Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 1/1 kur. 7-10
  • Maoni Yaliyosawazika ya Kulinda Heshima Yako

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maoni Yaliyosawazika ya Kulinda Heshima Yako
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Je! Mkristo Anahitaji Kulinda Heshima Yake?
  • Namna ya Kushughulikia Tatizo la Kulinda Heshima
  • Sifa Tatu za Kikristo Zenye Thamani Kubwa
  • Wewe Ungefikia Hatua Gani Katika Kulinda Heshima Yako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Uwe Mnyoofu Katika Mambo Yote
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
  • Jipatanishe kwa Unyenyekevu na Njia ya Yehova ya Wokovu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Usijifikirie Mwenyewe Kuliko Ilivyo Lazima
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 1/1 kur. 7-10

Maoni Yaliyosawazika ya Kulinda Heshima Yako

BIBLIA inaonyesha kwamba tamaa ya kulinda heshima ilianza karibu na wakati ambao jamii ya mwanadamu ilianza kuwako. Kwa kweli, dhambi ya kwanza kabisa ya kibinadamu ilifuatwa na jaribio la kulinda heshima.

Huenda wewe ukawa unajua habari za vile Adamu na Hawa, wazazi wetu wa kwanza, walivyomtenda Mungu dhambi kwa kula tunda lililokatazwa. Mwishowe, ikawa lazima waeleze sababu gani walitenda uhalifu huo. Majibu yao yalikuwa ya namna inayostahili kuangaliwa; Wakati Adamu alipolazimishwa kuungama, alijaribu kulaumu Hawa na hata Yehova Mungu mwenyewe. Alisema: “Huyo mwanamke uliyenipa awe pamoja nami ndiye aliyenipa matunda ya mti huo, nikala.” Hawa, pia, alijaribu kuepuka lawama. Alisema: “Nyoka alinidanganya, nikala.”​—Mwanzo 3:8-13.

Wewe umepata kushawishwa utende kwa njia kama hiyo? Unapokuwa umekabiliwa na jambo fulani ulilofanya vibaya, umejaribu kulaumu wengine? Watu wengine watajaribu kufanya jambo lo lote ili waepuke kukubali wazi hivi: “Nasikitika. Nilifanya kosa.” Lakini, kujaribu kulinda heshima hakubadili mambo. Adamu na Hawa waliadhibiwa kwa dhambi zao wajapojitolea visababu.​—Mwanzo 3:16-19.

Anania na Safira ni watu wengine waliooana ambao walifikiria sana kulinda heshima yao. Walijaribu kudanganya kundi la kwanza la Kikristo kwa kusema uongo mtupu, kwa wazi wakitaka kujifanyia sifa, heshima, kati ya waamini wenzao. Maudhiko ya Mungu yalionyeshwa alipoleta kifo chao. (Matendo 5:1-11) Je! Yehova hangechukua mambo kwa njia kama hiyo leo ikiwa, kwa mfano, Mkristo angedai kwa uongo kuwa anafanya mengi katika utumishi wa Mungu kuliko yale anayofanya kweli kweli? Au, je! Yehova hangechukizwa ikiwa, kwa njia nyingine yo yote, tungejaribu kujifanya kwa udanganyifu kwamba tuko tofauti na namna tulivyo hasa?​—Yakobo 3:17.

Je! Mkristo Anahitaji Kulinda Heshima Yake?

Kufikiria kulinda heshima kunaelekea mara nyingi zaidi kuleta matokeo mabaya. Hiyo ni kwa sababu kunategemea wazo lenye kosa. Linakuwa na dhana ya kwamba sifa ya mtu ndiyo ya maana kupita mambo yote. Hiyo si sawa. Pia, huenda kulinda heshima kukawa kunategemea kiburi, au maoni ya kujihesabia ubora unaopita kiasi. Jambo hilo halipendezi Yehova.​—Mithali 16:18.

Ni kweli kwamba Biblia inasema: “Heri sifa njema kuliko marhamu nzuri.” (Mhubiri 7:1) Lakini, hilo linataja sifa ambayo mtu amejipatia kwa ustahili, hasa machoni pa Yehova, kwa muda wa maisha ya kufanya kazi njema. Halihusu heshima. ambayo mtu anadai wengine wampe awe anaistahili au haistahili.

Ni kweli pia kwamba ili mwanamume awe mzee Mkristo ni lazima ‘ashuhudiwe mema na watu walio nje.’ (1 Timotheo 3:7) Huo ‘ushuhuda mwema,’ hata hivyo, unatokana na mwenendo wake wa Kikristo na jamaa yenye utaratibu mzuri, wala hauji kwa sababu ana digrii ya chuo, kazi ya ukubwa, au anatumia fedha nyingi akinunulia rafiki zake vitu.

Kwa wazi Yesu Kristo hakuhesabu heshima yake mwenyewe mbele ya wengine kuwa bora kupita kiasi. Alipohubiria maskini, watoza kodi na watenda dhambi badala ya kushirikiana na viongozi wa kidini, inaonekana jambo hilo lilimpotezea heshima nyingi machoni pa wanaume hao wenye kiburi. (Yohana 7:45-48) Lakini Yesu hakuondoshwa kando asifanye mapenzi ya Baba yake wa kimbingu kwa sababu hakuwa akitafuta utukufu wake mwenyewe. Kwa kweli, wakati mmoja alisema: “Nikijitukuza mwenyewe, utukufu wangu si kitu.” (Yohana 8:49-54) Yeye alitosheka kungojea Baba yake amtukuze. Hata hivyo, matendo ya Yesu yalimletea sifa njema mbele za Mungu na wanadamu wenye kufikiri inavyofaa.

Ndivyo ilivyo kwetu pia. Tukijaribu kujitukuza wenyewe, hasa kwa kuficha mambo, au kwa kujionyesha tuko namna ambavyo hatuko, ni wazi hilo ni kosa na mwishowe linakuwa jambo lisilo na faida. Ni afadhali zaidi kufikiria namna Mungu anavyotuona. Yesu mwenyewe alisema: “Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni.”​—Mathayo 5:11, 12.

Ndivyo Yesu alivyoona, hasa baada ya kukamatwa. Viongozi wa kidini walimpeleka mahakamani kisha wakajaribu kuchafua sifa yake kwa kutumia mashahidi wa uongo. Baadaye alichekwa na kudhihakiwa. Taji ya miiba iliwekwa juu ya kichwa chake kwa nguvu, na akavikwa vazi la rangi ya zambarau kwa kudharau uhakika wa kwamba yeye alikuwa Mfalme. (Marko 14:55-65; 15:17-20) Halafu, Yesu alipokuwa akifa, watawala wenye kufurahia hilo walisimama kandokando ya mti wa mateso wakimfanyia mzaha. Hata njia aliyokufa kwayo ilionwa na Wayahudi kuwa ya aibu sana. (Luka 23:32-38; Wagalatia 3:13) Katika yote hayo, je! Yesu alijaribu kutetea sifa yake au kulinda heshima yake? Hapana. Bali, Maandiko yanatuambia kwamba ‘alidharau aibu.’ (Waebrania 12:2) Jambo la maana zaidi machoni pake lilikuwa kutukuza jina la Baba yake. (Yohana 14:4, 11) Na thawabu ya Kristo ilikuwa kubwa kweli kweli katika mbingu kwa sababu ya mwenendo mwema huo. Ni mfano wa kutokeza kama nini kwetu leo!—1 Petro 2:21, 22.

Namna ya Kushughulikia Tatizo la Kulinda Heshima

Basi, je! Mkristo anapaswa kushughulikiaje tatizo la kulinda heshima? Kwa kweli, kuna pande mbili za jambo hilo za kufikiriwa: kushughulika kwetu na wengine, na maoni yetu juu ya sisi wenyewe.

Katika kushughulika na wengine, Mkristo anapaswa kujaribu kuepuka kuwaingiza katika hali ambazo wanajisikia wakilazimika kujaribu kulinda heshima yao. (Mathayo 7:12) Kwa hiyo, upendo na kujitia katika hali ya wengine kutafanya mwangalizi anayetoa shauri au sahihisho afanye hivyo kwa fadhili, kwa huruma​—“kwa roho ya upole.” (Wagalatia 6:1) Mkristo anayehubiria mtu asiyeamini “habari njema” atafanya hivyo kwa busara, “kwa upole na kwa hofu.” (1 Petro 3:15) Kwa njia hiyo hatamuumiza moyo wala kumwaibisha mtu huyo asiyeamini akisema mambo yasiyo sahihi au anapokuta kwamba kumbe imani anazothamini sana ni za uongo. Tena, Mkristo hapaswi kuharibu sifa ya mtu mwingine kwa kueneza porojo zenye madhara juu yake.​—Mithali 16:28.

Tunapojitazama wenyewe, lazima tutambue kwamba ukomavu wa Kikristo unatakwa ili kuepuka mtego wa kulinda heshima. Hata Ayubu aliingia katika mtego huo. Lakini ni kweli kwamba alikuwa chini ya mkazo mwingi. Taabu zake zilitia ndani ugonjwa mbaya sana, kufa kwa jamaa yake na kuvunjwa moyo na mke wake. Halafu watatu wenye kuitwa rafiki ati wakaja na kumshitaki juu ya kutenda dhambi kwa siri. Hapo ndipo Ayubu alipotoa maneno mengi ya kujitetea sana. Alijitangaza kuwa ‘mwenye haki badala ya Mungu.’ (Ayubu 32:2) Lakini Ayubu aliposikia fikira zenye hekima za Elihu na hasa vikumbusho vya Yehova mwenyewe, kufikiri kwake kulirudishwa katika usawaziko unaofaa. Ndipo Ayubu alipompa Mungu utukufu badala ya kulinda heshima yake na kujaribu kujitetea. Kwa sababu hiyo, alibarikiwa sana.​—Ayubu 42:1-6, 12, 13.

Kwa hiyo, Mkristo anahitaji kujichunguza kwa uangalifu. Mara nyingi ni vigumu kutambua kwamba tatizo linalosumbua mtu hasa ni kulinda heshima yake. Huenda ikawa kwamba katika kujaribu kudanganya wengine, tumefaulu kujidanganya wenyewe pia. Moyo ni wenye hila na unaweza kutufanya hivyo. (Yeremia 17:9) Hasa ndivyo ilivyo tunapokuwa chini ya mkazo wa moyoni au tunapokuwa katika hali ya kuvunjiwa heshima. Lakini, kuchanganua kufikiri kwetu kwa njia ya sala kutatusaidia tuone namna hali ilivyo hasa. (Zaburi 139:23, 24) Mara tukiisha kuijua ilivyo, kama Ayubu tunaweza kusaidiwa kwa kurudishiwa usawaziko wetu na Neno la Mungu na ndugu zetu Wakristo.

Mara nyingi yanayotutia wasiwasi si maoni ya wapinzani, bali ni ya watu tulio na uhusiano wa karibu nao. Huenda Mkristo aliyekomaa akavumilia dhihaka katika mtaa wake kwa ajili ya “habari njema.” Lakini huenda akaona ni vigumu kukubali kosa au kuungama dhambi ndani ya kundi na, kama anavyofikiri, awe katika hatari ya kupoteza heshima ambayo Wakristo wenzake wanampa. Huenda akaona aibu nyingi watoto wake wakifanya kosa, na huenda akajaribu kunyamaza lisijulikane.

Jambo hilo linaweza kupata hata mwangalizi wa Kikristo. Ingawa hivyo, kwa kweli mzee aliye katika hali hiyo anayeungama waziwazi tatizo lake anataka kufaidi kundi na anawekea wengine mfano mwema. Watu wanaofikiri kwa njia inayofaa watamheshimu kwa unyofu wake. Kwa upande mwingine, kujaribu kuepuka lawama, au kufunika vile yeye au jamaa yake imefanya, ni woga. Jambo hilo linaweza kuongoza kwenye kusema uongo pia. Mambo yote hayo mawili yanachukiza Mungu.​—Ufunuo 21:8.

Sifa Tatu za Kikristo Zenye Thamani Kubwa

Kwa hiyo, tunahitaji kusitawisha sifa zitakazotusaidia kushinda tamaa ya kulinda heshima. Ni sifa gani? Unyofu ni moja. (Waebrania 13:18) Ikiwa tunathamini unyofu, hatutataka kujifanya tuko namna ambavyo hatuko, kama inavyokuwa karibu sikuzote wakati kulinda heshima kunapohusika. Huenda hilo likawa jambo gumu. Ndiyo sababu huenda tukahitaji unyenyekevu na ushujaa pia kutusaidia tuendelee kuwa wanyofu, pamoja na sisi wenyewe na pamoja na wengine pia. (Mithali 15:33; 1 Wakorintho 16:13) Tena, unyenyekevu utashinda fahari ya uongo inayotufanya tutake mara ya kwanza kulinda heshima yetu.

Ndiyo, ushujaa, unyofu na unyenyekevu utatusaidia tuepuke mtego wa kulinda heshima. Paulo alisema kwamba wengine walimwona yeye kuwa mpumbavu. (1 Wakorintho 4:10) Je! wewe unajali ikiwa watu wanakuona kuwa mpumbavu ikiwa unajua moyoni mwako kwamba unafanya mapenzi ya Mungu? Au kuogopa maoni ya watu wengine kunakuzuia usifanye yanayofaa? Hasa vijana-matineja wanahitaji ushujaa, unyofu na unyenyekevu ili kutetea kanuni zinazofaa badala ya kuanza kulinda heshima yao na kufuata wingi wa watu.​—1 Petro 4:4.

Yesu alilinganisha wale wanaotumikia Mungu na “watumwa wasio na faida.” (Luka 17:10) Je! wewe unajichukua mwenyewe hivyo? Au unafikiri wewe ni mtu wa maana sana? Paulo alitutia moyo ‘tusinie makuu kupita inavyotupasa kunia.’ (Warumi 12:3) Pia alitutia moyo ‘tusitende neno lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu, kila mtu akimhesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yake.’​—Wafilipi 2:3.

Maandiko yanaonyesha waziwazi kwamba katika kundi la Kikristo hakuna nafasi ya kulinda heshima, au ya kujipatia wenyewe heshima. Zile sifa za maana za Kikristo za unyenyekevu, ushujaa na unyofu zinapingana kabisa na kulinda heshima. Huenda lisiwe jambo jepesi kufikiri kwa njia hiyo, hasa kama tumekulia katika utamaduni unaothamini kulinda heshima ya mtu kuwa jambo bora kupita yote. Lakini, kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu, Wakristo wanaweza kufanya mabadiliko katika njia ya kutenda. Hata ‘roho ya nia zao’ inaweza kubadilika, ikiwa wanataka kweli kweli ibadilike. (Waefeso 4:23) Kwa hiyo uwe macho kuziona hatari za kulinda heshima yako. Ujue kwamba ni mtego wa mwili wenye dhambi, na, kwa vyo vyote, uepuke!

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki