Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 7/1 kur. 8-13
  • ‘Nuru Imemeta kwa Ajili Wenye Haki’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Nuru Imemeta kwa Ajili Wenye Haki’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MFANO WA IBRAHIMU
  • DANIELI NA MANABII WENGINE
  • YESU NA MITUME WAKE
  • MATAIFA YASIYO YA KIYAHUDI
  • Namna Yehova Anavyoongoza Watu Wake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • ‘Ee Mungu, Utume Nuru Yako’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Yehova Anafunua Kusudi Lake
    Ufalme wa Mungu Unatawala!
  • Kuongezeka kwa Nuru Katika Nyakati za Kisasa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 7/1 kur. 8-13

‘Nuru Imemeta kwa Ajili Wenye Haki’

“Nuru yenyewe imemeta kwa ajili ya mwenye haki, na shangwe ikawajia walio wanyofu katika moyo.”​—Zaburi 97:11, NW.

1. Ni kitu gani kimoja kinachotofautisha wenye haki na waovu?

NI KITU kipi kimoja kinachotofautisha wenye haki na waovu, watumishi wa kweli wa Yehova Mungu na wale walio katika utumwa wa adui ya Mungu, Shetani Ibilisi? Bila shaka zaidi ya jambo jingine lo lote ni uhakika wa kwamba wenye haki, watumishi wa kweli wa Yehova Mungu, wanafurahia nuru. “Nuru yenyewe imemeta” kwao kweli kweli. (Zaburi 97:11, NW) Kwa habari ya waovu, wanatembea gizani. Ndiyo, “njia ya wenye haki ni kama mng’ao wa kwanza wa mapambazuko, uking’aa zaidi na zaidi mpaka kuwe nuru kamili ya mchana. Walakini njia ya waovu ni kama giza jingi sana; hawajui ni nini kinachowakwaza.”​—Mithali 4:18 19, New International Version.

2. Kuongezeka kwa nuru kwenye njia ya wenye haki kunaweza kufananishwaje?

2 Angalia kwamba kung’aa kwa nuru kwenye njia ya wenye haki ni jambo linalotokea hatua kwa hatua. Inazidi ‘kung’aa zaidi na zaidi.’ Tunaweza kufananisha jambo hilo na mtu anayeamka kabla ya mapambazuko na kutembea kwa miguu kupitia sehemu za mashambani. Huenda akaona kwa utusitusi jengo likiwa mbali, lakini hapo kwanza hawezi kujua kama ni ghala au ni nyumba. Polepole kunapopambazuka na anapokaribia anaweza kuona kuwa ni nyumba. Baada ya muda mfupi anaweza kuona kuwa ni nyumba ya mbao, wala si ya mawe. Kisha, baadaye, anaweza kuona rangi ya nyumba hiyo, na kadhalika.

3. Ni mambo gani yanayohusika katika kuongezeka kwa nuru?

3 Hivyo ndivyo imekuwa kwa watumishi wa Mungu. Kwa kutazama mambo fulani kutoka umbali wa wakati na tukiwa na nuru ndogo tu juu ya habari hiyo, mara nyingi tumeyaona mambo kwa njia isiyo kamili na hata isiyo sahihi. Katika hali hizo huenda tukawa tuliongozwa na maoni tuliyotangulia kuwa nayo. Walakini kwa kadiri nuru inavyong’aa zaidi na tunapokaribia zaidi matukio, ndipo ufahamu wetu wa kutimizwa kwa makusudi ya Mungu unapokuwa wazi zaidi. Tunafahamu unabii mbalimbali kwa kadiri ambavyo roho takatifu ya Yehova inavyotoa nuru juu yake, unapotimizwa katika matukio ya ulimwengu au katika mambo yanayowapata watu wa Mungu. Je! si ndivyo Yehova Mungu ameshughulika na watumishi wake tangu nyakati za zamani? Hakika ndivyo imekuwa!

MFANO WA IBRAHIMU

4, 5. Mungu alimfunuliaje Ibrahimu kusudi lake polepole?

4 Mfikirie Ibrahimu, mwanamume wa imani ambaye Mungu alimwita rafiki yake. (Isaya 41:8; Yakobo 2:23) Ujapokuwa uhusiano wake wa karibu na Yehova Mungu, hapo kwanza hakufahamu kikamili makusudi ya Mungu. Tunaweza kuona jambo hilo kutokana na matukio mbalimbali katika maisha ya Ibrahimu—ufahamu wake ulikua polepole. Mungu alimwita atoke katika nchi yake ya nyumbani, akamwambia kwamba Yeye angemfanya awe taifa kubwa na kwamba kupitia kwake jamaa zote za dunia zingejibariki. Walakini Ibrahimu hakujua mambo yote kwa undani; tunasoma kwamba yeye alitii ingawa hakujua alikokuwa akienda.’ (Waebrania 11:8) Zaidi ya hayo, ingawa Mungu alimwahidi kwamba uzao wake ungepewa nchi hiyo, Ibrahimu hakujua namna jambo hilo lingekuwa hivyo. Hata alionyesha kuhangaika kwamba huenda mtumishi wake Eliezeri akarithi nyumba yake. Kisha Yehova alionyesha wazi namna mambo yalivyokuwa, kwa kumwambia Ibrahimu hivi: “Atakayetoka katika viuno vyako ndiye atakayekurithi.” (Mwanzo 12:1-3, 7; 15:2-4) Kwa kuwa mke wa Ibrahimu, Sara, alikuwa, tasa, yeye alimwuliza Ibrahimu afanye ngono na mjakazi wake, Hajiri, naye akamzaa Ishmaeli. Baadaye Mungu alimweleza Ibrahimu kwamba mrithi wa ahadi angetokea kupitia Sara.​—Mwanzo 17:15-17.

5 Kwa hiyo tunaweza kuona kwamba, ingawa kila jambo ambalo Yehova alimfunulia Ibrahimu moja kwa moja lilikuwa kweli, bado Ibrahimu hakufahamu kwa njia sahihi namna Mungu angetimiza kusudi lake. Hata hivyo, yeye aliendelea kuonyesha imani na kumngojea Yehova, na akafunuliwa mambo zaidi kwa kadiri wakati ulivyopita. Vivyo hivyo, wakati Yehova alipomwamuru amtoe mwanawe Isaka kama dhabihu juu ya Mlima Moria, Ibrahimu hakujua kwa ukamili namna jambo hilo lingetimizwa. Lakini yeye alikuwa na imani kwamba Mungu angetokeza uzao kupitia Isaka hata kama Mungu angelazimika kumfufua Isaka kutoka kwa wafu.​—Waebrania 11:17-19.

DANIELI NA MANABII WENGINE

6, 7. (a) Ni maneno gani ya Danieli yanayoonyesha kwamba Mungu anafunua mambo kwa wakati Wake mwenyewe tu? (b) Kuhusu jambo hilo mtume Petro anatoa ushahidi gani?

6 Kati ya manabii wengi ambao Yehova aliwapendelea kwa kuwapa ufunuo wa moja kwa moja alikuwapo Danieli, ‘mtu aliyependwa sana’ na Mungu. (Danieli 10:11, 19) Yehova alimpa habari yenye kutaja mambo waziwazi kuhusu wakati wake mwenyewe na nyakati za baadaye; hata hivyo Danieli hakufahamu mambo yote yaliyohusika. Kuhusu baadhi ya njozi alizoona, yeye alisema hivi: ‘Nilisikia, lakini sikuelewa.’ Alipouliza habari zaidi yeye aliambiwa hivi: “Enenda zako, Danieli; maana maneno haya yamefungwa, na kutiwa muhuri, hata wakati wa mwisho.” (Danieli 12:8, 9) Vivyo hivyo, Yehova Mungu aliendelea kuwafunulia watumishi wake manabii kweli nyingi. Hata hivyo kulikuwako mambo mengi ambayo hawakupata kuyafahamu.

7 Hiyo ndiyo sababu mtume Petro aliweza kuandika hivi: “Kuhusu wokovu wenyewe huo, uchunguzi wa makini na utafutaji wa uangalifu ulifanywa na manabii waliotabiri juu ya fadhili zisizostahilika zilizokusudiwa kwa ajili yenu. Waliendelea kupeleleza ili wajue ni majira gani hasa au ni majira ya namna gani ambayo ile roho iliyokuwa ndani yao ilikuwa ikionyesha kuhusu Kristo ilipokuwa ikishuhudia mapema juu ya mateso ya Kristo na juu ya matukufu yatakayofuata hayo. Ilifunuliwa kwao kwamba, si wao wenyewe, bali ninyi, ndinyi mliokuwa mkihudumiwa na wao mambo ambayo sasa mmekuwa mkitangaziwa.” Kwa kweli, hata malaika hawakuwa na ufahamu kamili juu ya namna makusudi ya Mungu yangetimizwa.​—1 Petro 1:10-12, NW.

8. Ulizo la Yohana Mbatizaji lilionyeshaje kwamba ufahamu wake haukuwa kamili?

8 Wa mwisho kati ya manabii hao alikuwa Yohana Mbatizaji. Mungu alimtumia atayarishe njia mbele ya Kristo Yesu. (Luka 1:16, 17; 2:76-79) Yohana alipendelewa sana kupokea kutoka kwa Mungu ishara iliyomtambulisha Masihi, na katika kumjulisha kwa Israeli. (Yohana 1:26-36) Hata hivyo, Yohana hakufahamu wazi mambo yote yaliyohusu kuja kwa kwanza kwa Yesu. Jambo hilo linaonyeshwa na uhakika wa kwamba wakati Yohana alipokuwa gerezani aliwapeleka wanafunzi wake kwa Yesu wakiwa na ulizo hili: “Wewe ndiwe yule ajaye, au tumtazamie mwingine?” Ulizo la Yohana halikuwa wonyesho wa kukosa imani bali lilikuwa wonyesho wa tamaa ya kutaka kupewa uthibitisho fulani. Bila shaka Yohana alifarijiwa na jibu la Yesu ambalo lilielekeza kwenye kazi zake.​—Mathayo 11:2-6.

YESU NA MITUME WAKE

9. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu hakufahamu kikamilifu makusudi ya Babaye?

9 Mungu anafunulia watumishi wake mapenzi yake kwa wakati wake mwenyewe tu, na jambo hilo lilimhusu hata Yesu Kristo. Bila shaka Yesu alipokea habari za moja kwa moja alipokuwa na Babaye mbinguni. Hata hivyo yeye mwenyewe hakujua ni wakati gani mwisho ungekuja wa taratibu ya mambo yetu iliyopo. Ndiyo sababu yeye alikiri hivi: “Walakini habari ya siku ile na saa ile hakuna aijuaye, hata malaika walio mbinguni, wala Mwana, ila Baba peke yake.”​—Mathayo 24:36.

10, 11. (a) Ni kauli gani yenye makosa ambayo wanafunzi wa Yesu walikata kuhusu Ufalme huo? (b) Kwa sababu gani Yesu aliwaambia wanafunzi wake mambo machache tu juu ya wakati ujao na juu ya mambo mengine?

10 Yesu mwenyewe alitenda kulingana na kanuni inayotajwa katika Mithali 4:18 katika kushughulika na wanafunzi wake. Yeye aliwaambia mengi juu ya Ufalme huo: kwamba yeye angeenda zake na kwamba angerudi baada ya muda mrefu na kuwapeleka nyumbani pamoja naye katika mbingu. Hata hivyo, yajapokuwa hayo yote, mitume wake walishikilia wazo la kwamba ufalme wa Kimasihi ungerudishwa uwe ufalme wa Daudi katika Yerusalemu. Hiyo ndiyo sababu walimwuliza hivi Yesu aliyefufuliwa: “Bwana, unarudishia Israeli ufalme wakati huu?” Yesu aliwaambia kwamba kulikuwako mambo ambayo hawangeweza kufahamu wakati huo, kwa kusema hivi: “Si shauri lenu kupata kujua nyakati au majira ambayo Baba ameweka katika mamlaka yake mwenyewe.”​—Matendo 1:6, 7, NW.

11 Maneno ambayo Yesu aliwaambia mitume wake yanaonyesha kuna wakati unaofaa wa kupata ufahamu juu ya mambo fulani ya makusudi ya Mungu: “Bado nikali ninayo mengi ya kuwaambia, lakini hamwezi kuyastahimili hivi sasa.” (Yohana 16:12) Jambo hilo linaonyesha kwamba Mungu anawapa watumishi wake ufahamu wa mapenzi yake kwa kulingana na uwezo wao wa kuelewa na kutumia ufahamu huo. Ni kweli kwamba Yesu aliwaambia mitume wake kwamba roho ya Mungu ingewaongoza “kwenye kweli yote.” (Yohana 16:13) Walakini je! Yesu alimaanisha kwamba tangu siku ile walipopokea roho takatifu wangefahamu kweli yote, wasihitaji kupata ufahamu zaidi baadaye? Mambo ya hakika yanaonyesha kwamba hivyo sivyo ilivyokuwa.

MATAIFA YASIYO YA KIYAHUDI

12, 13. (a) Wafuasi wa Yesu walipata kuthamini nini kwa wazi zaidi katika Pentekoste, na jambo hilo lilikuwa na matokeo gani juu yao? (b) Ingawa Yesu alikuwa amewapa mgawo wa kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, ni wakati gani kwa mara ya kwanza walipoanza kufanya hivyo, na kwa sababu gani wakati huo ndio uliokuwa wa kwanza?

12 Katika siku ya Pentekoste mwaka 33 W.K. wanafunzi hao walipokea roho takatifu pamoja na kuthamini kweli kwa njia iliyo wazi zaidi kuhusu kufufuliwa kwa Yesu, kupaa kwake kwenda mbinguni na maana ya ufalme wa Mungu. Maarifa hayo yaliwatia juhudi ya kuwaambia wengine “habari njema.” Hata ingawa Yesu alikuwa amesema walipaswa kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, hapo mwanzo walihubiri kati ya Wayahudi, waongofu wasio Wayahudi na kisha, baada ya muda, kwa Wasamaria. Hawakufahamu kwamba walipaswa kuwaendea Mataifa wasiotahiriwa. (Mathayo 28:19, 20, NW) Bila shaka Yehova hakutoa ufahamu huo, kwa sababu unabii wa Danieli ulikuwa umesema kwamba Masihi angeweka agano pamoja na Wayahudi mpaka mwisho wa juma la 70.​—Danieli 9:24-27.

13 Wakati “juma” hilo lilipokwisha katika mwaka 36 W.K., Yehova Mungu alitenda kwa kufaa kwa kufungua “habari njema” kwa watu wa mataifa. Petro alihitaji msaada kweli kweli ili arekebishe fikira zake kabla ya kuingia katika nyumba ya Mtaifa asiyetahiriwa ambaye kulingana na Sheria alikuwa mchafu. Alipaswa kuagizwa alipokuwa akiona namna ya njozi: “Vitu Mungu alivyotakasa, wewe usiviite vichafu.” Kwa hiyo Petro na wale mitume wengine walipaswa kubadili maoni yao juu ya jambo hilo. Petro alifanya hivyo na alitumiwa na Mungu kuwatangazia Mataifa kwamba njia inayoelekeza kwenye ufalme wa Mungu wa kimbinguni ilikuwa imefunguliwa.​—Matendo 10:9-43, ZSB.

14. Miaka mingi baadaye Wakristo wa kwanza walipokea nuru gani kuhusu matakwa ya torati ya Musa?

14 Hata hivyo, miaka 13, baadaye, tohara ilikuwa inabishaniwa na Wakristo fulani. Ilikuwa lazima kwa Paulo na wanafunzi wengine waende Yerusalemu ili wazungumze jambo hilo pamoja na mitume na wazee wengine, ambao wakati huo walikuwa washiriki wa baraza inayoongoza ya makundi ya Kikristo. Baraza hiyo ilisikiliza aliyosema Petro juu ya kuongolewa kwa Kornelio, na ushuhuda wa Paulo juu ya matendo makuu ambayo Mungu alikuwa ametenda kuhusiana na huduma ya Paulo kwa Mataifa. Kisha wakatafakari yale ambayo Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho lilikuwa linasema juu ya jambo hilo. Kwa msaada wa roho takatifu walikata maneno inavyofaa, yaani, kwamba ingawa kanuni fulani za mwenendo zilitakiwa, haikuwa lazima Mataifa watahiriwe na kufuata torati ya Musa ili wawe Wakristo.​—Matendo 15:1–16:5.

15, 16. (a) Ni maneno gani ya Paulo yanayoonyesha kwamba yeye alitambua kweli inafunuliwa hatua kwa hatua? (b) Mtume Petro alitoa ushuhuda gani kama huo?

15 Miaka sita hivi baada ya mkutano huo, Paulo aliandika barua yake ya kwanza kwa Wakorintho, ambayo katika hiyo alisema hivi juu ya Wakristo waliozaliwa kwa roho wakati wake: “Kwa maana tunafahamu kwa sehemu; na tunafanya unabii kwa sehemu; lakini ijapo ile iliyo kamili, iliyo kwa sehemu itabatilika. Maana wakati wa sasa tunaona kwa kioo kwa jinsi ya fumbo; wakati ule tutaona uso kwa uso; wakati wa sasa nafahamu kwa sehemu; wakati ule nitajua sana kama mimi nami ninavyojuliwa sana.” Kwa hiyo hata kufikia wakati huo Wakristo waliozaliwa kwa roho, kutia mtume Paulo mwenyewe, walikuwa bado hawajaongozwa na roho takatifu kwenye maarifa kamili ya kweli yote. Maarifa yao yalikuwa yangali ya sehemu tu, kwa kadiri ambayo Mungu alikuwa amewapa ufahamu kufikia wakati huo. Walakini yalitosha mahitaji waliyokuwa nayo wakati huo.​—1 Wakorintho 13:9, 10, 12.

16 Miaka tisa baada ya Paulo kuandika mambo hayo yaliyotangulia, au karibu mwaka 64 W.K., Petro aliwaandikia nini Wakristo wenzake? Baada ya kuzungumza juu ya kubadilika sura ambako kulithibitisha Yesu kuwa Mwana wa Mungu, yeye aliendelea kusema hivi: “Kwa hiyo sisi tunalo neno la unabii lililohakikishwa zaidi; nanyi mnafanya vizuri katika kuliangalia kama taa inayong’aa mahali penye giza, mpaka siku itakapopambazuka na nyota ya asubuhi izuke, ndani ya mioyo yenu.” (2 Petro 1:16-21, NW) Kwa hiyo bado Wakristo walihitaji kuyachunguza Maandiko, na kukaza fikira kwenye neno la kiunabii, ambalo lingekuwa kama taa inayong’aa mahali penye giza. Lazima waendelee kufanya hivyo mpaka wakati mabaki Wakristo watakapopokea zawadi yao kwenye ufunuo mtukufu wa Yesu Kristo.

17. (a) Kitabu cha Ufunuo kilipotolewa, ni kweli gani mpya walizopata kujua Wakristo? (b) Nuru zaidi ingeng’aa juu ya kitabu hicho wakati gani?

17 Miaka 32 baada ya Petro kuandika barua yake ya pili, au miaka 63 baada ya Pentekoste mwaka 33 W.K., mtume Yohana alipokea njozi na akaandika mfululizo wa njozi unaofanyiza kitabu cha Ufunuo. Katika njozi hizo hesabu fulani za kweli kuhusu makusudi ya Mungu zilifunuliwa kwa Wakristo waliozaliwa kwa roho kwa mara ya kwanza. Kwa mfano, kwa njia hiyo walipata kujua kwamba wanaume na wanawake 144,000 wangekombolewa kutoka kwa mataifa yote wawe warithi washirika pamoja na Yesu Kristo mbinguni na wangetawala wakiwa wafalme, makuhani na mahakimu katika ufalme wa Kimasihi wa urefu wa miaka 1,000. (Ufunuo, sura 7, 14 na 20) Hata hivyo Wakristo wa wakati huo wa mapema hawakuwa na maarifa kamili. Wanafunzi wa Neno la Mungu leo wanaweza kuona kwamba njozi za Ufunuo, ingawa huenda zikawa ziliwafundisha na kuwatia moyo Wakristo wa siku za Yohana, ni zenye thamani ya pekee kwa wale wanaoishi katika “siku ya Bwana,” ambayo tumo ndani yayo sasa. (Ufunuo 1:10) Kwa hiyo Ufunuo 5:1-14 kwa njia ya mfano unasimulia kitabu fulani cha kukunja, chenye muhuri mbalimbali iliyopasa kufunguliwa ili kitabu hicho cha kukunja kifunguliwe. Hiyo inaonyesha kwamba wakati wa kutimizwa kwa unabii mbalimbali wa Ufunuo lazima pawepo kufunuliwa kwa hatua kwa hatua kwa maarifa na ufahamu kwa kadiri kila muhuri ulivyofunguliwa kwa wakati wake.

18. Basi, ni kwa njia gani Yehova Mungu aliwafunulia kweli watumishi wake katika nyakati za kale na katika karne ya kwanza?

18 Kwa hiyo tunaweza kuona kwamba, kwa habari ya watumishi waaminifu wa Yehova katika nyakati zilizotangulia Ukristo na kundi la Wakristo watiwa mafuta la karne ya kwanza Wakati wa Kawaida wetu, wote hawakuwa na maarifa na ufahamu kamili. Iliwapasa waendelee kufanya maendeleo, wakirekebisha ufahamu wao kwa kadiri walivyotambua na kuona kutimizwa kwa hatua kwa hatua kwa makusudi ya Yehova. Kwao, njia ya mwenye haki kweli kweli imekuwa kama “Nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa.” (Mithali 4:18) Nuru ilipoongezeka, maarifa yao yaliongezeka, wakafahamu kikamilifu zaidi kweli bora sana ambazo Yehova aliendelea kuwafunulia.

19. Mungu alimwambia nini nabii Danieli kuhusu maarifa na ufahamu katika “wakati wa mwisho’?

19 Walakini namna gani juu ya watumishi wa Yehova katika wakati wa mwisho? Malaika mmoja alikuwa amemwambia Danieli hivi: “Wewe, Ee Danieli, yafunge maneno haya, ukakitie muhuri kitabu, hata wakati wa mwisho; wengi wataenda mbio huko na huko [katika Neno la Mungu], na [kwa sababu hiyo] maarifa [ya kweli] yataongezeka.” (Danieli 12:4) Katika mstari wa 10, inasemwa hivi zaidi juu ya watumishi wa Mungu: “Wengi watajitakasa, na kujifanya weupe, na kusafika; bali wabaya watatenda mabaya; wala hataelewa mtu mbaya awaye yote; bali wao walio na hekima ndio watakaoelewa.” Je! huko kufunuliwa mambo kungekuja wakati ule ule mmoja? Ili watambuliwe kuwa “walio na hekima” je! ingehitaji watumishi wa Mungu wawe na maarifa na ufahamu kamili wenye maelezo ya kina kirefu hata wasihitaji kufanya marekebisho yo yote au mabadiliko, baada ya muda fulani, kuhusu maoni yao ya mafundisho au mambo mengine? Maulizo hayo na mengine yatazungumzwa katika makala zinazofuata.

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

Jinsi Yehova alivyoshughulika na watumishi wake katika nyakati zilizopita inaonyesha kwamba kufahamu makusudi yake mara nyingi kunakuja polepole.

Ibrahimu hakujua kabisa jinsi ahadi ya Mungu kuhusu “uzao” ingetimizwa.

Danieli hakufahamu matokeo ya mwisho ya unabii wake mbalimbali.

Yohana Mbatizaji, ambaye alimtayarishia njia Masihi, baadaye aliuliza ajulishwe kama mwingine alikuwa anakuja.

Yesu mwenyewe hakujua siku wala saa ya ile “dhiki kubwa.”

Mitume walipaswa kujifunza hatua kwa hatua kwamba ufalme huo ni wa kimbinguni na kwamba Mataifa, pia, wangeweza kuurithi.

Ni baada tu ya kupokea kitabu cha Ufunuo ndipo Wakristo wa kwanza walipojua kwamba utawala wa Kristo ungekuwa na urefu wa miaka 1,000 na kwamba angekuwa na warithi washirika 144,000.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Wakati wa matembezi ya mapema asubuhi vitu vinaonekana wazi zaidi mtu anapovikaribia zaidi na giza linapogeuka polepole na kuwa nuru

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki