Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 8/15 kur. 6-8
  • Maisha Unayoweza Kuyachagua

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maisha Unayoweza Kuyachagua
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUSUDI LA YEHOVA LITASHINDA
  • Mungu Ana Kusudi Gani kwa Dunia?
    Imani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
  • Uhai Una Kusudi Tukufu
    Ni Nini Lililo Kusudi la Uhai?
  • Paradiso Inayotajwa Katika Biblia Iko Wapi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Matazamio Mazuri Ajabu ya Kibinadamu Katika Paradiso Yenye Ufurahishi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 8/15 kur. 6-8

Maisha Unayoweza Kuyachagua

KUNA maisha mengine ambayo unaweza kuyachagua sasa. Ni maisha yasiyonyauka kama ua wala yasiyofifia kama majani wakati wa kiangazi. Maisha hayo hayajawi na maumivu na hali za kukatisha mtu tumaini. Si maisha yenye kuzungukwa na kutokutii wala uhalifu, vita wala njaa kali, magonjwa yenye kuambukia watu wengi wala kifo. Siku za maisha hayo si chache, bali hazina mwisho. Siku zayo hazijawi na taabu, bali na furaha isiyoelezeka. Ni maisha yaliyokusudiwa yapatikane na mwanadamu aliyeumbwa na Yehova Mungu hapo kwanza.

Ni maisha gani hayo? Je! ni raha nyingi ajabu mtu akiwa mbinguni, akiwa amejilaza kwa starehe juu ya wingu lenye kumwendesha huku na huku, naye mwenyewe akiwa anacharaza kinubi (chombo cha muziki) kwa kuelea-elea angani katika umilele? Hapana! Siyo maisha hayo ambayo waotaji ndoto wanaojikalia kitako wamekuwa wakifikiria ndiyo maisha yanayopatikana mbinguni. Ili tuone namna yalivyo maisha haya unayoweza kuchagua sasa, acha tuliendee Neno la Mungu tujue kusudi lake lilikuwa nini kwa kuumba mwanamume na mwanamke.

Watu wawili hao wa kwanza walipewa amri, si ya kimbinguni, bali ya kidunia. Mungu aliwaambia hivi: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.” Kutiisha dunia kunamaanisha kuitunza, si kuiharibu. Hiyo inaonekana wazi kutokana na mgawo aliopewa mwanadamu katika Edeni: “[Yehova] Mungu akamtwaa huyo mtu, akamweka katika bustani ya Edeni, ailime na kuitunza.”​—Mwanzo 1:28; 2:15.

Kama jamaa ya kibinadamu ingaliendelea kuongezeka kisha Edeni pawe mahali padogo mno, kusudi la Mungu lilikuwa kwamba watu hao wenye kuongezeka watawanyike nje ya mipaka ya bustani hiyo, waende wakiwa na mbegu au vishina walivyokata vya mimea mikamilifu ya Edeni, wakavipande katika maeneo mapya na kuyalima maeneo hayo sawasawa na ile jamaa ya kwanza kabisa katika Edeni. Basi kama wanadamu wangaliendelea kuienea dunia wangaliitiisha kwa kuigeuza iwe paradiso, mpaka hali ya Edeni iwe imesambaa, na bustani ya Mungu iwe ya dunia nzima.

Katika paradiso hiyo ya dunia nzima mwanadamu angetawala wanyama kwa upendo na kuaminiana nao, wala si kwa kuwazoeza wanyama hao kwa kutumia ukatili wa kuwacharaza-charaza kwa fimbo, wala kwa kuwafungia katika makao yaliyozungushiwa seng’enge, wala kwa kutumia bunduki hatari za kina-nimrodi wa siku hizi wenye kuua wanyama ovyo-ovyo. Wanadamu watiifu wangaliendelea kutawala wanyama kwa upendo mpaka milele.

Lakini utawala huo haukukaa sana. Dhambi iliingia ikaharibu ule utulivu mzuri wa bustani ya Edeni. Yehova alikuwa amempa mwanadamu amri hii: “Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula, walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” (Mwanzo 2:16, 17) Watu wawili wale wa kwanza hawakutii, wakala, kisha wakajiletea wenyewe na wazao wao kifo. Yehova aliwaondosha bustanini, akamwambia mwanamume hivi:

“Udongo umelaaniwa kwa sababu yako; kwa uchungu utakula ya matunda yake siku zote za maisha yako; michongoma na miiba utakuotesha; na utakula majani ya shamba; kwa jasho ya uso wako utakula mukate, hata utakaporudi kwa udongo; kwa maana umetwaliwa katikati yake; kwa sababu mavumbi wewe, na utarudi kwa mavumbi.”​—Mwanzo 3:17-19, Zaire Swahili Bible.

Yehova Mungu aliwapa wanadamu mwanzo mkamilifu. Wanadamu wamezidi kuingia katika hali mbaya. Lakini hilo si kosa la Mungu. “Yeye Mwamba [Yehova], kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, yeye ndiye mwenye haki na adili. Wametenda mambo ya uharibifu, hawawi watoto wake, hii ndiyo ila yao; wao ni kizazi chenye ukaidi, kilichopotoka.” (Kumbukumbu la Torati 32:4, 5) Tangazo linalofanana na hilo linasemwa kwenye Mhubiri 7:29: “Mungu amemfanya mwanadamu mnyofu, lakini wamebuni mavumbuzi mengi.” Au, ni kama vile James Moffatt anavyoitafsiri sehemu ya mwisho ya mstari huo akisema, “hila nyingi za werevu wamejitungia.”

Leo mwanadamu anaendelea kutenda mambo yenye uharibifu, akawa akitokeza misiba mikubwa kuliko wakati mwingine wo wote uliotangulia. Sasa dunia inaendelea kuharibika isiwe sayari yenye kukaliwa na watu kwa sababu ya mwanadamu kujifaidi mwenyewe kwa kutumia vibaya mimea na wanyama wa dunia bila kujali. Tena anatumia vibaya mali za asili na mazingira ya dunia. Yehova ndiye atakayekomesha jambo hili, naye anatangaza kwamba ‘atawaharibu hao waiharibuo dunia.’​—Ufunuo 11:18,

KUSUDI LA YEHOVA LITASHINDA

Yehova anakusudia dunia iendelee kuwapo milele: “Isitikisike milele.” Itakaliwa na watu milele: “Maana [Yehova], aliyeziumba mbingu, asema hivi; Yeye ni Mungu; ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu; Mimi ni [Yehova], wala hapana mwingine.”​—Zaburi 104:5; Isaya 45:18.

Kusudi la kwanza kabisa la Yehova lilikuwa kwamba dunia iwe paradiso, ijawe na watu wenye kujitolea utumishi wake ambao wangeitunza pamoja na mimea na wanyama wayo, watu ambao wangefanya mazingira yaendelee kuwa na hali nzuri ya kuleta afya. Angali ana kusudi hilo, na Yehova anatuhakikishia kwamba litatimizwa: “Ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”​—Isaya 55:11.

Toleo la Septemba 15, 1982 litaonyesha wazi furaha zitakazokuwapo kwa kuishi katika dunia iliyo paradiso.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki