Je! Biblia Inatabiri Mwisho wa Dunia?
MWISHO WA ULIMWENGU ni maneno matatu ambayo yametia woga mwingi ndani ya mioyo ya watu wengi katika karne zote za historia ya kibinadamu. Siku hizi maneno hayo hayana mkazo tena, kwa kuwa watu wanazidi kupunguza imani yao ya kidini. Lakini dini sizo peke yazo zinazotabiri kutakuwa na msiba mkubwa wa ulimwengu mzima. Wanasayansi wenye kujifunza mambo mbalimbali kuhusu wanadamu wanaonya kwamba kunaweza kutokea msiba mkubwa kwa jamii ya kibinadamu.
HOFU ZA WANASAYANSI
Wachunguzi wa miendo ya nyota wametaja matisho yasiyopungua manne yanayoelekea kumaliza uhai duniani. Chini ya kichwa cha habari chenye kusema “Maangamizi Manne Makubwa ya Kutoka Angani Yanayotisha Kuiharibu Dunia,” gazeti la Kifaransa la kisayansi Science et Vie liliyataja kuwa ni mlipuko wa nyota kubwa yenye kumeka-meka kwa nuru nyingi ajabu, moto mkubwa sana wenye kuwaka katika jua, kuanguka kwa nyota kubwa sana itakayokuwa ikimeta-meta iangukapo au kuingia kwa mfumo mzima wa sayari zinazoongozwa na jua katika mavumbi ya anga yatakayonyang’anya jua joto jingi sana mpaka dunia igandishwe na barafu.
Wakati ule ule, wenye kusomea elimu-viumbe na mazingira yavyo wanazidi kutoa onyo juu ya hatari za uchafuaji wa hewa, nchi na maji kwa matumizi mabaya ya vitu visivyo asili ya maumbile vinavyohatirisha afya na hata uhai wa wanadamu na wa wanyama. Ndiyo, uchafuaji unatia sumu katika hewa tunayopumua, katika ardhi na chakula kinachotoka humo, na katika bahari pamoja na samaki tunaowala.
Matisho hayo yanayoelekea kuharibu mazingira yakitenganishwa yafikiriwe moja baada ya jingine, itaonekana wazi kwamba hakuna moja peke yalo linaloweza kumaliza uhai duniani. Lakini yakijumlishwa pamoja, yanakuwa hatari yenye kuogofya. Katika mazungumzo ya kuhojiwa na gazeti la Paris L’Express linalotokea mara moja kwa juma, Maurice Strong, aliyekuwa katibu mkuu wa Mkutano Mkubwa wa Mazingira ya Ulimwengu, alisema yafuatayo hivi majuzi: “Mwanadamu akiendelea kushikilia nia hiyo ya kiburi kuelekea vitu vilivyoumbwa atatoweka mwishowe, ingawa sipendi kusema hivyo.”
Walakini, tisho linaloelekea zaidi sana kuharibu uhai duniani—lile ambalo limenenwa kuwa “Maangamizi Makubwa Sana ya Mwisho au Ufunuo wa Mwisho” na kuitwa “Armagedoni” kwa njia isiyofaa—ndilo linaloelekea zaidi sana kutokeza vita ya dunia nzima ya kutumia makombora ya nyukilia. Mataifa ya ulimwengu yaliyo na ulinzi wa kijeshi yamelundika sana silaha za nyukilia zenye uwezo wa kulipuka unaolingana na tani kadha za nuru ya TNT kwa kila mwanamume, mwanamke na mtoto aliyepo duniani. Si ajabu kwamba tisho la vita ya nyukilia linasemwa linaweza kuleta mwisho wa ulimwengu!
MAKANISA YANAFUNDISHA NINI?
Kwa mamia ya mamilioni ya Wakatoliki na Waprotestanti wengi maneno kama “Siku ya Maangamizi,” “Siku ya Hukumu” au “Mwisho wa ulimwengu” yanamaanisha siku ya mwisho ya watu kuagizwa wajibu kwa nini walitenda walivyotenda na ya uharibifu wa dunia. Chini ya kichwa cha habari yenye kusema “Mwisho wa Ulimwengu,” kitabu chenye kuaminika Dictionnaire de Theologie Catholique kinasema hivi: “Kanisa Katoliki huamini na kufundisha kwamba ulimwengu wa sasa, ukiwa kama Mungu alivyoufanya na ukiwa kama ulivyo sasa, hautadumu milele. Viumbe vyote vionekanavyo vilivyofanywa na Mungu muda wa vizazi vyote . . . vitaacha kuwa hai kisha vigeuzwe viwe uumbaji mpya.”
Makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yanafundisha kwamba mwishowe kabisa mwanadamu atakuwa ama na furaha kubwa ya milele katika mbingu au adhabu ya milele katika “hell” (wanaposema ni mahali pa moto wa mateso). Kulingana na maoni yao, dunia haikukusudiwa na Mungu iendelee kuwapo. Lakini wanachuo wa kidini wa Kikatoliki na Kiprotestanti wanajua wazi kwamba Biblia inasema ufalme wa Mungu uje ili mapenzi ya Mungu yatendwe ‘duniani kama mbinguni.’ (Mathayo 6:10) Wanajua kwamba hilo ni moja la mambo yaliyo ya maana zaidi ambayo Wakristo wanapaswa kuomba yatendeke. Wanaijua sana pia ahadi ya Biblia juu ya “dunia mpya” ambamo haki itakaa. (2 Petro 3:13, NW; Ufunuo 21:1-4) Lakini mafundisho ya Kikatoliki na Kiprotestanti juu ya maandiko hayo na mengine mengi yanayoitaja dunia katika kusudi la Mungu hayataji mambo waziwazi, na hata yanajaribu kuepuka kuyataja mambo hayo.
Kwa upande mwingine, wakiisha kusema kwamba watu wazuri wote watakwenda mbinguni na waovu waende “hell” (panapodhaniwa kuwa mahali pa moto wa mateso), wengi wa wanachuo wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wanafanya haraka-haraka kutumia maandiko kama linalosema “Mbingu na nchi zitapita” (Mathayo 24:35) ili ‘wathibitishe’ kwamba dunia itaharibiwa. Wanapenda sana kujiepusha wasifikirie hata kidogo kwamba wataishi duniani, nao hawataki kufundisha habari za dunia katika mafundisho yao. Wanapenda sana kuyatafsiri vibaya maneno “mwisho wa ulimwewengu” yanayopatikana katika tafsiri fulani-fulani za Biblia kuwa yanamaanisha mwisho wa dunia.—Mathayo 24:3.
MAONI YA BIBLIA
Basi, Biblia ina maana gani inaposema “mwisho wa ulimwengu”? Kwanza inafaa kuangaliwa kwamba maneno yanayotafsiriwa kuwa “mwisho wa ulimwengu” na tafsiri fulani-fulani yanatafsiriwa na nyingine kuwa “kufungika kwa kizazi” (Revised Standard Version, chapa zote mbili, ya Kiprotestanti na ya Kikatoliki,) “kumalizika kwa kizazi” (Marshall—The Interlinear Greek-English New Testament) au “umalizio wa taratibu ya mambo” (New World Translation). Maneno “kufungika,” “kumalizika” au “umalizio” ndizo tafsiri zenye kulenga maana zaidi za neno la Kigiriki synteʹleia, nalo ni tofauti na neno telos (linalomaanisha mwisho au mwisho kamili; linganisha Mathayo 24:6, 14). Vivyo hivyo, “kizazi” na “taratibu ya mambo” ndizo tafsiri sahihi zaidi za neno ai·onʹ, lililo tofauti na neno koʹsmos, ambalo kwa ujumla linamaanisha ulimwengu ambao ni wanadamu.
Jambo la kupendeza ni kwamba neno koʹsmos halipatikani hata mahali pamoja katika maandiko yaliyo na maneno ambayo nyakati nyingine hutafsiriwa vibaya kuwa “mwisho wa ulimwengu.” Kwa hiyo usemi huo haumaanishi mwisho wa jamii ya kibinadamu. Unamaanisha umalizio wa taratibu mbovu ya mambo, kufungika kwa kipindi kirefu cha wakati (ai·onʹ) chenye matendo mabaya ya “waandamu wasiomcha Mungu.”—Linganisha 2 Petro 3:7.
Mbali sana na kutabiri mwisho wa dunia, Biblia inatolea watu ahadi ya wakati ujao ulio mzuri sana kuhusiana na sayari yetu malidadi. Lakini lazima kwanza taratibu mbovu ya sasa iondolewe kabisa duniani. Basi mwisho wa taratibu hii ni jambo la kutumainiwa kwa matazamio mazuri, kama itakavyoonyesha makala inayofuata.