Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 6/1 kur. 6-10
  • Je! Inawezekana Kweli Kuwa na Mwenendo Safi Kuhusu Ngono?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Inawezekana Kweli Kuwa na Mwenendo Safi Kuhusu Ngono?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “MWENENDO WENYE KUCHUKIZA MNO WA ROMA”
  • ‘IKIWA MUNGU FULANI ANAFANYA HIVYO, MBONA MIMI NISIFANYE?’
  • “SOKO LA UASHERATI”
  • MWUJIZA WA KIADILI
  • ULE “MFANO” BORA
  • SHINDANO LA KILA SIKU
  • Vijana, Je! Mwenendo Safi Unaosemwa na Biblia Ndiyo Njia Bora?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Je! Ni Busara Kutofanya Ngono Kabla ya Kufunga Ndoa?
    Kupata Faida Zote za Ujana Wako
  • Ngono Kabla ya Ndoa
    Amkeni!—2013
  • Maoni Yako Juu ya Ngono—Yanafanyiza Tofauti Gani?
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 6/1 kur. 6-10

Je! Inawezekana Kweli Kuwa na Mwenendo Safi Kuhusu Ngono?

TUNAISHI ndani ya ulimwengu ambao umejaa sana ngono, na jambo hilo limekuwa na matokeo kwa vijana na wazee pia. Huenda ukaona kama mwanamume mmoja kijana, aliyesema hivi: “Kila kitu kutuzunguka kinakaza fikira kwenye ngono. Ni jambo la kawaida kama kupumua na kulala. Kila wakati unapochukua gazeti, au kufungua televisheni, unaiona. Unapokuwa dukani, unapoendesha motokaa, unapokuwa kazini, unapokuwa shuleni​—unaiona! Namna watu wanavyotenda, wanavyosema na namna wanavyovaa wakati wote ni mambo yenye kuvuta fikira kwenye mwili wa kibinadamu na ngono. Hicho ndicho kichwa cha mazungumzo namba moja.” Tarakimu za karibuni zinaonyesha kwamba, ulimwenguni pote, hesabu zisizopata kuonekana tena za matineja (vijana)—hata wale ambao hawajafikia utineja​—wanafanya ngono kabla ya ndoa.

UINGEREZA: “Ni msichana mmoja tu kati ya wasichana sita wanaomaliza miaka ya utineja ndiye angali bikira na mmoja kati ya wanne kwanza anafanya ngono kabla ya miaka 16,” ndivyo unavyoonyesha uchunguzi wa 1980.

KANADA: “Mweneo mkubwa wa mama matineja ambao hawajaolewa,” ndivyo ripoti ya serikali ya 1979 inavyosema.

AMERIKA: ‘Wanne kati ya wanaume vijana watano na wawili kati ya wanawake vijana watatu wamefanya ngono kufikia miaka 19,’ ndivyo uchunguzi mmoja wa 1981 unavyoonyesha.

JAPAN: Katika miji mingine ‘akina mama wasioolewa walioko kwenye miaka ya mwisho-mwisho ya utineja na miaka ya mwanzo-mwanzo ya 20 wamekuwa na ongezeko la mara 60 kati ya 1970 na 1979.’

UFARANSA: “Zaidi ya nusu ya wasichana wa shule wa Ufaransa wanadai wanafanya ngono kwa kawaida,” ndivyo uchunguzi wa 1980 unavyoonyesha.

“Kutungwa Mimba Wakati wa Utineja ni Tatizo Linaloongezeka la Ulimwengu,” ndivyo kichwa kikuu cha habari kinavyosema katika makala ya gazeti katika Brazil Herald. Makala hiyo ilionyesha maongezeko kama hayo katika Uingereza, Wales, Ujeremani ya Mashariki na Urusi. Asilimia 85 ya visa vyote vinavyoripotiwa vya magonjwa ya kisonono na kaswende vinahusu vijana. Maradhi hayo yamekuwa yenye kuambukia watu wengi ulimwenguni pote.

Hata hivyo si vijana wote wamefuata mtindo “Usafi wa adili unaharibu bure.” Wengi wameamua kwamba watangojea mpaka wakati wa ndoa kabla hawajafurahia ngono. Walakini si rahisi kwao kuendeleza usafi wao wa adili na ‘kujiepusha na uasherati,’ kama Biblia inavyoamuru. (1 Wathesalonike 4:3) Kwa kufaa huenda wao wakauliza hivi: ‘Je! kuna uwezo wo wote unaopatikana wa kumsaidia mtu akabili mtindo wenye kutisha wa kufanya ngono za ovyo-ovyo?

Ndiyo, upo. Ushuhuda wenye kutokeza wa uwezo huo ulionekana miaka 2,000 iliyopita wakati wa kipindi chenye kukosa sana adili kati ya vipindi vyote vilivyoandikwa katika historia.

“MWENENDO WENYE KUCHUKIZA MNO WA ROMA”

Mkuu wa kiserikali Seneka alikuwa shahidi aliyejionea mwenyewe hali katika ulimwengu wa Waroma wakati Ukristo ulipoanza. Yeye alikubali hivi: ‘Kila siku tamaa ya kufanya mabaya inakuwa kubwa zaidi. Uovu umekuwa na nguvu nyingi kushinda mioyo ya wote hata kwamba ukosefu wa hatia haupo kabisa.’ Juvenal, ambaye vilevile aliishi wakati wa kipindi hicho, anaandika juu ya “mwenendo wenye kuchukiza mno wa Roma.”

Wamekufa ganzi’ ndivyo mwandikaji mmoja wa Biblia alivyosimulia watu wa siku zake. (Waefeso 4:19) Ngono za ovyo-ovyo zilionwa kuwa jambo la kawaida. Mwanahistoria wa kale Lampridius alisema juu ya kipindi hicho kwamba ilikuwa lazima mtu asiyeoa awe na msichana ambaye angeweza kufanya ngono naye kwa ukawaida, “kwa sababu ilikuwa haiwezekani akae pasipo mmoja.” Walakini ni nini kilichotokeza mazoea hayo machafu?

‘IKIWA MUNGU FULANI ANAFANYA HIVYO, MBONA MIMI NISIFANYE?’

Miungu ya Waroma, ambayo kwa sehemu kubwa ilikuwa imeiga ile ya Wagiriki, ilionwa kuwa ndiyo violezo vya tabia. Walakini ilikuwa miovu kama nini! Venasi na Flora ilikuwa malaya isiyo na haya, Bakasi alikuwa mungu mlevi, Makyuri alikuwa mnyang’anyi wa barabarani na Apolo alikuwa mtongozi wa wanawake. Hata Jupita, aliyekuwa mungu mkuu na mwenye hekima zaidi ya miungu yote hiyo, yasemekana alikuwa amefanya uzinzi au zinaa ya maharimu (uasherati na watu wa ukoo mmoja) na wanawake 59!

Mifano hiyo ilikuwa na matokeo gani kwa watu? Mchezo mmoja wa kuigiza wa kipindi hicho unaonyesha mwanamume kijana akitafakari (akifikiria) kama anapaswa au hapaswi kufanya uasherati pamoja na mrembo (msichana) mmoja kijana. Kisha anaona picha ya Jupita akimtongoza mwanamke. Halafu anawaza hivi “Ikiwa mungu fulani anafanya hivyo, mbona mimi nisifanye, mimi niliye mwanadamu?” na “kwa hiyo nikaamua kuufanya.” Mchezo huo ulionyesha namna maisha ya kweli yalivyokuwa, kwa maana Seneka aliandika kwamba uasherati haukumfanya mtu aone aibu yo yote “alipoona miungu haikuwa bora zaidi yake.” Bila shaka wenye kutokeza mawazo hayo ya miungu walikuwa ‘wana wa Mungu’ wasioonekana kwa macho ya kibinadamu walioasi katika siku za Noa, wakaja duniani ili wafanye uasherati pamoja na binti za wanadamu. Ingawa wapotovu hao wa ngono walirudi kwenye makao ya roho, wameendelea kuujaza ujamii wa wanadamu roho ya ufisadi.​—Mwanzo 6:1-4; Yuda 6, 7.

“SOKO LA UASHERATI”

Mwandikaji wa karne ya pili Athenagorasi anadai kwamba wengine katika wakati huo walikuwa wameanzisha “soko la uasherati, na kuanzisha sehemu zenye kujulikana sana za vijana kwa ajili ya anasa mbovu za namna zote.” Ndani ya “soko” hilo “lililouza” hadharani ngono haramu, mlikuwa na jumba hilo la michezo ya kuigiza. Mazungumzo ya maonyesho yalikazia maisha ya upendo usiofaa wa miungu hiyo. Wenye kuigisha mara nyingi walivaa “mavazi yenye kubana sana mwili” ambayo yalionyesha uchi. Pamoja na hayo, kwenye kuta za nyumba na mahekalu, mara nyingi katika mahali pa waziwazi, kulikuwako michoro ya “uovu usioelezeka,” nyakati nyingine ikionyesha hata ngono. Sanamu za miungu miovu, ambayo mara nyingi ilionyeshwa ikiwa uchi, zilikuwa mahali pa waziwazi penye kuonekana hata na vijana. Vilevile, vijana walipata kwa urahisi vitabu vyenye matumizi ya lugha chafu zaidi na masimulizi machafu zaidi yaliyopata kuandikwa. Akili zilichafuliwa tangu uchanga na usomaji, au kwa kusomewa na wengine, vituko vya uasherati vya miungu ya kiume na ya kike.

Kuongezea hayo, kulikuwa bafu (viogeo) zenye kupendwa sana na watu wengi zilizotumiwa na watu wote, ambazo zilionwa kuwa “nyumba za umalaya zenye kupewa jina la heshima”; nyumba za michezo, ambamo vijana na wanaume wengi wazee-wazee walifanya mazoezi wakiwa uchi, na ambayo yakawa mapango ya ulawiti; na sikukuu, ambazo zilikuwa karamu za watu wote za uasherati na ulevi. Hali ilikuwa kama ile tu inayosimuliwa na barua ya mtume Paulo kwa Wakristo Waroma. Akitaja juu ya wale ‘waliosujudia kiumbe na kukiabudu badala ya Muumba’ na waliofuata adili zilizokuwapo wakati huo, yeye aliandika hivi: “Mungu aliwaacha wafuate tamaa zao [za ngono] za aibu, hata wanawake wakabadili matumizi ya asili kwa matumizi yasiyo ya asili, wakawakiana tamaa, wanaume wakayatenda yasiyopasa.” (Warumi 1:24-27) Masimulizi ya Paulo yalikuwa sahihi kabisa, kwa maana, upotovu wa adili za ulimwengu wa Wagiriki na Waroma ulitokeza mojalapo la mazoea yenye kuchukiza sana katika historia​—wanaume wazee kufanya ulawiti na wavulana. Zoea hilo chafu lilitukuzwa na mashairi na michezo ya kuigiza, na jamii yote iliambukiwa nalo.

Ikiwa ungaliishi wakati huo, na kila mahali ulipogeuka ukaona uchafu huo wa kiadili, ingalikuwa vigumu kama nini kuendelea kuwa safi. Ndiyo, kwa mwanamume kijana au mwanamke kijana kuendelea kuwa mwadilifu kwa kweli ingehitaji nguvu za adili na kushikamana na kanuni. Hata hivyo, katikati ya hayo yote, na kama kwamba kwa mwujiza wengine walionyesha uadilifu huo.

MWUJIZA WA KIADILI

Baada ya kutaja namna ya watu waovu waliojaa mji wa kale wa Korintho​—Waasherati, wazinzi, walawiti na wengine kama hao​—mtume Paulo, katika barua yake aliyoliandikia kundi la Kikristo lililokuwako huko, aliandika hivi: “Baadhi yenu mlikuwa watu wa namna hii; lakini mlioshwa.” (1 Wakorintho 6:9-11) Mafundisho ya Ukristo wa kweli yalikuwa yametoa nguvu za kiadili hata kwamba wenye kuufuata wakaweza kubadilika na kujiepusha na ufisadi.

“Pengine asili yenye kutokeza sana ya fundisho la Ukristo ilikuwa mkazo ule uliowekwa juu ya usafi wa adili,” ndivyo alivyomalizia William Sanger katika kitabu chake The History of Prostitution ambacho kinazungumza kwa urefu juu ya adili za kale. Yeye anaongeza hivi: “Tangu mwanzo, jamii za Kikristo zilijivunia kwa haki usafi wa adili zao.” Ni nini kilicholeta sifa hiyo? Kwa msaada wa Mungu waliweza kuiga “mfano” bora kuliko ule wa miungu yenye kuwashwa nyege.

ULE “MFANO” BORA

“Jivikeni utu mpya,” ndivyo Paulo alivyoshauri, “ambao kupitia maarifa sahihi unafanywa mpya kulingana na mfano wa Yeye aliyeuumba.” (Wakolosai 3:10, NW) Kupitia habari ya Maandiko yaliyoongozwa na Mungu na kwa mafundisho na mfano wa Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, Wakristo waliweza kupata “maarifa sahihi” ya sifa za Mungu wa kweli Yehova. “Mfano” wake ulikuwa tofauti kabisa na ule wa miungu ya Waroma.

Wakristo wa kweli walimwona Muumba wao kuwa Baba yao wa kimbinguni ambaye aliwapenda na kuwatunza. (1 Petro 5:6, 7) Walijifunza namna sikuzote alivyotenda kwa haki ya hukumu, haki na rehema Yeye alikuwa safi na mtakatifu. (Kumbukumbu la Torati 32:4; 1 Petro 1:15, 16) Wao walichochewa na sifa zake, na walijitahidi kufuata shauri hili lililoongozwa kwa roho: “Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa.” (Waefeso 5:1, NW) Kama ilivyoonyeshwa kupitia Kristo, walimwona Mungu kuwa rafiki aliyepo wakati wote. Wao wangeweza kumpenda. Roho ya upendo wa kweli ilijaza mioyo yao na ikawachochea wafanye kazi za Kikristo.

Mungu aliwasaidia Wakristo hao wa kwanza kupitia roho takatifu yake, ambayo iliwapa “uwezo unaopita ule wa kawaida.” Vilevile, kwenye mikutano yao ya kidini walikumbushwa juu ya uhitaji wa kuendelea kuwa safi kiadili. Kwa kushikamana karibu na washiriki wao ndani ya udugu wa Kikristo waliweza kuwa waaminifu. (2 Wakorintho 4:7, NW; Waebrania 10:24-26) “Sisi ambao hapo kwanza tulifurahia uasherati, sasa tunajitahidi kuwa safi,” ndivyo alivyosema Justin Martyr wa karne ya pili aliyedai kuwa Mkristo. Hata hivyo, kujitahidi hivyo kuwa safi kiadili hakukuwa rahisi.

SHINDANO LA KILA SIKU

Hatupaswi kusahau kwamba Wakristo wa kwanza walikuwa wakiishi katika ulimwengu uliopotoka adili. Wengine waliokuja kuwa Wakristo walikuwa wa “nyumbani mwa Kaisari.” (Wafilipi 4:22) Wakati huo, Nero ndiye aliyekuwa Kaisari, na maovu yake ya kiadili yanajulikana sana. Yeye alipanga kuwe tafrija zenye uchafu mwingi sana. Hata “alimwoa” kijana mwanamume “kwa kufuata desturi zote za ndoa ya kawaida.”a Hata hivyo wale wa “nyumbani mwake” waliokuwa Wakristo (pengine wakuu wa serikali au watumishi) waliendelea kuwa safi kiadili yajapokuwa mazingira hayo.

Wakristo katika Roma walikuwa wenye kukazwa sana na watu wa umri wao na walidhihakiwa. Kwa mfano, Seneka anaonyesha wazo la kawaida lililokuwapo anapoandika hivi: “Ye yote asiyefanya ngono anadharauliwa.” “Usafi wa adili ni uthibitisho wa kukosa uzuri tu.” Inaripotiwa kwamba wengine walilalamika hivi: ‘Ai, alikuwa mwanamke kama nini! Mwasherati lo!, mkware lo! Ai, alikuwa kijana kama nini! mpotovu lo!, mwenye tamaa lo! Sasa wamekuwa Wakristo​—ni sikitiko kama nini!’

Walakini wanafunzi hao wa kwanza hawakuwa wa kusikitikiwa. Wangeweza kuinua vichwa vyao juu kwa kujiheshimu. Walikuwa na dhamiri safi. Wakiwa “watoto wa nuru” walieneza ujumbe wao kwenye mapana na marefu bila kuona haya yo yote. (Waefeso 5:8) Je! hungaliona kuwa pendeleo kutambuliwa kuwa mmoja wa “miamba” hiyo yenye kufuata adili katika bahari hiyo yenye uchafu? Njia yao ya maisha yenye kutosheleza ilitofautiana sana na ile ya watu wa mataifa ‘ambao hawakumjua Mungu na wakafuatia tamaa yao nyingi ya ngono’ kwa hasara yao wenyewe.​—1 Wathesalonike 4:5, NW.

Kwa mfano, katika karne hiyo ya kwanza, maisha hayakuwa na kusudi kwa watu wengi. Walikuwa wamenywea kupita kiasi kikombe chenye kulevya cha anasa​—wakajaribu kila njia ya kujifurahisha. Hakuna cho chote chenye kuvutia, wala utamu wo wote uliobaki​—na vilevile hakukuwako uradhi wo wote. Kulingana na maandishi ya Juvenal, mlawiti mmoja, ambaye alipokuwa mzee-mzee alikataliwa na mpenzi wake, alilia hivi: “Sasa hatua bora yangu ni nini baada ya miaka yote hii iliyotumiwa vibaya na matumaini yaliyokatishwa? Nguvu nyingi za maisha zitanyauka haraka mno, maisha yetu ya taabu duniani yanakwisha: Tunapokunywa, tunapotikisa shada za maua na manukato na wasichana, uzee unatupata, pasipo kuonekana.” Hata hivyo, hakuna kukatishwa tamaa ko kote wala taabu iliyowapata wale Wakristo waaminifu.

Hata ingawa wafuasi wa kweli wa Yesu walipaswa kushindana kila siku ili waendelee kuwa safi kiadili, amani yao ya akili ilifanya jambo hilo listahili kufanywa. Kuepuka mazoea machafu ya kutumia viungo vya uzazi kuliwezekana.

Je! tunaona nguvu za adili kama hizo leo? Ndiyo. Vijana wengi wasiohesabika ulimwenguni pote watasema kwamba inawezekana kuwa mwadilifu. Hao ni vijana wanaoshirikiana na makundi ya Mashahidi wa Yehova. Ujapokuwa uvutano wenye kuharibu adili katika tafrija na maisha ya kirafiki ya jamii ya leo​—sawa na yale ya Roma ya kale​—vijana hawa, wakiwa kikundi, wako tofauti kabisa wakiwa mifano mizuri sana ya usafi

Hata hivyo vijana wengine wanaoshirikiana na makundi hayo ya Kikristo wana matatizo kuhusiana na jambo hilo. Hata wengine waliolelewa katika nyumba za Kikristo pindi kwa pindi wanaacha kuthamini adili za Biblia. Vijana Wakristo wanawezaje kuendeleza usafi ule ule wa adili ulioonekana wazi kabisa kati ya Wakristo wa kweli wa karne ya kwanza​—vijapokuwa vizuizi vikubwa sana? Wazazi wao wanaweza kuwasaidiaje? Makala mbili zifuatazo zimekusudiwa zitoe msaada unaofaa.​—Ona ukurasa 10.

[Maelezo ya Chini]

a Annals (Tarehe, IX, 37) cha mwanahistoria Mroma Takitasi.

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Tarakimu za karibuni zinaonyesha kwamba hesabu zisizopata kuonekana tena za vijana wanafanya uasherati

[Blabu katika ukurasa wa 9]

Ujapokuwa “Mwenendo wenye kuchukiza mno” wa Roma ya kale, Wakristo wa kwanza walikuwa kama miujiza ya usafi wa adili

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki