Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 10/15 kur. 22-24
  • Maswali Kutoka Kwa Wasomaji

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maswali Kutoka Kwa Wasomaji
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Habari Zinazolingana
  • Je! Kucheza Kamari Kwafaa Wakristo?
    Amkeni!—1994
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Kucheza Kamari
    Amkeni!—2015
  • Wazoezwaji Wapya wa Uchezaji Kamari—Vijana!
    Amkeni!—1995
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 10/15 kur. 22-24

Maswali Kutoka Kwa Wasomaji

● Biblia inatoa uongozi gani kuhusu kucheza kamari? Kwa mfano, je! ingekuwa vibaya Mkristo akiweka pesa ndogo-ndogo kando ili kuzishindania katika mchezo wa karata unaochezwa kwa kusudi la kujifurahisha tu?

Maandiko hayatoi msingi wa kuweka sheria yo yote ngumu ya kupinga kila shindano, hata liwe dogo namna gani, la kushindania kitu kilichowekwa kando na watu wawili ili kiwe cha mwenye kupata jawabu la kweli la jambo wanalobishania. Hata hivyo yanatusaidia tuone kwamba kucheza kamari ni kosa zito, kosa linaloweza kufanya mtu aondolewe asiwe katika kundi la Kikristo na katika ufalme wa Mungu.

Nyakati nyingine maneno “cheza kamari” na “kucheza kamari” yanatumiwa juu ya utendaji mbalimbali unaohusu hali ya pata-poteza. Huenda mtu akasemwa kwamba ‘anacheza kamari’ juu ya biashara mpya anayoanza au anayonunua, kwa sababu hana uhakika kama itamletea faida au la. Lakini mazungumzo yanayofuata ni juu ya namna ya “kucheza kamari” ambamo watu wanawekeana vitu fulani kando ili mwenye kupata jawabu la kweli avichukue viwe vyake. Kwa mfano: “Kucheza kamari hufafanuliwa kwa ujumla kuwa ni kupenda kwa mtu kujitia katika hatari ya kupoteza kiasi fulani cha pesa akishindwa na mwenzake anayepata jawabu la kweli la mchezo au tukio jingine wanaloshindania.” (Encyclopedia Americana) Biblia haizungumzi waziwazi habari za kucheza kamari kwa namna hiyo.

Waamuzi 14:11-19 inaeleza habari za jaribio lenye kuhusu malipo ambalo Samsoni alifanyia wenzake, lakini hiyo haikuwa namna ya kucheza kamari bali ulikuwa ni mpango wa akili nyingi alioutumia ‘akitaka kisa juu ya’ Wafilisti maadui. Wala matumizi ya kutupa “kura” katika Israeli hayakuwa kucheza kamari; yalikuwa njia ya kupata uongozi wa Mungu au kumaliza magombano. (Mit. 16:33; 18:18; 1 Sam. 14:41, 42) Na ingawa Waebrania walicheza michezo na walikuwa wakifanya mbio za miguu, hakuna ushuhuda wa kuonyesha kwamba waliwekeana kando vitu vya kuchukuliwa na mwenye kushinda wengine. (Yer. 12:5) Kitabu Encyclopcedia of Religion and Ethics (cha habari zinazohusu dini na mwenendo ufaao) cha Hasting kinatoa maoni haya: “Maadamu [Waisraeli] waliendelea kuwa watu wa ukulima, walielekea kuwa ndio watu wa pekee wasiokuwa na ule uovu wa kucheza kamari. Katika Babeli walipata kuwa watu wa biashara, wakachangamana na watu ambao kati yao michezo ya bahati-nasibu ilikuwa sehemu ya kawaida ya maisha ya kila siku.”​—Kitabu cha 6, uku. 164.

Katika habari hii Isaya 65:11, 12 inataja “yule mungu wa Bahati Nzuri” (NW) au Nasibu Nzuri ambaye wacheza-kamari Wababeli walimtegemea awasaidie. Kama vile mistari hiyo inavyotaja, Mwisraeli ye yote aliyeandaa meza ya chakula kwa ajili ya miungu hiyo ya kisanamu ya bahati angekuwa akifuata mwendo wa ukafiri (wa kuasi imani).

Kwa kweli, kisa cha pekee katika Biblia ambacho kingeweza kuhesabiwa kama kucheza kamari ni kile kilichotukia wakati askari Warumi walipotupa kura za kuamua ni nani angejipatia vazi la ndani la Yesu.​—Mt. 27:35; Yohana 19:23.

Ingawa Biblia haizungumzi kwa urefu habari ya kucheza kamari, inatupa kanuni zinazosaidia kuchunguza na kuona jinsi kucheza kamari kulivyo. Kanuni hizo zinaonyesha wazi kwamba inampasa mtu aliye Mkristo akumbuke kusudi la kucheza kamari na mambo kunayoyatokeza mara nyingi.

Watu wa mahali pengi wanakubali kwamba mara nyingi kucheza kamari kunamfanya au kumchochea mtu awe mwenye pupa. Hilo ni jambo la maana kuangaliwa na Wakristo, kwa maana Biblia inakataza “pupa” kwa uthabiti. Mungu anatufahamisha kwamba “watu wenye pupa” hawatarithi ufalme wake, na kwamba kutamani visivyo vya mtu kunahesabiwa kuwa sawa na kuabudu sanamu. Kwa hiyo, Wakristo wanyofu wanapaswa waepuke mazoea yanayoweza kuwafanya waonyeshe wazi kwamba ni wenye pupa na hivyo wapungukiwe sana na utukufu wa Mungu.​—Kol. 3:5; 1 Kor. 6:9, 10, NW; Rum. 3:23.

Bila shaka, pupa inaweza kuonekana wazi kwa njia nyingi. Huenda mtu akaonyesha pupa nyingi mno katika kula kwake, akiwa mlafi kwa njia hiyo. Au, huenda kunywa mno kwa pupa kukamfanya awe mlevi. (Tito 1:12, 13; Mit. 23:20; 1 Tim. 3:3) Walakini, kula ni sehemu ya kawaida ya maisha inayohitajiwa. Na hata furaha ambayo watu wengine hupata kwa kunywa vileo kwa kiasi inahusu kawaida ya maumbile, wakinywa kinywaji ambacho ni sehemu moja ya maji-maji yanayonywewa kila siku ili mwili uweze kuyayeyusha upate nguvu. Kwa hiyo “pupa” haihusianishwi mara nyingi au kwa wepesi na vitu hivyo kama inavyohusianishwa na kucheza kamari.

Pupa ya kucheza kamari ni sababu moja kubwa inayoleta wingi wa uhalifu na jeuri inayohusiana na michezo ya kamari ya kumaliziana pesa kikweli. Lakini hata mtu akicheza kamari peke yake, mara nyingi kusudi la kufanya hivyo linakuwa ni pupa. Je! watu wengi hawachezi kamari kwa sababu ya kutumainia kushinda wajipatie kile ambacho wenzao watapoteza? Jambo hilo linakubaliwa hata na watu ambao mawazo yao hayaitegemei Biblia hasa. Profesa D. M. Smyth alieleza hivi: “Kwa kuendeleza michezo ya bahati-nasibu serikali zinatokeza moja ya sifa zilizo mbaya zaidi za kibinadamu—pupa. Zinasaidia kuleta upotovu wa maisha ya kibinadamu, si maendeleo. . . . Wenye kuendeleza michezo ya bahati-nasibu wanatia watu moyo wawe na maoni ya kwamba ni sawa mtu kujipatia faida kwa kuletea watu wengi hasara.”​—Gazeti Star (Nyota) la Toronto.

Hata hivyo, huenda mtu fulani akafikiri hivi: ‘Namna gani nikicheza mchezo wa kirafiki wa karata au wa ubaoni pamoja na watu wa ukoo wangu? Tunaweza kuwekeana kando hesabu ndogo-ndogo za pesa ili mshindi azichukue, na kwa njia hiyo hakuna atakayeshinda ajipatie pesa nyingi au apate hasara kubwa. Je! kufanya hivyo si kujifurahisha tu bila kufanya kosa, bila pupa yo yote?’

Huenda wengine wakatoa hoja hiyo. Lakini po pote pesa zinapotumiwa, hata ziwe ni za kiasi kidogo namna gani, hatari iliyopo i wazi. Kufanya hivyo kunaweza kuwa kama ‘kulilia wembe,’ na hasa lingekuwa jambo la hatari kutia watu moyo wacheze kamari ikiwa watoto wapo kati ya wachezaji. Kwa nini msitumie kalamu tu kuandika hesabu ambazo kila mtu anajipatia, au mtumie njia nyingine kuucheza mchezo huo kwa kusudi la kujifurahisha tu? Wazee wa kiroho kundini wasingepaswa kujiingiza katika linalofanywa kwa upande huo. Wasingejaribu kutoa sheria-sheria kama walivyofanya viongozi wa kidini wanaosimuliwa kwenye Luka 6:1-5. Walakini, wakipata habari kwamba hali ya kiroho ya wanaohusika imo hatarini, wanaweza kuwapa mashauri yenye fadhili kwa kuwa ndio ‘wanaoendelea kulinda nafsi’ za kundi.​—Ebr. 13:17, NW.

Mifano ya mambo ya kweli yaliyotendeka inaonyesha kwamba wengi ambao walipata kuwa wacheza-kamari wenye pupa na wenye mazoea ya kuicheza walianza kwa kushindania vitu vidogo vidogo ‘ili kujifurahisha’ ati. Wakaona kwamba wangeweza kushinda kiasi kidogo halafu wakashawishwa wajaribu kushinda kiasi kikubwa zaidi. Mazoea hayo yenye pupa yanaweza kumkwamisha mtu humo hata iwe vigumu kuyaacha, hata yamwingize katika maisha ambayo hapo kwanza asingaliweza kufikiria kuyafuata. Mtu mmoja aliyekuwa mcheza-kamari katika Canada alieleza hivi: “Mimi nina mpwa wa kike ambaye hupata hasara ya dola 100 kila juma. Inamlazimu mumewe afanye kazi mbili. Watoto wake wanaumwa na njaa ajabu. Mpwa huyo huwa na mazoea ya kuomba-omba, kukopa kisha kuiba ili acheze.”

Mara nyingi kusudi la kucheza kamari huwa ni kiburi pia. Kuweza kushinda hutokeza roho ya kiburi katika mtu. Lakini Mungu anasema: “Kiburi na majivuno . . . nakichukia.” Waabudu wa kweli wanatiwa moyo wasitawishe hali ya kujifikiria kwa kiasi na kuwa na unyenyekevu.​—Mit. 8:13; 11:2; 22:4; Mik. 6:8; Yak. 4:16.

Mara nyingi wacheza-kamari wanamtukuza ‘Bibi Bahati.’ Kwao neno “bahati” halimaanishi matokeo mazuri tu, bali ni kitu chenye kuwaongoza kipitacho nguvu za kibinadamu kama mungu. Pupa na kiburi ni mambo yanayosukuma wacheza-kamari waitumaini “bahati.”

Mara kwa mara kucheza kamari kunaletea mtu uvivu. Kunatia watu moyo wajidanganye kwamba watapata kitu cha bure, hata kuwasukuma waseme uongo au wapunje wenzao ili kushinda, badala ya kuwasukuma wafanye kazi. Lakini Neno la Mungu linatoa mashauri yenye kupinga uvivu na kuhimiza watu wawe wenye busara ya kutunza vitu vyao kwa njia nzuri, wawe wenye bidii na kufanya kazi kwa kujikaza. “Ikiwa mtu hataki kufanya kazi, basi, asile chakula.”​—Mit. 5:9-11; Efe. 4:28; 2 The. 3:10.

Matunda mabaya ya kucheza kamari yanajulikana sana hata kwamba katika mitaa mingi wacheza-kamari hudharauliwa, hata ikiwa kucheza kamari kunaruhusiwa na sheria. Hivyo, tamaa ya kutaka “kushuhudiwa mema na watu walio nje,” na kuepuka kufanya wengine wazichukie ‘habari njema za ufalme’ inaongezea sababu zinazowafanya Wakristo wengi waepuke kabisa kabisa namna zote za kucheza kamari.​—1 Tim. 3:7, 10; Mt. 24:14; 1 Kor. 9:11-23; 2 Kor. 6:3.

Wale wanaotumikia kama ‘wachungaji wa lile kundi’ wana haki ya kutaka kusaidia Wakristo wenzao waepuke mambo yanayoweza kuharibu hali yao ya kiroho. Kwa hiyo, mtu akihusika katika mchezo wa kamari kisha aonyeshe kikweli kwamba ana maelekeo ya kuwa na pupa au kutokeza mengine ya matunda mabaya yanayohusiana na kucheza kamari, wazee watataka kumsaidia. Wanaweza kutoa mashauri faraghani au mbele ya watu wote wanapoona maelekeo hatari ya kuingilia pupa. (1 Pet. 5:2, 3; Gal. 6:1) Na ikiwa Mkristo anafuatia mwendo wa pupa bila kutubu, huenda hata ikawa lazima kumwondoa kundini, kupatana na maongozi yaliyo katika Neno la Mungu, linalosema, “Mwondoeni yule mbaya miongoni mwenu.” Paulo anaongeza kusema: “Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, wala wevi, wala watamanio [wenye pupa, NW], wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi.”​—1 Kor. 5:11-13; 6:9, 10.

Walakini, ni mara chache mambo yanapofikia hatua hiyo, kwa maana Wakristo wa kweli wanaepuka kabisa namna zote za kucheza kamari. Wao wanataka kuzaa matunda ya roho, si kushiriki katika utendaji unaojulikana kuwa wenye kuchochea pupa na kuzaa kazi za mwili. (Gal. 5:19-23) Wanauthamini ubora wa kujipatia riziki yao kupitia kazi ya unyofu. Ni kama vile mtume Paulo alivyoonya kwa upole: “Twawasihi, ndugu, . . . mjitahidi kutulia, na kutenda shughuli zenu, na kufanya kazi kwa mikono yenu wenyewe, kama tulivyowaagiza; ili mwenende kwa adabu mbele yao walio nje, wala msiwe na haja ya kitu cho chote.”​—1 The. 4:10-12.

Wakristo wanaviona vitu walivyo navyo—hata maisha yao na pesa zao au mali zao—kuwa wamevitoa viwe vya Mungu. Watalazimika kumpa Mungu jibu kwa sababu ya njia yao ya kuvitumia vitu hivyo. Kwa hiyo badala ya kuharibu wakati wao na kuponda pesa katika shughuli za kamari zinazoweza kutokeza pupa ndani yao na kuumiza watu wengine, wao wanautumia wakati wao na pesa zao kwa njia zitakazomtukuza Yehova (Mit. 3:9) Kwa njia hiyo ‘wanatenda mema wanakuwa matajiri kwa kutenda mema, wakiwa tayari kutoa mali zao, washirikiane [wagawane, NW] na wengine.’ Na, kama vile Paulo alivyoandika, ‘wanajiwekea akiba iwe msingi mzuri kwa wakati ujao, ili wapate uzima ulio kweli kweli.’​—1 Tim. 6:17-19.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki