘hakingepita’ mpaka yatokee kikweli mambo hayo yote yanayopasa kutokea katika wakati wa mwisho.​—Luka 21:10-12, 32.

5. Kristo angekuwaje na wafuasi wake wa kweli katika karne zote, lakini hilo ndilo alilomaanisha tu alipotoa ishara ya “kuwapo” kwake?

5 Ni matukio gani ya maana yenye kuhusiana na “umalizio wa mfumo wa mambo” yangetangazwa na ishara hiyo? Wanafunzi wa Yesu walimuuliza hivi: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo [Kigiriki, pa·rou·siʹa] kwako?” (Mathayo 24:3, NW) “Kuwapo” kwa Kristo kungemaanisha nini? Kungemaanisha zaidi sana ya kuwa katika hali ya kiroho na wafuasi wake wa kweli wakati wa kukutana pamoja au kutekeleza mgawo wao wa kufanya wanafunzi. Yeye angekuwa akitegemeza wafuasi wake kwa jinsi hiyo katika karne zote. (Mathayo 18:20; 28:18-20) Hata wanatheolojia wa Jumuiya ya Wakristo wanakubali kwamba neno “kuwapo” lilichukua maana ya pekee. The New International Dictionary of New Testament Theology kinasema: “Wazo la parousia sasa linakamatana na tazamio la kanisa la kuonekana kwa Kristo kwenye mwisho wa kizazi.” Kutoka mwanzo mmoja mpaka mwingine, Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanawatia moyo Wakristo waishi wakitazamia kuwapo kwa Kristo.​—Mathayo 24:3, 27, 37, 39; Yakobo 5:7, 8; 2 Petro 3:3, 4; 1 Yohana 2:28; Ufunuo 1:7; 22:7.

6. (a) Kuwapo kwa Kristo kungemaanisha nini kwa huu mfumo mbovu wa mambo? (b) Kuwapo kwa Kristo kungekuwa na matokeo gani kwa Wakristo wapakwa mafuta ambao walikuwa wamekufa wakiwa waaminifu na wale ambao wangali hai duniani?

6 Kuwapo kwa Kristo kungemaanisha “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3, NW; Marko 13:4) Kungemaanisha kwamba mfumo wa mambo mbovu uliopo umeingia kwenye “wakati wa mwisho” wake, au “siku za mwisho.” (Danieli 12:4, 9; 2 Timotheo 3:1-5) Kungemaanisha kwamba alikuwa amepokea kutoka kwa Babaye agizo la kuelekeza utawala wa Ufalme juu ya dunia ‘kati ya adui zake.’ (Zaburi 110:2; 2:6-9; Ufunuo 11:15-18) Kabla ya kuuhukumu ulimwengu kwa ujumla, Kristo angekagua kundi lake mwenyewe na kufufua Wakristo wapakwa-mafuta waliokufa wakiwa waaminifu. (1 Wakorintho 15:21, 23; 1 Wathesalonike 2:19; 3:13; 4:13-17; 2 Wathesalonike 2:1) Wakristo wale wapakwa mafuta ambao wangali duniani na wenye kutenda kwa uaminifu wakiwa “mtumwa” wa Kristo kwa kuendelea kukesha kiroho na kutoa ‘chakula cha kiroho kwa wakati wake’ wangewekwa na Kristo juu ya “vitu vyake vyote,” au faida za Ufalme duniani. (Mathayo 24:45-47; Luka 12:42-44) Huyo “mtumwa mwaminifu mwenye akili” angepaswa kushiriki na kusimamia kazi ya ulimwenguni pote ya kuhubiri “habari njema hizi za ufalme,” ‘ndipo mwisho uje.’​—Mathayo 24:14, NW.

7. Hata wakati wa kuwapo kwa Kristo, Wakristo walipaswa waendelee kulinda waone ishara gani nyingine, na ni kwa nini wanapaswa kuendelea kusali Ufalme wa Mungu “uje”?

7 Wakristo wa kweli walipaswa ‘kuendelea kulinda’ kwa ajili ya mambo hayo yote ambayo yangethibitisha walikuwa wakiishi wakati wa kuwapo kwa Kristo na “umalizio wa mfumo wa mambo.” Lakini hata “wakati wa mwisho,” walipaswa waendelee kulinda waone “ishara ya Mwana wa Adamu,” ‘kuja’ kwake kutekeleza hukumu dhidi ya mfumo mbovu wa mambo wa Shetani. (Mathayo 24:30, 44; Marko 13:26, 35; Luka 12:40; 21:27; 2 Wathesalonike 1:7-10) Kwa hiyo, ingawa ‘angekuwapo’ na Ufalme wake ungekuwa tayari umekwisha kusimamishwa, yeye pamoja na Ufalme wake angepaswa ‘kuja’ ‘kuvunja na kuharibu’ mataifa na falme za ulimwengu wa Shetani. (Danieli 2:44) Hiyo inaeleza ni kwa sababu gani, baada ya kutoa sehemu za “ishara” ya kuwapo kwake, Kristo aliongeza hivi: “Mwonapo mambo hayo yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu.” (Luka 21:31) Ndiyo, hata wakati wa kuwapo kwa Kristo, Wakristo wangali wangesali Ufalme wa Mungu uje, na wangali wangehitaji ‘kuendelea kuangalia’ na ‘kuendelea kukesha’ kwa ajili ya wakati uliowekwa wa “mwisho” na “ukombozi” wao.​—Marko 13:7, 29, 32-37; Luka 21:9, 28.

Ni Nani Wamejithibitisha Kuwa ‘Wenye Kulinda’?

8. Yataje kwa mara nyingine mambo ambayo Wakristo walipaswa kuendelea kulinda wayaone?

8 Tumetoka tu kuona kwamba Wakristo walihitaji kuishi wakitazamia mwisho wa “nyakati za mataifa zilizowekwa” (NW). Walipaswa kulinda waone ‘ishara ya kuwapo kwa Kristo na umalizio wa mfumo wa mambo.’ Walipaswa watazamie kufufuliwa kwa Wakristo wapakwa mafuta ambao walikuwa wamekufa wakiwa waaminifu na kutambulishwa waziwazi kwa jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili”’ ambaye angewekwa aangalie faida za kidunia za Ufalme wa Kristo. Mwishowe, “mtumwa” huyo angeendelea kutoa chakula cha kiroho, na kuongoza katika kuhubiri “habari njema za ufalme . . . katika dunia yote inayokaliwa na watu” kabla ya “mwisho.” “Ishara ya Mwana wa Adamu” ingetokea kwa “kuja” kwake ili kuharibu mfumo mbovu wa mambo ya Shetani.

9. Ni nani waliothibitika kuwa wanalinda wanoe mwisho wa “nyakati za mataifa zilizowekwa,” na gazeti Mnara wa Mlinzi wa Sayuni liliwasaidiaje Wakristo waendelee kukesha kiroho?

9 Ni nani wamejithibitisha kuwa ‘wenye kulinda’ waone mambo hayo yote? Mapema hata mwaka wa 1876 Charles T. Russell wa Pittsburgh, Pennsylvania, alikuwa akilinda kwa makini aone mwisho wa “nyakati za mataifa zilizowekwa,” au “majira ya Mataifa.” (Union Version) Mwaka huo alichapisha makala yenye kichwa “Nyakati za Mataifa: Zinakwisha Wakati Gani?” Katika makala hiyo alisema kwamba “nyakati saba zitakwisha 1914 A.D.” Kuanzia mwaka wa 1880, habari iyo hiyo ilichapishwa katika safu za Mnara wa Mlinzi wa Sayuni (Kiingereza). Toleo la Machi 1880 lilisema: “‘Nyakati za Mataifa’ zinaendelea mpaka 1914, na ufalme wa kimbingu hautatawala kikamili mpaka wakati huo.” Ni kweli kwamba wanafunzi wa Biblia walioandika makala hizo, wakati huo, hawakuwa na ufahamu kamili wa Biblia na historia juu ya mambo ambayo yangemaanishwa hasa na hizo “nyakati za mataifa zilizowekwa,” kama vile sisi tunavyofahamu mambo hayo leo.a Lakini jambo la maana ni kwamba walikuwa ‘wakilinda’ na walisaidia kufanya Wakristo wenzao waendelee kukesha kiroho.

10. Maana halisi ya “kuwapo” kwa Kristo ilifanywaje ikawa wazi?

10 Kikundi icho hicho cha wanafunzi wa Biblia chenye kushirikiana na Charles Russell na gazeti Mnara wa Mlinzi wa Sayuni (Kiingereza) vilevile kilisaidia Wakristo wenye moyo mweupe wafahamu kwamba “kuwapo” kwa Kristo kwapasa kueleweka kuwa ni kusikoonekana, na kwamba hangerudi duniani atawale akiwa mfalme wa kimwili. Waliendelea kuelekeza fikira za “watu” wa Bwana kwenye matukio ya ulimwengu kwa kukamatana na “ishara” ya kuwapo kwa Kristo na “wakati wa mwisho.”

11. (a) Ni jambo gani ambalo halikufahamika kikamili wakati huo kwa habari ya falme za kidunia na kwa habari ya Wakristo wapakwa mafuta ‘kunyakuliwa’? (b) Ni ufahamu gani bora zaidi tulio nao leo wa Danieli 2:44 na 1 Wathesalonike 4:15-17?

11 Ni kweli kwamba ilidhaniwa kwamba kusimamishwa kwa Ufalme mbinguni kungemaanisha kuharibiwa kwa mara moja kwa falme za kidunia na kwamba Wakristo wapakwa mafuta ‘wangenyakuliwa’ wakajiunge na Wakristo wapakwa mafuta waliokufa ambao wangefufuliwa wakati wa kuwapo kwa Kristo. (2 Wathesalonike 2:1) Lakini ni nani anayeweza kuwalaumu kwa kutokuelewa kikamili wakati huo kwamba kazi kubwa ya kukusanya ilipasa ifanyike kati ya mwanzo na mwisho wa utimizo wa Danieli 2:44, au kwamba ‘kunyakuliwa’ kunakotajwa katika 1 Wathesalonike 4:15-17 kunahusu ufufuo wa mara moja wa wapakwa mafuta wanaokufa baada ya ufufuo wa kwanza?​—1 Wakorintho 15:36, 42-44; Warumi 6:3.

12. (a) Kristo alitazamia kukuta “mtumwa” wake mwaminifu akifanya nini alipofika ili akague nyumba yake, na alikuta nani akifanya hivyo? (b) Jamii ya “mtumwa” imeendelea kufanya nini tangu wakati huo?

12 Leo tunafahamu mambo hayo, kwa ajili ya nuru yenye kuongezeka ambayo imeng’arishwa na Neno la Mungu kupitia jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mithali 4:18) Kuhusu “mtumwa” huyo, Yesu alisema: “Ni nani basi yule mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambaye bwana wake alimweka juu ya nyumba yake, awape watu chakula kwa wakati wake? Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta akifanya hivyo. Amin, nawaambieni, atamweka juu ya vitu vyake vyote.” (Mathayo 24:45-47) Wakati Bwana Yesu Kristo aliyetawazwa alipokagua nyumba yake mwaka wa 1919, alikuta kikundi cha Wakristo wenye kushirikiana na gazeti Mnara wa Mlinzi kikijitahidi kwa ushikamanifu ‘kiendelee kulinda’ kwa kutoa ‘chakula cha kiroho kwa wakati wake.’ Mpaka siku hii ya leo, jamii hiyo ya “mtumwa” imeendelea kwa uaminifu kutoa chakula cha kiroho ili kuwezesha “watu” wa Bwana na wenzi wao ‘waendelee kuangalia, waendelee kukesha.’​—Marko 13:33, NW.

Kuwa Wenye Kukesha au Wenye Uzembe?

13. Ni maswali gani ambayo wale wanaochambua Mashahidi wa Yehova wanapaswa kujiuliza wenyewe?

13 Ni rahisi kwa makanisa yaliyoimarishwa ya Jumuiya ya Wakristo na watu wengine kuchambua Mashahidi wa Yehova kwa sababu vichapo vyao, nyakati nyingine, vilisema kwamba mambo fulani yangeweza kutokea katika tarehe fulani fulani. Lakini je, namna hiyo ya kutenda haipatani na dokezo la Kristo la ‘kuendelea kulinda’? (Marko 13:37, NW) Kwa upande mwingine, je, makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yametia moyo Wakristo wawe katika hali ya kulinda kwa kufundisha kwamba Ufalme ni “kutawala kwa Mungu katika mioyo yetu”? Badala yake, je, hayakutia moyo uzembe wa kiroho kwa kuliona tazamio la “mwisho” kuwa “halina maana” au “hadithi ya upuuzi”? Je! waasi wa imani wanaodai kwamba “siku za mwisho” zilianza katika Pentekoste na zinatia Kipindi cha Kikristo chote wameendeleza kukesha kwa Kikristo? Badala yake, je, hawakutokeza kusinzia kwa kiroho?

14. Kuna mifano gani ya watumishi waaminifu wa Yehova katika wakati uliopita ambao walikuwa na shauku sana ya kuona makusudi ya Mungu yakitimizwa?

14 Ni kweli kwamba matazamio fulani yaliyoelekea kuwa yanaungwa mkono na orodha ya tarehe za Biblia hayakutimia wakati yalipotarajiwa. Lakini si afadhali zaidi kufanya makosa fulani kwa sababu ya kuwa na shauku inayozidi ya kuona makusudi ya Yehova yakitimizwa kuliko kulala kiroho kwa habari ya utimizo wa unabii wa Biblia? Je! Musa hakuhesabu kwa makosa miaka 40 akijaribu kutenda kabla ya wakati ili aonde taabu ya Waisraeli? (Mwanzo 15:13; Matendo 7:6, 17, 23, 25, 30, 34) Je! mitume wa Yesu hawakuhangaikia sana kuona Ufalme ukisimamishwa, achia mbali kutokuelewa kwao Ufalme ulikuwa nini hasa? (Matendo 1:6; linganisha Luka 19:11; 24:21.) Je! Wakristo wapakwa mafuta katika Thesalonika hawakukosa subira wakitaka kuona “kuwapo kwa Bwana Yesu Kristo” na “siku ya Yehova”?​—2 Wathesalonike 2:1, 2, NW.

15. Ni mifano gani inayoonyesha kwamba si jambo lisilo la kimaandiko kutumia orodha ya tarehe kujaribu kujua ni wakati gani makusudi ya Mungu yanaelekea kutimizwa, na nini kimekuwa kilio cha wengi wa watumishi waaminifu wa Yehova, wa wakati uliopita na wa wakati huu?

15 Kwa msingi si jambo lisilo la kimaandiko kutumia orodha ya tarehe kujaribu kujua “wakati uliowekwa” wa kutimizwa kwa makusudi ya Mungu. (Habakuki 2:3, NW) Danieli alipiga hesabu ya wakati ambao kuachwa ukiwa kwa Yerusalemu kungepasa kukoma. (Danieli 9:1, 2) Baki aminifu la Kiyahudi la karne ya kwanza lilikuwa likitazamia kuja kwa Masihi kwa sababu walipiga hesabu ya mwisho wa wakati, kwa kutegemea unabii. (Danieli 9:25; Luka 3:15) Wakristo wa mwishoni-mwishoni mwa karne ya 19 na mapema katika karne ya 20 waliwezeshwa waishi wakitazamia utawala wa Ufalme wa Mungu kabla ya 1914 kwa sababu walipiga hesabu yaani wakati ambao “nyakati za mataifa zilizowekwa” zingepasa kumalizika. (Luka 21:24; Danieli 4:16, 17) Kwa hiyo, lilikuwa jambo lenye kufahamika juu ya sababu ambayo jitihada zilifanywa ili kutumia viishara vingine vya Biblia kujaribu kujua ni wakati gani matumaini ambayo yamengojewa kwa muda mrefu huenda yakatimizwa. Watumishi waaminifu wa Yehova katika wakati uliopita walilia hivi: “Ee [Yehova], hata lini?”​—Isaya 6:11; Zaburi 74:10; 94:3.

Ni Nini Sababu ya ‘Kuendelea Kuwa Tayari’?

16. (a) Je! andiko la Marko 13:32 lifahamike kuwa linamaanisha kwamba hatupaswi kuonyesha kupendezwa ko kote na wakati ambao mwisho utakuja? (b) Ni “ishara” gani inayoonekana wazi, lakini ni “ishara” gani nyingine tunayongojea?

16 Kwa kuwa Yesu alisema waziwazi kwamba hakuna mtu anayejua “siku ile” wala “saa ile” wakati Baba atakapoamuru mwanaye ‘aje’ dhidi ya mfumo mbovu wa mambo wa Shetani, huenda wengine wakauliza hivi: ‘Sababu gani ni jambo lenye kutaka hatua ya haraka kuishi ukitazamia mwisho?’ Ni kwa sababu Yesu alitumia mkazo uo huo akaongeza hivi: “Endeleeni kuangalia, endeleeni kukesha . . . endeleeni kulinda.” (Marko 13:32-35, NW) “Ishara” ya parousia ya Yesu imekuwa ikionekana wazi tangu mwaka 1914. Sasa tunangojea “ishara ya Mwana wa Adamu,” ‘ajapo’ akiwa Mtekelezaji wa Yehova.

17, 18. (a) Ni kwa nini Yesu aliagiza Wakristo wa karne ya kwanza waukimbie Yerusalemu mara tu walipoona ishara ya uharibifu wake uliokuwa umekaribia? (b) Ni kwa nini ingekuwa hatari kujaribu kupunguza uzito wa uharaka wa nyakati zetu?

17 Yesu alipowapa Wakristo Wayudea wa karne ya kwanza ishara ambayo ingewajulisha kwamba wakati ulikuwa umefika wa kukimbia kutoka Yerusalemu, alisisitiza juu ya uhitaji wa kuchukua hatua mara moja. (Luka 21:20-23) Kwa sababu gani hatua ya haraka ilitakwa, kwani miaka karibu minne ilikwisha tangu kutokea kwa ishara mwaka wa 66 W.K. na kutokea kwa uharibifu wenyewe mwaka wa 70 W.K.? Kwa sababu Yesu alijua kwamba wakikawia, wangekuwa wanaahirisha kukimbia kwao na hatimaye wanaswe na majeshi ya Roma.

18 Hali moja na hiyo leo, ingekuwa ni hatari kubwa kwa Wakristo kupunguza uzito wa uharaka wa nyakati zetu na kuwa na maoni ya kufanya mambo polepole ambayo yanaonyesha kutia shaka juu ya ukaribu wa mwisho.

19. Petro na Yesu walitoa onyo gani?

19 Parousia, au kuwapo, kwa Kristo sasa kumeendelea kwa miaka 70, na ‘kuja’ kwake kwa ajili ya “siku ya Yehova” ya kuua ulimwengu wa Shetani kunakaribia sana. Mtume Petro anasema kwamba siku hiyo “itakuja kama mwivi,” na anaongeza kwamba tunapaswa ‘kungojea na kukaribisha akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.’ (2 Petro 3:10-12, NW) Vilevile Yesu alituonya hivi: “Jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajia ghafula, kama mtego unasavyo. . . . Kesheni.”​—Luka 21:34-36.

20. Tunapaswa kushukuru kwa ajili ya nini, na tazamio linalofaa la Kikristo litatulindaje?

20 Mashahidi wa Yehova wanapaswa kuwa wenye furaha na shukrani kama nini kwa ajili ya kuwekwa wakikesha kiroho na jamii ya “mtumwa” mwaminifu aliye chonjo! Tazamio la Kikristo linalofaa litatulinda sisi wakati wa hizi “siku za mwisho” zenye hatari na litatusukuma tushiriki kwa bidii kuhubiri “habari njema hizi za ufalme.” Kwa kufanya hivyo tutakuwa tukisaidia wengine waendelee kulinda na kuokoka waingie katika mfumo mpya wa mambo ambamo “uadilifu utakaa.”​—2 Timotheo 3:1-5; Mathayo 24:14, NW; 2 Petro 3:13, NW.​—Kutoka w12/l/84.

[Maelezo ya Chini]

a Ona kitabu “Ufalme Wako Uje,” sura ya 14, na nyongeza yenye maelezo marefu ya sura hiyo mwishoni mwa kitabu.

Je! Wewe Unaweza Kukumbuka?

◻ Ni kwa nini Wakristo hawapaswi kupuuza wakati katika orodha ya Biblia?

◻ Neno “kuwapo” lilichukua maana gani ya pekee?

◻ Ni kwa nini ingali inafaa kusali Ufalme wa Mungu uje?

◻ Ungewajibuje wale wanaochambua Mashahidi wa Yehova juu ya mambo yanayohusu orodha ya tarehe?

◻ Kwa nini ni hatari kupunguza uzito wa uharaka wa nyakati zetu?

[Sanduku katika ukurasa wa 18]

Mambo Ambayo kwa Ajili Yake Wakristo Walipaswa Kuendelea Kukesha

Mwisho wa “nyakati za mataifa zilizowekwa.”​—Luka 21:24, NW.

“Ishara” ya kuwapo kwa Kristo “na ya umalizio wa mfumo wa mambo.”​—Mathayo 24:3–25:46, NW.

Kutambuliwa waziwazi kwa jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili.”​—Mathayo 24:45-47.

“Ishara ya Mwana wa Adamu,” ‘ajapo’ kutekeleza hukumu za Yehova.​—Mathayo 24:30.

[Picha katika ukurasa wa 17]

C. T. Russell na washiriki wake waliendelea kulinda

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki