“Kwa Kweli ni Nani Yule Msimamizi wa Nyumba Mwaminifu Mwenye Akili?”
“Kwa kweli ni nani yule msimamizi wa nyumba mwaminifu, mwenye akili, ambaye bwana yake atamweka juu ya baraza ya watumishi wake?”—Luka 12:42, NW.
1. Ulizo tunalokabili ni lenye umri wa miaka mingapi, na wale wanaokosa kupata jibu wanashindwa kupata nini?
ULIZO hilo sasa lina umri wa miaka zaidi ya 1,900. Mamia mengi ya maelfu leo wanaamini wamelipata jibu. Wale wasiopata jibu wanakosa kupata faida zenye matokeo juu ya wakati wao ujao wa milele. Ulizo ni hili: “Kwa kweli ni nani yule msimamizi wa nyumba mwaminifu, mwenye akili, ambaye bwana yake atamweka juu ya baraza ya watumishi wake ili aendelee kuwapa kipimo chao cha chakula kwa wakati unaofaa?”—Luka 12:42, NW.
2. (a) Kwa mara ya kwanza ulizo hilo liliulizwa wakati gani, na ni nani aliyeulizwa? (b) Ulizo hilo linapasa kuvutia nani, na kwa sababu gani?
2 Ulizo hilo liliulizwa kwa mara ya kwanza katika nchi ya Mashariki ya Kati, Israeli. Wakati wenyewe ulikuwa mwaka 32 wa Wakati wa Kawaida wetu, kati ya sherehe ya Kiisraeli ya vibanda katika vuli na sikukuu ya mzinduo wa hekalu lao lililojengwa upya katika Yerusalemu mapema katika majira ya baridi. Mtu aliyetokeza ulizo hilo ametokeza mabishano ulimwenguni pote. Jina lake ni Yesu Kristo. Kwa hiyo ulizo lake lapasa kuvutia kipekee Jumuiya ya Wakristo, kwa kuwa inasema kuwa yeye ni “Bwana” na inadai kuwa wanafunzi wake wamejaa ndani yayo.
3, 4. (a) Wasikilizaji wa Yesu walikuwa wanapendezwa na nini, na kwa hiyo aliwaambia wasiwe na woga juu ya nini? (b) Ni mifano gani miwili ambayo Yesu alitoa kuhusu uhitaji wa wao kuendelea kulinda?
3 Kulingana na masimulizi ya Biblia, ulizo hilo lenye kupenya ndani liliulizwa katika kujibu ulizo jingine na lilielekezwa kwa watu waliokuwa wanapendezwa na serikali kuu zaidi itakayopata kusimamishwa duniani, ufalme wa Muumba wa mbingu na dunia, “ufalme wa Mungu.” Ndiyo sababu Yesu Kristo alitangulia kuwaambia hivi wasikilizaji wake Waisraeli: “Msiogope, enyi kundi dogo! Kwa kuwa Baba yenu amependa kuwapeni huo utawala. Uzeni mali zenu zote mkawape maskini. Jifanyieni mifuko isiyochakaa, na jiwekeeni hazina mbinguni ambako haitapungua. Huko wezi hawakaribii, wala nondo hawaharibu. Pale hazina yako ilipo, ndipo pia na moyo wako utakapokuwa.”
4 “Kanda zenu ziwe zimefungwa viunoni, na taa zenu ziwe zinawaka; muwe kama watumishi wanamngoja bwana wao arudi kutoka arusini, ili atakaporudi na kubisha hodi, wamfungulie mara. Heri yao watumishi wale ambao bwana atakaporudi atawakuta wanakesha! Nawaambieni hakika, huyo bwana atajifunga ukanda kiunoni, atawakalisha mezani na kuwatumikia. Hata kama ni usiku wa manane au alfajiri, kama akiwakuta wako hivyo, heri yao. Muwe na hakika kwamba, kama mwenye nyumba angejua saa ambayo mwizi atakuja, angekesha, wala hangeiacha nyumba yake kuvunjwa. Na ninyi, hali kadhalika, jiwekeni tayari, maana Mwana wa mtu atakuja saa ile ambayo hamuidhani.”—Luka 12:32-40, HNWW
5. (a) Petro aliyaitaje maneno ya Yesu ya kusihi, na kwa hiyo jibu la Yesu lingeonwa kuwa nini? (b) Ulizo la Petro juu ya matumizi ya maneno ya Yesu linatokeza ulizo gani juu ya namna maneno ya Yesu katika kujibu yanavyohusu?
5 Yale ambayo Bwana Yesu Kristo alisema hapo, mtume Petro aliyaita “mfano,” kwa maana masimulizi ya Luka yanaendelea kusema hivi: “Petro akasema, ‘Bwana, unatuambia sisi mfano [parabolé] huo au ni kwa wote?’ “(Luka 12:41, Revised Standard Version na tafsiri nyingine) Basi, ni jambo la akili kwamba yale ambayo Yesu alisema katika kujibu yangeonwa kuwa mfano, ambao ungeonyesha au kufananisha mambo fulani halisi ambayo yangekuja wakati ujao. Yaani, jibu la Yesu katika Luka 12:42-44 lingekuwa sehemu ya mfano wa “msimamizi mwaminifu na mwenye hekima.” (RSV) sasa tunapouchunguza mfano huo, twapaswa kukumbuka ulizo la Petro, ambalo matumizi yake yanatokeza mfano huo unaofuata, yaani, “Bwana, unatuambia sisi mfano huo, au ni kila mtu?” (Luka 12:41, New International Version; The Living Bible) Basi, tunauliza, Je! mfano huo wa “msimamizi” unahusu jamii fulani ya “sisi,” yaani, mitume 12 wa Yesu Kristo, au ni kila mtu aliyekuwa akimsikiliza Yesu wakati huo na, leo, kwa kila mtu anayesoma mfano wa Yesu, hata dini yake iwe nini ndani au nje ya Jumuiya ya Wakristo? Je! mfano huo ni jambo linalohusu jamii au mtu mmoja mmoja?
“BWANA YAKE”
6. Yesu alijibu ulizo la Petro kwa mfano gani?
6 Yesu hakujibu moja kwa moja ulizo la Petro kuhusu “mfano” huo unaotangulia, bali alitoa mfano mwingine katika kujibu kwa kusema hivi: “Kwa kweli ni nani yule msimamizi wa nyumba mwaminifu, mwenye akili, ambaye bwana yake atamweka juu ya baraza ya watumishi wake ili aendelee kuwapa kipimo chao cha chakula kwa wakati unaofaa? Mwenye furaha ni mtumwa huyo, iwapo bwana yake anaporudi atamkuta akifanya hivyo! Mimi nawaambia kikweli, Yeye atamweka juu ya vitu vyake vyote.”—Luka 12:42-44, New World Translation.
7. “Bwana” ya msimamizi wa nyumba huyo anafananisha nani, na kwa hiyo wale wanaohusika pamoja na “bwana’’ huyo wanapaswa kuendeleza nia gani wakati huu wa “umalizio wa mfumo wa mambo”?
7 Hakuna mtu atakayetia shaka kwamba “bwana” ya huyo msimamizi wa nyumba mwaminifu anafananisha msimuliaji wa mfano huo, Bwana Yesu Kristo. Katika mfano uliotokeza ulizo la Petro, Yesu alijifananisha na bwana-arusi, ambaye, kwa sababu ya sherehe za ndoa, anarudi nyumbani wakati wa saa isiyojulikana ya usiku au mapema asubuhi. (Luka 12:35-40) Hakika, basi, wale wanaohusika katika utimizo wa mfano wa Yesu wanapaswa kulinda, sana-sana wakati wa “umalizio wa mfumo wa mambo.”—Mt. 24:3, NW.
8. Ni tangu wakati gani Yesu Kristo amekuwa “bwana” juu ya “baraza ya watumishi’’ na Ufunuo 7:1-8 unawasimulia namna gani?
8 Kwa habari ya mfano wa yule msimamizi wa nyumba, bwana huyo ana “baraza ya watumishi,” na huyo msimamizi wa nyumba ni mmoja wao. Jambo hilo linalingana na uhakika wa kwamba msimuliaji wa mfano huo, Bwana Yesu Kristo, ana nyumba kwa maana ya kiroho. Kuhusiana na hilo imeandikwa, katika Waebrania 3:4-6: “Maana kila nyumba imetengenezwa na mtu; ila yeye aliyevitengeneza vitu vyote ni Mungu. Na Musa kweli alikuwa mwaminifu katika nyumba yote ya Mungu kama mtumishi, awe ushuhuda wa mambo yatakayonenwa baadaye; bali Kristo, kama mwana, juu ya nyumba ya Mungu.” Nabii Musa alikuwa msimamizi juu ya nyumba ya yale makabila 12 ya Israeli mwanzoni mwa taifa hilo. Yesu Kristo, akiwa ndiye Musa Mkuu Zaidi, amekuwa akisimamia nyumba ya Israeli wa kiroho tangu siku ya Pentekoste ya mwaka 33 W.K. kufika wakati huu. Ufunuo 7:1-8 unafunua kwamba “nyumba” hiyo inajumuishwa na Waisraeli wa kiroho 144,000, waliogawanywa kuwa makabila 12, kila moja likiwa na 12,000. Hiyo ni “nyumba” ambayo imejumuishwa na wana wa kiroho wa Mungu, kama Kichwa wao mwenyewe Yesu Kristo. Wao kama jamii wanajumuishwa kuwa lile “kundi dogo,” ambalo, kama Yesu alivyosema, Yehova Mungu, Baba wa kimbinguni amekubali kuwapa ufalme wa mbinguni.—Kum. 18:15-18; Luka 12:32; Matendo 3:19-23.
9. Ikibishwa kwamba “msimamizi wa nyumba” huyo anafananisha mwanamume mmoja Mkristo, ambaye aliwekwa katika karne ya kwanza W.K., ni gumu gani tunalokabili juu ya kuweka wakati barabara wa kufika kwa bwana huyo?
9 Kwa hiyo wale wana wa kiroho wa Mungu, 144,000, wanajumuishwa kuwa “baraza ya watumishi” ambayo juu yake, Bwana Yesu Kristo, anamweka yule “msimamizi wa nyumba” wa mfano ule. Utambuzi wa “msimamizi wa nyumba” huyo wa mfano huo (Kigiriki, oikonómos, Kiebrania, so·khenʹ,—tafsiri ya Delitsch) lingali ni jambo linalobishaniwa na Wakristo wengi wa kujidai. Tukisema kwamba “msimamizi wa nyumba” huyo anafananisha mwanamume mmoja Mkristo, tunaingia ndani ya magumu yasiyoweza kushindwa. Kama hivi, mfano huo unaonyesha kwamba bwana ya huyo msimamizi wa nyumba anaenda zake katika safari fulani na, baada ya kutokuwapo kwa wakati usiojulikana, anarudi nyumbani wakati wa saa isiyojulikana. Katika karne ya kwanza W.K. saa kamili haingeweza kuwekwa, kwa maana wakati huo wanadamu hawakuwa na vifaa vya kisasa kama simu, upashanaji wa habari kwa radio na njia za kusafiria haraka zenye orodha za wakati uliowekwa.
10. Ni gumu gani linalotokea juu ya urefu wa umri wa mwanamume ye yote Mkristo wakati wa kufika kwa “bwana” huyo?
10 Kulingana na maneno ya Yesu, huyo “msimamizi wa nyumba” aliwekwa juu ya baraza ya watumishi” kabla bwana yake hajaondoka kwenda katika safari. Basi, kwa kuwa bwana ya huyo msimamizi wa nyumba alifananisha Bwana Yesu Kristo, “msimamizi wa nyumba” wake aliwekwa kabla ya kuondoka kwake kwa kupaa kwake kurudi mbinguni siku 10 kabla ya sikukuu ya kiyahudi ya Pentekoste, mwaka 33 W.K. “Msimamizi wa nyumba” huyo angekuwa hai na mwaminifu kwa daraka lake alilopewa wakati wa kurudi kwa Bwana yake. Sasa imekuwa karne 19 tangu Bwana Yesu Kristo alipoondoka akaenda nyumbani mwa Babaye wa kimbinguni. Kwa hiyo, mtu ye yote akibisha kwamba huyo “msimamizi wa nyumba” kwa mfano anafananisha mwanamume mmoja Mkristo katika kundi la Kikristo la kweli, yeye angewezaje kuwa hai leo baada ya kuwekwa na Yesu Kristo mwaka wa 33 karne yetu ya kwanza W.K.? Hakuna mtu aliyepata kuishi muda mrefu hivyo, hata Methusela mwenye kujulikana sana.—Mwa. 5:27.
11. Kwa hiyo, mahali pa kufananisha mwanamume mmoja Mkristo, “msimamizi wa nyumba” huyo anafananisha nani, na Maandiko yanaungaje mkono maoni hayo?
11 Kufikiri, kukiwa kunaungwa mkono na mifano kama hiyo ya Kimaandiko, kunaonyesha wazi kwamba huyo “msimamizi wa nyumba” (oikonómos) anafananisha jamii, kikundi, sawa na baraza ya wanasheria, baraza inayotambuliwa na sheria kama vile shirika linalotambuliwa na sheria ya nchi. Kwa mfano, Yehova Mungu aliliita taifa zima la Israeli ya kale “mtumishi wangu ambaye nimemchagua.” (Isa. 43:10, NW) Kwa njia iyo hiyo, huyo “msimamizi wa nyumba” anafanaisha ile “kundi dogo” la Waisraeli wa kiroho, jamii yote ya wanafunzi waliojiweka wakf na kubatizwa wa “bwana,” Yesu Kristo, ambao wamezaliwa kwa roho ya Mungu wapate urithi wa kimbinguni pamoja na “bwana” yao, Yesu aliyetukuzwa. “Msimamizi wa nyumba” hiyo aliye jamii alikuwa hai na alikuwapo ili awekwe na Bwana aliyekuwa akiondoka, na mabaki ya jamii hiyo ya “msimamizi wa nyumba” wako duniani leo na wanajithibitisha kuwa waaminifu kwa Bwana Yesu Kristo. Kwa kuwa kila mshiriki ni mwaminifu na mwenye akili, jamii yote pia ni yenye uaminifu na akili.
12. Kusudi la kumweka “msimamizi wa nyumba’’ huyo juu ya “baraza ya watumishi” lilikuwa nini, na je! mambo ya hakika yanaonyesha kusudi hilo limetimizwa na jamii ya “msimamizi wa nyumba” huyo?
12 Katika mfano huo “msimamizi wa nyumba” huyo aliwekwa juu ya “baraza ya watumishi” wa bwana yake “ili aendelee kuwapa kipimo chao cha chakula kwa wakati unaofaa.” (Luka 12:42, NW) Kupitia hiyo jamii ya “msimamizi wa nyumba” yenye washiriki wengi kusudi hilo limetimizwa kufika wakati huu. Wakati wa karne ya kwanza W.K. ndivyo ilivyokuwa, wakati wa siku za wale mitume 12 wa Yesu Kristo kufikia kifo cha mtume wa mwisho aliyeendelea kuwapo, Yohana, ambaye aliandika sehemu yake ya mwisho ya Maandiko Matakatifu karibu mwaka 98 W.K. (Yohana 21:20-23) Sasa, wakati wa huu “umalizio wa mfumo wa mambo” ulioanza katika mwaka wenye msiba wa 1914, ndio ungekuwa “wakati unaofaa” hasa kwa ‘kipimo cha chakula’ kugawanywa kwa “baraza ya watumishi,” na ndivyo imekuwa. Mabaki ya jamii ya “msimamizi wa nyumba” wamejithibitisha kuwa ni wenye uaminfu katika habari hiyo.—Mt. 24:3-14, NW.
13. Bwana Yesu Kristo alirudi kwa kusudi gani linalohusu jamii hiyo ya “msimamizi wa nyumba,” na kufikia wakati huo jamii hiyo ilikuwa ikifanya nini?
13 Jambo hilo linapatana na uhakika wa kwamba Bwana Yesu Kristo aliingia kwenya uweza wa Ufalme pamoja na Babaye wa kimbinguni katika mwisho wa Majira ya Mataifa mwaka 1914 na kwa njia hiyo, hatimaye, akakipata kile alichoondoka akachukue. (Luka 19:12) Hivyo angeweza kurudi pasipo kuonekana akiwa na umbo la kiroho, na kwa kusudi la kutoza hesabu “msimamizi wa nyumba” wake. Mpaka wakati huo wa kutoza hesabu, kugawanya ‘kipimo cha chakula kwa wakati unaofaa’ hakukuwa kumekuwa kazi rahisi. Walakini washiriki wa jamii ya huyo “msimamizi wa nyumba” wamefanya kazi pamoja katika kugawa hicho “chakula” cha kiroho hatua kwa hatua kwa kadiri ambavyo Yehova Mungu amewaita wengine wawe warithi wa huo Ufalme, washiriki wa lile “kundi dogo.”
KUWEKWA “JUU YA VITU VYAKE VYOTE”
14. Kwa sababu gani ungekuwa wakati wa furaha kwa “msimamizi wa nyumba’’ huyo wakati bwana yake angerudi na kumkuta akifanya kazi yake kama mtumishi?
14 Katika mfano wake wa yule “msimamizi wa nyumba” mwaminifu na mwenye akili, Bwana Yesu Kristo, alimtaja kuwa “mtumwa” na akasema: “Mwenye furaha ni mtumwa huyo, iwapo bwana yake anaporudi atamkuta akifanya hivyo!” Kwa sababu gani? Yesu anasema: “Mimi nawaambia kikweli, Yeye atamweka juu ya vitu vyake vyote.”—Luka 12:43, 44, NW.
15. Kwa sababu gani kuwekwa kwa “msimamizi wa nyumba’’ huyo juu ya “vitu vyote’’ vya bwana wake lingekuwa jambo la kumfurahisha?
15 Hiyo inamaanisha kwamba “mtumwa” huyo anapewa daraka kubwa zaidi akiwa “msimamizi wa nyumba,” kama thawabu ya kujionyesha kuwa mwaminifu na mwenye akili na kwa kuendelea kukesha wakati wote akitazamia kurudi kwa bwana yake. Kwa sababu gani hivyo? Kwa sababu bwana huyo alikuwa amefaulu kupokea kitu fulani baada ya safari yake na alirudi akiwa na zaidi ya alivyokuwa navyo alipoondoka. “Vitu vyake” vilikuwa vimeongezwa, na hivyo kulikuwa vitu vingi zaidi ambavyo huyo “msimamizi wa nyumba” wake mwaminifu angewekwa juu yavyo. Kwa kuendelea kuwa katika cheo hicho cha “msimamizi wa nyumba” ingeonyesha kutumikia katika cheo kikubwa zaidi. Bwana yake mwenyewe alikuwa amerudi akiwa na cheo kikubwa zaidi ya kile alichokuwa nacho alipoondoka kwenda kwenye mgawo fulani wake. Katika utimizo wa kisasa wa mfano huo, jambo hilo limetimia kwa mabaki ya jamii ya “msimamizi wa nyumba” na Bwana yake, Yesu Kristo aliyetukuzwa.
16. Ni maneno gani ya Yesu, yaliyosemwa muda mfupi baada ya mfano huo yanayoonyesha kwamba yeye alikuwa akitoa mfano huo wa “msimamizi wa nyumba’’ katika wakati wa moto-moto?
16 Hata hivyo, tunawezaje kuthibitisha kwamba huu ndio umekuwa wakati unaofaa kwa mabaki ya jamii ya “msimamizi wa nyumba” kuwekwa juu ya “vitu” vilivyoongezeka, au faida, za Bwana huyo? Mistari kadha baada ya mfano huo, Yesu alisema hivi: “Nilikuja kuwasha moto duniani, na ningetaka nini zaidi ikiwa tayari umekwisha kuwashwa?” (Luka 12:49, NW) Maneno hayo ya mfano yalipatana na yale ambayo Yohana Mbatizaji alikuwa ametabiri juu ya Yesu miezi michache tu kabla Yesu hajaanza huduma yake ya kidunia. Kati ya mambo mengine Yohana alisema hivi: “Yeye atawabatiza kwa roho takatifu na kwa moto. Ambaye pepeto [la kutenganisha nafaka na makapi] lake li mkononi mwake, naye atausafisha sana uwanda wake; na kuikusanya ngano yake ghalani, bali makapi atayateketeza kwa moto usiozimika.”—Mt. 3:11, 12.
17. Ni nani wa siku za Yesu wangepitia katika hali yenye moto, na msiba gani ukiwa ndio upeo?
17 Maneno hayo ya kiunabii yanaonyesha kwamba mwisho wenye moto wenye kuteketeza wa mfumo wa mambo wa Kiyahudi ulikuwa umekaribia. Kama makapi, wale Wayahudi wasiokuwa Wakristo wangepatwa na mambo moto-moto. Haya yangemalizikia na uharibifu wa Yerusalemu na kutawanywa kwa Wayahudi kutoka Palestina waende ulimwenguni pote. Majeshi ya Roma yalitekeleza jambo hilo mwaka 70 W.K.
18, 19. (a) Katika unabii wa Yesu juu ya ile “ishara” ya “umalizio wa mfumo wa mambo,” ni mfano gani aliotoa unaolingana na mfano wa yule “msimamizi wa nyumba”? (b) Je! washiriki wa jamii hiyo walijithibitisha kuwa waaminifu na wenye akili wakati wa umalizio wa mfumo wa mambo wa Kiyahudi katika Palestina, na mabaki ya jamii hiyo wamekuwa wakifanyaje wakati wa huu “umalizio wa mfumo mambo”?
18 Miaka 37 kabla ya kuteketeza “makapi” ya mfano kwa “moto” usiozimika katika mwaka 70 W.K., Yesu Kristo alitoa unabii wake wenye kutoa “ishara” ya “umalizio wa mfumo wa mambo” wa moto-moto ulimwenguni pote pamoja na ishara ya “kuwapo” kwake kusikoonekana katika roho. Baadaye katikati ya unabii huo alitaja “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ambaye angekuwa akifanya kazi duniani wakati mfumo wa mambo wa ulimwengu ungekaribia mwisho wake. Maelezo ya Yesu juu ya “mtumwa” huyo yanafanana sana na yale yanayomhusu yule “msimamizi wa nyumba mwaminifu, wenye mwenye akili.” Kwa wazi yanahusu jamii ile ile, walakini neno “msimamizi wa nyumba” linataja wazi namna ya kazi ambayo “mtumwa” huyo anafanya.
19 Ona maelezo ya Yesu; “Ni nani basi yule mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambaye bwana wake alimweka juu ya nyumba yake, awape watu chakula kwa wakati wake? Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta akifanya hivyo. Amin, nawaambieni, atamweka juu ya vitu vyake vyote.” (Mt. 24:45-47) Washiriki wa jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” jamii ya “msimamizi wa nyumba,” walitumikia kwa jitihada mpaka mwisho wa mfumo wa mambo wa Kiyahudi katika mwaka 70 W.K. Mabaki ya washiriki wa jamii ya “mtumwa,” jamii ya yule “msimamizi wa nyumba,” wamekuwa wakijithibitisha wenyewe kuwa waaminifu na wenye akili wakati wa “umalizio wa mfumo wa mambo” wa kisasa tangu mwaka wa 1914 W.K.
20. Wale ambao wanajumuishwa kuwa mabaki wa jamii “msimamizi wa nyumba” leo wanatambulika sababu ya kujipatanisha na maneno gani ya Yesu kabla hajapaa kutoka Mlima wa Mizeituni kurudi mbinguni?
20 Mabaki ya jamii ya yule “msimamizi wa nyumba” yanatambulikana kwa urahisi leo, kwa maana yanapatana na yale ambayo Yesu, aliye Bwana, aliwaambia wale ambao wangejumuishwa kuwa sehemu ya kwanza ya ile jamii ya “msimamizi wa nyumba.” Kabla tu hajapaa kutoka Mlima wa Mizeituni arudi mbinguni, Yesu aliwaambia hivi: “Ninyi mtakuwa mashahidi wangu mimi katika Yerusalemu na katika Yudea yote na katika Samaria na kwenye sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” (Matendo 1:8, NW) Kwa kuwa mashahidi wa Bwana Yesu Kristo wanafunzi hao Wayahudi walipaswa kuwa wakati uo huo mashahidi wa Mungu wake na Baba, Yehova. Hawakuacha kamwe kuwa mashahidi wa Yehova!
21. Kwa kuzaliwa kwa asili wanafunzi hao Wayahudi walikuwa mashahidi wa nani, nao walikuwa washiriki wa awali (kwanza) wa “msimamizi wa nyumba” huyo mwenye washiriki wengi wakati gani?
21 Wanafunzi hao Wayahudi walipaswa kuwa mashahidi wa Yehova, kwa maana kwa kuzaliwa walikuwa wa taifa lile ambalo Mungu aliambia hivi babu zao: “‘Ninyi ni mashahidi wangu,’ ndio usemi wa Yehova, ‘hata mtumishi wangu ambaye nimemchagua, . . . Kwa hiyo ninyi ni mashahidi wangu,’ ndio usemi wa Yehova, ‘nami ni Mungu.’ “(Isa. 43:10-12, NW) Kwa hiyo, hao mashahidi wa Yehova wa Kiyahudi sasa wangekuwa mashahidi wa Mwanawe Yesu Kristo pia. Katika siku ya Pentekoste, siku 10 baada ya kupaa kwake kurudi mbinguni, walibatizwa kwa roho takatifu na kwa njia hiyo wakapewa uwezo na Bwana yao aliyetukuzwa Yesu Kristo juu ya “baraza ya watumishi” wake, ili wawape chakula cha kiroho. Hivyo ndivyo walivyokuwa washiriki wa kwanza au wa awali wa “msimamizi wa nyumba” mwenye washiriki wengi. Waliipa jamii hiyo mwanzo mzuri.
22. Jamii ya “msimamizi wa nyumba” ni kikundi cha pekee cha watu kwa ajili ya jina la nani, na uhakika huo ulikaziwaje katika mkutano wa pekee huko Yerusalemu wakati fulani baada ya mwaka 36 W.K.?
22 Jamii hiyo ya “msimamizi wa nyumba” ni kikundi cha watu kwa ajili ya jina la Yehova. Uhakika huo ulikaziwa wakati fulani baada ya mwaka 36 W.K., kwenye mkutano wa pekee wa mitume na wazee wa kundi la Yerusalemu. Huko Yakobo, ndugu wa mzazi mmoja wa Yesu Kristo, alisema hivi: “Simeoni [yaani, mtume Simoni Petro] ametueleza jinsi Mungu hapo kwanza alivyowaangalia Mataifa [Mataifa wasiotahiriwa] ili achague watu katika hao kwa ajili ya jina lake.”—Matendo 15:1-14.
23. Katika huu “umalizio wa mfumo wa mambo” mabaki ya jamii ya “msimamizi wa nyumba” hawawezi kuepa kuwa mashahidi wa nani na kuitwa kwa jina la nani?
23 Watu hao wasio Wayahudi walikuwa sehemu ya jamii ya “msimamizi wa nyumba” ya karne ya kwanza. Kwa sababu hiyo, jamii hiyo ilikuwa watu waliotiwa mafuta kwa ajili ya jina la Mungu, jina ambalo ni Yehova. Wao waliitwa kwa jina la Mungu, Yehova. Hawangeweza kuepa kuwa mashahidi wake. Lazima iwe hivyo vilevile kwa mabaki watiwa mafuta wa jamii hiyo ya “msimamizi wa nyumba” leo, wakati ambapo “ishara” inayoonekana tangu mwaka 1914 inaonyesha kwamba bwana aliyerudi wa jamii hiyo ya “msimamizi wa nyumba” yupo na kwamba “umalizio wa mfumo wa mambo” umekaribia kufikia upeo wake kwenye Har–Magedoni.—Mt. 24:3, NW.
Katika kurudia makala hii juu ya “Msimamizi wa Nyumba Mwaminifu,” ungeweza kujibuje maulizo haya?—
■ Ni nani “bwana” wa mfano wa Yesu wa “msimamizi wa nyumba mwaminifu”?
■ Ni nani yule “msimamizi wa nyumba mwaminifu”?
■ Ni nani aliye “baraza ya watumishi”?
■ Katika Waebrania 3:6, ni nini ile “nyumba” ambamo juu yake Kristo anawekwa?
■ Kwa sababu gani yule “msimamizi wa nyumba mwaminifu” hawezi kuwa mtu mmoja?
■ Je! “msimamizi wa nyumba mwaminifu” ni yule yule “mtumwa mwaminifu mwenye akili”?
■ Jamii ya “msimamizi wa nyumba mwaminifu” inaongoza katika utendaji gani ambao unafanya iwezekane kutambua jamii hiyo leo?
[Picha katika ukurasa wa 12]
‘‘Kisha Petro akasema: ‘Bwana, je! unatuambia sisi mfano huo au unawaambia wote pia?’ Na Bwana akasema: ‘Kwa kweli ni nani yule msimamizi wa nyumba mwaminifu, mwenye akili?’”—Luka 12:41, 42a, NW.