“Mkaribishane”
“Basi, mkaribishane, kama Kristo alivyowakaribisha ninyi, kwa ajili ya utukufu wa Mungu.”—Rum. 15:7, Revised Standard Version; The Living Bible.
1. (a) Ni mataifa mangapi yamekaribishwa yawe washiriki katika tengenezo la Umoja wa Mataifa? (b) Limeshindwa kutokeza nini, na kwa hiyo ni jambo gani linaloogopwa wakati wote?
KUFIKA sasa mataifa 154 yamekaribishwa kwenye tengenezo la Umoja wa Mataifa. Mataifa yote yaliyo washiriki wake hayana maongozi yale yale ya kisiasa. Hata yana maoni ya uadui, walakini katika Umoja wa Mataifa yanajaribu kuwa “adui wenye urafiki.” Inaelekea kama kwamba wanafahamu ukweli wa yale ambayo mtunga mashairi na ambaye pia alikuwa mwandikaji wa habari za magazeti aliyosema: “Kwa umoja—twasimama. Kwa kujigawanya—twaanguka.” Umoja wa Mataifa unadai kuwa ni tengenezo la amani na usalama wa ulimwengu. Hata hivyo, baada ya miaka yote hiyo tangu Vita ya Ulimwengu ya Pili kumalizika katika mwaka 1945, haujatokeza yale yaliyosemwa na mwanasiasa Mwamerika Wendell Wilkie, “Ulimwengu mmoja, serikali moja.” Kwa hiyo kutatokea kwa Vita ya Ulimwengu ya Tatu yenye matumizi ya silaha za nuklea ni jambo linaloogopwa zaidi na zaidi.
2. Hata katika taifa lile lile, ni mambo gani yanayoweza kuleta upinzani juu ya raia mmoja asikaribishwe na raia wengineo?
2 Hata katika taifa lililo mshiriki wa Umoja wa Mataifa, huenda raia zake wasikaribishe raia wengineo wote kwenye kikundi chao cha kirafiki. Upendeleo unaongoza mambo. Matajiri hawakaribishi maskini. Washiriki wa dini moja hawakaribishi watu wa dini nyingine. Wafuasi wa chama kimoja cha kisiasa wanakataa kukaribisha wale wa chama cha kisiasa cha upinzani. Watu walioelimishwa sana wanapuza wale wenye elimu ndogo au wasiokuwa na elimu yo yote. Rangi ya ngozi ya mtu inamletea vizuizi kutoka kwa watu wenye rangi nyingine ya ngozi. Tofauti yaweza kuwa sababu ya taifa analotoka mtu. Hakuna hali ya mtu kukubaliwa mahali pote kwa msingi wa kwamba yeye ni mshiriki mwenzi wa jamii moja kubwa ya kibinadamu. Hivyo, mambo asiyopenda mtu na uadui unaamua mahali ambapo mtu anaweza kukubaliwa.
3. (a) Ni kwa njia gani Jumuiya ya Wakristo isivyo kuwa tofauti kwa habari ya mambo hayo yaliyotangulia kutajwa? (b) Je! Umoja wa Mataifa umekuwa afadhali kuliko Ushirika wa Mataifa katika kuwa wonyesho wa ufalme wa Mungu kupitia kwa Kristo?
3 Mambo hayo hayako tofauti katika Jumuiya ya Wakristo, hata ingawa inapasa iwe jamii ya mataifa ya Kikristo. Kwa sababu wao ni Wakristo wa jina tu, kwa kurudia-rudia wamekosa kutimiza yale ambayo yametabiriwa katika Isaya 2:4: “Watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.” Katika Jumuiya ya Wakristo watu ambao ni Wakristo kwa jina tu, kwa kuonyesha uzalendo wanapigania taifa lao mpaka kufa au kuua wapinzani wao. Hawana sababu thabiti ya kufurahia tengenezo la Umoja wa Mataifa, hata ingawa huko nyuma Desemba wa 1918 Baraza ya Shirikisho la Makanisa ya Kristo katika Amerika iliuita Ushirika wa Mataifa uliokuwa unakusudiwa kutokezwa kuwa ni “wonyesho wa kisiasa wa ufalme wa Mungu duniani.” Hakika tengenezo la Umoja wa Mataifa halijajionyesha kuwa wonyesho wa ufalme wa Mungu kupita kwa Kristo.
4. Paulo ambaye alitumia maneno ya unabii wa Isaya, alisema nini juu ya “yote yaliyotangulia kuandikwa”?
4 Hata hivyo, maneno yaliyotangulia kutajwa juu ya taifa kutoinua upanga juu ya taifa jingine na kutojifunza vita tena kamwe yanatimizwa kati ya wale wanaomwiga Yesu Kristo kweli kweli. Mwana huyo wa Mungu mwenye amani alitumia mara nyingi maneno ya unabii wa Isaya ulioandikwa wakati mrefu uliopita. Yeye alifanya hivyo ili kuwapa wafuasi wake maagizo. Mfuasi mmoja, mtume Paulo, aliandikia wanafunzi wa Kristo katika Rumi katika karne ya kwanza na akawakumbusha hivi: “Kwa kuwa yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi; ili kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini.”—Rum. 15:4.
5. Kwa habari ya uvumilivu, ni nani aliyetoa mfano bora zaidi kwa Paulo na kwa Wakristo wenzake?
5 Katika kutimiza mambo yaliyotangulia kuandikwa zamani katika Maandiko Matakatifu, Yesu Kristo alivumilia masuto na mateso hata kufika kwenye kifo cha aibu juu ya mti kama mhalifu wa kisiasa. Kwa kuvumilia mpaka kiwango hicho akawa mfano mkamilifu kwa wanafunzi wake, mfano ambao ungetia wanafunzi wake nguvu wavumilie kwa uaminifu mpaka mwisho.
6. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba, akiwa juu ya mti wa mateso, Yesu aliendelea kushikamana na tumaini lake, naye alitiwaje nguvu avumilie? (b) Kwa habari ya tumaini na uvumilivu, wafuasi wa Yesu wanafananaje naye?
6 Kwa sababu ya kuvumilia kwa uthabiti mpaka mwisho wa mwendo wa kidunia, Yesu alishikamana na tumaini lake alilopewa na Mungu. Kwa hiyo, angeweza kumwambia hivi mwivi yule mwenye kuhurumia aliyetundikwa kando yake: “Kweli nakuambia leo, Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.” (Luka 23:43, NW) Wakati wa saa zile zenye taabu juu ya mti wa mateso, Yesu alifarijika kwa kukumbuka mambo “yaliyotangulia kuandikwa” kumhusu, na kwa njia hiyo alitiwa nguvu nyingi sana. Vivyo hivyo, wafuasi wake waliojitoa ambao wanapatwa na masuto mengi yanayomsingizia Yehova Mungu na Yesu Kristo wanashikilia imara tumaini lao la wakati ujao ambalo limo katika Maandiko yaliyoongozwa na Mungu. Wao pia wanafarijiwa sana na Maandiko “yaliyotangulia kuandikwa.” Tumaini lao, ambalo msingi wake ni Maandiko yenye kutegemeka kabisa, “halikatishi tamaa.”—Rum. 5:5, NW.
7. Kundi lote lapasa liwe na nia ya akili ya nani, nalo hilo linahusuje wao kumtukuza Mungu?
7 Tunalopaswa kufanya ni kuwa na hali ya akili ambayo Yesu Kristo alikuwa nayo wakati wa mateso yake yote katika ulimwengu wenye uadui. Kulingana na hilo mtume Paulo aliandika sala hii: “Sasa Mungu anayetoa uvumilivu na faraja aruhusu katikati yenu mwe na nia ile ile ya akili ambayo Kristo Yesu alikuwa nayo, ili kwa kupatana kwa kinywa kimoja mmtukuze Mungu na Baba wa Bwana yetu Yesu Kristo.” (Rum. 15:5, 6, NW) Kwa kusitawisha nia hiyo ya akili kwa kuiga Yesu Kristo, aliye Mfano wetu, tutaendelea kuwa na umoja tukiwa kundi la wanafunzi wake. Nia iyo hiyo ya akili katika kikundi inafanya watu waseme mamoja. Kwa hiyo inaonekana kama kwamba ni “kinywa kimoja” kinachosemea kundi lote kwa nguvu zaidi na kwa kuvuta zaidi. Hiyo inafaa sana. Kutukuza Mungu na Baba ya Bwana yetu Kristo kwa umoja kwapasa kukaziwa sana. Twapaswa kuunganisha sauti zetu kuhusiana na Yule anayepaswa kutukuzwa. Ama sivyo msikiaji hangefahamu wazi ujumbe unaotolewa.
UKARIBISHAJI WENYE MFANO WA KRISTO
8. Huenda mambo gani yalielekea kuharibu umoja wa kundi lililoandikiwa barua na Paulo katika Rumi?
8 Katika matengenezo au ujamii mwingi wa taratibu hii ya mambo wengi wanaweza kuwa na maelekeo ya kutokukaribisha wapya wanaokuja kwa sababu ya chuki ya kitaifa au ya rangi. Inaweza kuwa kwa sababu ya kadiri ya elimu, au kwaweza kuwa tofauti za kidini. Huko nyuma katika Rumi ya kale ya karne ya kwanza W.K. huenda kukawa kulikuwako sababu za asili zenye kuleta mambo hayo yenye kugawanya.
9. Wakati huo washiriki wa kundi la Rumi walikuwa nani, na huenda tofauti za mashirika anayopendelea mtu binafsi zikawa zilitokezwa na nini?
9 Mtume Paulo hakuwa amefika Rumi, mji wa kibepari wenye watu wa mataifa mengi, bali alikuwa anatumaini kufika huko baada ya muda mfupi wa kuandikia kundi lililokuwa huko barua yake iliyoongozwa na Mungu. Baada ya kukaza fikira juu ya kuambilika kwa Yesu Kristo akiwa mfano mkamilifu, Paulo aliendelea kusema hivi: “Basi mkaribishane, kama Kristo alivyotukaribisha sisi pia, kwa sababu ya utukufu wa Mungu.” (Rum. 15:7, NW) Jambo moja ni kwamba, “wote walioko Rumi, wapendwao na Mungu, walioitwa kuwa watakatifu,” walitia ndani Wayahudi wa asili waliotahiriwa na Watu wa Mataifa wasiotahiriwa au wasio Wayahudi, watu huru na watumwa. (Rum. 1:7; 3:1-6; Flp. 4:22) Kwa hiyo kati ya Wakristo hao Waroma kulikuwako tofauti za kidini na za vyeo katika ujamii, na yote hayo yakatokeza maoni mbalimbali na maono ya mtu kuwa mwaminifu kwa watu wa namna yake tu. Vilevile huenda hiyo ikawa ilifanya mtu apendelee mashirika yake.
10. Yesu aliwekaje kiolezo kwa habari ya namna tunavyopaswa kukaribishana, na alifanya hivyo kwa sababu gani?
10 Akiondoa hayo yote kando, Paulo aliwashauri wote ‘wakaribishane,’ wakifanya hivyo kwa shauku, kwa uchangamfu, kwa unyofu, kwa kuthamini kikweli Mkristo mwenzao, mwamini mwenzao. Hicho kilikuwa kiolezo kikamilifu cha kufuata kuhusiana na jambo hilo, maana Paulo anasema tufanye hivyo “kama Kristo alivyotukaribisha sisi pia.” Alipokuwa duniani, je! Yesu hakusema hivi: “Ye yote ajaye kwangu sitamtupa nje kamwe”? (Yohana 6:37) Ndiyo! Akiwa mtu mkamilifu, angaliweza kututenga kwa sababu ya kutokamilika kwetu na hali yetu ya dhambi. Walakini yeye hakufanya hivyo. Sababu gani hakufanya hivyo? Paulo anasema sababu yenyewe, kwa kuongeza maneno haya: “Kwa sababu ya utukufu wa Mungu.” Akiwakaribisha wote wenye kumwamini, Kristo alimletea Mungu utukufu, maana hiyo ilitukuza ukarimu wa Mungu na tamaa yake ya kwamba wanadamu wote waokolewe kupita kwa dhabihu ya ukombozi ya Mwanawe Yesu Kristo. Ilikuwa kama Yesu mwenyewe alivyosema: “Mungu aliupenda ulimwengu [wa wanadamu], hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.
11. Sababu gani kukaribisha wapya wanaokuja kunafanya Mungu atukuzwe, na kwa hiyo Yesu aliyetufuliwa aliwaambia wanafunzi wake katika Galilaya wafanye nini?
11 Vivyo hivyo, wakati sisi, tukiwa waigaji wa Yesu Kristo, tunapowakaribisha kundini watafutaji wote bila kujali kabila, rangi, dini ya zamani, cheo katika ujamii au elimu ya kidunia, hiyo inatokeza utukufu kwa Mungu. Inawapa wote wanaokaribishwa kwa njia hiyo maoni yanayofaa kumwelekea Yehova Mungu. Akionyesha nia yake ya kukaribisha waamini wote wa kweli kwenye kundi ambalo yeye alikuwa Kichwa chalo cha kiroho, Yesu aliyefufuliwa aliwaambia wanafunzi wake katika “Galilaya ya mataifa” namna ya kufanya, akisema hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”—Isa. 9:1; Mt. 28:16-20, NW.
12. (a) Tunapokaribisha wengine kwa sababu ya utukufu wa Mungu tunasaidiwaje? (b) Tunapokwenda nyumba kwa nyumba tunaondoaje shtaka lo lote la hatia ya damu juu ya Mungu?
12 Tunapokaribisha wote wanaokuja bila kubagua twachochewa tukikumbuka kwamba tunafanya hivyo “kwa sababu ya utukufu wa Mungu.” Kufanya hivyo kunachochea waliokaribishwa wathamini ukarimu wa uchangamfu wa Mungu na wamtukuze wao wenyewe. Tunapotoka mahali pa mikutano yetu na kwenda nyumba kwa nyumba tukatangaze habari njema za ufalme wa Mungu kwa wote tunaokuta, tunaonyesha kwamba ‘tunakaribishana, kama Kristo alivyotukaribisha sisi pia, kwa sababu ya utukufu wa Mungu.’ Mwendo huo unamletea Mungu utukufu ambaye sisi tu mashahidi wake bila kujali kama wale tunaowatembelea wanathamini ujumbe wa Ufalme au sivyo. Wale wanaokubali ujumbe wa Ufalme mwishowe watajiunga kumtukuza Mungu aliyewapelekea wajumbe wake wa Ufalme. Wale wasiokubali ujumbe wetu wa wokovu tuliopewa na Mungu watafahamu wakati wa baadaye kwamba Yehova Mungu alikuwa amewafikiria naye alikuwa amewapelekea mashahidi wake waaminifu, na hivyo wasiwe na sababu ya kumtafutia Mungu kosa. (Eze. 33:33) Hivyo Mungu anakuwa bila shtaka kuhusiana na damu yao.
KUWA “MHUDUMU” BAADA YA KUWA SEREMALA
13. Sababu gani Mungu hawezi kushtakiwa kuwa mwenye upendeleo kwa ajili ya kutoa nafasi za kwanza kwa watu waliokuwa wachache zaidi ya wengine ulimwenguni?
13 Hata hivyo, ni nani waliokuwa wa kwanza kuwa na nafasi ya kujifaidi na mpango wa Mungu? Ni watu wale ambao kupita kwao tulipata Biblia Takatifu. Walikuwa Wayahudi wa asili. Basi, je! Mungu hakuwa anaonyesha upendeleo, sana-sana tukikumbuka kwamba watu wasio Wayahudi walikuwa wengi zaidi ya Wayahudi waliotahiriwa hata miaka 1,900 iliyopita? Kijuu-juu huenda mambo yakaonekana kuwa hivyo. Walakini ilikuwa lazima Mungu aanzie mahali fulani, naye alianza na wale ambao alikuwa amefanyia babu zao ahadi za pekee, yaani, Wayahudi waliotahiriwa. Hata hivyo, faida za mwisho za Mungu kufuata mwendo huo hazingekuwa za Wayahudi wa asili au Waebrania peke yao. Kwa hiyo je! kuna sababu ya haki kulalamika juu ya jambo hilo? Hakuna hata moja!
14. Hivyo, Mwana wa Mungu aliyetoka mbinguni hakuwa na budi kuwa mwanamume wa namna gani, na wale wa namna yake walimkaribisha namna gani?
14 Na tusisahau kwamba Mungu alikuwa amefanya ahadi zisizoweza kuvunjwa kwa watu wenye kustahili kuhusiana na wazao wao wa asili, Wayahudi. Hivyo Mwana wa Mungu alipaswa kuja chini kutoka mbinguni ili atimize ahadi hizo za Baba yake wa kimbinguni. Hiyo ilimtaka azaliwe akiwa mshiriki wa kabila lenye kuchukiwa na mataifa yote, wale ambao Mungu alikuwa amefanya ahadi ya kitaifa pamoja nao. Hata hivyo, akiwa Myahudi, Mwana wa Mungu hakukaribishwa na Wayahudi wengi wenzake, kama vile tu mwandikaji wa historia ya kidunia ya Mwana wa Mungu anavyosema: “Alikuja kwake, wala walio wake hawakumpokea.”—Yohana 1:11.
15. Yesu alifanya kazi ya namna gani katika Nazareti, na kwa kufanya hivyo, je! alikuwa akitumika akiwa ‘mhudumu wa agano la waliotahiriwa?
15 Kwa hiyo kwa kundi la Kikristo katika Rumi, ambamo wote hawakuwa Wayahudi wa asili, mtume Myahudi Paulo aliandika hivi: “Kwa maana nasema, ya kwamba Kristo amefanyika mhudumu wa agano la [waliotahiriwa] kwa ajili ya kweli ya Mungu kusudi azithibitishe ahadi walizopewa baba zetu; tena ili Mataifa wamtukuze Mungu kwa ajili ya rehema zake.” (Rum. 15:8, 9a) Huko Nazareti katika Galilaya, katika nyumba ya baba yake mlezi, Myahudi Yusufu aliyetahiriwa, Yesu aliyekuwa anakua alijifunza kuwa seremala. Kwa kuzaliwa katika kabila la Yuda Yesu hakuwa wa jamaa ya kikuhani au kabila la Walawi wenye kutumika hekaluni. Kwa asili asingeweza kuwa mmoja wa watumishi wa hekalu katika Yerusalemu. Walakini je! Yesu Mwana wa Mungu alikuja duniani atumike tu na afe akiwa seremala? Hasha! Kwa hiyo kwa yeye kuwa ‘mhudumu wa agano la waliotahiriwa’ mengi yanamaanishwa zaidi ya yeye kuwa seremala kama baba yake mlezi, Yusufu.
16. Ili atumike zaidi kwa watu wasiokuwa wa mji wake wa Nazareti peke yake akiwa seremala, Yesu alianza kufanya nini?
16 Kama Yesu angefanya kazi ya useremala peke yake huko Nazareti, bila shaka hangetimiza huduma yake iliyokuwa imetabiriwa. Kwa hiyo Baba yake wa kimbinguni, Yehova Mungu, alimpa kitu tofauti cha kuanza, ili awe ‘mhudumu wa waliotahiriwa,’ si watu wa mji wa Nazareti tu, bali wa taifa lote. Hivyo, alipokuwa mwenye umri wa miaka 30 akaacha kabisa kazi yake ya useremala.
17. Kati ya kazi ambayo Yesu alifanya baada ya kubatiza na kutiwa mafuta na kazi ya kuhani mkuu wa Kiyahudi hekaluni, ni ipi iliyokuwa ya maana zaidi?
17 Yesu alianza kazi ya namna gani baada ya kubatizwa na Yohana Mbatizaji, Mlawi, na baada ya kubatizwa kwa roho takatifu ya Mungu? Je! ulikuwa utumishi wa chini kuliko ule wa makuhani wa hekaluni na Walawi, ambao walikuwa “wahudumu” wa kweli wa Mungu katika Yerusalemu? Bila shaka kila mtu anayefahamu mambo ya hakika atakubali kwamba alianza utumishi rasmi, “huduma,” wala si kazi ya kidini tu. Ni kama vile Biblia ya English Revised Version inavyosema kwa maneno haya: “Kristo amekwisha kufanywa mhudumu wa tohara kwa ajili ya kweli ya Mungu, ili athibitishe ahadi walizopewa baba zetu.” (Rum. 15:8; pia Authorized au King James Version) Hakika alikuwa akifanya utumishi uliohusu taifa zima, akiwa na cheo cha mhudumu, si kwa kuwekwa na mwanadamu bali na Mungu, Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. Yale ambayo Yesu alifanya baada ya kubadili kazi yake duniani yalikuwa ya maana kwa kadiri kubwa zaidi ya utumishi wa kidini wa kuhani mkuu wa Kiyahudi huko Yerusalemu.
18. Ingawa hakutambuliwa kuwa “mhudumu” na taifa lo lote la kidunia, sababu gani Yesu alikuwa “mhudumu” wa ‘waliotahiriwa’?
18 Kama vile tu Yesu Kristo asingeweza kufanya utumishi wo wote wa kidini hekaluni huko Yerusalemu na hivyo kushindana na makuhani na Walawi huko, vivyo hivyo asingeweza kufanya utumishi wa kidini katika hekalu lo lote la mataifa yasiyo ya Kiyahudi, katika Rumi, Athene, au mahali penginepo po pote, na bila shaka hangejaribu kufanya hivyo. Hata hivyo alikuwa hana budi kuwa ‘mhudumu kwa waliotahiriwa’ kwa ajili ya ukweli wa Mungu. Namna gani hivyo? Kwa sababu alipaswa ‘kuzithibitisha ahadi ambazo [Mungu] aliwapa baba zao,’ Waebrania, si Watu wa Mataifa. Kwa mfano, ‘babu’ yao Abrahamu alikuwa na wana wengi waliozaliwa na wanawake watatu, walakini Mungu alimchagua mwana pekee wa Abrahamu aliyezaliwa na mke wake wa kwanza, Sara, apokee ahadi aliyopewa Abrahamu, yaani, Isaka. Naye Isaka alikuwa na wana mapacha wawili, walakini Mungu alimchagua pacha mdogo, Yakobo, ambaye alikuja kuitwa baadaye Israeli, ili aendeleze ahadi aliyopewa Abrahamu kuhusu “uzao” ambao kupitia kwao mataifa yote ya dunia yangejibariki. Muda si muda wale wana 12 wa Yakobo wakazaa yale makabila 12 ya Israeli, ambayo pamoja nayo, yakiwa taifa, Mungu alifanya agano lake na taifa zima kwa njia ya nabii Musa akiwa mpatanishi.
19. Sababu gani Yesu hakuzaliwa katika kabila la Lawi, na ni nani waliomkaribisha duniani, na mahali gani?
19 Baadaye, taifa la Israeli lilipokwisha kuchagua liwe na mfalme wa kibinadamu akiwa mwakilishi mwenye kuonekana wa Yehova, Yeye alifanya ahadi Yake ya kifalme na Mfalme Daudi wa kabila la Yuda. Hivyo, Masihi aliyeahidiwa au Kristo, alipaswa awe katika ukoo wa jamaa ya Daudi. Hiyo inaeleza sababu gani Yesu alizaliwa katika mji wa nyumbani kwa Daudi, Bethlehemu, akiwa mrithi wa Daudi kwa kuzaliwa na bikira Myudea, Mariamu. Malaika wa kimbinguni walimkaribisha duniani. Kwa hiyo Mwana wa Mungu kutoka mbinguni hangeweza kuepuka kuzaliwa akiwa Myahudi. Ahadi zisizoweza kuvunjwa za Baba zilipasa kuthibitishwa au kuondolewa lawama. Mungu hangejiruhusu aonekane kuwa mwongo.
20. Ingawa Yesu alikuwa mmoja wa ‘waliotahiriwa,’ watu wa mataifa yasiyo ya Kiyahudi walikuwa wanangoja kupokea nini, na sababu gani?
20 Yesu alifurahi sana kushirikiana na Baba yake wa kimbinguni. Hivyo, kwa hakika ‘akafanyika mhudumu wa agano la waliotahiriwa.’ Alitahiriwa kama wao. Miaka mitatu na nusu baada ya kifo na kufufuliwa kwa Yesu, Wayahudi waliotahiriwa walionyeshwa kibali ya pekee. Lakini bado Watu wa Mataifa wasiotahiriwa, au wasio Wayahudi, wangekaribishwa kwenye tengenezo la kitheokrasi la Yehova. Jambo hilo lingekuwa ni kuthibitisha ahadi zisizoweza kuvunjwa za Yehova ambazo alifanya na wanadamu.