Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 12/15 kur. 8-13
  • Wenye Furaha ni Wale Ambao Mungu huwatia adabu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wenye Furaha ni Wale Ambao Mungu huwatia adabu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUTIANA ADABU KWA UPENDO MTU NA MWENZAKE
  • KUTENDA KWA IMARA
  • “MWEKENI HUYU KATIKA HALI YA KUTIWA ALAMA”
  • KUFANYA MKUTANO NA HALMASHAURI YA WAZEE
  • Ufanye Nini Unaposhauriwa?
    Amkeni!—2014
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Kudumisha Amani na Usafi wa Kutaniko
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 12/15 kur. 8-13

Wenye Furaha ni Wale Ambao Mungu huwatia adabu

“Heri mtu yule umwadibuye, na kumfundisha kwa sheria yako.”​—Zab. 94:12.

1, 2. Inatupasa tujisikie namna gani juu ya kutiwa adabu kwa njia ya kimungu?

NI WAKATI gani uliokuwa mara yako ya mwisho kushindwa kutimiza njia na kanuni zenye haki za Mungu, kwa kunena au kwa kutenda? Inaelekea kwamba si lazima ufikirie wakati wa nyuma sana, na inaelekea utazifikiria saa chache au siku chache tu zilizopita, kwa sababu sisi sote hutenda dhambi, tukishindwa kuuonyesha utukufu wa Mungu ifaavyo.​—1 Fal. 8:46; 1 Yohana 1:8-10.

2 Tunaweza kuwa wenye furaha kwamba Yehova hutamani kututia adabu naye anaweza kufanya hivyo kwa sababu ya upendo wake. “Awaadibuye mataifa asikemee [asikaripie, NW]? Amfundishaye mwanadamu asijue? Ee [Yehova], heri mtu yule umwadibuye.” ‘Tukijiacha tutiwe adabu’ na Yehova, tutakuwa heri (wenye furaha), kwa sababu tutakuwa na upatano naye.​—Zab. 94:10, 12.

3. Ni habari gani ambazo kwa kufaa zitazungumzwa?

3 Wakristo wanaweza kuutumaini uhakikisho unaotolewa na Biblia kwamba, “Bwana humwadhibu kila anayempenda.” (Ebr. 12:6, HNWW) Kwa hiyo, tunapendezwa kutokeza mazungumzo yanayotegemea Biblia juu ya mambo ya kukaripia, toba na kutenga na ushirika. Makala mbili za mfululizo wa mazungumzo hayo zimo katika toleo hili la Mnara wa Mlinzi, na zile nyingine tatu zilizobaki zitachapishwa katika toleo linalofuata. Makala tano hizo na ziwasaidie wote wapate ufahamu mzuri wa kanuni za Maandiko zinazohusika, kisha ‘warekebishwe upya, wafarijiwe, wafikiri kwa kupatana, waishi kwa kuamanika’ (kufuatia amani).​—2 Kor. 13:11, NW.

4, 5. Yehova Mungu anatutiaje adabu?

4 Mara nyingi Mungu hutia watu adabu kwa njia ya uanana na upole mwingi hivi kwamba huenda hata tukashindwa kujua tumetiwa adabu. Labda tunasoma jambo fulani katika Neno lake linalotuondosha kwenye mwendo usiofaa au jambo hilo linasahihisha kufikiri kwetu. Nyakati nyingine huenda Mungu akatutia adabu kwa njia ya kutoboa mambo wazi zaidi na hata inayoelekea kidogo kuwa yenye maumivu. Hata hivyo yeye anakijua kipimo na njia ya kutia adabu inayotufaa zaidi. (Yer. 30:11) Ni jambo zuri kama nini tunapokubali kwa kupenda atuadibu, kwa maana Mungu hutia adabu akiwa na upendo kama vile baba amfanyavyo mwana mpendwa! Vilevile ni jambo la hekima sana tukikubali kuadibiwa na Yehova Mungu kwa njia yenye kikomo au mipaka fulani badala ya kuadhibiwa mpaka tukaangamie kabisa.​—Yer. 10:24; Ebr. 12:5.

5 Nyakati nyingine Mungu hutia adabu kwa kutumia wanadamu. Yeye alilipelekea taifa la Israeli manabii na waamuzi. Lakini anaweza kutia adabu kwa njia yenye hekima hata kwa kutumia mtu mmoja. Mmoja wa “wafariji” wa uongo wa Ayubu alilazimika kukubali kwamba Ayubu alikuwa ‘ameadibu wengi.’ (Ayubu 4:3, NW; 16:2) Bila shaka ilikuwa baraka kubwa kutiwa adabu kwa njia yenye hekima na Ayubu, mwanamume mwenye utawa kweli kweli! Hata hivyo, tunaweza kujiuliza hivi, ‘Je! mimi ninakuwa na nia ya kukubali nitiwe adabu kwa njia kama hiyo yenye kunisaidia, kutiwa adabu na mwanadamu lakini adabu hiyo ikiwa inaitegemea hekima kamilifu ya Mungu?’

KUTIANA ADABU KWA UPENDO MTU NA MWENZAKE

6. Ni juu ya msingi gani tunaweza kutiwa adabu na ndugu?

6 Yesu aliuonyesha msingi wa kutufanya tutazamie kutiwa adabu sisi wenyewe na kuwatia wengine pia adabu. Katika maneno yanayohusu visa vya mtu binafsi kutendwa kosa zito, ambayo pia kwa kanuni yanaweza kutumiwa katika hali nyingi, Yesu alisema: “Ikiwa ndugu yako atenda kosa, mtie adabu; ikiwa atubu, msamehe.” (Luka 17:3, The New American Bible) Vilevile, mtume Paulo aliandika kwamba “mtumishi wa Bwana” anapaswa awe ‘akiwatia adabu kwa subira na uanana’ watu wale wengine.​—2 Tim. 2:24, 25, NAB.

7. Ni jambo gani linalopasa kufanywa kukitukia dhambi nzito?

7 Wachungaji, au waangalizi waliowekwa kundini wanapendezwa na kila Mkristo mmoja mmoja, na pia wanapendezwa na kulilinda kundi lote kwa ujumla. (Ebr. 13:17; 1 Pet. 5:2, 3) Kwa hiyo, wakati mtu fulani anapotumbukia katika dhambi nzito, wanapaswa waelezwe jambo hilo. Inampasa mtenda dhambi mwenyewe ‘awaite wazee wa kundi.’ Au, Mkristo mwingine ye yote anayepata kujua habari za hiyo dhambi nzito anapaswa awaeleze wazee kwa sababu ya kumhangaikia mkosaji na kuhangaikia usafi wa kundi. (Law. 5:1) Basi, huenda wazee wakaweza kumsaidia aliyetumbukia katika kosa, wakimgeuza aelekee upande mwingine na hivyo ‘waiokoe nafsi yake na kifo.’​—Yak. 5:14, 16, 19, 20, NW.

8. Tuvioneje vikosa vya ndugu zetu?

8 Kuna hali za kupungukiwa au makosa yasiyo mazito kadiri hiyo ambayo huenda Wakristo waliokomaa wakaweza kuyashughulikia kwa kutia mtu adabu na kumpa msaada unaotegemea Biblia. Bila shaka, inatupasa tujiangalie tusiwe watu wa kulaumu-laumu mno vikosa vya mtu mwingine, kwa maana Mungu anatuhimiza tuwe wastahimilivu na kuchukuliana. (Kol. 3:12, 13) Inatupasa tuwe na ‘unyenyekevu wa akili, tukifikiria kwamba wale wengine ni wakubwa kuliko sisi, tukiangalia, si mapendezi yetu tu binafsi, bali pia mapendezi yale ya wengine.’ (Flp. 2:3, 4, NW) Mungu anatuhakikishia kwamba “ni uzuri kwa upande [wetu] kupita na kuliacha kosa nyuma.”​—Mit. 19:11, NW.

9, 10. Ni jambo gani lingeweza kufanywa ndugu akielekea kuwa anachukua hatua ya uongo?

9 Tena, huenda ukatokea wakati tunapoona kwamba Mkristo mwenzetu anachukua hatua ya uongo au anaelekea kuingia hatarini kwa sababu ya kufuata kielelezo kibaya. Kwa mfano, tunaposhirikiana karibu-karibu na ndugu huenda tukaona kwamba yeye ana maelekeo ya kunywa sana. Yeye haonekani kuwa mlevi, lakini ni wazi kwamba ‘anatumia mvinyo sana.’ (1 Tim. 3:8) Kwa hiyo angeweza kuadibiwa kwa njia yenye kumsaidia. Lakini aadibiwe na nani?

10 Paulo aliwaandikia hivi Wakristo Wagalatia: “Hata ingawa mtu achukua hatua fulani ya uongo kabla ya yeye kuijua, ninyi mlio na sifa za kiroho jaribuni kumrekebisha upya mtu huyo katika roho ya upole.” (Gal. 6:1, NW) Mkristo mwenye sifa za kiroho anaweza kutia mtu adabu katika njia mbalimbali akitumia fadhili na busara. Kwa mfano, angeweza kusema jambo fulani katika mazungumzo ya kikawaida tu hata isionekane kama kwamba ametoa shauri la kukusudia. (Mit. 15:23) Au, anaweza kutoa maonyo ya upole faraghani. Hata hivyo—na hili ni jambo la maana kabisa—jitihada yake isisukumwe na roho ya kulaumu, bali itokane na kumhangaikia mtu huyo kwa upendo.​—1 Kor. 13:4, 5.

11. Kina ndugu na dada katika Filipi wangaliweza kusaidiaje katika tatizo ambalo wengine wa huko walikuwa nalo?

11 Ziko hali nyingine pia ambazo ndugu na dada wa Kikristo wanaweza kusaidia. Paulo aliandika hivi juu ya tatizo fulani lililokuwa katika Filipi:

“Euodia mimi namshauri kwa bidii nyingi na Sintike mimi namshauri kwa bidii nyingi wawe na akili moja katika Bwana. Naam, mimi nakuomba wewe pia, mshiriki mwenzangu wa karibu aliye wa kweli, uendelee kuwasaidia wanawake hawa ambao wamefanya jitihada kubwa upande kwa upande pamoja na mimi katika zile habari njema.” (Flp. 4:2, 3, NW)

Inaonekana palikuwa na tatizo fulani au utofautiano mkubwa kati ya wanawake hawa Wakristo waliotiwa mafuta. Kwa uhakika mtume hakuwa akiwahimiza Wafilipi wajiunge na upande wa huyu wala wa huyu katika utofautiano huo. Kufanya hivyo kungalilitenganisha sana kundi, kukitokeza vikundi vyenye kutetana, kuleta kijicho na ugomvi. (1 Kor. 1:10-13; 3:2-9) Hiyo ni hatari kubwa sana ambayo ilikuwa lazima iepukwe. Hata hivyo, kina ndugu na dada wangeweza kuwa kama yule “mwenzangu wa karibu aliye wa kweli” katika Filipi kwa kuwapa kitia-moyo chenye adabu ili wawe na umoja wa Kikristo, wawe wenye kusameheana na kufanya kazi pamoja kwa upendo, bila ya wao kuwa wapekuzi (wachunguzaji wasiofaa) wa masikitishano au maoni ya wanawake hao. (Mt. 5:23-25; Efe. 4:1-6, 31, 32; Tito 2:3-5) Wewe ukitiwa na mwabudu mwenzako adabu hiyo yenye kutolewa kwa kusudi zuri, ione kuwa wonyesho wa fadhili.​—Zab. 141:5.

KUTENDA KWA IMARA

12, 13. Ni namna gani ya kosa zito zaidi linaloweza kuwa katika kundi?

12 Mara fulani fulani huenda kukawa na Mkristo mwenye kufuata mwendo usiopatana na maelekezo ya Mungu na asiyebadilika ajaposaidiwa hata na wazee. Hapa hamaanishwi mtu mwenye kutofautiana utu tu na mwenzake. Wala haimaanishwi kwamba ni mtu ambaye bado anahitaji wakati wa kukua akomae Kikristo, mwenye kuonyesha kwa njia mbalimbali anahitaji kuendelea kukua. Paulo alikubali wazi kwamba kungekuwa na Wakristo wasiokomaa wanaopaswa kusaidiwa kwa subira, kwa upendo na tamaa ya kutaka kuwaona wakifanya maendeleo. (Rum. 14:1; 15:1; 1 Kor. 13:11; Flp. 3:15, 16) Lakini, kando na hayo, huenda kukawa na mtu fulani anayechagua kufuatia mwendo ambao kwa wazi unapingana na shauri la Mungu, ingawa mwendo huo haujafikia bado kiwango cha kuwa dhambi nzito.

13 Lisiwe jambo la kushtua mtu kwamba mara kwa mara kunaweza kuwako Wakristo fulani wa namna hiyo. Biblia inasema: “Basi katika nyumba kubwa havimo vyombo vya dhahabu na fedha tu, bali na vya mti, na vya udongo; vingine vina heshima, vingine havina.” (2 Tim. 2:20, 21) Kundi lililinganishwa na nyumba ambayo ndani yayo huenda wakawamo watu wengine mmoja mmoja wenye mfano wa vyombo visivyoheshimika, ambao njia zao au mavutano yao yanaweza kuharibu hali njema. Timotheo na Wakristo wale wengine waaminifu walionywa ‘wajitenge’ na vyombo hivyo visivyoheshimika.​—Linganisha Warumi 16:17.

14, 15. Kulitokea tatizo gani katika kundi la Thesalonike, na Wakristo wanaweza kutendaje kukiwa na tatizo kama hilo?

14 Kulingana na ufahamu huo na matumizi hayo ya maneno ya Paulo, tunaona kwamba kulikuwa na kisa cha namna hiyo katika Thesalonike wa kale. Kundi lote kwa ujumla lilishauriwa kwamba watu fulani, ambao kwa wazi walikuwa wenye afya na miili yenye nguvu, wasingetaka kufanya kazi. Watu hao wachache walitaka kuishi kwa kuwanyonya wenzao, kinyume cha shauri la Mungu juu ya uvivu. Kwa hiyo Paulo akaandika: “Ndugu, twawaagiza katika jina la Bwana Yesu Kristo, jitengeni nafsi zenu na kila ndugu aendaye bila utaratibu, wala si kwa kufuata mapokeo mliyoyapokea kwetu.”​—2 The. 3:6; Mit. 20:4; 24:30; Mhu. 5:12, 18; 10:18.

15 Naam, huenda akawako mtu ambaye ‘hakujiacha aadibiwe kwa maneno matupu tu,’ kutia na mashauri ya Maandiko kutoka kwa wazee kundini, naye anajikaza tu akitenda kinyume cha kanuni za Mungu. Ikiwa hivyo, Wakristo wanaweza kujisikia wakilazimika ‘kujitenga’ na mtu huyo, kama alivyoshauri Paulo.​—Mit. 10:17; 29:19, NW.

“MWEKENI HUYU KATIKA HALI YA KUTIWA ALAMA”

16. Paulo aliwapa Wathesalonike shauri gani?

16 Akiendelea na kuwashauri Wathesalonike juu ya watu wavivu, wasio na utaratibu, Paulo aliandika hivi: “Ikiwa mtu ye yote hatii neno letu kupitia barua hii, mwekeni huyu katika hali ya kutiwa alama [jihadharini na mtu huyo, UV], acheni kushirikiana na yeye, ili apate kuaibishwa. Hata hivyo msimwone yeye kama adui, bali endeleeni kumwonya kwa upole kama ndugu.” (2 The. 3:14, 15, NW) Kwa hiyo, Wakristo wanaweza ‘kumtia alama’ (kujihadhari) mtu anayejikaza tu akizidi kuzipuza kanuni za Mungu.

17. (a) Kwa sababu gani uangalifu unahitajiwa katika kulitumia shauri hilo? (b) Yesu alisema nini juu ya habari hii?

17 Walakini, tunahitaji kuwa waangalifu sana katika kutumia shauri hilo la kimungu. Katika hali yetu ya kutokukamilika, huenda tukawa na maelekeo ya kuhukumu wengine kwa kutegemea mambo ambayo sisi binafsi tunayapenda au tusiyoyapenda, kama vile kuhusu namna za mavazi au za kujipamba. Kwa mfano, ikiwa mavazi ya dada fulani hayakosi kuwa ya adabu njema, si yenye kuleta heshima mbaya wala hayawagutushi kina ndugu kwa ujumla, inatupasa tujue kwamba dada huyo hafanyi lisilofaa bali yeye ana mapendezi yaliyo tofauti tu na yetu. (Mwa. 37:3, 4; Yohana 19:23; 1 Tim. 2:9, 10) Sisi hatukufanywa waamuzi wa ndugu na dada zetu juu ya vijambo vidogo vidogo visivyo na maana vinavyohusu maoni yanayotofautiana, mapendezi au namna zenye kutofautiana za dhamiri. (Rum. 14:4, 10-12) Au, hata ikiwa mtu anakosea katika kijambo kidogo sana, lazima tulikumbuke shauri la Yesu:

“Msihukumu, msije mkahukumiwa ninyi. Kwa kuwa hukumu ile mhukumuyo, ndiyo mtakayohukumiwa; . . . Basi, mbona wakitazama kibanzi kilicho ndani ya jicho la ndugu yako, na boriti iliyo ndani ya jicho lako mwenyewe huiangalii?”​—Mt. 7:1-3.

18. Jambo gani lifanywe ikiwa ni wazi mtu fulani anakosa kufuata shauri la Mungu?

18 Walakini, namna gani kama kuna mtu ambaye ni wazi anaendelea kuziacha kanuni za Mungu, labda akiwa mvivu mno au mwenye kulaumu-laumu watu mno, ‘mwenye kupaya-paya maneno yasiyo na faida’ ambaye daima ni ‘mjishughulushi wa kile kisichomhusu yeye’? (2 The. 3:11, NW) Au, huenda tatizo likawa la kujitungia mpango ili ajifaidi na vitu vya kimwili vya wengine, kujitia katika tafrija ambazo kwa wazi hazifai, au kuhusika katika mwenendo unaotilika mashaka ambao kwa sasa haujafikia kiwango cha kustahili kufanyiwa hukumu.a Wazee wamejaribu kumsaidia mtu huyo, lakini yeye anazidi kujikaza tu na huenda akawa akiharibu wengine kundini au kuwa hatari kwa wengine. Wazee wanaweza kulizungumza jambo hilo na kumpa mzee mmoja kati yao mgawo wa kutolea kundi hotuba ya Maandiko yenye uthabiti na yenye kutoboa mambo waziwazi. Bila ya kutaja jina la huyo ‘mkosa utaratibu,’ kwa njia hiyo huenda wazee wakaweza ‘kufunga kinywa cha’ mtu huyo asiyejali mipango.​—Tito 1:10-13, NW.

19. Wengine kundini wanaweza kutendaje ikiwa tatizo hilo linazidi kuendelezwa?

19 Hali kama hiyo ikiwa katika kundi, Wakristo mmoja mmoja wanaweza kujisikia wakilazimika ‘kumtia alama’ mtu huyo.b Paulo anaeleza kwa uchache yanayohusika katika kufanya hivyo, akisema: “Acheni kushirikiana na yeye, ili apate kuaibishwa.” (2 The. 3:14, NW) Hiyo ingemaanisha kupunguza ushirika wako wa mambo ya urafiki na mtu huyo ‘aliyetiwa alama.’ Haikupasi wewe utangazie wengine uamuzi huo ulioufanya kwa faragha, wala usijaribu kuambia wengine wafuatane na uamuzi wako. Bali wewe binafsi ungeepuka ushirika wa mtu ‘aliyetiwa alama,’ kulingana na mashauri yenye kuleta hali njema yaliyotolewa na wazee wa kundi. Ingawa hivyo, usingemkataa huyo kabisa kabisa, kwa maana bado yeye ni ndugu yako, Mkristo mwenzako ambaye Kristo alifia. Badala ya kuruhusu mbegu zo zote za ‘chuki’ zisitawi, inakupasa wewe ‘umkaripie.’ Kwa njia gani? Naam, zaidi ya wewe mwenyewe kuwa mfano mwema, ikiwa utalitii kwa fadhili lakini kwa imara lile agizo la “Acheni kushirikiana na yeye” hiyo itakuwa njia moja ya kumtia adabu. Lakini wewe unaweza kufanya mambo mengine kumsaidia.​—Law. 19:17; Tito 2:7, 8.

20. Ikiwa wewe ‘umemtia alama’ mtu fulani asiye na utaratibu, una daraka gani?

20 Bado utakuwa karibu na Mkristo huyo ‘aliyetiwa alama’ kwenye mikutano ya kundi na katika utumishi wa shambani. Hivyo, huenda ukapata nafasi ya kutimizia wajibu ule mwingine ulio nao katika ‘kumtia alama’: “Msimwone yeye kama adui, bali endeleeni kumwonya kwa upole kama ndugu.” (2 The. 3:14, 15, NW) Wewe ukishindwa kutimiza daraka lako linalohusu upande huu wa shauri la Mungu, bali badala yake umtende ‘aliyetiwa alama’ kama adui, mwendo wako unaweza kuwa usio wa upendo kama ule wake.

21. Lengo la mpango huu unaopatana na Biblia ni nini? (Hes. 35:12; Kum. 19:11, 12)

21 Inatumainiwa kwamba ‘aliyetiwa alama’ ataaibika. Huenda akajua kwamba wewe unamwepuka usishirikiane naye kiurafiki kwa sababu unafuata uongozi wa Maandiko. Kumtia adabu hivyo huenda kukamsaidia ‘ainyoshe mikono iliyolegea na magoti yaliyopooza, ili kitu kilicho kiwete kisipotoshwe, bali afadhali kiponywe.’ Kwa kuwa hesabu kubwa sana za ndugu wanaoshirikiana na kundi la Mungu leo ni watu washikamanifu, inaelekea ni mara chache Wakristo watakapolazimika ‘kumtia alama’ ndugu asiyefuata utaratibu. Lakini ikitukia kwamba ndugu amekosa utaratibu, labda kumtia adabu, pamoja na kuendelea kumwonya kwa upole, ‘kutaleta matunda yenye amani,’ yaani, haki.​—Ebr. 12:11-13.

KUFANYA MKUTANO NA HALMASHAURI YA WAZEE

22, 23. Visa vya dhambi nzito vishughulikiwe namna gani?

22 Kama vile ambavyo tumeona (katika fungu la 7), mtu ambaye ‘ametenda dhambi nzito’ anahitaji mazungumzo pamoja na ‘wazee wa kundi.’ (Yak. 5:14, 15) Wanaume hao wamo katika cheo kizuri cha kuweza kumtia adabu ya kimungu mtu ambaye ameghafilika na kutumbukia katika dhambi yenye kusikitisha sana. Wao wanaweza kumpa msaada wa kiroho anaouhitaji.​—Mit. 6:23.

23 Kwa kawaida halmashauri yenye wazee watatu ndiyo inayopangwa ishughulikie kisa cha kosa zito. Wao hawatendi kama waamuzi (mahakimu) tu au ‘mapolisi wa kiroho.’ Wao ni wachungaji wa kundi, na ndivyo wanavyojithibitisha kuwa wanaposhughulika na mkosaji mmoja. Mchungaji-kondoo wa halisi haonyeshi roho ya kulipa kisasi, ya ukatili wala ya kutafuta-tafuta makosa. Na iwe ivyo hivyo kwa wazee. Wao wapo ili kusaidia, si kulaumu. (Yuda 23) Mradi (lengo) wao ni kumgeuza mtenda dhambi aiache njia yake, ikiwezekana.​—Yak. 5:19, 20.

24. Wazee hujaribu kumfanyia nini mtenda dhambi?

24 Hata hivyo, wakati wazee wanaposhughulika na dhambi yenye kusikitisha sana, lazima ‘washikamane sana na neno lile la uaminifu,’ ‘waweze kushauri kwa bidii nyingi kwa fundisho ambalo ni lenye afya na kukaripia pia wale wanaopinga.’ (Tito 1:9, NW) Kwa hiyo wasijizuie kumwonyesha wazi mkosaji kutokana na maandiko ubaya wa mwendo wake na sababu inayofanya ahitaji kurekebisha njia yake. Wanamtaka atubu arudie amani pamoja na Mungu.​—1 Pet. 3:10-12.

25. Ni mambo gani mengine tunayohitaji kujifunza?

25 Ingawa hivyo, ni kwa njia gani inawapasa wazee wakaripie watenda makosa? Toba ya kimungu ni nini? Toba hiyo inaonyeshwaje? Inawapasa wazee washughulikie visa vya dhambi nzito namna gani ikiwa toba imeonyeshwa? Je! ni lazima mkosaji akaripiwe mbele ya kundi zima? Mambo hayo yanazungumzwa katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

a Mfano unaohusu mtu kutembea na mwanamke au mwanamume akiwa bado hajawekwa huru na Maandiko aoe au aolewe tena ulizungumzwa katika “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti The Watchtower la Agosti 1, 1980. Katika Kiswahili habari hizo zitakuwa katika toleo la Februari 1, 1982.

b ‘Kutia mtu alama’ kunamaanisha kumwangalia kwa njia ya pekee. Tofautisha jambo hilo na kule kumwangalia kwa njia nzuri kunakotajwa katika Zaburi 37:37; Wafilipi 3:17 na Waebrania 13:7.

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

SISI TUNAHUSIKAJE KATIKA KUTIA ADABU KWA NJIA YA KIMUNGU?

Nyakati nyingine Mungu hututia adabu kupitia Biblia au misaada ya kujifunzia Biblia.

Au huenda Mkristo, hasa mzee, akatuonyesha kosa kwa upendo.

Ikiwa wengine wanakataa kuacha mwendo usio na utaratibu, wazee wanaweza kulazimika kuamsha fikira za kundi na kulionya juu ya mwendo au tabia inayohusika.

Inatupasa tujisikie kwamba sisi watu mmoja mmoja tunapaswa ‘kutia alama’ (2 The. 3:14, 15, NW) watu wo wote wanaokosa utaratibu kwa njia hiyo.

Tukifanya hivyo, tutaepuka kushirikiana nao, LAKINI inatupasa pia tutimize wajibu wetu wa kuwasaidia na kuwaonya kwa upole watu hao wasio na utaratibu, maana bado wao ni ndugu zetu wa Kikristo.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Kama ungemwona Mkristo mwenzako akielekea kuingia hatarini, je! ungemtolea shauri lenye fadhili?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Paulo alishauri “uendelee kuwasaidia” wale wanaohitaji mashauri ya kuwatia adabu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki