Wewe Ungefikia Hatua Gani Katika Kulinda Heshima Yako?
WEWE unaweza kuona uhusiano kati ya kujinyonga na kujaribu kufanya mambo usiyoweza kwa sababu wengine wamefanya? Au kati ya kuingia katika deni kubwa kwa ajili ya sherehe ya kidini ya kutapanya fedha, na kukataa kukubali kushindwa katika mabishano? Uhusiano ni kwamba kila moja la mambo haya labda linaongozwa na tamaa ya mtu kulinda heshima yake.
Je! ni vibaya kulinda heshima yako? Si lazima liwe ni jambo baya kudumisha heshima ya kibinafsi. Yesu alipotuamuru ‘tupende jirani zetu kama nafsi zetu wenyewe,’ alimaanisha kwamba kungekuwa na kiasi fulani cha kujifikiria sisi wenyewe. (Mt. 22:39) Kuwa na hali ya kujiheshimu kunatusaidia tujidumishe kuwa safi, wenye kutegemeka na wanyofu. Ni nani anayetaka kufikiriwa kuwa mchafu, asiyetegemeka na mdanganyifu?
Lakini, kuna hatua ya kulinda heshima kupita kiasi. Kufanya hivyo kunatoa wazo la kwamba sifa au heshima yetu ndilo jambo la maana kupita yote. Kwa mfano, kulingana na mtazamaji mmoja, katika Japani “kuepuka aibu ni jambo la mamlaka . . . kama vile kuwa na ‘dhamiri safi,’ ‘kuwa katika hali inayofaa machoni pa Mungu,’ na kuepuka dhambi kulivyo katika desturi za Magharibi.” Ili kuepuka aibu, au kulinda heshima, mtu angekuwa tayari kujinyima mambo fulani, kama vile Mkristo angejinyima ili kudumisha dhamiri safi. Wakati mmoja huko Japani, watu wengine hata walijiua kwa kujichoma na kutoa nje matumbo yao wakati walipotishwa kutendwa jambo la aibu. Wewe ungefikia hatua hiyo katika kulinda heshima yako?
Mambo Ambayo Watu Wanafanya Kulinda Heshima Yao
Katika nchi za Mashariki, bado watu wengine wanajiua wanapoona heshima yao ikielekea kuharibiwa, ingawa kwa kawaida hawajichomi na kutoa nje matumbo yao siku hizi. Wanajinyima mambo mengine, pia. Wakati wa sikukuu ya wafuasi wa Buddha, katika maeneo mengine ni kawaida ya jamaa fulani-fulani kutumia mshahara wa juma zima kwa kununua chakula kimoja cha sherehe ili wasipoteze heshima machoni pa jirani zao. Mahali pengine, huenda mwanamume akapeleka mgeni kwenye mkahawa ulio wa bei ya juu zaidi mjini ili kumfurahisha. Labda mwanamume huyo hana fedha za kuweza jambo hilo, na inaelekea mgeni mwenyewe angependelea zaidi kula katika nyumba ya mtu huyo. Lakini mkaribishaji anajisikia ni lazima afanye hivyo ili kulinda heshima yake.
Katika nchi moja, desturi ni kwamba wakati binti ya mwanamume anapoolewa, mwanamume huyo ndiye atakayewapa hao waliooana karibuni nyumba iliyotiwa vifaa vya matumizi. Baba anajipatia heshima akitia vifaa vizuri ndani ya nyumba hiyo. Kwa hiyo, watu wengine wanaingia sana katika madeni ili kufanya hivyo. Kwa kawaida, bwana-arusi ndiye anayetoa mahari kwa ajili ya anayekuwa mke wake. Ili kulinda heshima yake, huenda kijana mwanamume akaingia pia katika deni ili kutoa mahari nyingi. Lakini, baba ya bibi-arusi, ambaye labda ana deni tayari baada ya kutoa ile nyumba yenye vifaa, ataelekea kukataa mahari hiyo kwa kuirudisha. Hangetaka apoteze heshima kwa kuzikubali fedha hizo.
Wewe ungefikia hatua hiyo ili kulinda heshima yako? Wengi wanaifikia. Ziko njia nyingine, pia, ambazo mtu anaweza kupatwa na tamaa ya kulinda heshima yake. Katika nchi moja ya Mashariki, wakati mtu anapotaka kuwa Mkristo, mara nyingi anashtakiwa juu ya kupotezea jamaa yake heshima kwa “kujiunga na dini ya Magharibi.” Bila shaka, Ukristo si “dini ya Magharibi,” lakini ndivyo unavyoonwa katika nchi hiyo. Ingawa hatutaki kuudhi watu isivyo lazima, kwa wazi si jambo la hekima kuepuka kufanya tunayojua kuwa haki kwa kuogopa kupoteza heshima.
Maelekeo ya Ulimwenguni Pote
Maelekeo ya kutaka kulinda heshima hayaonekani katika nchi za Mashariki tu; ni ya ulimwenguni pote. Kwa mfano, chukua lile jambo la mtu kujaribu kufanya mambo asiyoweza kwa sababu yamefanywa na wengine. Fikiria mwanamume mwenye motakaa inayofaa kabisa mahitaji yake. Siku moja jirani yake ananunua motakaa ya namna mpya, ya bei ya juu. Yule mwanamume, ambaye alikuwa ametosheka vizuri na motakaa yake kabla ya hapo, sasa anaacha kutosheka. Kwa sababu gani? Anaionea aibu. Ile motakaa mpya ya jirani yake inafanya gari lake lionekane kuwa kuukuu. Kwa hiyo ananunua motakaa mpya asiyohitaji wala asiyoiweza. Jambo linalomchochea, yaani kuaibika machoni pa jirani zake, linafanana sana na lile lililosukuma watu fulani wa Mashariki kujiua kwa kujichoma na kutoa nje matumbo.
Halafu tena, je! umepata kukasirika wakati mtu fulani alipokupa shauri au sahihisho? Je! ulijiwazia hivi: “Huko ni kunionea! Yeye ni nani hata anionyeshe makosa? Hata yeye mwenyewe ni ovyo tu!” Kwa kufanya hivyo ulikuwa ukijitetea. Kwa sababu gani? Kwa sababu fahari, au heshima yako, ilikuwa imeguswa.
Nyakati nyingine huenda mtu akajinyima kwa kufanya jambo kubwa ili alinde heshima yake. Labda anatenda dhambi nzito. Anashindwa kujikaza akubali hilo mbele ya wengine na kumaliza jambo hilo. Kosa lake linapojulikana kisha Wakristo waliokomaa wanalizungumza naye, anakataa kwamba hakulitenda. Kwa sababu ya aibu au ugumu wa moyo, hata anakuwa na nia ya kujitenga na kundi la Kikristo, hivyo akitia hatarini uhusiano wake na Muumba wake na tumaini lake la uzima wa milele. Wewe ungefikia hatua hiyo ili kulinda heshima yako?
Halafu, namna gani mtu fulani akikutenda wewe dhambi? Je! ni jambo jepesi kwako kumtolea msamaha? Au unadai “haki”? Nyakati nyingine huenda Mkristo akatenda mwingine dhambi. Aliyekosewa anapelekea wazee wa kundi jambo hilo, kisha mtenda dhambi anakaripiwa na kurudishwa. Lakini aliyetendwa dhambi anashindwa kusahau jambo hilo. Anafikiri wazee walichukua mambo juu-juu na anaona kwamba dhara alilotendwa halikuchukuliwa kwa uzito vya kutosha. Kwa sababu gani anawaza hivyo? Je! ingeweza kuwa kwamba anaona fahari yake iliyopunguzwa ni ya maana zaidi kwake kuliko kurudishwa kwa ndugu mwenye kukosa? Yaani, heshima yake inastahili kwamba mtenda dhambi apewe taabu?
Mifano mingine mingi ingeweza kutajwa. Umepata kuona mtu anayekataa kukubali amefanya kosa, hata wakati mambo ya uhakika yanapokuwa wazi kabisa kwa kila mtu mwingineye yote? Au unajua mtu fulani asiyependa kupewa maoni, anayechukizwa na kuudhika anapotoa maoni yasiyokubaliwa na wengine, au mwenye shingo ngumu na asiyeacha kushikilia maoni yake? Je! unafahamiana na mtu fulani mwenye majivuno ya kupita kiasi juu ya kazi yake ya umashuhuri au elimu yake ya juu, au, tofauti na hivyo, mwenye kuona aibu kwa sababu hana elimu hiyo? Tabia zote hizo zinaweza kuwa vionyesho vya mtu kuhangaikia heshima yake binafsi.
Kwa hiyo, ingefaa Mkristo ajiulize: “Mimi ningefikia hatua gani katika kulinda heshima yangu? Kwa kweli, ninapaswa kulionaje shauri lote la kulinda heshima yangu?”