Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 8/15 kur. 22-24
  • “Mtumwa Mwaminifu” Atoa “Chakula Kwa Wakati Wake

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Mtumwa Mwaminifu” Atoa “Chakula Kwa Wakati Wake
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • USHUHUDA WA KULA CHAKULA CHA KIROHO CHA KWELI
  • SABABU GANI MAREKEBISHO YA UFAHAMU?
  • “JUU YA VITU VYAKE VYOTE”
  • ‘MTUMWA MBAYA’
  • FURAHI PAMOJA NA WATUMISHI WA YEHOVA WENYE KULISHWA VEMA
  • “Mtumwa” Ambaye Ni Mwaminifu na Mwenye Busara
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • “Ni Nani kwa Kweli Mtumwa Mwaminifu na Mwenye Busara?”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Je! Wewe Unathamini “Mtumwa Mwaminifu Mwenye Akili”?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Wakristo Wanalishwaje Kiroho?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 8/15 kur. 22-24

“Mtumwa Mwaminifu” Atoa “Chakula Kwa Wakati Wake

BAADA ya vita ya ulimwengu ya kwanza (ya 1914 mpaka 1918), makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yaliunga mkono Ushirika wa Mataifa nao wakasihi Wakristo wa jina wauunge mkono. Tofauti yake, Wanafunzi wa Biblia hawakushindwa kamwe kuelekeza fikira kwa Ufalme kuwa tumaini pekee la wanadamu na kuufunua Ushirika wa Mataifa kuwa kitu cha kibinadamu ambacho kina lazima ya kushindwa.

Mpaka wakati huu wa leo, makanisa ya jumuiya ya Wakristo yameambukiwa na roho ya ulimwengu huu, na upendaji wake wa mali, mawazo ya mageuzi (evolution), uchambuzi wa Biblia na filosofia zinazokanusha kweli ya Biblia. Wengi wamekubali ufisadi wa ulimwengu, uasherati, uzinzi na kulalana kwa watu wa namna moja, ambayo yametokeza kuvunjika kwa ndoa na maisha ya jamaa, uasi wa vijana na watu wazima, kuenea kwa magonjwa ya kisonono na kaswende na kuongezeka kwa jeuri. Makanisa yamejitia katika ulimwengu huu, yakitegemeza tawala za mtu mmoja katika nchi fulani na kuunga mkono kabisa ugaidi (ujeuri) na utendaji wa kuvunja sheria katika nchi nyingine.

USHUHUDA WA KULA CHAKULA CHA KIROHO CHA KWELI

Tofauti yake, kundi la ulimwenguni pote la Mashahidi wa Yehova limeendelea kuwa jaminifu kwa mafundisho ya Biblia. Wanashikilia kanuni safi za adili ambazo zinapatana na hekima inayotoka juu. Mashahidi wanaheshimu sana ndoa na maisha ya jamaa, wanasitawisha matunda ya roho nao wanaendeleza uhusiano wa karibu na Mungu. (Gal. 5:22-26; Yak. 3:17, 18) Kwa msaada wa gazeti hili na vitabu vinginevyo vya kujifunza Biblia wanaendelea kujenga imani yao na maarifa sahihi kupitia kwa funzo la kibinafsi la Biblia na kushiriki katika mikutano ya kundi. Kwa sababu ya kuwa na hakika katika ufalme wa Mungu, wanaendelea kutokuwamo kabisa Katika mizozo ya ulimwengu huu nao wanatii ifaavyo “mamlaka iliyo kuu” ya kiserikali, wakilipa “Kaisari yaliyo ya Kaisari, na Mungu yaliyo ya Mungu.”​—Mt. 22:21; Matendo 5:29; Rum. 13:1-10.

SABABU GANI MAREKEBISHO YA UFAHAMU?

Huenda wengine wakauliza hivi: ‘Ikiwa Mashahidi wa Yehova wanapata “chakula kwa wakati wake,” sababu gani maoni yao juu ya mafundisho fulani yamebadilika kwa kadiri wakati ulivyopita?’ Biblia inajibu hivi: “Njia ya wenye haki ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa hata mchana mkamilifu.” (Mit. 4:18) Kama vile kundi katika karne ya kwanza lilivyokuwa na maarifa yasiyo kamili kabisa, ndivyo ilivyo na “mtumwa mwaminifu mwenye akili” leo. Maarifa juu ya mambo mengi ya kiroho yanakuwa kamili makusudi ya Mungu yanapotimizwa tu. (1 Kor. 13:9-12) “Mtumwa” huyo hajatiwa pumzi ya Mungu bali anaendelea kuchunguza Maandiko na kuchunguza sana matukio ya ulimwengu, pamoja na hali ya watu wa Mungu, ili kufahamu utimizo unaoendelea wa unabii wa Biblia. Kwa sababu ya vizuizi vya kibinadamu, nyakati nyingine kwaweza kuwa ufahamu usio kamili na wenye makosa juu ya jambo fulani ambalo huenda likasahihishwa baadaye.

Walakini hiyo haimaanishi kwamba “mtumwa” huyo anapaswa kuacha kuchapa maelezo fulani mpaka ufahamu wa mwisho ulio kamili upatikane. Hapo kwanza, wanafunzi wa Yesu hawakujua kwamba Ufalme ungekuwa wa kimbinguni, walakini Yesu alijua kwamba maarifa yao yangeongezeka chini ya uongozi wa roho takatifu na hivyo hakusita kuwapa mgawo wa kuwa mashahidi wake. (Matendo 1:6-8; Yohana 14:25, 26) Kwa kweli, mojalapo la mambo yenye kutambulisha jamii ya “mtumwa mwaminifu” ni kukesha kiroho, pamoja na kuheshimu Neno la Mungu sana. (Mt. 24:43, 44) Iwapo rekebisho linahitaji kufanywa, jamii hii inakuwa na unyenyekevu na ni yenye kukubali kufundishwa hata kukubali jambo hilo na kufanya badiliko hilo, hiyo ikishuhudia jamii hiyo ni yenye uaminifu kwa Yehova na Neno lake.

“JUU YA VITU VYAKE VYOTE”

Yesu alisema kwamba kama angekuta “mtumwa” akitoa “chakula kwa wakati wake” kwa watu wa “nyumba,” angemweka “juu ya vitu vyake vyote.” (Mt. 24:45-47) Daraka hilo zaidi, kubwa kuliko kutoa chakula cha kiroho kwa wanafunzi waliotiwa mafuta, lingetia ndani kuhubiri hukumu za Mungu kwa mataifa na vilevile kutumika kama chombo cha Mungu cha kukusanya “mkutano mkubwa” wa wanaume na wanawake kutoka kwa mataifa yote washirikiane na kundi. Kukusanya “kondoo wengine” na kuwatolea chakula cha kiroho kunajenga tumaini lao la kupata uzima wa milele duniani.​—Isa. 2:1-4; Zek. 8:23; Mt. 25:31-46; Yohana 10:16; Ufu. 7:9-17.

‘MTUMWA MBAYA’

Katika Mathayo 24:48-51 ‘mtumwa mbaya’ anatajwa. Hiyo haionyeshi kwamba “mtumwa mwaminifu” anakosa uaminifu, hata kwamba watu wa “nyumba” wakose ulinzi. Lakini kuna uwezekano kwamba huenda watu mmoja mmoja wa jamii hiyo ya “mtumwa” wapoteze imani juu ya kurudi kwa Bwana. Kwa kusema mioyoni mwao, “Bwana wangu anakawia,” waache kulinda na hivyo wafungue njia ya kuacha kweli yote ya Kikristo. Watu hao mmoja mmoja wanaweza kufikia hatua ya kushambulia waliokuwa ‘watumwa wenzao’ hapo mbeleni. Ingawa hawafanyi kazi pamoja kama tengenezo, watu hao wanaokengeuka wanakuwa jamii ya watu wasioaminika.a

FURAHI PAMOJA NA WATUMISHI WA YEHOVA WENYE KULISHWA VEMA

Ingawa vikundi mbalimbali vya Jumuiya ya Wakristo vinaendelea kufa njaa kiroho, kundi la ulimwenguni pote la mashahidi wa Yehova waliotiwa mafuta na wenzi wao, “Kondoo wengine,” wanaendelea kulishwa vema kiroho na ni wenye furaha. (Isa. 65:13-16) Jamii ya “mtumwa” inaendelea kujitambulisha kwa utendaji wa kutoa chakula cha kiroho na kwa kuwapo kwa kundi la ulimwenguni pote lenye kulishwa vema kiroho. Pamoja na hayo, “mtumwa” anajulikana kwa sababu ya kuwa na maoni na nia zile zile za watumishi waaminifu wa Yehova wa nyakati zilizotangulia Ukristo na mapema katika nyakati za Ukristo.

Maoni na nia hizo ni kama vile: Uhakika kamili katika Yehova na kumtegemea. (Mit. 3:5-7) Kukubali kabisa Biblia nzima kuwa kweli, kuwa kiongozi chenye roho ya Mungu kwa ajili ya wanadamu. (Zab. 119:160; Rum. 15:4; 1 The. 2:13; 2 Tim. 3:16, 17; 2 Pet. 1:20, 21) Kufuata hatua za Yesu Kristo kwa unyenyekevu, hata kufikia kujinyima na kuvumilia mateso kwa furaha. (1 Pet. 2:21; Mt. 16:24) Kutambua kwamba watumishi wa Mungu wanapaswa kuwa wenye kukubali kufundishwa, si wenye kujitegemea, na kwamba lazima waendelee kutafuta. (Zab. 25:9; Mt. 7:7) Kukubali kwamba watu wa Yehova lazima wajikaze sana katika utumishi wake, kuhubiri na kufanya wanafunzi. (Luka 13:24; Mt. 24:14; 28:19, 20) Kutafuta kwanza ufalme wa Mungu na haki yake.​—Mt. 6:33, 34.

Hayo ni baadhi tu ya maoni ya Kimaandiko yanayotambulisha kundi moja, la kweli la watu wa Yehova leo. Lakini yanatoa msingi wa kusihi wasomaji wetu wote washirikiane kabisa na kundi la Mashahidi wa Yehova. Vilevile wewe unatiwa moyo uendelee kujifunza Biblia pamoja na gazeti hili na vitabu vinginevyo kama gazeti hili ambavyo vinapatikana, ukilinganisha kwa uangalifu unayojifunza pamoja na Maandiko Matakatifu. (Matendo 17:11) Kwa njia hiyo, unaweza kuendelea kulishwa vema “chakula kwa wakati wake” na unaweza kushiriki furaha ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” katika kumtolea Yehova utumishi mtakatifu unaokubalika.

[Maelezo ya Chini]

a Tazama God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached, kur. 357-362, mafungu 55-65

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki