Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Katika Mathayo 4:1 inasemekana kwamba “Yesu alipandishwa na roho nyikani, ili ajaribiwe na Ibilisi.” Je! hiyo inamaanisha roho takatifu ya Mungu?
Roho takatifu ya Yehova ndiyo iliyomwongoza Yesu aende nyikani, baada ya ubatizo wake. Yesu alifunga kula, na huo ungekuwa wakati wa kutoa sala na kutafakari. (Linganisha Mathayo 4:2; Marko 1:35; Luka 5:16.) Yaelekea Yehova aliutumia Wakati huo kupashana habari na Mwanawe mzaliwa wa pekee, ili ampe maagizo, maarifa zaidi na mahakikisho yenye uchangamfu, ili kumtayarisha kwa yale yaliyokuwa mbele.
Yehova angeweza kutangulia kujua kwamba kwa kumwongoza Mwanawe kwenda nyikani kuhusiana na kusudi Lake mwenyewe, vilevile, mwishowe kungeleta jaribu kutoka kwa Ibilisi. Hata hivyo kishawishi kilichokuja mwishoni mwa siku 40 ambazo Yesu alikaa nyikani halikuwa ni jambo ambalo Mungu alipanga. Mahali pake, ni jambo lililoruhusiwa tu.
Ni jambo lenye maana kwamba yaliyompata Yesu yalifanana na yale yaliyompata Musa. Nabii huyo alikuwa juu ya mlima kwa siku 40 alipokuwa akipokea agano la Torati na maagizo yaliyohusu sehemu yake akiwa mpatanishi. (Kut. 24:18; 34:28) Yesu, nabii mkuu zaidi ya Musa, lazima awe alipokea maagizo nyikani kuhusu lile agano jipya ambamo ndani yalo wafuasi wake wangeingizwa wakiwa Waisraeli wa kiroho na ambalo yeye angetumika akiwa mpatanishi. (Kum. 18:18, 19; Luka 22:20, 28-30) Na kama Musa alivyokabili jaribu kali la ushikamanifu na ukamilifu wake aliposhuka na kuwaona Waisraeli wakiabudu ndama wa dhahabu na wakitaka kurudi Misri, Yesu vilevile alijaribiwa vikali sana mwishoni mwa yaliyompata wakati wa zile siku 40.—Kut. 32:15-35.