Shukrani kwa Msaada wa Utibabu
Yesu Kristo, Mwana wa Mungu alifanya maponesho mengi ya kimwujiza. Pindi moja aliponesha wakoma 10. Lakini wao waliitikiaje?
Daktari Luka anasimulia hivi: “Na mmoja wao [wale kumi] alipoona kwamba amepona, alirudi, huku akimtukuza Mungu . . . akaanguka kifudifudi miguuni pake akamshukuru.” Halafu Yesu akatokeza maulizo haya yenye kutokeza kufikiri: “Hawakutakaswa wote kumi? Wale kenda wa wapi?”—Luka 17:11-18.
Ingawa Mungu hawezeshi wanadamu leo wafanye maponesho ya kimwujiza, tunaitikiaje tunapopewa msaada wa utibabu unaofaulu na daktari stadi? Je! sisi ni kama wale wakoma tisa, au kama yule mmoja? Sana sana inafaa mtu aonyeshe kuthamini kwake ikiwa, kwa sababu ya katao lake lenye msingi wa Biblia la kutokubali kutiwa damu mishipani, daktari anampasua pasipo kutumia damu.—Matendo 15:28, 29.a
Hivi karibuni mwanamume mzee-mzee alifanyiwa upasuaji mgumu katika Brooklyn, New York. Baadaye, yeye aliandika barua ya kuwashukuru madaktari wa upasuaji, na moja akaandikia hospitali hiyo. Sehemu ya barua aliyoiandikia hospitali hiyo inasema hivi:
‘Mabwana:
‘Juma kadha zimepita tangu nilipotoka katika hospitali yenu. Ninataka kuwashukuru na kuwaonyesha kuthamini kwangu kwa ajili ya kuniweka kiunga nyonga kingine.
‘Nina umri wa miaka 83. Nimekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova kwa miaka mingi. Nilikuwa ninajua vizuri kabisa uhakika wa kwamba umri wangu na masadikisho yangu juu ya katazo la Biblia la kutumia damu lilifanya tatizo langu liwe gumu zaidi. Bila shaka, hatutazamii miujiza kutoka kwa madaktari na hospitali, walakini tunathamini wanapokuwa wenye ufahamu, wenye kushirikiana na wanapojiweka katika hali ya wengine. Hospitali yenu, wafanya kazi wake na madaktari walitimiza hayo.
‘Ninafikiria mambo mazuri tu ya kusema juu ya wauguzi wenu. Nimekuwa mpishi kwa miaka mingi na kwa hiyo ninasifu wapishi wenu, vilevile. Lazima niongeze kwamba kuona wasafishaji wanapoizunguka hospitali wakiisafisha kunampa mgonjwa uhakika, kwa kuwa anajua wafanya kazi wanajali na wenye kusimamia wanafanya vizuri.
‘Idara yenu ya utibabu wa mwili iliniwezesha nisimame kwa miguu yangu, nitembee-tembee, na nilistaajabishwa sana na jinsi mambo yalivyotendeka. Ninawaheshimu sana madaktari nilioshughulika nao, yaani, Madakt. Scalafani na Vitali.
‘Kupendezwa kwenu na jamaa ya kibinadamu kwa kuwapa namna hiyo ya utumishi ni kwa kusifika. Ingawa siwezi kuwapa utumishi uo huo mnaofanya, ninajaribu sana kuwasaidia watu kwa njia ya kiroho. Sasa hali yangu ya mwili ni bora zaidi na inaniwezesha kuendelea kuwonyesha jirani zangu upendo. Lengo langu ni kuwakumbusha jinsi Yehova Mungu alivyo Muumba Mkuu.
‘Kwa unyofu, G. P.’
Kuthamini huko kwa kikweli kunatofautiana sana na kutokushukuru ambako kumeongezeka sana leo. Kunaonyesha kwamba mtu anayekuonyesha anawafikiria wengine. Na Mkristo anapotoa shukrani kwa ajili ya msaada wa utibabu, jambo hilo linaweza kutokeza hali nzuri wakati mwingine daktari au wauguzi wanapoombwa watumie ustadi wao na wakati uo uo waheshimu msimamo wa Biblia juu ya damu.
[Maelezo ya Chini]
a Ona kijitabu Jehovah’s Witnesses and the Question of Blood (Les Témoins de Jehovah et La Question Du Sang), kilichochapishwa na Sosaiti.