Sehemu Yenye Kuonekana ya Tengenezo la Mungu
1, 2. (a) Je! ni jambo jipya au jambo la hivi karibuni kusikia Yehova akitajwa kuwa Mume? (b) Isaya 54:1-5, 13 anathibitishaje jibu hilo?
KWA watu ambao wamesoma Biblia sana si jambo jipya wala si jambo la hivi karibuni kusikia Mungu akitajwa kuwa Mume. Yesu Kristo mwenye aliposema: “Imeandikwa katika manabii, Na wote watakuwa wamefundishwa na [Yehova]” (Yohana 6:45), alikuwa anatumia maneno ya unabii unaozungumza juu ya Mungu akiwa Mume. Unabii huo, Isaya 54:1-5, 13, unasema hivi (kwa sehemu):
2 “Imba, wewe uliye tasa, wewe usiyezaa; . . . Kwa sababu Muumba wako ni mume wako; [Yehova] wa majeshi ndilo jina lake; na Mtakatifu wa Israeli ndiye Mkombozi wako; . . . Na watoto wako wote watafundishwa na [Yehova]; na amani ya watoto wako itakuwa nyingi.”
3. Wakati mtume Paulo alipotumia maneno ya unabii uo huo wa Isaya katika Wagalatia 4:27, je! alikuwa anazungumza juu ya mwanamke halisi wa kidunia hata iwe ni kwa maana gani?
3 Mtume Paulo alitumia unabii uo huo wa Isaya, sura ya 54, aliposema hivi: “Kwa maana imeandikwa, Furahi, wewe uliye tasa, usiyezaa; Paza sauti, ulie, wewe usiye na utungu; Maana watoto wake aliyeachwa pekee ni wengi kuliko wa huyo aliye na mume.” (Gal. 4:27) Bila shaka hapo mtume Paulo hakuwa akizungumza juu ya wanawake halisi duniani, maana Yehova Mungu hakuwa Mume wa mwanamke fulani mmoja kwa njia ya halisi au ya mfano. Kile kilichokuwa “mke” wa Mungu kwa usemi wa mfano kilikuwa kikubwa zaidi.
4. Basi hilo “jambo kubwa zaidi” ni nini?
4 Ni nini hicho? Tengenezo la Mungu, ambalo aliliumba kwa ajili yake na ambalo haliwezi kushawishwa liamini kwamba Mungu ni mwongo mchoyo! Akiwa kama mume, atalifanya lizae “uzao,” au watoto, ambao kupitia huo Mungu ataharibu Shetani na tengenezo aliloanzisha na Adamu na Hawa.
5. Aliye mkuu wa “uzao” unaozungumzwa katika Mwanzo 3:15 alitokezwa wakati gani, na namna gani hivyo?
5 “Uzao” wa “mwanamke” au “mke” wa Mungu ulianza kutokezwa ukiwa mwana wa Mungu pekee mbinguni. Wakati gani? Wakati ambapo uhai wake ulipohamishwa kwenye tumbo la uzazi la bikira Myahudi Mariamu, apate kuwa na mimba ya mtoto, katika mwaka wa 2 K.W.K. Kufika wakati huo uhai wake ulikuwa umekuwa katika makao ya roho, mbinguni. Kwa hiyo Mariamu hakuwa “mwanamke” yule wa Mwanzo 3:15. Wala Mariamu hakuwa mama ya wale ambao Ufunuo 12:17 huita “wazao wake waliosalia.”—Angalia Wagalatia 4:26-31.
6. (a) Alipokuwa duniani akiwa mwanamume mkamilifu, Yesu alikuwa sehemu ya tengenezo gani? (b) Wanafunzi wa Yesu walianza kuwa sehemu ya tengenezo la Mungu la kiroho wakati gani?
6 Kama vile mwanamume wa kwanza duniani, Adamu, alivyokuwa “mwana wa Mungu” na alivyokuwa sehemu ya tengenezo la Mungu la ulimwenguni pote wakati angali alikuwa mkamilifu katika shamba la Edeni, ndivyo Yesu alipokuwa mwanamume mkamilifu duniani alivyokuwa sehemu yenye kuonekana ya tengenezo la Mungu la wana. (Luka 3:21-38) Akitoa sala kwa Mungu, Yesu alisema hivi kuhusu yeye na wanafunzi wake: “Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.” (Yohana 17:14, 16) Baadaye Yesu alimwambia hivi liwali Mrumi, Pontio Pilato: “Ufalme wangu sio wa ulimwengu huu.” (Yohana 18:36) Hiyo ni kwa sababu Yesu Kristo alikuwa sehemu ya tengenezo la Mungu la kiroho, “mwanamke” wa Mungu, Yesu akiwa ndiye mkuu wa “uzao” wake. Tangu siku ya Pentekoste mwaka 33 W.K. na kuendelea, wakati Yesu aliyetukuzwa mbinguni alipomimina roho takatifu juu ya wanafunzi wake waaminifu duniani, walipata kuwa sehemu ya “uzao” wa “mwanamke” wa Mungu. Walikuwa washiriki wa sehemu inayoonekana ya tengenezo la Mungu la kiroho. Ingawa walikuwako ulimwenguni, hawakuwa sehemu yake.—Matendo 2:1-47.
7. Yesu Kristo anayetarajia kuwa mume ana “bibi arusi” wa namna gani, naye “bibi arusi” huyo anasema nini kulingana na Ufunuo 22:17?
7 Kwa sababu ya hayo yanayotangulia, hata Yesu Kristo anasemekana kuwa Bwana-arusi akitarajia kuwa na “bibi arusi.” Bila shaka, yeye si mwanamke wa halisi. Iwapo yeye si mwanamke wa halisi, basi yeye ni nani? Yeye ni “bibi arusi” mwenye washiriki wengi, “bibi arusi” aliye jamii, na hivyo ni tengenezo linalofuata, linaloiga na kufanya mapenzi ya anayetarajia kuwa Bwana-arusi. Ukitaka unaweza kuliita ecclesia, kusanyiko, kundi. (Kum. 4:10; 9:10; 18:16, Tafsiri ya Septuagint ya Kigiriki; Matendo 7:38) Kitabu cha mwisho cha Biblia kinamtaja huyo anayetarajia kuwa mwenzi wa kimbinguni wa Kristo aliyetukuzwa kinaposema hivi, katika Ufunuo 22:17: “Na [r]oho na Bibi-arusi wasema, Njoo!”
8. (a) Katika 2 Wakorintho 11:2 mtume Paulo anafananisha kundi la Kikristo la siku zake na kitu gani? (b) Kwa kuwa Paulo anatumia maneno ya Zaburi 45 kuhusiana na Yesu, basi, yule mwanamke anayeletwa kwa mfalme wa Kimasihi awe Bwana wake ni nani?
8 Paulo aliandikia ecclesia au kundi katika Korintho, Ugiriki, hivi: “Naliwaposea mume mmoja, ili nimletee Kristo bikira safi.” (2 Kor. 11:2) Katika Waebrania 1:8, 9 mtume Paulo anatumia Zaburi 45 kumhusu Yesu Kristo akiwa Mwana wa Mungu. Zaburi hiyo ya kiunabii inamfananisha Mwana huyo wa Mungu na Bwana-arusi, maana Zaburi 45:13-15 inaendelea kusema hivi: “Binti mfalme yumo ndani ana fahari tupu, mavazi yake ni ya nyuzi za dhahabu. Atapelekwa kwa mfalme na mavazi yaliyofumwa kwa uzuri. Wanawali wenzake wanaomfuata, watapelekwa kwako. Watapelekwa kwa furaha na shangwe, na kuingia katika nyumba ya mfalme.”
9. Yohana Mbatizaji alimfananisha Yesu Kristo na nini, naye alifananisha kundi la wanafunzi wa Yesu na nini?
9 Hata Yohana Mbatizaji alimfananisha Yesu Kristo na Bwana-arusi na wanafunzi wake wa wakati ujao na anayetarajia kuwa bibi-arusi. Kwa sababu ya kuwa na pendeleo la kutanguliza wanafunzi wa kwanza kwa Yesu aliyebatizwa na kutiwa mafuta, Yohana alisema hivi: “Nalisema, Mimi siye Kristo, bali nimetumwa mbele yake. Aliye naye bibi arusi ndiye bwana arusi; lakini rafiki yake bwana arusi, yeye anayesimama na kumsikia, aifurahia sana sauti yake bwana arusi. Basi hii furaha yangu imetimia.” (Yohana 3:28, 29) Yohana Mbatizaji hakutazamia kuwa sehemu ya “bibi arusi” wa kiroho wa Kristo. Yeye aliendelea kuwa “rafiki yake bwana arusi” tu. Hata hivyo, akiwa kama wale wanawali wa Zaburi 45:13-15 alifurahi bila choyo.
10. (a) Sababu gani ni sahihi kusema kwamba jamii ya “bibi arusi” ni sehemu inayoonekana ya tengenezo la Mungu la kiroho? (b) Hali hiyo inaungwaje mkono na yale ambayo Paulo aliandika kuhusu Kristo ambaye ni Kichwa katika barua alizoandikia Warumi na Wakorintho?
10 Jambo kuu katika mambo hayo yote ni kwamba Bwana-arusi wa kimbinguni ni sehemu ya tengenezo la Mungu la kiroho na ndivyo ilivyo jamii ya anayetarajia kuwa “bibi arusi,” aliyezaliwa kwa roho ya Mungu anapokuwa angali duniani, sehemu inayoonekana ya tengenezo la Mungu la kiroho. Ukweli wa hali hiyo unathibitishwa na uhakika wa kwamba “bibi arusi” huyo, mwenye mume aliye kichwa chake, ndiye mwili wa Kristo wakati uo huo. Paulo aliandikia hivi ecclesia, au kundi, katika Roma: “Vivyo hivyo na sisi tulio wengi tu mwili mmoja katika Kristo, na viungo, kila mmoja kwa mwenzake.” (Rum. 12:5) Paulo aliandikia hivi kundi katika Korintho: “Kwa maana kwa [roho moja] sisi sote tulibatizwa kuwa mwili mmoja, . . . Basi ninyi mmekuwa mwili wa Kristo, na viungo kila kimoja peke yake.” (1 Kor. 12:13, 27) Kwa kuwa sasa Kichwa cha mwili huo wa kiroho, Yesu Kristo aliyetukuzwa, ni sehemu ya tengenezo la Mungu la kiroho, ndivyo washiriki wa “mwili” wake walivyo sehemu ya tengenezo la Mungu, sehemu yake inayoonekana kwa wakati huu. Si kosa kusema kwamba wao ni tengenezo la Mungu linaloonekana duniani. “Mungu ameutayarisha mwili.” (1 Kor. 12:24, The Jerusalem Bible) “Walakini Mungu ameutengeneza mwili.”—The Riverside New Testament ya William G. Ballantine.
WATU WA MUNGU WALIO TENGENEZO, WALIOWEKWA WAKF DUNIANI LEO
11. Baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, sababu gani kulikuwako uhitaji wa kujitengeneza upya kwa upande wa mataifa ya kilimwengu na vilevile kwa upande wa “wazao [mwanamke] waliosalia”?
11 Ilikuwa lazima taratibu ya mambo inayoonekana ya Shetani itengenezwe upya kwa ajili ya mataifa yaliyoharibiwa na vita mwishoni mwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza katika 1918. Mwigishaji mpya alikuwa amekuja juu ya jukwaa la mambo ya mataifa yote akiwa ndio kina Bolsheviki au Wakomunisti, ambao walitokeza mapinduzi yenye jeuri katika Urusi na kutawala kisiasa juu ya milki yake yenye kuenea sana katika Ulaya na Asia. Ulikuwa ulimwengu wenye mambo kama nini ambao “wazao [wa mwanamke] waliosalia” walipaswa kuukabili! Ilikuwa lazima wajitengeneze upya. Walipaswa kuuangalia wakati ujao kwa maoni mapya na yaliyo tofauti kabisa, kwa msaada wa unabii wa Biblia uliokuwa unafahamika nao kuliko wakati mwingineo uliotangulia. Uthibitisho wenye kutosheleza ulikuwako, kutokana na hesabu ya tarehe ya Biblia na unabii na kutokana na matukio ya ulimwengu, kwamba nyakati za Mataifa yasiyo ya Kiyahudi, “majira ya mataifa” yaliyowekwa, yalikuwa yamemalizika katika Oktoba wa 1914. (Luka 21:24) Tangu wakati huo ulimwengu wa kale umekuwa katika “wakati wa mwisho” wake au katika “siku za mwisho” zake. (Dan. 12:4; 2 Tim. 3:1) Ikiwa hivyo, ulikuwa wakati kwa kikundi kipya cha watu, si Wakomunisti, bali watu wenye kumwogopa Mungu, kutokea juu ya jukwaa la mambo ya ulimwengu. Kuwatambua hao kulikuwa wazi kwa kadiri wakati ulivyoendelea.
12. (a) Tumaini la kidunia la watu hao wenye kumwogopa Mungu ambao sasa walikuwa wanatokea kwenye tamasha ya kilimwengu lilianza kutangazwa wakati gani na wapi kabla ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza kumalizika? (b) Kwa hiyo kitabu chenye kichwa “Kinubi cha Mungu,” kilichochapishwa mwaka 1921, kilihusianisha Yohana 10:16 na nani?
12 Wao walikuwa wanatarajia kuokoka uharibifu wa taratibu ya kale ya mambo kwenye Har–Magedoni nao wangeingia kwenye taratibu mpya ya mambo chini ya ufalme wa kimbinguni wa Kristo. Hiyo ingewapa nafasi ya kutokufa watoke juu ya uso wa dunia, ambayo Ufalme ungebadili iwe paradiso. Tumaini hilo, ambalo halikupata kutangazwa hivyo hapo kwanza, lilitangazwa waziwazi katika Los Angeles, California, U.S.A., katika Februari 1918, kabla Vita ya Ulimwengu ya Kwanza haijamalizika miezi zaidi ya minane baadaye. Wenye kuwa na tumaini hilo hawangetazamia kwenda mbinguni kamwe ili wawe sehemu ya tengenezo la Mungu huko juu. Baada ya vita hiyo kuu maoni mapya yalitwaliwa kuhusu maneno ya kiunabii ya Yesu ambayo yameandikwa katika Yohana 10:16. Kwa hiyo katika 1921 Sosaiti ilichapisha kitabu chenye kichwa “Kinubi cha Mungu,” (Kiingereza) ambacho kilisema hivi katika mafungu 577, 578, katika ukurasa 345:
“Yesu alithibitisha kwamba wale watakaookolewa si wale tu watakaokwenda mbinguni aliposema hivi: ‘Kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia.’ (Yohana 10:16) ‘Zizi hili’ linamaanisha kanisa; na baada ya jamii hiyo kuchaguliwa, basi wote wanapaswa kuwa na nafasi ya kuja kwenye zizi la Kristo. Na hiyo ni kweli kwa sababu aliwanunua wote kwa damu yake yenye thamani.
“Mungu alimfanya Nabii Daudi aandike hivi: ‘Mataifa yote ambayo umeyafanya yatakuja na kuabudu mbele zako, Ee Bwana; nao watatukuza jina lako.’ (Zaburi 86:9) Huo ni uthibitisho zaidi wenye kuunga mkono kwamba wote lazima wawe na nafasi.”
13. Kwenye kusanyiko la Los Angeles la 1923, hotuba ya msingi ilihusianishaje mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi pamoja na Yohana 10:16?
13 Katika mwaka 1923 kusanyiko la siku tisa lilifanywa huko Los Angeles, California, likafikia upeo wake kwa mkutano wa watu wote kwenye Jengo la Michezo hapo siku ya Jumapili, Agosti 26. Mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi, katika Mathayo 25:31-46, ulizungumzwa, nayo maelezo yakawa tofauti na yale ya kawaida ya Jumuiya ya Wakristo juu ya mfano huo. “Kondoo” hao walionyeshwa kuwa ni wale wale “kondoo wengine” ambao Yesu alitabiri juu yao katika Yohana 10:16. Hotuba yenye kueleza, kama ilivyochapishwa katika toleo la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Oktoba 15,1923, ilisema hivi (katika ukurasa 310, fungu la 33):
“Tunaamini kwamba kuna mamilioni katika linaloitwa kanisa kwa jina tu ambao wangali wanaendelea kushikamana nalo kwa sababu wanamheshimu Bwana; nao wanaliona hilo lenye kuitwa kanisa kwa jina tu kuwa linatumiwa na Bwana kwa njia fulani. Hesabu kubwa yao hawaamini kwamba wamewekwa safi kwa ajili ya Bwana, nao hawana matumaini ya kimbinguni au tamaa hiyo. Twaamini hapo itapatikana jamii iliyotajwa na Bwana wetu kuwa kondoo. (Yohana 10:16) Basi twakata maneno kwamba kondoo na mbuzi wa ule mfano wanadai kuwa Wakristo, wafanyiza Jumuiya ya Wakristo, na wote wanadai wanafanya kazi katika jina la Bwana.—Mathayo 7:21-23.”
14. Katika toleo lake la Januari 15, 1924, gazeti Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) lilisema nini juu ya wakati wa kukusanywa kwa “kondoo wengine”?
14 Mwaka uliofuata toleo la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Januari 15, 1924 lilitoa maelezo zaidi (kwenye ukurasa wa 26, mafungu 2 na 3), likasema hivi:
“‘Na ni kwake watakakokusanyika watu.’ —Mwanzo 49:10.
“Huo ni usemi wa kiunabii unaohusu kazi ya Kristo. Wakati wa utimizo wake unakaribia. Inamaanisha kwamba watu wa kila taifa, mbari na lugha, wanaotamani na kupenda haki, watakusanywa kwa Bwana. Yesu alisema: ‘Na kondoo wengine ninao ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja.” (Yohana 10:16) Kondoo ni mnyama mtulivu, mwenye amani na mwenye kufundishika; hivyo anatumiwa kufananisha watu wanaopenda amani na kutamani vitu bora.”
15. Toleo la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Agosti 15, 1934, lilionyeshaje kwamba fadhili za Mungu zinasaidia kuokoa wengine pia, si kuokoa “kundi dogo” tu liende mbinguni?
15 Mwongo mmoja wa miaka baadaye toleo la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Agosti 15,1934, lilisema hivi katika fungu lake la kwanza (ukurasa 243):
“Fadhili za upendo za Yehova zinapewa wote wale wanaotafuta kwa juhudi kujua na kufanya mapenzi yake. Anawapa fadhili zake watu wanaomwamini Bwana Yesu Kristo. (Yohana 3:16) Yesu Kristo ndiye njia ya Mungu iliyotolewa ya uzima, walakini si watu wote wanaopata uzima watakaokuwa viumbe wa kiroho. Kuna kondoo wengine ambao si wa ‘kundi dogo’. (Yohana 10:16) Ni hao wa baadaye, au ‘kondoo wengine’, ambao, baada ya kuja kwa Kristo Yesu kwenye hekalu ili ahukumu, anawaambia maneno haya: ‘Njoni, mliobarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme mliowekewa tayari tangu kuumbwa ulimwengu.’ (Mt. 25:34)”
(Tazama pia fungu la 28 kwenye ukurasa 248.)
16. Kwenye kusanyiko la Washington, D.C., wa 1935, “mkutano mkubwa” ulielezwa kuwa jamii gani ya “kondoo,” na mamia ya walioalikwa kipekee waliitikiaje habari hiyo siku iliyofuata?
16 Mwaka uliofuata, 1935, ulikuwa mwaka wenye kuanzisha kipindi kingine. Kusanyiko lenye maana lilifanywa huko Washington, D.C., na wale wanaotamani kuwa “kondoo wengine” wa yule Mchungaji Mwema walialikwa hasa. Hiyo ilionyesha kwamba sasa hatua ya kweli ilikuwa inachukuliwa kukusanya hao “kondoo wengine.” Siku ya Ijumaa, Mei 31, hotuba ilitolewa ambayo ilionyesha “kondoo wengine” (au, Wayonadabu) kuwa wale walio washiriki wa “mkutano mkubwa” ambao watakaa duniani, kama inavyotabiriwa katika Ufunuo 7:9-17. Kujitokeza kwa wahudhuriaji wengi wa kusanyiko hilo wawe wa huo “mkutano mkubwa” kulionyeshwa na uhakika wa kwamba, siku iliyofuata, 840 walijitoa wabatizwe majini kuwa wonyesho wa wakf wao usio na masharti kwa Yehova Mungu kupitia kwa Mchungaji Mwema Yesu Kristo.
“JINA JIPYA” LA SEHEMU YA KIDUNIA
17. Katika toleo lake la Machi 1, 1925, gazeti Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) lilieleza kuzaliwa kwa mtoto wa kiume katika Ufunuo, sura ya 12 kuhusu tukio gani lenye kutokeza?
17 Lakini, turudi kwenye mwaka ule wenye maana wa 1925. Njozi iliyokuwa imefahamika vibaya kwa muda mrefu katika Ufunuo 12:1-17 ilielezwa wazi. Toleo la gazeti Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) liliondolea mbali wazo la kwamba kuzaliwa kwa mtoto wa kiume na yule “mwanamke” mbinguni kulifananisha kuzaliwa kwa upapa kutokana na taratibu ya dini kafiri katika karne ya nne. Badala yake, kuzaliwa kwa mtoto huyo wa kiume kulionyesha kuzaliwa kwa ufalme wa Kimasihi wa Mungu na “mwanamke” wake, tengenezo lake la kimbinguni lililo kama mke. Jambo hilo lilitokea mbinguni mwishoni mwa Nyakati za Mataifa yasiyo ya Kiyahudi, “majira ya mataifa” yaliyowekwa, katika vuli ya 1914 W.K. Sehemu hii ya kidunia ya tengenezo la kiroho la Yehova ilisisimuliwa na ufunuo huo!
18. Katika mwaka 1925 fikira zilikazwa kwenye uhakika wa kwamba wakati ulikuwa umekaribia Mungu ajifanyie nini? (b) Kupatana na hayo, makundi ya wale walio katika “zizi hili” la Mchungaji Mwema yalifanya nini katika mwaka 1931?
18 Ilisisimua zaidi, katika mwaka 1925! Uhakika wenye kutokeza ulipata kuwa wazi kwamba wakati ulikuwa umefika wa Mungu kujifanyia jina. Uhakika huo ulitangazwa waziwazi kiangazi cha mwaka huo kwenye kusanyiko la eneo hilo lililofanywa katika Indianapolis, Indiana, U.S.A. (2 Sam. 7:23; Isa. 64:1, 2) Kwa kupatana na kusudi la Mungu la kujitwalia kutoka kwa mataifa “watu kwa ajili ya jina lake,” katika Julai wa 1931 jina “mashahidi wa Yehova” likajulishwa ulimwengu, wakati kwa kufaa na kwa kuazimia, maelfu ya wale walio wa “zizi hili” la Mchungaji Mwema walipopitisha jina hilo la Kimaandiko la watu wa Mungu waliojiweka wakf na kubatizwa. (Isa. 43:10, NW) Mfano huo, uliowekwa kwenye kusanyiko la Columbus (Ohio), ulifuatwa na makundi ya wale wa “zizi hili” duniani
19. Kulingana na maneno ya tafsiri iliyochapwa upya ya Yohana 10:16, “kondoo” wote wa Mchungaji Mwema leo wamo katika “zizi hili”?
19 Yesu Kristo alitofautisha wafuasi wenye mfano wa kondoo wa “zizi hili” na wale wa “kondoo wengine.” Kulingana na Biblia ya English Revised Version ya 1884, yeye alisema hivi: “Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili: wao pia lazima niwalete, nao watasikia sauti yangu; nao watakuwa kundi moja, mchungaji mmoja.”—The Emphatic Diaglott ya 1864; Rotherham, ya 1903.
20. Sana-sana tangu mwaka 1935, Mchungaji Mwema amefanya “kondoo” gani wawe tengenezo lenye umoja duniani?
20 Wale wa “zizi hili” walikuwa sehemu ya tengenezo la Mungu la kiroho, wao wakiwa ni “waliosalia” wa “uzao” wa kiroho wa mwanamke wa Mungu, anayesemwa katika Ufunuo 12:17. Kwa kuwa wale “kondoo wengine” si wa “zizi hili,” wao si sehemu ya tengenezo la Mungu la kiroho. Wao si sehemu ya “kundi dogo” wanaopewa na Baba ya kimbinguni “ufalme.” (Luka 12:32) Walakini katika masika ya 1935 Mchungaji Mwema Yesu Kristo kwa kufaa alianza kuwaleta hao “kondoo wengine” wenye tumaini la kidunia kwenye ushirika wenye kukubalika pamoja na mabaki waliozaliwa kwa roho wa “zizi hili.” Kisha wakawa “kondoo” waliotabiriwa katika mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi, katika Mathayo 25:31-46. Hivyo Mchungaji Mwema anaunganisha kondoo” wa “zizi hili” pamoja na “kondoo wengine” ili wawe “kundi moja” tu chini yake akiwa “mchungaji mmoja.” Hivyo “kundi” hilo linakuwa tengenezo moja.
21. Mabaki wa ‘’zizi hili” la wenye mfano wa kondoo watafanya kazi pamoja na “kondoo wengine” wakiwa “kundi” moja lililo tengenezo mpaka wakati gani, na kisha ni marekebisho gani yatakayofanywa?
21 Jambo hilo linaweka msingi kwa hao wote wenye mfano wa kondoo, wenye tumaini la kimbinguni au la kidunia, wafanye kazi pamoja sasa wakiwa tengenezo duniani. Kutenganishwa ambako lazima kutokee mwishowe kati ya jamii hizo mbili kutakuja kwa sababu “kondoo” wa “zizi hili” watakuwa wamemaliza mwendo wao wa kidunia nao watapata “ufufuo wa kwanza,” wawe sehemu ya tengenezo la kimbinguni lisiloonekana. (Ufu. 20:6) Wale wa “kundi dogo” wakiwa wamekwisha kwenda wote, itakuwa lazima marekebisho yafanywe kati ya “kondoo wengine” wanaobaki, ili hao wote watumikie kwa umoja wakiwa raia za Daudi Mkuu Zaidi, Mfalme wa Kimasihi Yesu Kristo.—Ufu. 22:16.
—Kutoka The Watchtower May 1, 1981.
[Picha katika ukurasa wa 20]
Leo “kundi dogo” na wale “kondoo wengine” ni “kundi moja,” tengenezo moja la mashahidi washikamanifu wa Yehova