Je! Kitabu Hiki Kinaweza Kukusaidia Ufanikiwe?
HAKUNA mtu ye yote duniani anayeweza kuwa na hakika ni vitabu vingapi ambavyo vimetengenezwa katika historia yote ya wanadamu. Kwa kweli, mtu mmoja mwenye hekima alisema hivi wakati mmoja: “Hakuna mwisho wo wote wa kutunga vitabu vingi; na kusoma sana huuchosha mwili.” (Mhu. 12:12) Ni kweli kama nini!
Hata hivyo kuna kitabu kimoja ambacho hakifanani na vingine. Kwa tafsiri za kawaida, kina vitabu vimoja vimoja 66. Sura zake ni 1,189. Na, katika tafsiri nyingi, kina mistari 31,102.
Iwapo ungesoma na kutafakari mstari mmoja tu kila siku, ingekuchukua zaidi ya miaka 85 kukimaliza kitabu hicho. Hiyo ni zaidi ya urefu wa kawaida wa maisha leo. Kwa kweli, kitabu ambacho tunasema juu yake kinasema hivi juu ya wanadamu: “Siku za miaka yetu ni miaka sabini, na ikiwa tuna nguvu miaka themanini; na kiburi chake ni taabu na ubatili, maana chapita upesi tukatokomea mara.”—Zab. 90:10.
Kitabu hicho ni Biblia. Na ili kuisoma vizuri ingehitaji zaidi ya maisha ya kawaida ya kibinadamu.
INAHESHIMIWA SANA
Abraham Lincoln, rais wa 16 wa United States, alisema hivi wakati mmoja: “Nasadiki kwamba Biblia ndiyo zawadi bora kabisa ambayo Mungu amepata kuwapa wanadamu.” Kweli kweli, Biblia inaheshimiwa sana na mamilioni. Kwa mfano mwandikaji wa vitabu Henry van Dyke alisema hivi:
“Iliandikiwa Mashariki na mtindo wake ni wa Mashariki, nayo Biblia inahusu hali zote za ulimwengu zilizo za kawaida nayo imeenea nchi baada ya nchi na kupendwa kila mahali. Imetafsiriwa katika mamia ya lugha yenye kuvuta mioyo ya watu. Watoto husikiza hadithi zake kwa mshangao na kupendezwa, na watu wenye hekima huzitafakari kama mifano ya maisha. Waovu na wenye kiburi wanatetemeshwa na maonyo yake, walakini kwa wenye kuugua na kutubu inasema nao kwa sauti ya kutuliza. Imejiingiza katika mawazo yetu yatupendezayo; hata kwamba usemi wake bora ni Upendo, Urafiki, Huruma, Kujitoa kwa Mungu, Kumbukumbu, Tumaini. Mtu ye yote mwenye hazina hiyo si maskini wala mkiwa.”
Kwa sababu ya maoni yao ya kidini, watu wengine huenda wakachochewa waseme mambo mazuri sana juu ya Biblia. Kusema jambo zuri juu yake kwaweza kuonekana kuwa ‘jambo linalofaa kufanywa.’ Hata hivyo, inaelekea kwamba wengine wamekuwa wenye kuchukua kwa uzito sana kufuata maarifa ya Maandiko Matakatifu. Kwa mfano, John Quincy Adams alisema hivi: “Kwa miaka mingi nimefanya liwe zoea kusoma Biblia yote mara moja kila mwaka.”
Ingekuwa namna gani kama ungeisoma Biblia yote mara moja kila mwaka? Vipi kama ungefanya hivyo bila haraka haraka bali ukitafakari. Je! ubora wa maisha yako ungekuwa na maendeleo? Ungekuwa na haki ya kufikiri hivyo ikiwa mkuu wa serikali wa Uingereza W. E. Gladstone alisema kweli. Yeye alisema hivi: “Biblia ina Asili ya Pekee, na ina tofauti kubwa sana na [vitabu vingine] vyote.”
Basi, kwa sababu hiyo una haki ya kuuliza hivi: Je! maarifa zaidi ya Biblia yanaweza kunifaidi kweli kweli? Je! naweza kutazamia kitabu hiki, ambacho kwa kawaida kinashirikishwa na Ukristo, kinisaidie nifaulu maishani?