Maswali kutoka kwa Wasomaji
● Katika ule mfano wa “talanta,” ni nani wanaofananishwa na wale watumwa watatu?—Mathayo 25:14-30.
Kwa kuwa watumwa wote watatu wamo kati ya watu wa nyumba ya ‘bwana wao,’ wanasimamia wote wanaotazamiwa kuwa warithi wa ufalme kimbingu, wakiwa na uwezo wenye kutofautiana wa kufanya mambo na nafasi mbalimbali za kuongeza faida za Ufalme. Tangu Pentekoste 33 W.K. na kuendelea mpaka siku hizi, watumwa fulani waliotiwa mafuta wangekuwa na uwezo mkubwa zaidi, nguvu na nafasi nyingi zaidi za kuongeza “mali” za bwana wao alizowakabidhi wamtunzie. Mitume na wengine wenye mapendeleo makubwa zaidi ndio wangekuwa katika kila kikundi cha “talanta” tano. Kwa kuwalinganisha na hao, wengine wangeweza kufanya machache zaidi kwa sababu ya hali zao. Hata hivyo, wote walitakwa wawe wakijitoa na kufanya kazi kwa nafsi yote, na wote wangepokea thawabu ile ile moja.
Hata yule mtumwa aliyepewa “talanta” moja hakutangulia kuandikiwa kwamba angeshindwa kufaulu hata akijaribu namna gani, hapana. Kama yeye angaliongeza “talanta” ile moja ziwe mbili, inaelekea kwamba angalipokea thawabu ile ile ya ‘kuingia katika furaha ya bwana wake.’ Kwa sababu alikuwa ‘mlegevu’ na “mbaya,” anafananisha wale wenye kutazamiwa kuwa warithi wa Ufalme wanaogeuka na kuwa wasio waaminifu. Hao wanapoteza thawabu yo yote, zaidi ya kupoteza mapendeleo yao.
Washiriki wa Jumuiya ya Wakristo wanajisema kuwa ndio watumwa wa kweli wa Bwana, Yesu Kristo, lakini maneno na matendo yao yanawaonyesha kuwa hawastahili kuwa kati ya watu wa nyumba ya Bwana, hata kama wanadai sana kwamba wanastahili. Basi wao hawafai kuwa wanaotazamiwa kuwa warithi wa ufalme wa kimbingu.