Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 6/15 kur. 5-7
  • “Mwisho wa Ulimwengu” Ni Tazamio Zuri

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Mwisho wa Ulimwengu” Ni Tazamio Zuri
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • SABABU GANI “ULIMWENGU” WA ZAMANI LAZIMA UPOTELEE MBALI
  • HOFU ZA WANASAYANSI HAZINA MSINGI
  • “DUNIA MPYA” YENYE HAKI—NAMNA GANI?
  • NAMNA YA KUOKOKA
  • Je, Dunia Itaharibiwa?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Mamilioni ya Walio Hai Sasa Hawatakufa Kamwe Wamalizike Katika Dunia Yetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Je, Dunia Itaharibiwa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2021
  • Kujihakikisha Tunastahili Kuingia Katika Taratibu Mpya ya Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 6/15 kur. 5-7

“Mwisho wa Ulimwengu” Ni Tazamio Zuri

“KUNA hatari za kiuchumi na za kiadili, vita, majaribio ya kuua watawala, kuteka wasafiri wa nchi za kigeni, mashindano ya kuunda silaha zaidi, maafa yanayotokana na njaa kali na kuwako kwa wakimbizi——kwa kweli jamii ya kibinadamu ni gonjwa sana. . . . Lakini hata ulimwengu fulani ukifikia mwisho si lazima iwe kwamba ulimwengu mzima umefikia mwisho.” Ndivyo lilivyosema gazeti la kila siku Le Monde la Paris chini ya kichwa cha maneno yenye kuuliza “Mwisho Unaotajwa na Ufunuo Ndio Huu?”

Kwa kujua au bila kujua, mwandikaji wa mistari hiyo aliyataja maoni ya Biblia. Maandiko yanaonyesha kwamba ulimwengu mmoja (ukiwa na maana ya “taratibu ya mambo”) unaweza kufikia mwisho bila ya ulimwengu mzima (ukiwa na maana ya dunia na wakaaji wayo wote) kuharibiwa. Zaidi ya hilo, kama tutakavyoona, hali zenyewe zilizotajwa na gazeti hilo la Kifaransa kuwa ushuhuda wenye kuonyesha kwamba “kwa kweli jamii ya kibinadamu ni gonjwa sana” zilitabiriwa katika Biblia kuwa sehemu ya ishara inayoonyesha sasa tunaishi kwenye “umalizio” wa “taratibu mbovu ya mambo” na kwamba tuko kwenye pambazuko la “kizazi” kingine kitakachokuwa na hali tofauti—-‘taratibu mpya ya mambo.’

SABABU GANI “ULIMWENGU” WA ZAMANI LAZIMA UPOTELEE MBALI

Maneno “mwisho wa ulimwengu” yanayoshtua watu kwa kuwatia baridi ya woga yametumiwa vibaya na wahubiri wa Jumuiya ya Wakristo kuogopesha watu ili waunge mkono makanisa yao. Kigiriki cha kwanza kabisa cha maneno hayo kina maana ya “umalizio wa taratibu ya mambo.” Kwa hiyo, huenda mtu akauliza: Kwa nini ni lazima taratibu ya sasa itoweke?

Sababu kubwa ni kwamba hilo ndilo kusudi la Mungu. Kwa nini? Kwa sababu tangu taratibu ya mambo ya sasa itokee muda mfupi baada ya gharika ya siku za Noa, imezidi kuwa mbaya. (Mwanzo 10:8-12; 11:1-9) Haikufanyizwa na Yehova Mungu. Bali, nyakati zote watumishi wa kweli wa Mungu wamenyanyaswa na hata wakateswa na “watawala wa hii taratibu ya mambo.” (1 Wakorintho 2:6, NW) Na hiyo si ajabu sana, kwa maana mtume Paulo anamwita Shetani “mungu wa hii taratibu ya mambo.” (2 Wakorintho 4:4, NW) Hata kama ni sababu moja tu ingechaguliwa ya kuiondolea mbali taratibu hii, sababu ya kwamba “watawala wa hii taratibu ya mambo” ndio ‘waliomtundika Bwana mwenye utukufu,’ Kristo Yesu, ingetosha kuistahilisha uharibifu.—1 Wakorintho 2:8, NW.

Mpango wa ulimwengu uliopo sasa umejionyesha wazi namna ulivyo kwa kuzidi kutenda dhambi nyingi, mabaya na uasi juu ya Mungu na mapenzi yake. Umekuza udhalimu, uonezi na jeuri—kati ya watu mmoja mmoja na kati ya mataifa. Biblia inauita “taratibu mbovu ya mambo iliyopo sasa.” (Wagalatia 1:4, NW) Hauwezi kubadilishwa uwe mzuri. Kwa hiyo, lazima upotelee mbali!

HOFU ZA WANASAYANSI HAZINA MSINGI

Lakini huo hautakuwa mwisho wa sayari-Dunia. Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, wanasayansi wamekuwa na hofu za kutokea kwa ‘maangamizi makubwa ya angani yanayotisha kuiharibu dunia.’ Walakini hofu hizo ni makisio tu ya mambo ambayo labda yanaweza kutokea, nao wenye kuwa nazo hawamfikirii mtu aliye wa maana zaidi katika ulimwengu mkubwa wa juu na chini: Mungu na kusudi lake kwa dunia.

Pierre-Paul Grasse, mshiriki wa Chuo cha Sayansi cha Kifaransa, anasema hivi:

“Utaratibu mzuri wa maumbile haukuvumbuliwa na akili ya mwanadamu wala haukuanzishwa na mtu fulani mwenye ufahamu mwingi. Bali, huo ni utaratibu uliothibitishwa kuwa mzuri sana na wanafisikia na wastadi wa hesabu kama kina Planck na Einstein. Kuwako kwa utaratibu mzuri kunaonyesha lazima kuwe na mtu fulani mwenye akili nyingi aliyetangulia kuwako ndipo utaratibu huo ukaweza kutokea. Mtu huyo mwenye akili nyingi hawezi kuwa ni mwingine isipokuwa Mungu.”

Ndiyo, wanasayansi wengi zaidi na zaidi wamekata kauli ya kwamba ni jambo la akili zaidi kukubali kuna Muumba mwenye akili nyingi badala ya kueleza namna ulimwengu mkubwa wa juu na chini ulivyotokea, wakisema ni kwa “bahati” tu.

Kwa kuwa Mungu yuko, sasa swali ndilo hili: Yeye anakusudia kuifanya nini dunia yetu? Neno lake, Biblia, linajibu hivi: “[Yehova], aliyeziumba mbingu, asema hivi; Yeye ni Mungu, ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu; Mimi ni [Yehova].” (Isaya 45:18) Yehova Mungu hakuiumba dunia akiwa na kusudi la kuja kuiharibu baadaye. (Zaburi 104:5) Kusudi la Mungu ni kwamba dunia “ikaliwe” na jamii yenye haki ya wanaume na wanawake waliojiweka wakf wafanye mapenzi yake. Ndiyo sababu Yesu aliwafunza Wakristo kusali hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe, ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.”—Mathayo 6:9, 10.

“DUNIA MPYA” YENYE HAKI—NAMNA GANI?

Kwa kuwa tumekwisha kuonyesha kwamba Yehova Mungu, “aliyeiumba dunia,” “aliyefanya imara,” ana kusudi lililo wazi sana kuhusiana na sayari tunamoishi, sasa lililobaki kufahamiwa nasi ni maana ya Biblia inapotaja “dunia mpya” ambamo “haki itakaa.”—2 Petro 3:13, NW.

Ni wazi kwamba “dunia mpya” iliyoahidiwa haiwezi kuwa inamaanisha sayari mpya. Inalomaanisha linaweza kufahamika kwa kutumia ufahamu mzuri kuyafikiria mambo yote yanayohusika katika barua ya pili ya Petro. Kutoa mfano mmoja wa mambo yatakayotukia karibuni kabla ya kuanzishwa kwa “dunia mpya,” Petro anaitaja gharika ya siku za Noa. Anataja ‘dunia [Kigiriki, ge] ikisimama imara nje ya maji na katikati ya maji kwa lile neno la Mungu; na kwa njia hizo ule ulimwengu [Kigiriki, koʹsmos] wa wakati huo ulipatwa na uharibifu wakati ulipogharikishwa kwa maji.’—2 Petro 3:5, 6, NW.

Ni “ulimwengu” gani ulioharibiwa na Gharika? Mapema katika barua iyo hiyo, Petro anaandika hivi: “Naye [Mungu] hakukosa kuadhibu ulimwengu [koʹsmos] wa kale, bali alimlinda Noa, mhubiri wa haki, salama pamoja na wengine saba wakati alipoleta gharika juu ya ulimwengu [koʹsmos] wa watu wasiomwogopa Mungu.” (2 Petro 2:5, NW) Kwa hiyo “ulimwengu wa watu wasiomcha Mungu” ulifikia mwisho kupitia Gharika. Lakini dunia na wanadamu wachache sana waliokuwa katika dunia yenyewe walibakia pamoja nayo.a Jamii mbovu ya wanadamu wasiomcha Mungu ndiyo iliyoharibiwa, wala si sayari-Dunia.

Vivyo hivyo, “Dunia” ya mfano, yenye kufananisha jamii ya wanadamu wapotovu ambayo imeongezeka tangu wakati wa Gharika ndiyo anayoitaja Petro anapoendelea kusema: “Kwa neno lile lile zile mbingu na dunia zilizopo sasa zimewekwa akiba kwa ajili ya moto nazo zimewekewa ile siku ya hukumu na ya kuharibiwa watu wasiomwogopa Mungu.” (2 Petro 3:7, NW) Ndiyo, kama vile Sayari-Dunia ilivyobaki isiangamie wakati wa mwisho wa “ulimwengu wa watu wasiomwogopa Mungu” uliokuwako kabla ya Gharika, ndivyo itakavyobaki isiangamizwe na “moto” au isiangamizwe wakati wa “kuharibiwa” kwa “watu wasiomwogopa Mungu” pamoja na serikali zao. Serikali hizo, na jamii mbovu ya kibinadamu zinazoitawala, ndizo “zile mbingu na dunia zilizopo sasa.”—Linganisha Ufunuo 21:8.

Petro anaongeza kusema: “Lakini ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo sisi tunangojea kulingana na ahadi yake [Mungu], na katika hizo haki itakaa.” Ni wazi kwa maneno hayo anamaanisha serikali mpya yenye haki (ufalme wa Mungu ukiwa chini ya Kristo) na jamii ya kibinadamu yenye tabia mpya.—2 Petro 3:13, NW.

NAMNA YA KUOKOKA

Ijapokuwa wanadamu wengi sana wenye kufikiria matukio ya wakati ujao wanatazamia mambo mabaya yanayowafanya waomboleze huhusu wakati ujao wa dunia na jamii ya kibinadamu, Wakristo wanaoiamini Biblia kweli kweli na kuifuata wana matazamio mazuri sana. Wao wanafahamu kwamba hatari ambazo zimetokea duniani kwa mshindo mkubwa tangu mwaka wa 1914 ni “ishara” ambayo Yesu aliwaambia wafuasi wake wawe macho kuiona. Yesu aliongeza kusema: “Basi mambo hayo yaanzapo kutokea, changamkeni, mkaviinue vichwa vyenu, kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia. . . . mwonapo mambo hayo yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu. Basi, kesheni ninyi kila wakati, mkiomba, ili mpate kuokoka katika hayo yote yatakayotokea.”—Luka 21:10, 11, 25, 26, 28, 31, 36; Mathayo 24:3, 7-13, NW.

Mashahidi wa Yehova si “manabii wenye kutangaza maangamizi tu,” bali wao kwa sasa wanazitangaza habari njema zipitazo habari nyingine zote, kwamba ufalme wa Mungu unakaribia kuchukua usimamizi wa dunia. Wao wanayatimiza maneno ya unabii wa Yesu: “Na habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho [telos] utakapokuja.” (Mathayo 24:14, NW) “Mwisho” huo utamaanisha uharibifu wa taratibu mbovu ya mambo ya sasa, mwisho wa udhalimu, uonezi, vita, njaa kali, magonjwa—ndiyo, mwisho wa kutaabika na wa kifo chenyewe!—Ufunuo 21:1-5.

Kwa kweli, “mwisho wa ulimwengu” si jambo la kuogopwa. Bali, ni jambo la kutumainia kwa tazamio zuri, kwa sababu utaleta upesi taratibu mpya ya mambo yenye haki juu ya dunia hii malidadi ambayo Mungu ‘ameikaza juu ya misingi yake, isiweze kutikiswa milele na milele.’—Zaburi 104:5, The Jerusalem Bible.

[Maelezo ya Chini]

a Ili upate uthibitisho wa kwamba kulikuwako na gharika ya dunia nzima, angalia sura ya 3 ya kitabu Is the Bible Really the Word, of God? (La Bible estelle Vraiment la Parole de Dieu?), kilichochapwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ufalme wa Mungu unakaribia kuanza kuitawala dunia

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki