Neno la Mungu Li Hai
Maadhimisho ya Kukombolewa
LO! KULIKUWA kukombolewa kwa ajabu namna gani! Taifa la Israeli lilikuwa utumwani Misri, naye Farao alikataa kuwaacha waende wakiwa huru. Kwa hiyo Yehova akawaagiza Waisraeli waue mwana-kondoo na kunyunyiza damu yake juu ya vizingiti vya milango ya nyumba zao, kama unavyoweza kuona. Usiku huo huo malaika wa Yehova alipita juu ya nyumba zenye damu katika vizingiti vya milango lakini akawaua wana wazaliwa wa kwanza katika nyumba za Wamisri wote. Ndipo Farao alipowaacha Waisraeli waende wakiwa huru.
Je! kukombolewa huko kwa Waisraeli kulikuwa kamili kweli? Basi, wazaliwa wao wa kwanza walikuwa hai; wao walikombolewa kutoka utumwani Misri na mwishowe wakaingizwa ndani ya “nchi imiminikayo maziwa na asali.” (Kut. 13:5) Lakini bado watu hao walipatwa na magonjwa; walizeeka na kufa. Hawakukombolewa kutokana na dhambi na matokeo yake, kifo.
Baadaye, Yesu Kristo alionekana duniani. Siku moja Yohana, aliyekuwa amembatiza Yesu, alielekeza kidole kwake na kusema: “Tazama, Mwana-kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu!” (Yohana 1:29) Kama vile damu ya mwana-kondoo wa Kupitwa ilivyomaanisha kukombolewa kwa mzaliwa wa kwanza wa Kiisraeli, ndivyo damu ya Kristo iliyomwagwa chini iwezavyo kukomboa watu. Inaweza kutoa ukombozi bora zaidi, ulio kamili. Wale wanaozoea kuiamini dhabihu ya Kristo wataondolewa dhambi zao. (Yohana 3:16, 36) Wataweza kuishi milele bila kuzeeka wakati wo wote, bila kuwa wagonjwa wala kufa.—Ufu. 21:4.
Yesu alianzisha chakula cha pekee kuadhimisha ukombozi huu mkubwa, na hasa kwa sababu unawahusu wale watakaofufuliwa wawe warithi pamoja naye wa ufalme wa kimbinguni. Jioni iliyotangulia kutundikwa kwake mtini, Yesu aliwapa mikononi mitume wake waaminifu mkate na kusema: “Chukueni, leni. Huu unamaanisha mwili wangu.” Halafu akawapa kikombe cha divai na kusema: “Nyweni kutoka kwacho, ninyi nyote; kwa maana hii inamaanisha ‘damu ya agano’ yangu, ambayo itamwagwa chini kwa ajili ya wengi kwa msamaha wa dhambi.” Vilevile, Yesu akasema: “Endeleeni kufanya hili katika ukumbusho wa mimi.”—Mt. 26:26-28; Luka 22:19, 20, NW.
Kwa hiyo huu ulipasa uwe mwadhimisho wa kila mwaka katika kushika ukumbusho wa kifo cha Yesu. Wakati wa pindi hii ya pekee yale yanayomaanishwa na kifo cha Kristo, si kwa warithi wa Ufalme peke yao bali kwa wanadamu wote wenye kuamini, yanarudiwa kutajwa na kukaziwa sana juu ya akili na moyo. Mashahidi wa Yehova wanakukaribisha ujiunge nao katika mwadhimisho wa ukumbusho huu mwaka ujao, Aprili 8. Uhudhurie kwenye Jumba la Ufalme lililo karibu zaidi na wewe. Ukawaulize Mashahidi wa Yehova wa kwenu wakati barabara wa kufanya hivyo.