Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 10/15 kur. 3-7
  • Kumtumikia Mungu Nyakati za Magumu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kumtumikia Mungu Nyakati za Magumu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UPINZANI KUTOKA KWA MUME WANGU
  • MIAKA MIWILI YENYE FURAHA
  • IMANI YATIWA NGUVU NA MAJARIBU
  • SISI SOTE TWAPAINIA
  • JAMAA NZIMA YETU YAFUNGWA GEREZANI
  • BAADA YA KUFUNGULIWA GEREZANI
  • Zaidi ya Miaka 40 Chini ya Marufuku ya Ukomunisti
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Yehova Huwapa Thawabu Kubwa Wale Wanaoishika Njia Yake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Kumkaribia Mungu Kulinisaidia Niwezane na Hali
    Amkeni!—1993
  • Miaka Zaidi ya 50 ya ‘Kuvuka’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 10/15 kur. 3-7

Kumtumikia Mungu Nyakati za Magumu

KATIKA kipupwe cha mwaka wa 1946, theluji nzito ilikuwa ikianguka katika mashariki ya nchi ya Ulaya ninapoishi. Siku hii ninayosema theluji ilizuia magari-moshi yasifanye kazi, kwa hiyo mimi niliyangoja kwenye kituo nipelekwe jijini, lakini wapi, hakuna. Mtu fulani akanielekezea kidole kwenye kijiji kidogo ambako ilisemwa kwamba bas zilikuwa zikifanya kazi. Lakini nilipokwenda huko, nikakuta hakuna bas zilizokuwa zikisafiri. 

Mara kadha wakati wa miezi kadha iliyopita nilikuwa nimeondoka jijini nikakae peke yangu kwenye miti mingi. Nikiwa mahali hapo pasipo na kelele, nilikuwa nikipiga magoti na kumpelekea Mungu sala. Baada ya kuiokoka miaka mibaya sana ya Vita ya Ulimwengu ya Pili, sala ya namna hiyo tu ndiyo iliyonipa amani na uradhi. Nilikuwa Mkatoliki mwenye kumwamini sana Mungu, lakini sikufarijiwa sana na kusali kanisani mbele ya sanamu zisizo na uhai. Kwa kweli, kwa kuutazama mwenendo wa mapadre nilikaza nia nisirudi tena kanisani. 

Siku hii ninayosema—nikiwa nimekwama mahali hapo kwa muda bila kujua la kufanya, nikiwa mwenye njaa na uchovu—niliiona ishara “Joko la Mikate” juu ya mojayapo nyumba za kijiji. Ingawa bibi mwenye nyumba hiyo alinijulisha kwamba hilo joko la mikate lilikuwa halifanyi kazi, yeye alinifadhili akanipa mkate mdogo kati ya ile yake mwenyewe. Nikauliza: “Unaweza kuniruhusu niketi na kupumzika, tafadhali?” 

Nilipokuwa nimeketi, nikaona kitabu juu ya meza. Nilipojua ni Biblia, nikapendezwa sana sana. Niliongea na mwanamke huyo na mumewe kwa muda mrefu, nikagundua wao walikuwa Mashahidi wa Yehova. Niliyosikia yalikuwa kama maji safi kwa msafiri mwenye kiu. Waliniambia wangenitembelea Jumapili itakayofuata. 

Jumapili iliyofuata nilikuwa tayari. Hata nilikuwa nimetayarisha chakula ili tupate wakati mwingi zaidi kuzungumza bila jambo la kututatiza. Lakini hawakuja. Mume wangu alinitaka niisahau hii “dini mpya.” Mimi nilikuwa nimekata sana tamaa, hata nikafikiria kujiua. Lakini ndipo binti yangu mkubwa zaidi alipoleta barua kutoka kwa wale Mashahidi. Hawakuwa wamesahau! Baada ya muda mfupi tulikuwa tukisaidiwa kujifunza Biblia katika nyumba yetu. Watoto wangu walishiriki, kutia na binti yangu, wa miaka 15, mwana wangu, wa miaka 10, na binti yangu mdogo zaidi, wa miaka tisa. Wote walitayarisha masomo yao vizuri, wakiandika majibu ya maulizo katika vitabu vya kuandikia mambo ya maana. 

Mimi nikaanza kueleza wengine mambo tuliyokuwa tukijifunza, na kufanya hivyo kulinipa nguvu za kiroho na furaha. Katika Agosti 1947 binti yangu mkubwa zaidi na mimi tulibatizwa, na kwa njia hiyo tukaonyesha wakf wetu kwa Yehova Mungu. 

UPINZANI KUTOKA KWA MUME WANGU

Mara nyingi mume wangu alikunywa pombe, akaniletea matata kweli kweli. Alitukataza tusiende kwenye mikutano ya Kikristo. Kwa hiyo nyakati nyingine binti yangu na mimi tulikuwa tukienda kulala mapema, halafu, wakati yeye hakuwa akitutazama, tukawa tukivaa nguo zetu na kuondoka nyumbani. Siku moja, akiwa na shoka mkononi, alinipigia kelele kubwa akisema angenimaliza. Akalizungusha-zungusha shoka, lakini, kwa sababu alikuwa amekunywa sana, shoka lilinikosa, likaanguka nyuma yangu. Nikaweza kupona. 

Mume wangu aliongeza mashambulio yake, na siku moja akajaribu kuniua kwa kutumia jisu kubwa la kukatia nyama. Binti yangu mdogo zaidi na mimi tulikimbilia nyumba ya Mashahidi waliokuwa jirani, huku mume wangu akitufuata moja kwa moja. Kwa sababu Mashahidi hao hawakumfungulia mlango, alivunja madirisha, kisha ikawa lazima polisi waje kuamua jambo hilo. 

Mwanzoni mwa masika ya mwaka wa 1948 mume wangu alikata maneno yake ya mwisho: “Mkae nyumbani au mwende mkamfuate Yehova!” Mimi nilichagua kuondoka nyumbani, kuviacha vyumba vyetu vinne vyenye vifaa, badala ya kuyaacha mambo tuliyokuwa tumejifunza. Nilichukua vitu vyangu mwenyewe tu na watoto wangu watatu. Vitu vyote tulivyochukua vingeweza kubebwa na mtu mmoja. 

MIAKA MIWILI YENYE FURAHA

Baada ya hayo yaliyonipata nilikuwa na uchovu wa kimwili na wa akili, lakini jambo moja ni kwamba nilikuwa huru nisipatwe na mateso ya kijamaa. Mashahidi walioishi nje ya jiji walituchukua tukae kwao. 

Mei 1948 binti yangu mkubwa zaidi alianza kupainia, kama vile kazi ya kuhubiri wakati wote ya Mashahidi wa Yehova inavyoitwa. Alikwenda sehemu ya kusini ya nchi, na baadaye akatutia moyo tujiunge naye. Tulipofika, huko hakukuwa na kundi la Mashahidi wa Yehova. Mimi niliweza kupata kazi, na vilevile vyumba viwili vyenye vifaa. Chumba chetu chenye piano (chombo cha muziki) tulikiweka kando kiwe kama Jumba la Ufalme. 

Tulianza kuhubiri na kupata wenye kupendezwa. Mashahidi wa jiji jirani walikuja na kutoa hotuba za watu wote za Biblia na kutusaidia tuzidi kukomaa kiroho. Wakati wa likizo la shule mwaka wa 1949 binti yangu mdogo zaidi alifanya kazi ya painia wa likizo, halafu mwaka uliofuata yeye na ndugu yake wakabatizwa. Walakini, jambo lililotokea mwaka wa 1950 liliyakatiza maisha yenye furaha, yangawa magumu, niliyokuwa nimeishi pamoja na watoto wangu wapendwa. 

IMANI YATIWA NGUVU NA MAJARIBU

Kazi ya Mashahidi wa Yehova ilipigwa marufuku, na karibu wote wenye kujulikana na polisi, kutia na mimi mwenyewe na binti yangu mkubwa zaidi, walikamatwa. Kwa njia hiyo sikuweza kutunza mwana wangu wa miaka 13 na binti yangu wa miaka 12. Jamaa moja ilichukua mwana wangu, na nyingine binti yangu. 

Binti yangu mkubwa zaidi alifunguliwa gerezani baada ya miezi mitatu. Mimi nilikuwa gerezani miezi minne zaidi. Nilipofunguliwa, niliagizwa niondoke kwenye eneo hilo. Tulichukua mavazi na matandiko yetu tu halafu sisi wanne tukaenda kwenye jiji jingine na huko Mashahidi wakatuchukua tukae kwao. Mambo yaliyonipata nilipokuwa gerezani, na katika kuhama kwangu kwenda eneo jingine, yaliitia nguvu imani yangu na kuthamini kwangu uangalizi na uongozi wa Yehova. 

Baada ya miezi michache binti yangu mkubwa zaidi alianza kupainia tena. Walakini, kwa sababu ya marufuku hakuweza kuhubiri nyumba kwa nyumba. Kwa hiyo alitembelea waliokuwa tayari wanapendezwa, akiwapa vitabu vya kuwasaidia kujifunza Biblia kisha akajifunza nao Biblia. 

Mwaka wa 1952 mwana wangu alimaliza shule. Halafu tukahamia mji uliokuwa mbali kilomita zaidi ya 100 (maili 60) na huko yeye na mimi tukaanza kazi kwenye kiwanda cha kupasua mbao. Kwa kuwa nilifanya kazi nusu mchana, nilifurahi kuweza kuanza kupainia. 

Muda mfupi baada ya hapo Mashahidi kadha, kutia na mwana wangu na mimi, walikamatwa kwa kuuhubiri ujumbe wa Biblia. Walakini, kwa sababu tulikuwa na kazi ya kimwili, tuliachwa huru baada ya siku mbili tu. Wengi kati ya Mashahidi wale wengine walifanyiwa kesi, wakapokea hukumu za kufikia miaka 15 gezani. Lakini sisi tuliendelea kuhubiri na baada ya muda mfupi watu 35 walibatizwa katika eneo letu. 

Binti yangu mkubwa zaidi alikamatwa mwaka wa 1953. Wakati wa uchunguzi alipigwa na baadaye akahukumiwa kukaa gerezani miaka minne. Karibu na wakati huu binti yangu mdogo zaidi alimaliza shule, halafu yeye na ndugu yake wakaanza kupainia. Mwaka uliofuata, wakati binti huyu alipokuwa na miaka 16 tu, alikamatwa na kufungwa gerezani mwezi mmoja. Halafu akawekwa ndani ya makao ya wasichana wenye umri mdogo waliokuwa wamekataa kutii sheria. 

Kwa kuwa mimi nilikuwa nikiwindwa na polisi kwa sababu ya utendaji wangu wa kuhubiri, sikuweza kuihudhuria kesi ya binti yangu mahakmani. Kwa kuwa yeye hakuwa na uangalizi wa wazazi, alihukumiwa kukaa kwa muda usiojulikana katika makao ya kurekebisha watu. Kwa sababu ya sifa yake nzuri, alitumainiwa akapewa kazi ya kupeleka ujumbe na kwenda kununua vitu vya makao hayo mjini, basi tukaweza kuonana mara kadha. Nyakati hizo zilikuwa zenye furaha wee! 

Ndipo mimi nilipopelekwa kwenye mji mwingine nikapainie. Ulikuwa wakati wenye kunijaribu. Binti zangu wawili walikuwa gerezani. Nami sikumwona mwana wangu mara nyingi sana, kwa kuwa alikuwa akipainia katika sehemu tofauti ya nchi. Walakini, tulionana kwenye mikutano ya mapainia, ambayo nyakati nyingine ilikuwa na urefu wa siku kadha. Karamu hizi za kiroho zilifanywa katika nyumba zilizojificha zaidi za Mashahidi. Loo! zilikuwa pindi zenye furaha kama nini! 

Kuelekea mwisho wa mwaka wa 1955 niliombwa nisaidie kutokeza na kusafirisha pia vitabu vya kusaidia watu wajifunze Biblia. Ilikuwa kazi ngumu, lakini tulijua ilikuwa ya maana sana. Tulipata nguvu kwa kuona furaha ya kina ndugu waliofurahia sana kuupokea “mkate” (ndivyo ilivyouita Mnara wa Mlinzi) na “kitumbua” (jina tulilovipa vijitabu). Pia, wakati wo wote nilipokuwa bila kazi nilihubiri katika bustani za starehe, nikianza mazungumzo na watu na kuanzisha ziara za kurudia. 

SISI SOTE TWAPAINIA

Mwanzoni mwa mwaka wa 1956 binti yangu mdogo zaidi aliachwa huru, akaanza tena utumishi wa painia mahali alipouachia. Karibu miezi mitatu baadaye binti yangu mkubwa zaidi alifunguliwa gerezani, naye pia akarudia kupainia moja kwa moja. Alipokwisha kuwekwa huru, sisi wanne tulionana kwenye mkutano wa mapainia, nasi tutalikumbuka jambo hilo nyakati zote. 

Kwa muda wa miaka mitano iliyofuata tulionana mara kwa mara. Mwanzoni, kila mmoja wetu alipainia katika eneo tofauti. Kwa hiyo mahali po pote tulipoonana palikuwa “nyumbani.” Nyakati zote funiko la chini ya dari lilikuwa anga la samawati, na nyakati nyingine sakafu yetu ilikuwa majani, au theluji, ikitegemea majira ya mwaka. 

Tulianza kutumia mashine za umeme za kunakilia katika kutokeza vitabu vya kusaidia watu wajifunze Biblia. Wakati mmoja nyumba iliyokuwa na vifaa vya kuchapia na karatasi ilichomeka ikabomoka. Wakuu waligundua kwamba mlikuwa na mashine ya kuchapia katika nyumba hii iliyoteketea, lakini hakuna aliyekamatwa. Halafu tukashiriki katika kazi ya pekee. Mimi nilisaidia kupanga chapa za kitabu malidadi Kutoka Paradiso Iliyopotea Mpaka Paradiso Iliyopatikana. 

Tulitumia likizo letu la kiangazi mwaka wa 1961 kama jamaa pamoja na ndugu wakaribishaji katika kijiji cha kuvulia samaki. Tukaweza kupumzika kando ya bahari na kupata nguvu za kufanya kazi mwaka utakaofuata. Hatukujua mambo yaliyokuwa yakitungoja. 

JAMAA NZIMA YETU YAFUNGWA GEREZANI

Katika Agosti binti yangu mkubwa zaidi alikamatwa, na mwana wangu pia. Halafu, miezi mitatu baadaye, binti yangu mdogo zaidi na mimi tukakamatwa. Tulizuiwa zaidi ya mwaka mmoja ili mambo yetu yachunguzwe. 

Tulipokuwa tumezuiwa, nilifanya ombi nimwone daktari wa meno wa gerezani. Nilipokuwa nikingoja mstarini, mwanamke mfungwa aliyekuwa karibu na mimi aliniuliza sababu gani mkubwa wa jumba la wafungwa alinipigia kelele kubwa jana yake. Nilipomwambia ni kwa sababu nilizungumza na Mashahidi wenzangu nilipokuwa nikitembea kunyosha miguu, msichana aliyekuwa karibu na mwanamke huyu akanishika kwa nguvu. Akanikumbatia kwa furaha, akisema kwamba yeye pia alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Yeye alikuwa akitumikia kifungo cha miaka mitatu kwa sababu ya kutokeza vitabu vya kusaidia watu wajifunze Biblia. Wakati huo sikujua kwamba mwishowe yeye angekuwa binti mkwe wangu—“binti yangu wa tatu.” 

Nilipokuwa nimefungwa nilisemezana kwa ukawaida na watoto wangu kwa njia ya barua. Kila barua ilifunguliwa na kuchunguzwa mara mbili. Tulianza kuingiza habari nyingi zaidi za ki-Biblia katika barua ili wenye kuzichunguza wapate ushuhuda juu ya makusudi ya Mungu. Siku moja mwanamke mzee, aliyekuwa mkubwa wa idara moja, aliniita nitoke kwenye kijumba changu cha gereza. Akanielekeza upande mwingine wa gereza tuzungumze, akaniuliza jinsi nilivyokuwa nimewalea watoto wangu. Akanieleza wao walikuwa wakivumilia gerezani kwa subira nyingi. Akasema pia kwamba watu wote waliokuwa kazini walipendezwa sana na barua zetu. 

Mwanzo wa mwaka wa 1963, karibu mwaka mmoja na nusu baada ya kukamatwa kwetu, ndipo walipoianza kesi mahakmani. Kesi hiyo ilichukua siku tatu. Binti yangu mkubwa zaidi alihukumiwa kifungo cha miaka mitatu gerezani, naye mwana wangu akapata cha miaka miwili. Binti yangu mdogo zaidi na mimi tuliachiliwa. Adhabu yetu ilionwa kuwa ni kumaliza wakati wetu tukiwa gerezani. 

BAADA YA KUFUNGULIWA GEREZANI

Tulipofunguliwa, ndugu wakaribishaji walimchukua binti yangu na mimi tukae kwao kisha wakatusaidia turudiwe na afya. Muda mfupi baadaye mwana wangu alifunguliwa, na sisi watatu tukaishi na kina ndugu. Mimi nilianza kazi kwenye sehemu ya kuyeyushia chuma na kukifinyanga, mwanangu akapata kazi ya reli na binti yangu akafanya kazi ya afisi. Tukiwa nyumbani, baada ya kazi, sisi sote tulisaidia kupanga herufi za chapa ya pili ya kitabu “Let God Be True” (Mwacheni Mungu Awe wa Kweli). 

Binti yangu mkubwa zaidi alifunguliwa gerezani Septemba mwaka wa 1963. Tukalirudia lile eneo tulikokuwa tumefanya kazi miaka 15 zamani. Tukapata nyumba kuukuu huko na, kwa msaada wa kina ndugu waliokuwa jirani, tukaweza kuitengeneza upya. Watoto wote walianza kupainia tena. 

Mume wangu alikuwa ametutafuta, lakini kwa sababu tulikuwa katika utendaji wa kuhubiri wakati wote, hakutupata kamwe. Mimi nilijua alikoishi, na kwa hiyo baada ya miaka 10 ya kutengana niliwatia moyo watoto wangu wamtembelee. Wakati huu yeye alikuwa angali mnywaji wa pombe. 

Halafu, mwaka wa 1963, nikapata habari kwamba mume wangu alikuwa ameacha kunywa. Nikamtumia anwani yetu aweze kuwatembelea watoto. Alipokuja kututembelea mara ya kwanza, mwana wangu alikuwa amekwisha kuoa. Aliona kwamba tulikuwa tukiishi kwa amani na mapatano. Yeye alikuwa mgeni kwenye arusi ya binti yetu mkubwa zaidi, na baada ya hapo alionyesha kutaka Mashahidi wa Yehova wamtembelee nyumbani kwake. 

Baadaye akaja tena tuzungumze. Yalikuwa mazungumzo mafupi na magumu sana. Aliungama kwamba alikuwa na hatia ya kuvunja sheria ya Mungu na sheria ya nchi. Baada ya miaka 22 ya kutengana  alirudi aishi pamoja nasi. Muda mfupi baadaye, Aprili 4, 1971, akabatizwa kama mmoja wa Mashahidi wa Yehova. 

Leo, mwana wangu na binti zangu wana jamaa zao wenyewe, nami ni nyanya mwenye furaha, mwenye wajukuu wa kiume wanne na wajukuu wa kike wawili. Tumepata furaha nyingi na kuuona uongozi, ulinzi na msaada wa Yehova. Mimi ninasadiki sana sana kwamba hata mmoja wa wale wanaovumilia kwa juhudi katika utumishi wa Yehova hatakosa kutimiziwa matumaini yake. Kwa moyo wangu wote mimi nimemtumaini Yehova na maneno yake yenye uhakikisho, “Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa.” (Ebr. 13:5)—Imetolewa.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki