Je! Tunakaribia Har–Magedoni?
“Kwa kuwa wakati huo kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo [tena] kamwe.”—Mt. 24:21.
1. (a) Watu wengine wanafahamu “Har–Magedoni” kuwa na maana gani? (b) Je! Har–Magedoni ni vita nyingine tu kati ya mataifa?
NENO “Har–Magedoni” hutoa sauti yenye kutisha katika masikio ya watu wengi. Wengine wanalifahamu kuwa lina maana ya “mwisho wa ulimwengu” wakati ambapo uhai wote wa kibinadamu utaangamizwa na dunia kuachwa katika hali ya kutoweza kukaliwa, pengine kwa njia ya vita yenye kutumia silaha za nuklea kati ya mataifa. Ni kweli, neno la Kiingereza “Armageddon” au “Har–Magedoni,” humaanisha tukio lenye kuleta uharibifu mkubwa, vita. Walakini Biblia husema kwamba ni “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi,” inayopiganiwa katika mahali panapoitwa “Har–Magedoni.”—Ufu. 16:14, 16.
2. Je! Har–Magedoni itamaanisha mwisho wa wanadamu, au wa dunia?
2 Je! vita ya Mungu ya Har–Magedoni ingeweza kumaanisha mwisho wa wanadamu wote, au mwisho wa sayari hii? Sivyo, hata kidogo. Neno la Mungu mwenyewe latuhakikishia hivi: “[Yehova], aliyeziumba mbingu, asema hivi; Yeye ni Mungu; ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu.”—Isa. 45:18.
3. Har–Magedoni itatimiza jambo gani?
3 Ijapokuwa Har–Magedoni haitamaanisha mwisho wa wanadamu wote, wala wa dunia, bila shaka itamaanisha mwisho wa taratibu ya mambo (au, “ulimwengu”) kama vile tuujuavyo. Har–Magedoni itakuwa njia ya Mungu ya kuponda-ponda na kufutilia mbali taratibu za leo za kisiasa, kiuchumi, kijamii na kidini ambazo zimeleta huzuni nyingi sana. “Nimeazimia,” asema Yehova, “kuwakusanya mataifa, ili nizikutanishe falme, nipate kuwamwagia ghadhabu yangu; naam, ukali wote wa hasira yangu.” (Sef. 3:8) Hivyo, vita ya Mungu ya Har–Magedoni itamaanisha kutekelezwa kwa hukumu yake mbaya juu ya “wafalme,” “mataifa” na “falme.” Wengine watakaopatwa na hukumu hii mbaya, yasema Biblia, ni wale wanaounga mkono hii taratibu mbovu ya mambo, yaani, “majemadari,” “watu hodari,” “waungwana,” “watumwa” na “wadogo kwa wakubwa.”—Ufu. 16:14; 19:18.
4. Unabii wa Biblia unaeleza kuwa hali zitakuwaje baada ya Har–Magedoni?
4 Mwisho wa taratibu iliyopo utatayarishia njia taratibu mpya kabisa iliyofanywa na Mungu, jamii ya kibinadamu ambayo kwayo mapenzi ya Mungu yatafanywa “hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mt. 6:10) Katika taratibu hiyo mpya baada ya Har–Magedoni, watuambia unabii wa Biblia, “haki itakaa.” (2 Pet. 3:13, NW) Litakuwa jambo lenye kuburudisha na kusisimua kama nini baada ya karne nyingi hizo za kutendewa isivyo haki, kuteseka, maumivu ya moyoni na machozi! Mapenzi ya Mungu yakiwa yanafanywa duniani pote na hali zenye haki zikiwa zimesimamishwa, wakati wa furaha isiyopata kuonekana wakati wo wote uliotangulia utaanzishwa. Biblia inatabiri hivi: “Wenye upole watairithi nchi, [nao] watajifurahisha kwa wingi wa amani.” (Zab. 37:11) Si ajabu kwamba Yesu aliiita “Paradiso.”—Luka 23:43, ZSB.
“DHIKI KUBWA” INAYOKUJA
5. “Dhiki kubwa” ni nini, nasi twajuaje kwamba itakuwa ya muda mfupi tu?
5 Vita ya Mungu ya Har–Magedoni itakuwa ndiyo sehemu ya kumalizia ya kipindi cha wakati kinachoitwa “dhiki kubwa.” Yesu alisema juu yacho hivi: “Kwa kuwa wakati huo kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo [tena] kamwe.” (Mt. 24:21) Tukifikiria misiba ambayo imepata kutokea katika wakati uliopita, inakuwa wazi kwamba hiyo “dhiki kubwa” inayokuja itakuwa wakati wa msuko-suko usio na kifani katika historia yote ya wanadamu. Walakini kwa rehema, utakuwa wakati mfupi sana, ambao Mungu ‘atafupiza.’ —Mt. 24:22.
6. Ni kwa sababu gani tunaweza kuelekeana na “dhiki kubwa” tukiwa na uhakika?
6 Walakini, ijapokuwa hiyo “dhiki kubwa” itakuwa ndiyo wakati wa taabu zaidi, twaweza kufarijiwa na uhakika wa kwamba unatangulia tu wakati ulio bora zaidi—katika taratibu mpya ya Mungu. Tena, kuna taraja lenye furaha sana kwamba watu wengi wanaoishi sasa watauokoka wakati huo wa taabu unaokuja! Neno la Mungu linaahidi kwamba “mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha,” ‘watatoka katika dhiki ile iliyo kuu’ wakiwa waokokaji. Hata sasa Mungu amefuta kila chozi katika macho yao. (Ufu. 7:9, 14,17) Kwa sababu hiyo, Yesu alikuwa na mataraja mazuri sana kwa wakati ujao, ijapokuwa alijua kwamba wanadamu wangeelekeana na “dhiki kubwa.” Haya ndiyo maneno yake yanayojaa tumaini: “Mambo hayo yaanzapo kutokea, changamkeni, mkaviinue vichwa vyenu, kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia.”—Luka 21:28.
7. Ni kwa sababu gani wengine wanaona kwamba mambo ya wanadamu yanakaribia upeo fulani?
7 Kwa makumi mengi ya miaka, Mashahidi wa Yehova peke yao wamekuwa na shughuli nyingi katika mataifa yote wakitoa onyo juu ya wakati huu wa taabu unaokuja ambao utafikia upeo wake kwenye Har–Magedoni. (Marko 13:10) Hata hivyo, katika nyakati nyingine, wengine wanafahamu kwamba jambo fulani lenye kuleta uharibifu mkubwa linakaribia, kwa kuwa wanaona hali za ulimwengu zikizidi kuwa mbaya bila kuwa na tumaini lo lote la kweli au lenye kudumu la kuleta maendeleo. Kwa mfano, katika Mei 4, 1980, mhariri wa gazeti Miami Herald, Jim Hampton aliandika hivi:
“Je! wewe, kwa maoni yako, unaliona tatizo likikua, kama lile ninaloona likikua ndani yangu? Tatizo kubwa linalokufanya usilale usingizi usiku, likikuambia kwamba kuna kasoro kubwa katika nchi yako, katika ulimwengu wote? Tatizo linaloogopesha mara nyingine kwa sababu umepata kufahamu kwamba Har–Magedoni si fumbo tu la maneno unalosoma katika Biblia, [bali] ni kweli? Na kwamba kwa mara ya kwanza maishani mwako kuna hali inayoelekea sana kuchochea ugomvi na kutokeza Har—Magedoni?
“Mimi ninalo tatizo hilo. Sioni haya kusema hivyo, kwa sababu nimeuliza rafiki wengi kama nao wanaona hivyo, wote wanaona hivyo. . . .
“Hata mtu asiyefikiri sana anaweza kujumlisha matukio yote yenye uharibifu mkubwa ya miaka michache iliyopita na kupata kufahamu kwamba ulimwengu unaingia kipindi chenye maana kubwa kama vile kipindi cha kuelevuka, kipindi cha usitawi wa viwanda, au kipindi cha kutumia mashine za umeme. Kitabadili milele namna ya maisha ya wanadamu.
“Lakini tofauti na vipindi hivyo, vilivyoleta faida kubwa kwenye maendeleo ya ustaarabu, [kipindi] hiki . . . kinaelekea sana kuleta mabaya ya namna ambayo ulimwengu haujapata kuona kamwe.”
Ijapokuwa mhariri huyo hakuwa akiiona Har–Magedoni katika maoni ya Kibiblia, alikuwa sahihi katika kusema kwamba wanadamu wanakaribia wakati wa taabu “ya namna ambayo ulimwengu haujapata kuona kamwe.” Wanachokaribia wanadamu hasa ni ile “dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo [tena] kamwe,” kama vile alivyotabiri Yesu.
8. Tunahitaji habari gani, na kwa sababu gani?
8 Kwa hiyo ikiwa tunapenda uzima nasi twataka tupate kuishi katika taratibu yenye haki yenye kufanywa na Mungu, tunahitaji sana kujifunza juu ya “dhiki kubwa” hiyo inayokuja na upeo wake. Har–Magedoni. Tunahitaji majibu yenye mamlaka kwa maulizo kama vile: Twajuaje kwamba tunakaribia kweli kweli hiyo “dhiki kubwa”? Ni tukio gani litakalokuwa ishara ya kweli kwamba imeanza kweli kweli?
TUNAVYOJUA KWAMBA TUNAKARIBIA
9, 10. Biblia inakielezaje kipindi cha wakati kinachofikia kwenye Har–Magedoni?
9 Wakati Yesu aliposema juu ya “dhiki kubwa” inayokuja, alitabiri vilevile baadhi ya matukio ambayo yangeonyesha kukaribia kwayo. Katika pindi moja wanafunzi wake walimwuliza ni nini ingekuwa “ishara” ya “mwisho wa taratibu ya mambo.” (Mt. 24:3, NW) Yesu alisema juu ya kizazi fulani cha watu ambao wangeanza kupatwa na magumu kwa kadiri isiyopata kuonwa hapo mbele. Alitabiri kwamba kizazi hicho kingepatwa na vita vya mataifa yote, magonjwa ya kipuku, na upungufu wa chakula pamoja na matetemeko ya ardhi “mahali hapa na mahali hapa.” Yeye aliyaita matukio hayo “mwanzo wa maumivu makali ya ghafula ya taabu.” Magumu hayo yangekuwa makubwa sana hivi kwamba kungekuwako “huzuni kuu ya mataifa, wasijue njia ya kutokea,” na watu wengi “wakizimia mioyo kwa sababu ya hofu na kutazamiwa kwa mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa na watu.”—Mt. 24:7, 8, 34, NW; Luka 21:10, 11, 15, 26, NW.
10 Kama miaka 32 hivi baadaye, mtume Paulo, akiwa chini ya uongozi wa roho takatifu ya Mungu, aliandika unabii juu ya “mwisho wa taratibu ya mambo,” akisema hivi: “[Katika] siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna.” Unabii huo wasema vilevile kwamba “watu wabaya na wadanganyaji wataendelea, na kuzidi kuwa waovu,” kuonyesha kwamba baada ya “siku mwisho” kuanza, mambo ya wanadamu yangeendelea kuharibika, yakifikia upeo wake wakati wa kutokea kwa ile “dhiki kubwa.”—2 Tim. 3:1-5, 13.
11, 12. Ni kwa sababu gani mwaka wa 1914 ulikuwa mwaka wenye maana katika historia?
11 Pasipo shaka yo yote, tunaishi sasa katika kipindi cha wakati ambacho katika hicho Yesu na waandikaji wa Biblia walioongozwa kwa roho kama vile Paulo walielekeza! Kwa kweli, kipindi hicho kimekuwa kikiendelea tangu mwaka wenye maana sana wa historia ya kisasa, mwaka wa 1914, uliokuwa mwanzo wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Wanahistoria wengi wanautaja kwa usahihi mwaka huo kuwa wenye kuleta mabadiliko kwa wanadamu, kwa sababu huo ndio wakati ambapo ulimwengu uliingia kwenye kipindi chenye magumu ambayo hayajapata kuonwa kamwe kwa kadiri kubwa namna hiyo duniani pote. Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilikuwa ushuhuda wa hilo, kwa kuwa ilikuwa mbaya zaidi kuliko vita nyingine yo yote iliyoitangulia, na ndiyo sababu, katika wakati huo, ilikuwa ikiitwa “Ile Vita Kuu.” Ilikuwa ndiyo vita ya kwanza ya ulimwengu wote. Ilikuwa vita ya jumla nayo ilitia ndani karibu kila nchi iliyomo duniani.
12 Kuhusu Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, Martin Kieffer aandika hivi katika utangulizi wa kitabu kiitwacho La Grande Guerre (Ile Vita Kuu), kilichoandikwa na Jemadari Richard Thoumin, kilichochapiwa Ufaransa hapo mwanzoni: “Damu na machozi ya vita ya Ulimwengu ya Kwanza vilibadili uso wa dunia.” Jemadari huyo aliandika vilevile hivi:
“Wakati mwishowe silaha zilipowekwa chini katika Novemba wa [mwaka] 1918, watu milioni kumi walikuwa wamepoteza uhai wao, na mara mbili ya hao walikuwa wamejeruhiwa au wakalemazwa. Si ajabu kwamba vita hiyo inaitwa ile “Vita Kuu’ . . .
‘Ukuu’ usio na kifani wa hiyo Vita ya Kwanza . . . ni kwa sababu ya kuenea pote na wingi wa vitu vilivyotengenezwa na viwanda ili vitumiwe na vitu vilivyoharibiwa . . . Nchi nyingi kadiri hiyo na majeshi makubwa kadiri hiyo hayajapata kamwe kupigana katika vita vikubwa kadiri hiyo; sehemu kubwa kadiri hiyo ya wapiganaji hazijapata kamwe kuuawa au kujeruhiwa; wanadamu hawajapata kamwe kwenda vitani wakiwa na silaha zenye nguvu kadiri hiyo.”
13. Ni matukio gani mengine yaliyotukia karibu na Vita ya Ulimwengu ya Kwanza yanayoonyesha kwamba “siku za mwisho” zilianza wakati huo?
13 Katika mwaka 1918, kabla ya vita hiyo kumalizika, yale maradhi ya kipuku ya homa ya Kispania yalianza kuenea katika dunia yakiua zaidi ya watu milioni 20, wengi zaidi kuliko idadi ya waliokufa katika vita. Wakati na baada ya vita hiyo, mamilioni mengi zaidi walikufa kwa sababu ya ukosefu wa chakula. Vilevile, matetemeko ya ardhi yaliua wengi: katika mwaka 1915 karibu watu 30,000 walikufa katika Italia; katika mwaka 1920 180,000 walikufa huko China, katika mwaka 1923 143,000 waliangamia katika Japan. Akiwa na sababu nzuri mleta habari Frank Peters aliandika hivi katika gazeti St. Louis Post-Dispatch: “Katika [mwaka] 1914 ustaarabu uliingia kwenye ugonjwa mkali na pengine wenye kuua.” Ndiyo, vita vya ulimwengu, magonjwa ya kupuku, upungufu wa chakula na matetemeko ya ardhi “mahali hapa na mahali hapa.” Bila shaka, matukio hayo yalikuwa “mwanzo wa maumivu makali ya ghafula ya taabu” aliyoyatabiri Yesu. “Siku za mwisho,” ule “wakati wa mwisho,” ulikuwa umeanza kweli kweli!—Mt. 24:8, NW; 2 Tim. 3:1; Dan. 12:4.
USHUHUDA ZAIDI
14. Ni kwa sababu gani twaweza kusema kwamba tumeingia ndani sana katika “siku za mwisho”?
14 Sasa, katika mwaka 1981, miaka 67 imepita tangu tarehe hiyo yenye maana ya mwaka 1914. Katika wakati huo, Vita ya Ulimwengu ya Pili ilitokea vilevile, ikaua watu milioni 55, ikamalizika huku miji miwili ikiwa imeharibiwa kwa kombora la atomiki, na kuanza kizazi chenye kutumia silaha za nuklea. Tangu wakati huo hali zaonyesha kwamba wanadamu wameshindwa kumaliza magumu yao, na kila sehemu ya taratibu hii ya mambo inaharibika. Hayo yote yanatuambia kwamba tumeingia ndani sana kwenye zile “siku za mwisho,” na kwamba matukio yanapiga mbio kuelekea ile “dhiki kubwa.”
15, 16. Wengine wanasema nini juu ya hali katika wakati wetu?
15 Kwa mfano, mwishoni mwa mwaka 1979 mtaalamu wa mambo ya uchumi Leonard Silk aliandika hivi: “[Katika] majira haya ya mapumziko, pengine bidhaa inayokosekana zaidi si mafuta bali tumaini. Kwa kuwa, [kipindi cha] miaka kumi cha 1970 na kitu kikiwa katika siku zake za mwisho, hatari zinazoukabili uchumi wa ulimwengu—na amani ya ulimwengu—zinaongezeka.” Mwandikaji wa habari Max Lerner alisema hivi katika masika ya mwaka uliopita, 1980: “Ulimwengu unaonekana kuwa umefikia mahali ambapo infuleshoni, migomo, kufilisika, kushikilia mambo bila akili na ukatili wenye kuogopesha [ni mambo] yanayokaribia sana kuhakikisha kwamba hakuna jambo linaloleta matokeo na hakuna ye yote anayeongoza [mambo]. Je! ye yote anaweza kuongoza mahali po pote?”
16 Wakati meya (wakuu wa miji) mikubwa katika United States (Amerika) walipoulizwa kwa sababu gani miji mingi hivyo ilikuwa katika hali mbaya sana, mmoja wao alijibu hivi: “Magumu yanaelekea kutoshindika. Ye yote asiyekatishwa tamaa hafikiri.” Meya mwingine aliulizwa kama miji imekuwa ‘isiyotawalika’ sasa, naye akasema kwamba mambo ya hakika ‘yanamfanya mtu kufikiri hivyo.’ Hali moja na hiyo, mwandikaji wa kitabu Scarcity (Ukosefu), alisema hivi: “kushambuliwa barabarani, kuvunja nyumba, kuuawa kwa mapolisi, uuzaji na ununuzi wa dawa za kulevya [ni mambo ambayo] yameleta hali inayokaribia sana mchafuko wa serikali ya miji mingi.”
17. Uchunguzi mkubwa ulikiongoza kikundi kilichoongozwa na afisa mwanasiasa mwenye kujulikana sana kifikie mkataa gani?
17 Aliyekuwa hapo zamani kiongozi wa Jamhuri ya Mwungano wa Ujeremani Willy Brandt aliongoza kikundi ambacho kilifanya uchunguzi juu ya hali za ulimwengu kwa muda wa miaka miwili. Walifikia mkataa huu hivi karibuni:
“Katika mwanzo wa [miaka ya] 1980 na kitu jamii ya ulimwengu inaelekeana na hatari kubwa zaidi kuliko wakati mwingine wo wote tangu Vita ya Ulimwengu ya Pili. Ni wazi kwamba hali ya uchumi ya ulimwengu inafanya kazi katika njia mbaya sana hivi kwamba inahatirisha faida za mataifa yote za wakati ujao ulio karibu na za ule ulio mbali utakaokuja. . . .
“Magumu ya umaskini na njaa yanazidi; tayari kunao [watu] milioni 800 walio maskini kabisa na idadi yao inaongezeka; upungufu wa nafaka na chakula kingine unaongeza taraja la njaa na kufa njaa. . . .
“Watoto kati ya milioni 20 na 25 walio chini ya umri wa miaka mitano wanakufa kila mwaka katika nchi zinazoendelea . . .
“Idadi fulani ya nchi maskini zinatishwa na uharibifu usioweza kuepukika wa taratibu za mazingira na viumbe vyake hali nyingine nyingi zikipatwa na upungufu wa chakula unaozidi kuongezeka na pengine watu wengi wakifa njaa. Katika uchumi wa mataifa yote kuna uwezekano wa . . . kuanguka na watu wengi wenye deni kushindwa kulipa deni zao kubwa, au banki kushindwa [kufanya kazi] . . . [na] kuongezeka kwa kushindania mamlaka juu ya mali kukiongoza kwenye vita vya kutumia jeshi.”
18. Ni matukio gani ya hivi karibuni katika mambo ya ulimwengu yanayothibitisha kwamba njia inatayarishwa kwa ajili ya “dhiki kubwa”?
18 Ongeza juu ya hayo yote kuharibika kwa maisha ya jamaa na ndoa katika miaka ya karibuni kunakojulikana sana, ongezeko kubwa sana katika uvunjaji wa sheria na jeuri ya kila namna, ongezeko kubwa sana la matumizi mabaya ya dawa za kulevya na ulevi, pamoja na ongezeko katika uasi wa vijana. Je! si wazi kabisa kwamba msingi wenyewe wa jamii ya binadamu unaharibika, kama alivyosema Yesu kuwa ingekuwa kabla tu ya kutokea “dhiki kubwa”? (Mt. 24:12) Kuongezea hayo, ebu fikiria hali hii yenye kuendelea kama vile ilivyoonyeshwa katika gazeti World Press Review: “Ulimwengu wa [miaka ya] themanini na kitu unaogopesha katika njia nyingi, si kwa sababu tu ya umaskini na ukosefu wa haki unaotaabisha wengi . . . bali kwa sababu ya mashine [zenye uwezo wa] kuharibu ulimwengu wote ambazo wanadamu wanacheza nazo.” Liliziita mashine hizo “zenye kuogopesha,” wala si ajabu, kwa kuwa gazeti la Uingereza New Scientist linaripoti hivi: “Katika ghala za silaha za vita kunayo leo, makombora ya nuklea karibu 60,000 yakiwa na nguvu za mlipuko unaolingana na tani milioni 16,000 za TNT (zinalingana na makombora 1,250,000 kama yale yaliyoangushwa Hiroshima).” Nyingine za silaha hizo ni zenye hatari sana hivi kwamba kombora moja peke yake laweza kuangamiza nchi ndogo, au sehemu ya nchi kubwa. Ndiyo, kwa mara ya kwanza katika historia, wanadamu wana uwezo wa kuangamiza sehemu kubwa ya uhai duniani.
19. Ni nani tunayepaswa kumtumainia atatue matatizo ya leo?
19 Je! tufikiri kwamba kwa njia fulani, hata hivyo, viongozi wa ulimwengu, kwa sababu huenda wakawa wanyofu, wenye akili, wenye maarifa na wenye nguvu, watatatua matatizo hayo? Ebu angalia anayosema Michael Blumenthal aliyekuwa hapo zamani Katibu wa Hazina wa United States: “Hakuna anayefahamu kabisa hali iliyopo. Hiyo inatia ndani maafisa wote wa serikali wanaotayarisha maongozi ya mambo ya serikali. Wao wanatatizwa kama vile wewe tu unapofungua gazeti asubuhi. Uhakika ni kwamba hakuna ye yote . . . ambaye ameweza kwa kweli kutabiri kwa kadiri yo yote ya usahihi matatizo ambayo tumeingia ndani yake.” Walakini Biblia ilifanya hivyo, nayo inaongeza shauri hili la hekima: “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake.” Badala yake, “Heri [yeye] ambaye . . . tumaini lake ni kwa [Yehova], Mungu wake. . . . Huishika kweli milele.” —Zab. 146:3-6.
20. Ni jambo gani tunaloweza kuwa na hakika nalo, na kwa hiyo tunahitaji kujibu ulizo gani?
20 Bila shaka, hali zote zilizotabiriwa katika unabii wa Biblia zipo hapa. Kwa kweli tumeingia sana katika “siku za mwisho” za hii taratibu ya mambo nasi tunakaribia sana sehemu ya mwisho, ile “dhiki kubwa” pamoja na Har–Magedoni yake itakayomalizia. Nalo ni jambo gani litakalokuwa ishara ya kutokea kwa hiyo “dhiki kubwa”? Ni tukio ambalo hata sasa limekwisha endelea sana. Ni tukio gani hilo? Mazungumzo juu yake yanafuata katika makala inayofuata.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Katika taratibu mpya ya Mungu, watu “watajifurahisha kwa wingi wa amani”