Kuongezeka kwa Nuru Katika Nyakati za Kisasa
“Njia ya wenye haki ni kama nuru ile nyangavu inayong’aa zaidi na zaidi mpaka mchana unapokamilika kabisa.”—Mithali 4:18, NW.
1. Tumekwisha kuchunguza ushuhuda gani juu ya utimizo wa Mithali 4:18?
MAANDISHI ya Biblia kutoka Mwanzo mpaka Ufunuo yanaonyesha kwamba njia ya watumishi wa Yehova imekuwa kweli kweli kama nuru nyangavu inayong’aa zaidi na zaidi wakati wote. (Mithali 4:18, NW) Katika siku za Yesu na mitume wake unabii mwingi uliohusu Masihi ulifahamika, kama Mathayo na waandikaji wengine wa vitabu vya Injili walivyothibitisha. Na kumiminwa kwa roho ya Mungu katika Pentekoste na Mataifa kupelekewa “habari njema” kuliambatana na ufahamu zaidi juu ya Neno la Mungu.—Matendo 2:14-36; 10:34-43; 15:6-21.
2. (a) Ni kwa sababu gani kukawa kipindi cha giza juu ya wafuasi wa kujidai wa Yesu Kristo? (b) Ni kitu gani kilichotimiza sehemu kubwa katika kazi ya mavuno ya kutenganisha?
2 Hata hivyo, baada ya mitume kufa kipindi cha giza kiliwameza polepole wafuasi wa kujidai wa Yesu Kristo. “Mbwa-mwitu wakali” walichukua uongozi. (Matendo 20:29, 30) Ikawa kama Yesu alivyotabiri katika mfano wake mmoja. Yeye alifananisha ufalme wa mbingu na “mtu aliyepanda mbegu njema katika shamba lake.” Kisha ‘adui akaja naye akarudia kupanda magugu katikati ya ile ngano.’ Kwa sababu hiyo, magugu yakakua zaidi katika shamba hilo la ulimwenguni pote la kidini, kwa karne nyingi sana. Walakini wakati wa mavuno unapofika kunakuwako kutenganisha. Wakati wa mavuno umetufikia sasa, kwa maana “mavuno ni umalizio wa taratibu ya mambo.” Kwa furaha, jamii ya “ngano” ya Wakristo wa kweli imekusanywa. Mambo ya hakika yanaonyesha kwamba nuru yenye kuongezeka wakati wote kwenye njia ya Wakristo hao inatimiza sehemu kubwa katika kuwatenganisha na “magugu” wenye kuvunja sheria, ambao mwisho wao ni uharibifu.—Mathayo 13:24-30, 36-43, NW.a
NURU JUU YA YEHOVA MUNGU NA NENO LAKE
3, 4. Ni mambo gani ya hakika kuhusu Muumba, Yehova Mungu, ambayo Wanafunzi wa Biblia wa kwanza walijifunza kuthamini?
3 Katika miaka ya mwanzo-mwanzo ya 1870 kikundi fulani cha wanafunzi wa Biblia chenye bidii na chenye nia ya kufahamu ukweli wa mambo kilianza kukusanyika ili kijifunze Neno la Mungu kama lilivyo kabisa. Mahali pa kufuata imani za Jumuiya ya Wakristo, walifuata Maandiko yaliyoandikwa kwa uongozi roho ya Mungu yawe mwongozo wao. Hekima, kiasi, upatano na uweza wa ujumbe wa Biblia, hayo yote yaling’aa mioyoni mwao. Iliwasadikisha juu ya ukweli ulio wazi kwamba kweli kweli kuna Muumba mwenye akili, tofauti na mafundisho yaliyokuwapo ya kutokusadiki kuwapo kwa Mungu na mageuzi ya viumbe. Wao walifahamu kwamba “lazima matokeo yatokezwe na visababishaji vyenye akili” na kwamba wingi mkubwa sana wa uumbaji, uzuri wa sura za viumbe, upendezi wavyo, utaratibu, upatano, namna nyingi za vitu vilivyoumbwa” vinamshuhudia kuwa ndiye Muumba mkuu.b (Warumi 1:20) Vilevile walipata wazo lililo wazi la utu wa Muumba, kwamba ana sifa nne za msingi, yaani, hekima isiyo na kikomo, uwezo mwingi mno, haki ya hukumu kamilifu na upendo usiolinganika.—Kumbukumbu 32:4; Zaburi 62:11; Mithali 2:6, 7; 1 Yohana 4:8.
4 Pamoja na hayo, walijifunza kuthamini kwamba Mungu ni wa “milele hata milele” na kwamba jina lake ni Yehova. (Zaburi 83:18; 90:2) Walipata kufahamu kwamba fundisho kuu la Jumuiya ya Wakristo—lile fundisho la kidini la Utatu wa Miungu—ni la upumbavu tena si la Kimaandiko. Nuru ya kweli ya Biblia iliwaonyesha kwamba Mungu ni “Yehova mmoja,” kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu (ushahidi wake mwenyewe unathibitisha kwamba Babaye ‘ni mkuu kuliko yeye’) na kwamba roho takatifu ya Mungu, tofauti kabisa na kuwa mtu (nafsi) wa tatu wa ule Utatu wa Miungu, ni ‘nishati ya Mungu anayoitumia kutimiza mambo mbalimbali.’c—Marko 12:29, NW; Yohana 14:28; Matendo 2:17, 18.
5. Wapenda kweli hao walichukua msimamo gani kuhusu Biblia?
5 Kwa ujasiri na kusadikishwa walihubiri kwamba Biblia ni Neno lililoandikwa kwa uongozi wa Mungu; kwamba kwa sababu ya sifa za Mungu ni jambo la akili kutazamia Muumba atoe ufunuo wa kimungu kwa uongozi wa wanadamu. Walieleza Biblia kuwa “kiangaza cha ustaarabu na uhuru.” Ndiyo “kitabu cha kale zaidi kilichopo; imeendelea kuwapo baada ya msukosuko wa karne 30.” Zaidi ya hayo, “vitabu vingine vyote vikiunganishwa pamoja vimeshindwa kuleta furaha amani na baraka kwa viumbe wenye kuugua lakini Biblia ikaweza.”d Wanafunzi hao wanyofu waliona uthibitisho ulio wazi kutokana na maisha yasiyo na choyo na ya kujinyima ya waandikaji wa Biblia kwamba makusudi yao yalikuwa safi. Kwa ujumla, walipata kuona kwamba ‘Biblia ina maelezo ya akili na yenye upatano ya visababishaji vya uovu, na kwamba inaeleza juu ya utatuzi na matokeo ya mwisho; na inatumika kuongoza na kutia nguvu watumishi wa Yehova Mungu.’
YESU KRISTO NA ULE UFALME
6. Wanafunzi wa Biblia hao walithamini kweli gani juu ya Yesu Kristo?
6 Tangu mwanzo, Wanafunzi wa Biblia hao wenye bidii (ndivyo walivyojiita), walifahamu waziwazi kweli za msingi kuhusu Yesu Kristo. Yeye ni “Mwana-mzaliwa-pekee” wa Mungu. Yeye aliishi kabla ya kuwa mwanadamu. Yeye alitoa uhai wake uwe “ukombozi kwa ajili ya wote.” Yeye alifufuliwa akiwa roho na akapaa mbinguni akiwa roho, naye angerudi akiwa roho—mfalme wa Kimasihi asiyeonekana wa ufalme wa Mungu. Habari ya kuja kwa pili kwa Kristo ni ya maana kweli kweli: Atakuja mara ya pili kwa sababu gani, jinsi gani na wakati gani?—Yohana 3:16, NW; 17:5; 1 Timotheo 2:5, 6; 1 Petro 3:18, NW.
7. Nuru yenye kuongezeka ilifunua nini juu ya ufalme wa Mungu na baraka zake?
7 Nuru iliyoendelea kuongezeka ilionyesha wazi Wakristo hao umaana wa ufalme wa Yehova kuwa utatuzi pekee wa matatizo ya wanadamu. Ufalme huo unafanyizwa na Yesu Kristo na washiriki wake 144,000, waliokombolewa kutoka kati ya wanadamu, na wanaotawala naye wakiwa wafalme na makuhani kwa miaka 1,000. Kwa msingi wa dhabihu ya ukombozi ya Kristo, Mfalme huyo atawafufua wote waliokombolewa waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho, wakiwa na mataraja ya uzima wa milele juu ya dunia iliyo paradiso. Kwa hiyo Biblia inatoa matazamio mawili kwa wale wanadamu waliookolewa—tazamio la kimbinguni kwa “kundi dogo” la warithi wa Ufalme, na uzima juu ya dunia kwa “kondoo wengine” wa Yesu, ambao wanatia “mkutano mkubwa” wa waokokaji wa ile “dhiki” kuu zaidi na vilevile wale mamilioni wengi sana waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho na watakaotoka na kufurahia uzima juu ya dunia iliyo paradiso.—Luka 12:32; Yohana 5:28, 29; 10:16; Ufunuo 7:9, 14; 14:1, 4; 20:6.
8. Ni ufahamu gani uliopatikana juu ya nafsi ya kibinadamu na hali ya wafu?
8 Vilevile nuru hiyo yenye kuongezeka iliwafunulia wanafunzi hao wa Biblia wenye kutaka kujua ukweli wa mambo kwamba mafundisho ya Jumuiya ya Wakristo juu ya asili ya nafsi ya kibinadamu na hali ya wafu ni yenye makosa kabisa! Walifahamu waziwazi kwamba wakati Adamu alipoumbwa yeye ‘alikuwa nafsi hai,’ na kwamba aliporudi kwenye ardhi kwa sababu ya kutokutii kwake, yeye alikufa akiwa nafsi, akakoma kuwapo. Ndiyo, yeye alirudi kwenye mavumbi aliyokuwa ametolewa kwayo hapo kwanza. Katika hali ya kuwa mfu hakuna kufahamu lo lote, hakuna utendaji wo wote. (Mwanzo 2:7; 3:19; Mhubiri 9:5, 10) “Mshahara wa dhambi ni mauti,” si mateso ya milele. Moto wa mateso na purgatori (matohara) yenye mateso ipo tu katika akili za wana-dini waliopotoshwa. Kuna haja ya kufufuliwa kwa sababu mtu anaacha kuwapo kabisa wakati wa kufa, ili afaidike na dhabihu ya Kristo.—Warumi 6:23.
MADARAKA YA KIKRISTO
9. Wakristo hao waliopewa maarifa walichukua msimamo gani kuhusu utakatifu?
9 Vilevile Wakristo hao walichukua kwa uzito yale Biblia inasema juu ya utakatifu wa kweli. Utakatifu huo haupasi kufahamika vibaya udhaniwe ni kujifanya mtawa au mwenye kufuata dini sana. Walifahamu kwamba wanapaswa kufuata kanuni za Biblia kama, “Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu.” (Waebrania 13:4) Walipata kuthamini kwamba hawawezi kuachilia au kuendekeza kati yao mazoea kama uasherati, uzinzi na kulalana kwa watu wa aina moja—mambo ambayo Biblia inalaani. (1 Wakorintho 6:9, 10) Vivyo hivyo, lazima waepuke kuvunja sheria kwa namna zote, na kumlipa “Kaisari yaliyo ya Kaisari,” na “Mungu yaliyo ya Mungu.” Ni lazima wawe wanyofu katika kushughulika kwao kwote na wengine, na kuifuata amri ya Kikristo: “Kama mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni vivyo hivyo.”—Mathayo 22:21; Luka 6:31.
10. Wakristo hao walitambua mapema kweli gani kuhusu mgawo wa Kikristo?
10 Kwa wazi hangaiko kuu la hao Wanafunzi wa Biblia lilikuwa kusitawisha utu kama wa Kristo. Vilevile, waliona uhitaji wa kutoa ushuhuda juu ya Mungu na Yesu. Walitambua kwamba kila Mkristo, akiisha kupokea nuru ya kweli, alikuwa na daraka la kuieneza nuru hiyo kwa wengine. Walitambua uhitaji wa kuwa mhudumu wa Mungu, na kuruhusu nuru ing’ae kwa mwenendo mzuri wa Kikristo na kwa maneno. (Mathayo 5:14-16) Kwa kweli, mwito huu ulitolewa kwa njia iliyo wazi kabisa: “Wahubiri 1,000 Wanatakiwa.” Hilo lilikuwa ombi la pekee kwa wale wasio na madaraka ya jamaa ambao wangeweza kutumia nusu au zaidi ya wakati wao kueneza “habari njema” kupitia karatasi zilizochapwa.
11. Ili mtu awe mhudumu Mkristo alihitaji kuchukua hatua gani, na kwa sababu gani tofauti iliyokuwapo ya viongozi wa kidini na watu wa kawaida ilikataliwa?
11 Ili kuwa mhudumu Mkristo, lazima kila mtu aliamini Neno la Mungu, atubu, aongolewe na kumwamini Mungu na Yesu Kristo kuwa Mkombozi wa wanadamu. Lazima mtu huyo ‘ajiweke wakf’ kwa Mungu, afanye mapenzi Yake na kubatizwa kwa kuzamishwa kabisa majini. (Matendo 3:19; Mathayo 28:19, 20) Kwa kuwa wote walikuwa wahudumu, Wakristo hao walikataa tofauti iliyokuwapo kati ya viongozi wa kidini na watu wa kawaida. Hata hivyo, kutokana na Neno la Mungu waliona haja ya kuweka wanaume wanaostahili wawe “wazee” na “mashemasi” ili waangalie mahitaji ya kila kundi.—Wafilipi 1:1; 1 Timotheo 3:1-10, 12, 13
12. Ni kweli gani kuhusu matengenezo waliyofahamu na kwa kufaa ni jambo gani lililofuata?
12 Nuru ilipozidi kuongezeka, walithamini zaidi na zaidi umaana wa kulitangaza jina la Yehova, na ufalme wake kuwa tumaini pekee la wanadamu. Vilevile waliona kwamba kuna matengenezo mawili katika ulimwengu wote na kwamba kila mtu ama ni wa tengenezo la Mungu ama la Shetani, la Shetani duniani likiwa linafanyizwa na biashara kubwa-kubwa, siasa zenye nguvu na dini kubwa-kubwa. Tengenezo la kimbinguni la Mungu la viumbe wa kiroho washikamanifu linawakilishwa duniani na mashahidi wake walio tengenezo. (Wagalatia 4:26; 2 Wakorintho 4:4) Kwa hiyo inakuwa kwamba Wakristo hawawezi kushiriki katika siasa wala kujiingiza katika jeuri kati ya mataifa; kwa kweli, hawawezi hata kushiriki katika mazoezi ya kutukuza taifa. Watumishi wa Yehova Mungu wanaunga mkono na kuupigania ufalme wake, ingawa si kwa silaha za kimwili.—Mathayo 26:52; Yohana 15:19; 18:36; 2 Wakorintho 10:4; Yakobo 1:27; 4:4.
13. Wanafunzi wa Biblia walikubali jina “mashahidi wa Yehova” baada ya kufahamu suala gani lenye kutokeza, na kwa sababu gani lilifaa sana?
13 Baada ya wakati watumishi hao waaminifu wa Yehova walitambua kwamba kutetewa kwa jina la Yehova ndilo suala kuu linalowaelekea wanadamu, na kwamba ni la maana zaidi kuliko wokovu wa viumbe vya kibinadamu. Hakika huo ulikuwa mmeto mwangavu wa nuru, uliong’aa zaidi kuliko cho chote kilichojulikana hapo mbele. Ukweli huo wenye kutokeza ulitofautisha hata zaidi dini ya Kikristo ya kweli na ya ubandia. Kweli hiyo nzito ilipokwisha kufahamika, baada ya muda mfupi Wakristo hao waliona kwamba jina lao (Wanafunzi wa Biblia), halikuwatofautisha vya kutosha, ingawa jina lenyewe lilikuwa sahihi. Kwanza, mgawo na kusudi lao la kwanza maishani ulikuwa kuwa mashahidi kwa ajili ya Yehova, zaidi ya kuwa wanafunzi wa Biblia. Wala jina Wanafunzi wa Biblia halikuwatofautisha na mamilioni waliodai wanajifunza Biblia, ambao walifuata kanuni za kidini zenye makosa. Kwa hiyo kwa uwezo wenye kuleta maarifa wa roho takatifu ya Mungu waliona kwamba jina lenye kuwafaa na kuwahusu kipekee ni lile lenye kupatikana katika Isaya 43:10-12, NW, yaani, “mashahidi wa Yehova.” Katika mwaka 1931, kwa furaha walilikubali jina hilo.
NURU YANG’AA JUU YA UNABII MWINGI NA JUU YA MIFANO
14. Nuru yenye kuongezeka ilifunua nini kuhusu unabii mbalimbali uliohusu kurudishwa?
14 Kufika wakati huo, watu wengi walikuwa na maoni kwamba kurudi kwa Wayahudi kwenye nchi ya kwao kulitimiza unabii wa Biblia. Walakini sivyo, unabii huo mbalimbali wa kurudishwa wenye kuvutia na kutia moyo ulitimizwa kwa mara ya kwanza katika karne ya sita K.W.K. wakati Wayahudi waliporudi kutoka Babeli, na utimizo wake mkubwa ni katika siku zetu juu ya Israeli wa kiroho. Tunaona uthibitisho wa utimizo wake katika paradiso ya kiroho ambayo ndani yake wamo “Israeli wa Mungu” na wenzi wao washikamanifu.—2 Wakorintho 12:4; Wagalatia 6:16.
15, 16. Ni nuru gani iliyoangazwa juu ya mifano miwili kati ya mifano ya Yesu?
15 Vilevile kukawa ufahamu ulio sahihi zaidi wa mifano ya Yesu. Mfano wenye kutokeza ulihusu mfano wa kondoo na mbuzi, ambao umeandikwa katika Mathayo 25:31-46. Kwa muda mrefu ilikuwa imefikiriwa kwamba mfano huo ungetimizwa wakati wa utawala wa Kristo wa miaka 1,000. Lakini ndipo Mashahidi wa Yehova walipofahamu kwamba haungeweza kamwe kuhusu wakati huo. Sababu moja ya ufahamu huo mpya ilikuwa kwamba wakati wa utawala wa mileani wa Kristo “ndugu” zake hawangekuwa duniani, na basi hawangekuwa na uhitaji wa vitu kwa sababu ya kuwa wagonjwa au kuteswa. Kwa hiyo lazima utimizwe sasa, wakati ambapo Yesu aliyetawazwa mbinguni anakusanya mataifa kwa hukumu, na jambo hilo linathibitishwa na mambo ya hakika yanayoonekana yakitimiza mfano huo.
16 Vivyo hivyo, mfano wa tajiri na Lazaro umefunuliwa wazi. Ilifahamika kwamba tajiri alifananisha, si taifa lote la Kiyahudi, bali viongozi wa kidini wanafiki waliokuwa tajiri katika siku za Yesu, na vivyo hivyo katika siku zetu viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo.—Luka 16:19-31.
17. Walipata ufahamu gani wenye kutokeza kuhusu kitabu cha Ufunuo?
17 Vivyo hivyo, nuru iliyoongezeka iliwafanya watumishi wa Yehova wathamini kwamba kitabu cha Ufunuo kinakuwa na utimizo wa upeo kuanzia na “siku ya Bwana,” yaani, tangu mwaka 1914, wala si wakati wa historia yote ya kundi la Kikristo tangu nyakati za mitume kufika wakati huu, kama ilivyodhaniwa wakati mmoja. (Ufunuo 1:10) Walipata kufahamu kwamba kuanza kwa “siku ya Bwana” kulionyeshwa na vita mbinguni ambayo katika hiyo Mikaeli (Yesu Kristo aliyetawazwa) na malaika zake walimtupa Shetani na malaika zake kutoka mbinguni. (Ufunuo 12:1-12) Watu wa Yehova walifurahi sana kufahamu kwamba kazi yao ya Ufalme ilikuwa imetabiriwa, sanasana katika Ufunuo sura za 2, 3, 6-11.
UTARATIBU WA KITHEOKRASI
18. Ilifahamika nini juu ya utaratibu wa kitheokrasi katika makundi ya Kikristo, na jambo hilo lilitekelezwaje?
18 Mifano mingi mingine inaweza kutolewa inayohusu kuongezeka kwa nuru katika nyakati za kisasa, lakini nafasi inaturuhusu tuonyeshe mwingine mmoja tu. Unahusu sheria ya kitheokrasi au mwongozo wa kusimamiwa na Mungu. Katika sehemu ya mwisho ya karne ya 19, Wanafunzi wa Biblia walisimamia makundi yao kwa njia ya kidemokrasi; walitaka kuepuka utaratibu wa kutawalwa na kiongozi mmoja wa kidini. Walakini katika mwaka 1938 walifahamu kwamba mpango huo wa kidemokrasi hauungwi mkono na Maandiko. Haukupatana na utaratibu wa kitheokrasi, ambao ni utawala wa Mungu kuja chini, mahali pa kuwa utawala wa wanadamu kwenda juu. (Isaya 60:1, 17-19) Kwa hiyo katika nyakati za karibuni zaidi, kwa uongozi wa roho takatifu, “mtumwa mwaminifu mwenye akili”e ndiye anayeweka wanaume katika makundi watumikie wakiwa wazee na watumishi wa huduma. (Matendo 20:28) Lazima wao wawe na sifa za Kimaandiko zinazotajwa katika 1 Timotheo 3:1-13 na Tito 1:5-9.
19. Kwa sababu gani haingetazamiwa kwamba nuru kamili ingetokea mara moja?
19 Kweli kweli, yote yaliyotangulia kutajwa yanaonyesha kwamba njia ya watu Yehova imekuwa ni kama nuru nyangavu zamani na sasa inayoangaza zaidi na zaidi wakati wote. (Mithali 4:18) Walipotoka katika giza tititi lenye kuifunika ‘Babeli Mkuu,’ milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, haingetazamiwa kwamba wangeona mambo yote mara moja kama yalivyo. (Ufunuo 17:5) Uangavu wa kweli iliyofunuliwa ungaliwapofusha, hata kuwavuruga kwa njia ya kiroho. Jambo hilo linaweza kulinganishwa na mtu anayetoka katika chumba chenye giza tupu na kuingia kwenye mwanga mwingi wa jua. Ingechukua wakati ili macho ya mtu huyo yajirekebishe kulingana na mng’ao wa ghafula wa mwanga mwingi wa jua.
20. (a) Nuru ya kweli yenye kutokea hatua kwa hatua imeangaza sehemu gani kubwa? (b) Bado kumebaki maulizo gani ya kuchunguzwa?
20 Na, kama tulivyokwisha kuona, nuru ya kweli ya hatua kwa hatua inahusu sehemu kubwa. Kuna ufahamu mbalimbali uliosafika wa mafundisho ya kidini, wa unabii, wa mwenendo wa Kikristo na mgawo wa Wakristo, wa maana ya mifano ya Yesu, wa utaratibu unaofaa wa kitengenezo katika kundi, na kadhalika. Yote hayo yako wazi kutosha. Lakini huenda wengine wakauliza hivi: kwa sababu gani inaelekea kwamba njia ya Wakristo wa kweli sikuzote haikwenda mbele moja kwa moja? Sababu yake ni nini? Ili kupata majibu ya maulizo hayo tunamwelekeza msomaji kwenye makala inayofuata.
[Maelezo ya Chini]
a Ona kurasa 102, 103 katika kitabu “Let Your Kingdom Come” kilichochapishwa na Sosaiti.
b Studies in the Scriptures, Kit. 1, kur. 29-35.
c “Chapa Mpya za Mnara wa Mlinzi,” (Kiingereza) Kit. 1, kur. 369-371.
d Studies in the Scriptures, Kit. 1, uku. 38.
e Yesu Kristo alitabiri kwamba angemweka huyo “mtumwa mwaminifu mwenye akili’’ juu ya vitu vyake vyote ili atoe chakula cha kiroho kwa wafuasi wake. Mambo ya hakika yaliyotangulia kuonyeshwa yanathibitisha kwamba “mtumwa” huyo ni jamii na anashirikiana na mashahidi Wakristo wa Yehova.—Mathayo 24:45-47.
[Sanduku katika ukurasa wa 18]
Watumishi wa kisasa wa Yehova walifahamu mapema kwamba:
Yehova ndiye Mungu wa pekee wa kweli na Yesu Kristo ni Mwanawe-mzaliwa-pekee.
Roho takatifu ni nguvu ya utendaji ya Mungu.
Nafsi inakufa na tumaini la wafu ni ufufuo.
Kristo atakuwa na warithi washirika 144,000 mbinguni, na wanadamu wengine watiifu watapokea uzima wa milele juu ya dunia iliyo paradiso.
Vilevile baada ya wakati kupita walifahamu:
Kwamba Mungu aliruhusu uovu kwa sababu ya suala la enzi kuu ya ulimwengu mkubwa wa juu na chini.
Kwamba unabii mbalimbali wa kurudishwa unahusu Israeli ya kiroho.
Kwamba Ufunuo unatimizwa katika “siku ya Bwana.”
[Picha katika ukurasa wa 17]
Ufahamu wa makusudi ya Yehova ambao umejulishwa kupitia “Mnara wa Mlinzi’’ umekuwa wazi zaidi na zaidi wakati wa miaka yote iliyopita