Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 11/15 kur. 18-23
  • “Furahini, Enyi Mataifa, Pamoja na Watu Wake”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Furahini, Enyi Mataifa, Pamoja na Watu Wake”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUKIRI WAZIWAZI KATI YA MATAIFA
  • FURAHA YA MATAIFA ILITABIRIWA
  • Serikali Yetu ya Ulimwengu Wote Inayokuja—Ufalme wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Hakuna Kudhuru Wala Kuharibu Katika Paradiso ya Kiroho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Je! Wewe Ungemtendeaje Balozi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Huu Ndio Wakati wa Kumkaribisha Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 11/15 kur. 18-23

“Furahini, Enyi Mataifa, Pamoja na Watu Wake”

1. Sababu gani Wayahudi ambao wangali wanashika sheria ya Musa siyo “watu wake” ambao pamoja nao mataifa wanapewa mwito “furahini”?

“WATU wake” ambao mataifa yote yanapewa mwito ‘wafurahi’ pamoja nao ni nani? (Rum. 15:10) Si Wayahudi. Wayahudi wa asili ambao mpaka sasa wanajaribu kushika sheria ya Musa wamechukiwa na kuteswa katika kipindi cha miaka 1,900 tangu mwaka 70 W.K., mwaka ambao Yerusalemu wa kale uliharibiwa na majeshi ya Kirumi yakiongozwa na Jemadari Tito. Hata Wayahudi wa asili wenyewe hawajafurahi pamoja na “watu wake,” watu wa Yehova. Mwishoni mwa wimbo ulioongozwa na Mungu ulioimbwa mwaka 1473 K.W.K., nabii wa Kiyahudi, Musa, ndiye aliyeimba hivi: “Furahini, enyi mataifa, pamoja na watu wake, kwa maana atalipa kisasi cha damu ya watumishi wake, naye atalipa kisasi adui zake na hakika atafanya upatanisho kwa ardhi ya watu wake.”​—Kum. 32:43, NW.

2. Kuhamishwa kwa wafuasi wa Yesu kutoka ‘katika nguvu za giza, na kuingizwa katika ufalme wa Mwana wa pendo lake’ kulianza wakati gani?

2 Wakati Paulo aliposema na kuonyesha matumizi ya maneno hayo aliyotaja ya Musa, mwaka 56 W.K. hivi, Yesu alikuwa amekufa, akafufuliwa na kupaa mbinguni muda mrefu kabla, katika mwaka 33 W.K. Kwa hiyo kuanza Pentekoste ya mwaka huo na kuendelea, “watu wake,” watu wa Yehova, walikuwa wanafunzi wa Yesu Kristo waliojiweka wakf, wakabatizwa na kuzaliwa kwa roho. Miaka fulani baadaye, 60-61 W.K. hivi, Paulo aliandikia washiriki wa “watu” wa Yehova katika Kolosai akasema hivi: “Mkimshukuru Baba [Yehova], aliyewastahilisha kupokea sehemu ya urithi wa watakatifu katika nuru. Naye alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake.” (Kol. 1:12, 13) Kuhamishwa huko kulianza siku ya Kiyahudi ya Pentekoste (Siwani 6) ya mwaka 33 W.K., baada ya Yesu kurudi mbinguni.

3. Kwa kuhamishwa kwenye ufalme wa kiroho wa Mwana mpendwa wa Mungu, walikuwa nini kwa niaba ya Mfalme huyo?

3 Siku hiyo, kupita kwa Mwana wake wa kifalme aliyetukuzwa, Yesu Kristo, Baba wa kimbinguni alimimina roho yake takatifu kwanza juu ya wanafunzi waliokuwa wakingoja, wapata 120 huko Yerusalemu. Kwa njia hiyo walihamishwa kutoka chini ya mamlaka ya giza ya kilimwengu wakaingizwa kwenye ufalme wa kiroho wa Mwana mpendwa wa Mungu, Yesu Kristo, aliye “nuru ya ulimwengu.” (Yohana 8:12) Ufalme huo wa kiroho ulisimamishwa na Yehova Mungu, na Yesu Kristo akiwa Mfalme wa kiroho alitumika akiwa mhudumu wa serikali ya Yehova. Ili kutimiza huduma yake anatumia wanafunzi wake waliozaliwa kwa roho walio duniani wakiwa “mabalozi walio mahali pa Kristo.” (2 Kor. 5:20, NW) Kulingana na Biblia ya English Revised Version, wao “basi ni mabalozi kwa niaba ya Kristo.” Kweli kweli “mabalozi” hao wana huduma, utumishi wa kiserikali.

4. (a) “Watu” wa Mungu ambao mataifa wanapaswa ‘kufurahi’ pamoja nao ni nani? (b) Mataifa yasiyo ya Kiyahudi yanapaswa kumtukuza Mungu kwa sababu gani?

4 “Mataifa yote yasiyo ya Waisraeli wa kiroho yanapasa ‘kufurahi’ pamoja na mabalozi hao. Wafurahie nini? Mhudumu aliye balozi, Mkristo Paulo anajibu anapoandika kwa kundi katika Roma na kusema: “Kristo amefanyika mhudumu wa agano la [waliotahiriwa: Wayahudi wa asili] kwa ajili ya kweli ya Mungu, kusudi azithibitishe ahadi walizopewa baba zetu; tena ili Mataifa wamtukuze Mungu kwa ajili ya rehema zake.” (Rum. 15:8, 9a) Rehema za Mungu kwa “Mataifa” zilikuwa nini?

5. (a) “Rehema” hizo za Mungu kuwaelekea Watu wa Mataifa wasiotahiriwa zilikuwa nini? (b) “Rehema” hizo zilianza wapi na kwa nani, kwa kukubaliwa waingie kwenye nini?

5 Huko nyuma katika karne ya kwanza W.K., “rehema” za Mungu zilikuwa: Yehova Mungu aliruhusu Watu wa Mataifa wasiotahiriwa waingie chini ya “ahadi” ambazo alikuwa amefanya na babu za Wayahudi waliotahiriwa. Kwa habari ya wasio Wayahudi waliotahiriwa, jambo hilo lilianza katika mwaka 36 W.K., wakati akida wa jeshi Mrumi Kornelio na jamaa yake na rafiki huko Kaisaria walipokubali huduma ya mtume Petro nao wakatiwa mafuta kwa roho takatifu ya Mungu na wakabatizwa. (Matendo, sura 10) Kama Kornelio na jamaa yake waliondoka Kaisaria wakarudi Italia ili wawe washiriki wa kundi huko Rumi, ambalo kufika wakati huo washiriki wake walikuwa waamini Wayahudi waliotahiriwa na yawezekana wakiwapo pia “waongofu” Wayahudi, sisi hatujui. (Matendo 2:1-10) Walakini kuanza wakati huo na kuendelea Mungu alionyesha “rehema” Watu wa Mataifa kwa kuwaruhusu waingie katika “ufalme” wa kiroho wa Mwanawe mpendwa, ijapokuwa hawakuwa wametahiriwa.

6. (a) Katika siku za Paulo, “rehema” za Mungu zilitia ndani kuruhusu mataifa wawe washiriki wa nini? (b) Sababu gani washiriki hao wa “rehema” za Mungu hawawezi kushiriki katika huduma za serikali za kilimwengu?

6 Kwa njia hiyo “Mataifa,” kama ni Wasamaria waliotahiriwa, Wamisri waliotahiriwa, au watu wasio Wayahudi ambao hawajatahiriwa, walipewa pendeleo la kuwa washiriki wa ‘uzao wa Abrahamu,’ ambao kupitia kwake jamaa zote za dunia zitajibariki. (Mwa. 12:3; 22:15-18; Gal. 3:3-29) Ingawa kwa sasa wamo katika ufalme wa kiroho wa Mwana wa pendo la Mungu, wale wote wanaojionyesha kuwa waaminifu mpaka kufa kwao hapa duniani watafufuliwa waingie kwenye ufalme wa kimbinguni wa Mungu. Huko watatawala pamoja na Kristo kwa miaka 1,000, ili wabariki jamaa zote za dunia. (Ufu. 20:4-6) Kwa sasa, wanapokuwa wangali na mwili duniani, wana “huduma” ambayo ni daraka lao kuitimiza wakiwa “mabalozi walio mahali pa Kristo” (NW), nayo ni kushiriki katika “huduma ya lile neno” (NW) linalohusu ufalme wa Yehova ulio mikononi mwa Kristo. Kwa sababu hiyo kwa kufaa hawawezi kuwa wahudumu wa serikali za kisiasa za ulimwengu huu unaoongozwa na Ibilisi.​—Matendo 6:4.

KUKIRI WAZIWAZI KATI YA MATAIFA

7. “Mabalozi” hao wanachukua msimamo gani kuhusiana na magomvi ya ulimwengu huu, na sababu gani wanaendelea kufurahi na kuwaalika wengine wajiunge nao katika jambo hilo?

7 “Mabalozi” wa Ufalme wanakuwa katika hali ya kutokuwamo kabisa kuhusiana na magomvi ya kilimwengu. Wanajua kwamba “nyakati za mataifa zilizowekwa,” zilimalizika mapema vuli ya mwaka 1914, wakati wa mwezi wa tatu wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. (Luka 21:24, NW) Wakati huo ruhusa ya Mataifa yasiyo ya Kiyahudi ya kutawala ulimwengu ilikwisha. Mataifa hayo ya kilimwengu, kutia na yale ya Jumuiya ya Wakristo, kwa kushupaza shingo yalikataa kukubali uhakika huo. Kwa hiyo wanapinga na kutesa mashahidi Wakristo wa Yehova wanaowaonyesha uhakika huo. Mateso hayo yote yanatokea kama yalivyotabiriwa katika unabii wa Biblia. Yajapokuwapo yote hayo, “mabalozi” wa ufalme wa Mungu uliosimamishwa wanaendelea kufurahi. Wanaalika watu wa mataifa yote wafurahi pamoja nao katika kutangaza ufalme ambao amempa Yesu Kristo kuwa daraka lake.

8. (a) “Mkutano mkubwa” wa watu wa mataifa yote umekusanywa kwenye upande wa ufalme wa Mungu uliosimamishwa tangu wakati gani? (b) Wao wanatambua nini waziwazi na wangependa kufurahia jambo gani la rehema?

8 Tangu masika ya mwaka 1935 (Mei) “mkutano mkubwa” wa watu wa mataifa yote ulianza kufurahi pamoja na “watu” hao wa Yehova waliotiwa mafuta, ambao walikuwa warithi wa ufalme wa kimbinguni. Watu wenye furaha ambao ni washiriki wa huo “mkutano mkubwa” wa watu wa mataifa yote wanapendezwa sana kuwa raia za kidunia wa ufalme wa Mungu wa mileani ulio mikononi mwa Kristo. (Ufu. 7:9-17; 22:17) Wanatambua waziwazi kwamba mwishoni mwa Nyakati za Mataifa katika mwaka 1914 “ufalme wa dunia umekwisha kuwa ufalme wa Bwana wetu [Yehova] na wa Kristo wake, naye atamiliki hata milele na milele.” (Ufu. 11:15) Wanajua kwamba wanaishi katika wakati wa kuvuka kutoka serikali za kisiasa ambazo zimehukumiwa maangamizi za ulimwengu huu waingie kwenye ufalme wa mileani wa Masihi wa Mungu, au Kristo. Wangependa sana kuishi wapite wakati huu wa badiliko na, bila kufa, waingie kwenye taratibu mpya duniani, chini ya ufalme huo wa Kimasihi. Hizo zingekuwa “rehema” nyingi sana kwao kutoka kwa Yehova Mungu.

9. (a) Wale walio washiriki wa “mkutano mkubwa” wa mataifa yote wameitikia mwaliko gani, nao wameonyeshaje jambo hilo? (b) Wakiwa wenye mfano wa kondoo, wamefanyiaje mema “ndugu” za kiroho wa Kristo wakati wa huu mwisho wa taratibu ya mambo?

9 Ndiyo, zimekuwa “rehema” nyingi sana upande wa Yehova kwamba “habari njema hizi za ufalme” zimehubiriwa “katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote,” na kwamba wamezipata. (Mt. 24:14, NW) Tangu masika ya mwaka 1935 washiriki wa “mkutano mkubwa” wamejifaidi na “rehema” za Mungu nao wameitikia mwaliko wa kujiweka wakf kwa Yehova Mungu kupitia kwa Kristo na wameonyesha wakf wao kwa kubatizwa katika maji. Mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi, ambao umeandikwa katika Mathayo 25:31-46, unaonyesha kwamba lazima wafanyie mema wateule wake, ndugu zake za kiroho, sasa wakati huu wa “mwisho wa taratibu ya mambo.” (Mt. 24:3, 31, NW) Hiyo inatia ndani kusaidia “ndugu” za kiroho wa Kristo katika kutangaza “habari njema hizi za ufalme” mpaka ‘dhiki kuu’ inayokuja ifike, ambayo namna yake haijapata kuwapo mbeleni. (Mt. 24:14-22, NW) Kwa sababu ya kushirikiana na mabaki ya “mabalozi walio mahali pa Kristo” (NW), wanakuwa na cheo kipya.

10. “Mkutano mkubwa” umekuwa na cheo gani kipya, nao wametoa utumishi gani pamoja na “mabalozi walio mahali pa Kristo”?

10 “Mkutano mkubwa” wa watu wenye mfano wa kondoo ambao wanakusanywa kwenye upande wa kulia wa Kristo wenye pendeleo wanatumika wakiwa wajumbe kwa ajili ya Kristo katika utumishi mtakatifu wa ufalme wake. Wamepewa ‘huduma” ya kutumika kwa ajili ya faida za serikali ya kifalme, “ufalme wa mbinguni.” Wanaonyesha shukrani zao kwa Yehova Mungu kwa utumishi mzuri sana wanaoutoa pamoja na “mabalozi” wa Ufalme.

FURAHA YA MATAIFA ILITABIRIWA

11. Huyo ambaye Daudi alisema ataliimbia jina lake ni nani, naye anamsimuliaje huyo?

11 Mtume Paulo anatumia maneno ya mtunga zaburi, Mfalme Daudi, anaposema namna mataifa watakavyokuja ‘kumtukuza Mungu kwa ajili ya rehema zake,’ anapoendelea kusema hivi: “Kama ilivyoandikwa, Kwa hiyo nitakushukuru kati ya Mataifa, nami nitaliimbia jina lako.” (Zab. 18:49; 2 Sam. 22:50; Rum. 15:9b) Mtunga zaburi huyo aliyeongozwa na Mungu alisimulia Huyo angekuwa nani ambaye angeliimbia jina lake, alipoongeza maneno haya ya kumaliza: “Ampa mfalme wake wokovu mkuu; amfanyia fadhili masihi wake, Daudi na mzao wake, hata milele.”​—2 Sam. 22:51.

12. (a) Yesu akiwa mwanadamu duniani, ‘alimkiri waziwazi’ Yehova kati ya mataifa namna gani? (b) Yesu aliyefufuliwa aliwaambia wanafunzi wake jambo la kufanya wakiwa “mabalozi” wake akiwa katika jimbo gani?

12 Daudi Mkuu Zaidi, yaani, Yesu Kristo, alipokuwa duniani akiwa mwanadamu mkamilifu, alimtolea Yehova Mungu sehemu kubwa ya shukrani na sifa katika taifa la Wayahudi. Aliuhubiri kidogo Ufalme kati ya Wasamaria na kwa mwanamke Mfoinike-Mshami ambaye alimkomboa bintiye na pepo. Vilevile sehemu kubwa ya kuhubiri kwake ilifanywa katika mahali panapoitwa na Isaya 9:1 “Galilaya ya mataifa.” Huko alifanya makao makuu ya shughuli yake ya kuhubiri juu ya Ufalme katika Kapernaumu, mji uliokuwa kando ya Bahari ya Galilaya. (Mt. 4:12-15) Baada ya kufufuliwa kutoka kwa wafu, ni katika “Galilaya ya Mataifa” alipowaambia wanafunzi wake wakiwa “mabalozi walio mahali pa Kristo”: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”​—Mt. 28:19, 20, NW.

13. (a) Ni siku gani na ni kwa namna gani wanafunzi wenye kungoja huko Yerusalemu walipewa mgawo wao wa huduma ya kibalozi? (b) Walianza ‘kumkiri’ Yehova waziwazi kati ya mataifa wakiwa wapi?

13 Siku kadha baada ya Yesu aliyefufuliwa kuwapa wanafunzi wake waliobatizwa mgawo huo, siku ya Pentekoste ya mwaka 33 W.K. ilifika. Asubuhi mapema siku hiyo Yesu aliyetukuzwa alimimina roho takatifu ya Yehova Mungu juu ya wanafunzi wapata 120 huko Yerusalemu. Kama matokeo ya kuhubiri kwao siku hiyo, Wayahudi na waongofu Wayahudi kama 3,000 walikubali habari za Ufalme nao wakabatizwa katika maji. Baadaye watu hao waliopokea roho takatifu walijiunga katika kazi ya kibalozi wakiwa mahali pa Kristo. Baada ya mateso kuanza katika Yerusalemu wengine walianza ‘kumkiri Yehova waziwazi’ kati ya Wasamaria na baadaye kati ya watu wa Mataifa wasiotahiriwa wa taifa la Rumi na wengine. Waliposikia Yehova akikiriwa waziwazi na kusifiwa kati yao, watu wa mataifa yote wangeweza kuliita jina lake kupita kwa Kristo wapate kuokolewa kwa rehema.

14. Halafu mtume Paulo alitaja maneno gani kutoka Kumbukumbu la Torati 32:43, na kwa hiyo wale waliokuwa watu wa Yehova walipaswa kufanya nini kwa ajili ya jambo hilo?

14 Mtume Paulo anataja unabii zaidi kuunga mkono hoja yake, anaposema hivi: “Na kwa mara nyingine anasema: ‘Furahini, enyi mataifa, pamoja na watu wake.’ “(Rum. 15:10, NW; Kum. 32:43, NW) Hata hivyo, watu wa mataifa yote wangewezaje kuwa na furaha pamoja na “watu” wa Yehova pasipo kusikia juu yake? Kwa hiyo wale walio “watu wake” walipaswa kuwahubiri juu ya ufalme wake wa Kimasihi.​—Rum. 10:13-15.

15. Ni kwa tendo gani na ni nani wanaopaswa kufuata mtajo wa Paulo wa Zaburi 117:1 ili mataifa mengi waitikie?

15 Mtume Paulo anatoa habari zaidi ya Kimaandiko yenye kuunga mkono kwa kusimulia juu ya yale ambayo Yehova alisema kupitia kwa mnenaji wake aliyeongozwa kwa roho: “Na kwa mara nyingine: ‘Msifuni Yehova, enyi mataifa yote, watu wote na wamsifu.’ “(Rum. 15:11, NW; Zab. 117:1) Ndiyo, ni rahisi kusema hayo, walakini mataifa yote, watu wote na mbari zote wanawezaje kufanya hivyo tusipowaambia juu ya Yehova na tusipowaeleza sababu gani anapaswa kusifiwa? Basi, kuhubiri katika mataifa yote juu ya ufalme wake mikononi mwa Kristo kwapasa kufanywe. Hiyo ndiyo “huduma” ambayo wamepewa mabaki ya warithi wa Ufalme na “mkutano mkubwa” wa wafanya kazi wenzao.​—Ufu. 7:9-17.

16. Mtajo wa Paulo kutoka Isaya 11:10 kuhusu “mzizi wa Yese” utatimizwaje?

16 Mtume Paulo anataja shahidi wa nne katika kuunga mkono hoja yake, akisema hivi: “Na kwa mara nyingine Isaya anasema: “Kutakuwako mzizi wa Yese, na kutakuwako mmoja mwenye kutokea atawale mataifa; mataifa wataweka tumaini lao kwake.’” (Rum. 15:22, NW; Isa. 11:10) Yese wa Bethlehemu alikuwa baba ya Daudi, ambaye Mungu aliweka awe mfalme juu ya makabila 12 ya Israeli. Daudi mwenyewe asingeweza kuwa “mzizi” wa uzima kwa baba yake wa kimwili. Kwa hiyo “mzizi wa Yese” wa kweli ulipasa uwe Yesu Kristo, aliyezaliwa katika Bethlehemu na katika kabila la kifalme la Yuda, kabila la Yese mwenyewe. Yesu atakuwa “mzizi” wenye kutoa uzima kwa babu yake wa kidunia Yese kwa kumfufua kutoka kwa wafu wakati wa utawala wake wa mileani.​—Ufu. 22:16.

17. Basi, ni nani “mzizi wa Yese” ambaye mataifa wanaweza kuweka tumaini lao kwake?

17 Daudi ‘alitawala mataifa’ alipotiisha mataifa yasiyo ya Kiyahudi yaliyokuwa yameachwa yaendelee kuwapo katika Nchi ya Ahadi. Hata hivyo, sasa Daudi amekuwa mfu tangu mwaka 1037 K.W.K., na watu wa mataifa hawawezi kuweka tumaini lao kwake. Kwa furaha wanaweza kuweka tumaini lao kwa Daudi Mkuu Zaidi, Yesu Kristo, “Shina na Mzao wa Daudi,” anayetawala sasa. (Ufu. 22:16) Kuweka kwao tumaini lao kwako, yeye aliye Daudi wa mfano, hakutakuwa kazi bure, au kusikofaa.

18. Ni nani kutoka mataifa yote waliokwisha tumaini lao kwa Mtawala huyo aliyeahidiwa, naye tayari anatawala nani?

18 Tangu mwaka 1935 mamia ya maelfu ya “mkutano mkubwa” unaotoka kwa mataifa yote, kabila zote, rangi zote na lugha zote wameweka tumaini lao kwa Mtawala ambaye hatawakatisha tamaa. Wanaonyesha jambo hilo kwa kutii amri yake ya kwenda kuhubiri “habari njema hizi za ufalme . . . katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14, NW) Tumaini la watu wale wa mataifa yote ambao wamekufa tangu dhambi yenye kuua ishambulie wanadamu linamtegemea Mfalme wa kimbinguni anayetawala sasa, Yesu Kristo. Tayari tangu atawazwe mwishoni mwa Nyakati za Mataifa mwaka 1914, anatawala watu wa mataifa yote wanaoamini na wenye tumaini. Bado atatawala juu ya wengi, wengi zaidi baada ya kuwafufua wanadamu wote waliokombolewa.

19. Basi, kuna sababu ya kuwafanya waamini wa mataifa yote wafurike kwa tumaini kwa kadiri wakati unavyoendelea kupita? na kuwa na furaha?

19 Basi, je! watu wa mataifa wana sababu ya ‘kufurahi’ pamoja na “watu” wa Yehova, Waisraeli wa kiroho? Ndiyo, kuna sababu kubwa zaidi ulimwenguni ya kufanya hivyo! Baraka yenye kupendeza anayotaja Paulo akimaliza mitajo yake kutoka kwa unabii inafaa kama nini hapa! Maana anasema hivi: “Mungu atoaye tumaini na awajaze furaha na amani yote kwa njia ya ninyi kuamini, ili mfurike kwa tumaini na nguvu ya roho takatifu.” (Rum. 15:13, NW) Haiwezi kukanushwa kwamba sala hiyo iliyoongozwa na Mungu inatimizwa juu ya mashahidi wote Wakristo wa Yehova katika pembe zote nne za dunia. Kutimizwa kwa unabii wa Biblia kunaonyesha kwamba tumaini letu lote tukufu linakaribia kutimizwa. “Furahini”!—Kutoka The Watchtower June 15, 1981

[Picha katika ukurasa wa 19]

Akida wa kijeshi Mrumi Kornelio, na jamaa yake na rafiki huko Kaisaria walijifaidi na huduma ya Petro

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki