Neno la Mungu Li Hai
Kwa Kweli ni Nani Anayetawala Ulimwengu?
MWENDO wa mataifa umefanana sana wakati wa maelfu ya miaka iliyopita hata kwamba wanahistoria wametokeza wazo la kwamba historia hujirudia yenyewe. Vita, maonezi na vitisho vimekuwa kawaida katika kuinuka na kuanguka kwa mataifa. Kwa sababu gani?
Je! yaweza ikawa kwamba uwezo ule ule usioonekana umetawala mataifa yote? Je! nguvu ile ile yenye kuongoza ndiyo imekuwa yenye lawama la vitendo vile vile vya jeuri?
Hakuna haja ya kukisia jambo hilo. Biblia inathibitisha waziwazi kwamba mtu fulani mwenye akili aliye na nguvu nyingi sana amekuwa na uvutano juu ya wanadamu na mataifa. Katika Neno la Mungu, Yesu Kristo anamwita mtu huyo mwenye nguvu nyingi sana “mtawala wa ulimwengu huu.” (Yohana 12:31, NW; 14:30; 16:11) Yeye ni nani?
Kusaidia kujibu ulizo hilo, ebu ifikirie hali iliyokuwako mwanzoni mwa huduma ya Yesu hapa duniani. Biblia inatuambia kwamba baada ya Yesu kubatizwa alikwenda jangwani, ambako alijaribiwa na Shetani Ibilisi. Sehemu ya jaribu hilo ilikuwa kwa namna ya mapendekezo matatu yaliyofanywa na Ibilisi kwa Yesu. La tatu kati yayo linaelezwa kwa njia hii:
“Kwa mara nyingine Ibilisi akamchukua mpaka kwenye mlima mrefu sana isivyo kawaida, na akamwonyesha falme zote za ulimwengu na utukufu wazo naye akamwambia yeye: ‘Vitu hivi vyote nitakupa iwapo utaanguka chini na kunifanyia mimi kitendo cha ibada.’”—Mt. 4:8, 9, NW.
Ibilisi alimtolea Kristo kitu gani? Kilikuwa ni “falme zote za ulimwengu.” Je! kwa kweli serikali zote za ulimwengu zilikuwa ni mali ya Ibilisi? Ndiyo, kwa maana kama sivyo ingewezekanaje amtolee Kristo hizo? Shetani alikuwa mtawala wazo asiyeonekana. Kwa sababu hiyo Yesu alisema hivi baadaye: “Ufalme wangu sio wa ulimwengu huu.”—Yohana 18:36.
Biblia inaeleza waziwazi kwamba mataifa yote yako chini ya uongozi wa Ibilisi, kwa kusema hivi: “Ulimwengu wote umo katika uwezo wa yule mwovu.” (1 Yohana 5:19, NW) Kwa kweli, Neno la Mungu linamwita Shetani “mungu wa hii taratibu ya mambo.”—2 Kor. 4:4, NW.
Habari hiyo inatusaidia tufahamu ni sababu gani mataifa yanachukiana na kujaribu kuharibiana ambapo ni tamaa ya asili ya watu wote wa kawaida kuishi kwa amani. Ndiyo, ‘Shetani anaidanganya dunia yote inayokaliwa na watu.’—Ufu. 12:9, NW; Efe. 6:12.
Hata hivyo, karibuni yote hayo yatabadilika. Wakati umekaribia sana wa Yesu Kristo aliyefufuliwa kummaliza Shetani na ulimwengu wake mwovu, na ahifadhi hai milele watumishi wa Mungu.—Ufu. 20:1-3; 1 Yohana 2:17.