Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Je, ‘kutia alama’ kunakotajwa katika 2 Wathesalonike 3:14 ni hatua rasmi ya kutaniko, au ni jambo ambalo Wakristo mmoja-mmoja hufanya ili kuepuka watu wasiokubali nidhamu?
Jambo ambalo mtume Paulo aliwaandikia Wathesalonike laonyesha kwamba kwa wazi wazee wa kutaniko huhusika katika ‘kutia alama.’ Hata hivyo, Wakristo mmoja-mmoja baadaye hutekeleza hilo, wakifanya hivyo wakiwa na malengo ya kiroho akilini. Twaweza kufahamu hilo vizuri zaidi kwa kuchanganua kikao cha awali cha shauri la Paulo.
Paulo alisaidia kuanzisha kutaniko la Thesalonike, akiwasaidia wanaume na wanawake wawe waamini. (Matendo 17:1-4) Baadaye aliwaandikia barua alipokuwa Korintho ili kuwapongeza na kuwatia moyo. Pia Paulo alitoa shauri lililohitajiwa. Aliwahimiza ‘waishi kwa utulivu na kushughulika na mambo yao wenyewe na kufanya kazi kwa mikono yao.’ Baadhi yao hawakuwa wakifanya hivyo, kwa hiyo Paulo akaongeza kusema hivi: “Twawahimiza nyinyi kwa bidii, akina ndugu, waonyeni kwa upole wale wasio na utaratibu, semeni kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo, tegemezeni walio dhaifu.” Ni wazi kwamba kulikuwako watu “wasio na utaratibu”a miongoni mwao ambao walihitaji shauri.—1 Wathesalonike 1:2-10; 4:11; 5:14.
Miezi kadhaa baadaye, Paulo aliandika barua yake ya pili kwa Wathesalonike, yenye maelezo zaidi juu ya kuwapo kwa Yesu kwa wakati ujao. Paulo pia alitoa mwongozo zaidi juu ya namna ya kushughulika na watu wasio na utaratibu ambao hawakuwa ‘wakifanya kazi bali walikuwa wakijiingiza katika lile lisilowahusu wao.’ Matendo yao hayakupatana na kielelezo cha Paulo akiwa mfanyakazi mwenye bidii na vilevile hayakupatana na agizo la wazi juu ya kufanya kazi ili kujitegemeza. (2 Wathesalonike 3:7-12) Paulo aliagiza hatua fulani zichukuliwe. Hatua hizo zilichukuliwa baada ya wazee kuwaonya kwa upole au kuwashauri watu wasio na utaratibu. Paulo aliandika hivi:
“Sasa tunawapa nyinyi maagizo, akina ndugu, . . . kujiondoa kutoka kwa kila ndugu anayetembea bila utaratibu na si kulingana na mapokeo mliyopokea kutoka kwetu. Kwa upande wenu, akina ndugu, msikate tamaa katika kutenda lililo sawa. Lakini ikiwa yeyote hawi mtiifu kwa neno letu kupitia barua hii, mfulize kumtia mtu huyu alama, komeni kushirikiana naye, ili apate kuaibika. Na bado msiwe mkimwona yeye kuwa adui, bali endeleeni kumwonya kwa upole kama ndugu.”—2 Wathesalonike 3:6, 13-15.
Kwa hiyo zile hatua zaidi zilitia ndani kujiondoa kutoka kwa watu wasio na utaratibu, kuwatia alama, kuacha kushirikiana nao, na bado kuendelea kuwaonya kwa upole kama ndugu. Ni nini kingewafanya washiriki wa kutaniko wachukue hatua hizo? Ili kutusaidia kuelewa hilo, acheni tutambulishe hali tatu ambazo Paulo hakuwa akikazia fikira hapa.
1. Twajua kwamba Wakristo si wakamilifu nao hukosea. Hata hivyo, upendo ni alama ya Ukristo wa kweli, ukitutaka tuwe wenye kuelewa na wenye kusamehe makosa ya wengine. Kwa kielelezo, huenda Mkristo akafokwa na hasira isivyo kawaida, kama ilivyokuwa kati ya Barnaba na Paulo. (Matendo 15:36-40) Au kwa sababu ya uchovu, huenda mtu akasema maneno makali na yenye kuumiza. Katika hali kama hizo, kwa kuonyesha upendo na kutumia shauri la Biblia, twaweza kufunika kosa hilo, tukiendelea kuishi, kushirikiana, na kufanya kazi na Mkristo mwenzetu. (Mathayo 5:23-25; 6:14; 7:1-5; 1 Petro 4:8) Ni wazi kwamba makosa ya aina hiyo siyo mambo ambayo Paulo alikuwa akishughulikia katika 2 Wathesalonike.
2. Paulo hakuwa akishughulikia hali ambamo Mkristo mwenyewe aamua kupunguza ushirika wake na mwingine ambaye njia zake au mitazamo yake si mizuri—kwa kielelezo, mtu aonekanaye kuwa mwenye kukazia sana fikira zake katika tafrija au vitu vya kimwili. Au huenda mzazi akapunguza ushirika wa mtoto wake na vijana wanaopuuza mamlaka ya wazazi, wachezao michezo kwa kuumizana au kwa njia yenye kuhatarisha, au wasiouchukua Ukristo kwa uzito. Hayo ni maamuzi ya kibinafsi yanayopatana na mambo tunayosoma katika Mithali 13:20: “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; bali rafiki wa wapumbavu ataumia.”—Linganisha 1 Wakorintho 15:33.
3. Kuhusu jambo jingine lenye uzito tofauti, Paulo aliwaandikia Wakorintho juu ya mtu azoeaye dhambi nzito wala hatubu. Watenda-dhambi hao wasiotubu walipaswa kuondolewa kutoka katika kutaniko. Ilikuwa ni kana kwamba Shetani alipasa kukabidhiwa mtu huyo “mwovu.” Baadaye, Wakristo waaminifu-washikamanifu hawakupaswa kuchangamana na watu hao waovu; mtume Yohana aliwahimiza Wakristo hata wasiwasalimu. (1 Wakorintho 5:1-13; 2 Yohana 9-11) Hata hivyo, jambo hilo nalo halipatani na shauri la 2 Wathesalonike 3:14.
Hali inayohusisha watu “wasio na utaratibu” ambayo inazungumziwa katika 2 Wathesalonike yatofautiana na hali tatu zilizo juu. Paulo aliandika kwamba hao bado walikuwa “ndugu,” waliopasa kuonywa kwa upole na kutendewa kama ndugu. Kwa hiyo, tatizo la ndugu hao “wasio na utaratibu” halikuwa jambo la kibinafsi kati ya Wakristo wala halikuwa zito vya kutosha hivi kwamba wazee wa kutaniko walipaswa kuchukua hatua ya kutenga na ushirika, kama vile ambavyo Paulo alifanya kuhusu ile hali ya ukosefu wa adili huko Korintho. Watu “wasio na utaratibu” hawakuwa na hatia ya dhambi nzito, kama yule mtu aliyetengwa na ushirika huko Korintho.
Watu “wasio na utaratibu” huko Thesalonike walikuwa na hatia ya kukengeuka kwa njia dhahiri kutoka katika Ukristo. Hawangekubali kufanya kazi, iwe ni kwa sababu walifikiri kwamba kurudi kwa Kristo kulikuwa kumekaribia au kwa sababu walikuwa wavivu. Isitoshe, walikuwa wakisababisha vurugu kubwa kwa ‘kujiingiza katika lile lisilowahusu wao.’ Yaelekea kwamba wazee wa kutaniko walikuwa wamewashauri tena na tena, kulingana na shauri la Paulo katika barua yake ya kwanza na mashauri mengine ya Mungu. (Mithali 6:6-11; 10:4, 5; 12:11, 24; 24:30-34) Na bado waliendelea katika njia iliyoletea kutaniko sifa mbaya na ambayo ingeenea miongoni mwa Wakristo wengine. Kwa hiyo mzee Mkristo Paulo, bila kutaja majina ya watu hao, alizungumzia hadharani ukosefu wao wa utaratibu, akifunua mwendo wao wenye kosa.
Pia alilijulisha kutaniko kwamba ingefaa wao wenyewe wakiwa Wakristo mmoja-mmoja ‘watie alama’ watu wasio na utaratibu. Hilo lilimaanisha kwamba watu mmoja-mmoja wapaswa kutambua watu ambao matendo yao yalilingana na mwendo ambao kutaniko lilikuwa limetahadharishwa dhidi yake waziwazi. Paulo aliwashauri ‘wajiondoe kutoka kwa kila ndugu anayetembea bila utaratibu.’ Bila shaka hilo halingemaanisha kumwepuka kabisa mtu huyo, kwa kuwa bado walipaswa ‘kuendelea kumwonya kwa upole kama ndugu.’ Wangeendelea kuwa na ushirikiano wa Kikristo naye kwenye mikutano na labda kwenye huduma. Wangeweza kutumaini kwamba ndugu yao angeitikia onyo la upole na kuacha njia zake zenye kusumbua.
‘Wangejiondoa’ kutoka kwake jinsi gani? Yaonekana, hilo lilihusu mambo ya kirafiki. (Linganisha Wagalatia 2:12.) Kukoma kwao kuwa na shughuli za kirafiki na tafrija naye kungeweza kumwonyesha kwamba watu wenye kanuni hawapendezwi na njia zake. Hata ikiwa hangeaibika na kubadilika, angalau wengine hawangeelekea kujifunza njia zake na kuwa kama yeye. Wakati huohuo, Wakristo hao mmoja-mmoja wapaswa kukazia mambo yafaayo. Paulo aliwashauri hivi: “Kwa upande wenu, akina ndugu, msikate tamaa katika kutenda lililo sawa.”—2 Wathesalonike 3:13.
Ni wazi kwamba shauri hilo la mtume si msingi wa kuwadharau au kuwahukumu ndugu zetu wanaoteleza au kukosea kidogo. Badala yake, lengo lake ni kumsaidia mtu anayechukua mwendo wenye kusumbua ambao wahitilafiana sana na Ukristo.
Paulo hakutunga sheria zenye mambo mengi kana kwamba alikuwa akijaribu kuanzisha utaratibu tata. Lakini ni wazi kwamba wazee wapaswa kwanza kumshauri na kumsaidia mtu asiye na utaratibu. Wasipofaulu na mtu huyo akiendelea katika njia yenye kusumbua na iwezayo kuenea, huenda wakakata kauli kwamba kutaniko lapasa kutahadharishwa. Wanaweza kupangia hotuba inayoeleza kwa nini ukosefu huo wa utaratibu wapasa kuepukwa. Hawatataja majina yoyote, lakini hotuba yao ya kuonya itasaidia kulinda kutaniko kwa sababu wasikivu watakuwa waangalifu zaidi na watapunguza utendaji wa kirafiki na watu wowote ambao kwa wazi wanaonyesha ukosefu huo wa utaratibu.
Yatumainiwa kwamba hatimaye mtu huyo asiye na utaratibu ataaibikia njia zake naye atachochewa abadilike. Wazee na wengine kutanikoni waonapo badiliko hilo, wao mmoja-mmoja wanaweza kuamua kuondoa mipaka ambayo wameweka juu ya kushirikiana kibinafsi naye.
Kwa muhtasari, basi: Wazee wa kutaniko huongoza katika kutoa msaada na shauri ikiwa mtu fulani anatembea bila utaratibu. Ikiwa haoni kosa la njia yake na anaendelea kuwa uvutano usiofaa, wazee wanaweza kulionya kutaniko kupitia hotuba ambayo huonyesha waziwazi maoni ya Biblia—iwe yahusu kufanya miadi ya kijinsia na wasioamini, au mwendo mwingine usiofaa. (1 Wakorintho 7:39; 2 Wakorintho 6:14) Wakristo katika kutaniko waliotahadharishwa hivyo wanaweza kujiamulia kupunguza kushirikiana kirafiki kwa njia yoyote na watu ambao kwa wazi wanafuata mwendo usio wa utaratibu lakini ambao bado ni ndugu.
[Maelezo ya Chini]
a Neno hilo la Kigiriki lilitumiwa kurejezea askari-jeshi ambao hawakudumisha utaratibu au wasio na nidhamu, na vilevile kwa wanafunzi watoro, waliokosa masomo ya shule yao.
[Picha katika ukurasa wa 31]
Wazee Wakristo huonya kwa upole watu wasio na utaratibu na bado huwaona kuwa waamini wenzao