Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Paulo alisema kwamba mwangalizi wa kundi lazima awe ni “mume wa mke mmoja.” Sababu gani apange hiyo kati ya sifa za kustahilisha watu kuwa waangalizi, kwa kuwa hakuna Mkristo angeweza kuoa wake wawili au wengi zaidi?
Katika 1 Timotheo 3:2 (NW) mtume Paulo aliandika hivi: “Kwa hiyo imempasa mwangalizi awe bila lawama, mume wa mke mmoja, mwenye kiasi katika mazoea.” Maneno yanayosema “mume wa mke mmoja” yangemaanisha kwamba mwanamume huyo hatiliwi mashaka yo yote na watu juu ya kufanya ubaya unaohusu ngono, kwamba yeye ni mfano mwema wa kufuata kiwango cha Kikristo juu ya ndoa.
Yesu alikuwa ameelekeza kwamba wanafunzi wake wanapaswa kushikilia mpango wa kwanza wa Mungu kuhusu ndoa, yaani, mume mmoja kuoa mwanamke mmoja. (Mathayo 19:5, 6) Kwa hiyo, hakuna mtu angeweza kubatizwa awe Mkristo mpaka kwanza aache kuwa na wake wengi. Hata hivyo ilifaa Paulo akakazia jambo hilo kwa wazee, kwa sababu ndoa ya wake wengi ilikuwa imeruhusiwa kati ya Wayahudi na ingeweza kufuatwa sana katika nchi ambako Ukristo ulienea. Mtu mpya mwenye kushirikiana na kundi angepaswa kuweza kuona kutokana na mfano wa wazee kwamba kuoa mke mmoja, si wengi, ndio mpango unaokubalika kwa Wakristo.
Lakini yale maneno yanayosema “mume wa mke mmoja’’ yanaweza kumaanisha zaidi ya hilo. Hali ya kutokujali sana maadili wakati huo ilionyeshwa na talaka zilizofanywa mara nyingi kwa sababu ndogo-ndogo na watu wakawa wakioa-oa wake wapya.
“Katika uhuru usiofaa kuhusu talaka, ulioruhusiwa na sheria ya Wagiriki na hata ya Waroma, lilikuwa jambo la kawaida sana mwanamume na mke wake kutengana na kuoana na watu wengine kabla mwenzi wao hajafa. Hivyo mwanamume angeweza kuwa na wake watatu au wanne walio hai; au, tuseme, wanawake ambao wote walikuwa wamekuwa wake zake kwa mfululizo.” (Kitabu The Life and Epistles of St. Paul, kilichoandikwa na Conybeare na Howson) Hali haikupasa kuwa hivyo kwa Mkristo. Ni wakati tu mwenzi wake wa ndoa angefanya “uasherati” (ufisadi mbaya sana unaohusu ngono) ndipo angekuwa huru kupata talaka na kuoa mwingine. (Mathayo 5:32; 19:9) Sifa ya “mume wa mke mmoja” ingemaanisha kwamba mzee angewekea wengine mfano kwa kutokuwa mwanamume aliyetolea mke talaka bila sababu za Kimaandiko kisha akaoa mwingine.
Wanachuo fulani wameelewa andiko la 1 Timotheo 3:2 kuwa linamaanisha kwamba mzee hawezi kamwe kuoa mara ya pili. Lakini, maneno aliyotangulia kuyasema Yesu na yale ambayo Paulo aliandika penginepo yanaonyesha kwamba halikuwa kosa kuoa au kuolewa upya, kwa hiyo kuoa tena kusingefanya mwanamume awe na lawama wala kusingemfanya awe hastahili kutumikia akiwa mzee kundini. Kumbuka Paulo aliandika kwamba wajane (na basi hata wajane-wanaume) wangefanya vizuri zaidi kuoa au kuolewa badala ya kuwaka tamaa au kuwa watu wenye kutumia saa zao zote wakijishughulisha na mambo ya watu wengine.—1 Wakorintho 7:8, 9, 36-39; 1 Timotheo 5:13, 14.
Kuwa kwa mzee “mume wa mke mmoja” kungetoa pia wazo la kwamba yeye hangekuwa na hatia ya kuwa na wake wawili au ya kufanya uzinzi. Angepaswa kuwa mtu asiyelaumika katika tabia za maisha yake ya ndoa, awe mtu mshikamanifu na mwaminifu kwa mke wake. Hivyo, The New English Bible inautafsiri mstari huo hivi, mwangalizi “lazima awe asiyeweza kusutwa, mwaminifu kwa mke wake mmoja.”
Kwa hiyo, Paulo aliposema kwamba mwangalizi lazima awe ni “mume wa mke mmoja,” alikuwa akitumia maneno machache kukazia pande mbali-mbali za mfano bora sana wa kiadili unaopasa kuwekwa na mzee aliyeoa. Angepaswa awezeshe mtu ye yote kumtazama na kuona kwamba huyo alikuwa mfano halisi wa mtu mwenye kufuata maoni mema sana ya ndoa yanayopatikana katika Ukristo wa kweli.