Neno la Mungu Li Hai
Inakuwaje Wakati wa Kufa?
LAZARO, rafiki mwema wa Yesu amekufa. Hata hivyo, Yesu awaambia wanafunzi wake hivi: “Rafiki yetu, Lazaro, amelala; lakini ninakwenda huko nipate kumwamsha.”
“Bwana, ikiwa amelala, atapona,” wakajibu wanafunzi.
Kusikia hayo, Yesu anawaambia waziwazi “Lazaro amekufa.”
Ni kwa sababu gani Yesu alisema kwamba alikuwa akilala hali kwa kweli yeye alikuwa amekufa? Inakuwaje wakati wa kufa? Kutazama ziara aliyofanya Yesu kwenda kumwona Lazaro kutasaidia kujibu maulizo hayo?
Martha, dada ya Lazaro anapofahamu kwamba Yesu alikuwa anakaribia, anakimbia ili amlaki. Upesi dada yake Mariamu pamoja na rafiki zao wote waja vilevile kumlaki Yesu. Yesu aonapo huzuni yao, analia. Auliza: “Mmemweka wapi?”
Wafikapo kwenye kaburi la ukumbusho—ni pango, nalo jiwe linalilalia—Yesu asema: “Liondoeni jiwe.” Kusikia hivyo, Martha anapinga, kama unavyoweza kuona, akisema: “Bwana, ananuka sasa.” Zimekuwa siku nne sasa tangu Lazaro afe. Hata hivyo, kwa kutiwa moyo na Yesu, jiwe linaondolewa.
Baada ya kusali kwa Mungu, Yesu anaita kwa sauti kuu: “Lazaro, njoo huku nje”! Naye anatoka! Anatoka akiwa hai, bado akiwa amefungwa kwa vitambaa vya kaburini. “Mfungueni, mkamwache aende zake,” asema Yesu.—Yohana 11:11-44.
Sasa fikiria hili: Hali ya Lazaro ilikuwa namna gani wakati wa hizo siku nne alipokuwa amekufa? Je! yeye alikuwa mbinguni? Alikuwa mtu mwema. Hata hivyo yeye hakusema lo lote juu yake kuwa mbinguni, Jambo ambalo bila shaka angefanya kama alikuwa huko. La, Lazaro alikuwa amekufa kweli kweli, hata kama vile Yesu alikuwa amesema. Basi ni kwa sababu gani hapo mwanzoni Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba Lazaro alikuwa akilala tu?
Basi, Yesu alijua kwamba Lazaro huyo aliyekuwa amekufa alikuwa hana fahamu, kama isemavyo Biblia: “Wafu . . . hawafahamu lo lote.” (Mhu. 9:5, NW) Lakini kama vile mtu anayeishi anavyoweza kuamshwa kutoka kwa usingizi mzito sana, vivyo hivyo Yesu angeonyesha kwamba, kwa njia ya uwezo aliopewa na Mungu, rafiki yake Lazaro angeweza kuamshwa kutoka kwenye mauti.
Kwa hiyo, hata kama vile mtu anayelala usingizi mzito sana asivyokumbuka lo lote anapokuwa amelala, ndivyo ilivyo na wafu. Hawafahamu lo lote. Wanakuwa hawapo tena. Walakini, katika wakati aliouweka Mungu, wafu waliokombolewa na Mungu watarudishwa kwenye uhai. Bila shaka ufahamu huo wapaswa utusukume tutake kujipatia kibali ya Mungu ili tupate kuingia katika mpango wake wa kufufuliwa kwenye uhai.—Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15.