Je! Wewe Utamsikiliza Mungu?
‘LAKINI kwa hakika Biblia imekuwapo kwa muda mrefu sana, na ulimwengu umo katika hali mbaya zaidi kuliko wakati mwingine wo wote uliopita!’ Hiyo ni kweli kabisa, na sababu ni kwamba watu wamekuwa hawamsikilizi Mungu akisema. Kwa sababu gani?
Katika visa fulani, wao hawapendezwi tu. Tangazo la karibuni lililotolewa na kikundi cha Wachunguzi wa Ubinadamu wa kidunia linasema hivi: “[ Sisi ] tunalikataa wazo la kwamba Mungu amejiingiza kimwujiza katika historia au akajionyesha wazi kwa wachache waliochaguliwa, au kwamba anaweza kuokoa au kukomboa wafanyao dhambi.” Kwa kweli, Mungu anasema leo, si kwa “wachache waliochaguliwa” peke yao, bali kwa wote watakaosikiliza. “Mungu . . . anawaagiza watu wote wa kila mahali watubu.” (Matendo 17:30) Hata hivyo, wo wote wanaolikataa hata wazo la Mungu kusema bila shaka hawatamsikiliza. Lazima wakati wao ujao uwe unaonekana kuwa wenye giza sana.
Ni kweli kwamba viongozi wengi wa ulimwengu wamedai kuwa wanamwamini Mungu. Hata hivyo, hawajasaidia kufanya mambo yawe afadhali sana. Kwa sababu gani ndivyo ilivyo? Sana-sana ni kwa sababu, kama mwanafalsafa (mwanafilosofia) Mfaransa Voltaire alivyosema wakati mmoja, “Watu wengi wenye cheo wa ulimwengu huu wanaishi kama kwamba hawaamini kuna Mungu.” Madai yao kwamba wanamwabudu Mungu hayakuwazuia wasichinjane, wasifanye vita vya uadui, uonezi, mateso na hila ambazo zimekuwa sehemu zenye kuendelea za historia. Ni wazi kwamba Mungu akisema, wao pia hawakusikiliza.
WENGINE WANASIKIA BALI HAWASIKILIZI
‘Hata hivyo, je! si kweli kwamba dini nyingi zinaitumia Biblia katika mahubiri yazo, na watu wanasikia maneno yayo kila Jumapili?’ Ni sahihi kusema hivyo. Walakini ingawa wanasikia, je! kweli kweli wanasikiliza, yaani, wanakaza fikira kwa yale wanayosikia?
Kwa mfano, makanisa mengi yanatumia ile sala ya “Baba Yetu” (au, “Sala ya Bwana”) katika ibada za Jumapili. Sala hiyo ni sehemu ya Biblia. Katika tafsiri moja ya Kikatoliki, maneno ya kwanza ya sala hiyo ni haya: “Baba yetu aliye mbinguni. Jina lako lifanywe takatifu. Ufalme wako uje. Mapenzi yako yafanywe duniani kama ilivyo mbinguni.”—Mt. 6:9, 10, Douay.
Mapenzi ya Mungu yanayopasa kufanywa duniani ni nini? Sehemu ya mapenzi hayo inasemwa katika ahadi hii: “Wenye upole watairithi [dunia], watajifurahisha kwa wingi wa amani.” (Zab. 37:11) Kulingana na ile sala ya “Baba Yetu,” amani hiyo italetwa na “ufalme” wa Mungu, serikali yake.
Kwa hiyo lilikuwa jambo la kuvutia huko-o-o nyuma mwaka 1965, baada ya Papa Paulo wa Tano kutembelea Umoja wa Mataifa, kusoma katika magazeti kwamba yeye alisema hivi: “Vikundi vya watu wa dunia wanageukia Umoja wa Mataifa kuwa tumaini la mwisho la upatano na amani.” (Sisi tumelaza maneno) Bila shaka usemi huo ulisaidia washiriki wa Umoja wa Mataifa waone kwamba kazi yao ni ya maana na inafaa. Walakini kama wao ndio waliokuwa tumaini la mwisho la amani, vipi juu ya ufalme wa Mungu? Kwa wazi Papa Paulo wa Tano hakuwa akisikiliza maneno ya sala ile ya “Baba Yetu.”
Kuna mifano mingine mingi inayoonyesha kwamba wakati watu wanapoisikia Biblia ikisomwa, mara nyingi hiyo ni desturi kwao tu, ila wanashindwa kukaza fikira na kufahamu maana ya yale inayoyasema.
KUSIKILIZA NA KUTII
Vilevile “kusikiliza” kunamaanisha “kufikiria kwa uzito.” Wengi leo wanafahamu kabisa yale ambayo Mungu anasema juu ya mambo fulani, walakini hawayachukui maneno yake kwa uzito. Wanafuata mawazo yao wenyewe. Kwa hiyo, hawasikilizi Mungu anaposema.
Mfano wa jambo hilo ni adili. Mungu anatoa kanuni iliyo wazi ya adili. Yeye anasema: “Waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti.”—1 Kor. 6:9, 10.
Watu wanaofuata uongozi wa kufanya mambo yawe ya kisasa, kutia viongozi wengi wa kidini, wanaikataa kanuni hiyo. Wanasema kuwa ni ya kizamani na wanatia moyo njia ya maisha ya ‘kufanya utakalo.’ Matokeo yamekuwa nini? Mweneo wa matineja (vijana) wenye mimba, utoaji wa mimba, magonjwa ya kisonono na kaswende, talaka na mchafuko wa maono ya ndani.
Jambo hilo halipasi kutushangaza. “Mungu hadhihakiwi; kwa kuwa cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna.” (Gal. 6:7) Sheria za Mungu za adili kama vile sheria zake za asili, zinatolewa kwa ajili ya ulinzi wetu na kutupa mema. Kupanda kumkaidi Mungu hakika kutaleta matokeo mabaya. Kukataa kanuni za Mungu ni kama kukataa sheria ya uvutano Hata maoni yetu ya kibinafsi yawe nini tunaikaidi kwa hasara yetu wenyewe!
MUNGU ANAPOSEMA, KUNA WO WOTE WANAOSIKILIZA?
‘Basi, kwa hiyo,’ huenda ukauliza, ‘ikiwa wanadini na viongozi wengi wa ulimwengu hawasikilizi Mungu anaposema, je! kuna ye yote anayesikiliza?’ Ndiyo, wengine wanasikiliza. Wakati mmoja Yesu alisema hivi: “Kila aliye wa hiyo kweli hunisikia sauti yangu.” Kwa kuwa yeye alieleza kwamba kila kitu alichosema kwa kweli kilitoka kwa Mungu, kumsikiliza Yesu ni sawa na kumsikiliza Mungu. Kwa hiyo wale ‘walio wa hiyo kweli’ wanamsikiliza Mungu.—Yohana 18:37; 7:16,17.
Na wao wanafanya zaidi ya kusikiliza. Wanatoka nje na kusaidia wengine wasikilize, pia. Yesu aliwaamuru hivi: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza . . . kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mt. 28:19, NW) Je! kuna ye yote anayefanya hivyo leo?—Mt. 7:16.
Wakati mmoja, ili apendeze rafiki, mwanamke kijana alitembelea kikundi cha kidini ambacho hakuwa ameshirikiana nacho hapo mbele. Kwa kuwa walikuwa wenye urafiki, yeye alimwuliza mmoja wao ulizo, ili aone tu kungetokea nini. Alistaajabu sana wakati alipopewa jibu la moja kwa moja kutoka katika Biblia. Kisha akaenda kwa mshiriki mwingine wa kikundi hicho, na akauliza ulizo hilo hilo. Alistaajabu, kwa kuwa huyo pia aliifungua Biblia na akampa jibu lile lile. Alirudia jambo hilo na akakuta kwamba, watu hao wameungana kidini, hawana mvurugo.
Jambo hilo lilimvutia mwanamke huyo. Pasipo kujua, alikuwa amejikuta katika sifa nyingine ya watu hao ‘upande wa kweli’: wao wanajitahidi wawe na “nia moja na shauri moja.” (1 Kor. 1:10) Wao wanakubali kwamba ‘kila andiko ni lenye pumzi ya Mungu.’ Kwa hiyo, wao wanajifunza, na kufundisha, si maoni ya watu bali yale ambayo Mungu anasema katika Biblia.—2 Tim. 3:16.
Polepole mwanamke huyo kijana aliacha maoni yake kwamba hakuna lo lote linaloweza kujulikana juu ya Mungu. Yeye alifurahi kusikiliza Mungu alipokuwa akisema. Mwishowe, akawa mshiriki mwenye kutenda wa kundi hilo la Mashahidi wa Yehova.
YALE ANAYOSEMA MUNGU
Je! wewe ‘ni wa ile kweli’? Basi utataka kusikiliza—kusikiliza kikweli, kwa maana ya kukaza fikira na kuweka moyoni yale anayosema Mungu. Kufanya hivyo kutakuweka kati ya wale wachache, kwa kuwa watu wengi leo hawamsikilizi Mungu. Kwa kusikitisha, kama Waisraeli wa kale, “wameipuza njia ya Yehova.”—Yer. 5:4, NW.
Hata hivyo, ni jambo la akili kuisikiliza hekima ya Mungu. “Kila [asikilizaye hekima ya kweli] atakaa salama, naye atatulia bila kuogopa mabaya.” (Mit. 1:20-33) Leo, wale wanaomsikiliza Mungu wanaongozwa waepuke hatari zinazotokana na kuishi katika ulimwengu huu usiokamilika. Kwa njia hiyo wanaepuka misiba ya kuepukika. Na karibuni, wakijithibitisha kuwa waaminifu, wataishi katika ulimwengu ambamo ‘mabaya’ hayatatokea tena. Wakati huo, Mungu “atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufu. 21:4.
Huo ndio ulimwengu ambao Mungu atawatayarishia wale ‘walio wa ile kweli.’ Je! ungependa kuwa sehemu yake? Basi lifanye liwe jambo kuu kusikiliza wakati Mungu anaposema. Mashahidi wa Yehova watakuwa wenye furaha kukusaidia wewe ufanye hivyo.
[Sanduku katika ukurasa wa 7]
Faida za kusikiliza Mungu anaposema
● Tumaini la dunia iliyo paradiso
● Uhakika katika wakati ujao
● Maisha ya jamaa yenye furaha sasa
● Kufurahia amani
● Umoja wa ibada ya kweli
● Imani kwa ufalme wa Mungu kupitia Kristo