Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 5/15 kur. 15-20
  • Mimweko ya Nuru—Mikubwa na Midogo (Sehemu ya Kwanza)

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mimweko ya Nuru—Mikubwa na Midogo (Sehemu ya Kwanza)
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Mtumwa Mwaminifu Mwenye Akili”
  • Mimweko ya Mapema ya Nuru Katika Nyakati za Kisasa
  • Mimweko Yenye Kuongezeka ya Nuru
  • Krismasi—Sikukuu ya Kipagani
  • Jina Jipya
  • Utetezi na “Umati Mkubwa”
  • Msalaba—Si Ishara ya Kikristo
  • “Mtumwa” Ambaye Ni Mwaminifu na Mwenye Busara
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • “Ni Nani kwa Kweli Mtumwa Mwaminifu na Mwenye Busara?”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Kuongezeka kwa Nuru Katika Nyakati za Kisasa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Mimweko ya Nuru Katika Nyakati za Kimitume
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 5/15 kur. 15-20

Mimweko ya Nuru—Mikubwa na Midogo (Sehemu ya Kwanza)

“Njia ya wenye haki ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa hata mchana mkamilifu.”—MITHALI 4:18.

1. Kwa nini kweli imefunuliwa hatua kwa hatua?

NI UTHIBITISHO wa hekima ya kimungu kwamba, kwa kupatana na Mithali 4:18, kufunuliwa kwa kweli za kiroho kumetokea hatua kwa hatua kupitia mimweko ya nuru. Katika makala inayotangulia, tuliona jinsi andiko hili lilivyotimizwa katika nyakati za kimitume. Ikiwa kweli zote za Kimaandiko zingefunuliwa mara moja, zingeangaza mno na kutatanisha—kama lile tokeo la kutoka katika pango lenye giza na kuingia katika jua jangavu. Isitoshe, kweli ifunuliwayo hatua kwa hatua huimarisha imani ya Wakristo kwa njia ya kuendelea. Hiyo hufanya tumaini lao kuwa jangavu zaidi na kufanya njia wanayopasa kutembea kuwa wazi zaidi.

“Mtumwa Mwaminifu Mwenye Akili”

2. Yesu alionyesha kwamba angetumia nani kuleta nuru ya kiroho kwa wafuasi wake, na chombo hicho chajumuisha nani?

2 Katika nyakati za kimitume Yesu Kristo aliona kuwa jambo la kufaa kutumia njia zenye nguvu zipitazo za kibinadamu kuwapa wafuasi wake mimweko ya mapema zaidi ya nuru. Tuna vielelezo viwili juu ya jambo hili: Pentekoste 33 W.K., na kugeuzwa kwa Kornelio katika 36 W.K. Baadaye, Kristo ameona ikifaa kutumia chombo cha kibinadamu, kama alivyotabiri: “Ni nani basi yule mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambaye bwana wake alimweka juu ya nyumba yake [“watumishi wake wa nyumbani,” NW], awape watu chakula kwa wakati wake? Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta akifanya hivyo. Amin, nawaambieni, atamweka juu ya vitu vyake vyote.” (Mathayo 24:45-47) Mtumwa huyo hawezi kuwa mtu mmoja tu kwa sababu alipaswa kuandaa chakula cha kiroho tangu kutaniko la Kikristo lilipoanza katika Pentekoste mpaka Bwana-Mkubwa, Yesu Kristo, alipokuja kutoza hesabu. Mambo ya hakika yaonyesha kwamba jamii ya mtumwa mwaminifu mwenye akili yajumuisha Wakristo wote watiwa-mafuta wakiwa kikundi duniani wakati wowote ule.

3. Ni nani waliotiwa ndani ya washiriki wa kwanza wa jamii ya mtumwa?

3 Ni nani waliokuwa miongoni mwa washiriki wa kwanza wa jamii ya mtumwa mwaminifu mwenye akili? Mmoja alikuwa mtume Petro, aliyetii amri hii ya Yesu: “Lisha kondoo zangu.” (Yohana 21:17) Washiriki wengine wa jamii ya mtumwa walitia ndani Mathayo, aliyeandika Gospeli inayoitwa kwa jina lake, na Paulo, Yakobo, na Yuda, walioandika barua zilizopuliziwa. Mtume Yohana, aliyerekodi kitabu cha Ufunuo, Gospeli yake, na barua zake, pia alikuwa mshiriki wa jamii ya mtumwa mwaminifu mwenye akili. Wanaume hawa waliandika kwa kutii utume wa Yesu.

4. ‘Watumishi wa nyumbani’ ni akina nani?

4 Ikiwa watiwa-mafuta wote wakiwa kikundi, hata wawe wanaishi wapi duniani, ni washiriki wa jamii ya mtumwa, basi wale ‘watumishi wa nyumbani’ ni nani? Ni haohao watiwa-mafuta lakini wakionwa kutoka kwa mtazamo mwingine—wakiwa mtu mmoja-mmoja. Ndiyo, wakiwa mtu mmoja-mmoja wao wangekuwa wa “mtumwa” au wangekuwa wa ‘watumishi wa nyumbani,’ ikitegemea ikiwa wanaandaa chakula cha kiroho au kushiriki kukila. Kwa kielezi: Kama ilivyorekodiwa kwenye 2 Petro 3:15, 16, mtume Petro arejezea barua za Paulo. Anapozisoma, Petro angekuwa mmoja wa watumishi wa nyumbani wanaojilisha chakula cha kiroho kinachoandaliwa na Paulo akiwa mwakilishi wa jamii ya mtumwa.

5. (a) Ni nini lililopata mtumwa huyo katika karne za baada ya mitume? (b) Ni maendeleo gani yaliyotokea katika sehemu ya mwisho ya karne ya 19?

5 Kwa habari hii, kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached kilisema hivi: “Kwa habari ya jinsi jamii ya ‘mtumwa mwaminifu mwenye akili’ imekuwapo na kutumika katika karne zilizopita baada ya kifo cha mitume wa Bwana-Mkubwa Yesu Kristo, hatuna rekodi hususa ya kihistoria. Kwa wazi kizazi kimoja cha jamii ya ‘mtumwa’ kililisha kizazi kilichofuata baadaye. (2 Timotheo 2:2) Lakini katika sehemu ya mwisho ya karne ya kumi na tisa kulikuwa na watu wenye kumhofu Mungu waliopenda chakula cha kiroho cha Biblia Takatifu na ambao walitamani kujilisha chakula hicho . . . Madarasa ya funzo la Biblia . . . yalianzishwa nayo yakafanya maendeleo katika kufahamu kweli za msingi za Maandiko Matakatifu. Wale wenye mioyo myeupe na wasio na ubinafsi miongoni mwa hawa wanafunzi wa Biblia walitamani kushiriki sehemu hizo muhimu za chakula cha kiroho pamoja na wengine. Wao walikuwa na roho ya uaminifu ya ‘mtumwa’ aliyewekwa rasmi kuwapa ‘watumishi wa nyumbani chakula cha kiroho kilichohitajiwa kwa wakati wake.’ Wao walikuwa wenye ‘akili’ katika kutambua kwamba ulikuwa wakati mzuri na ufaao na ni zipi njia bora za kukipakua chakula hicho. Walijitahidi kukipakua.”—Kurasa 344-345.a

Mimweko ya Mapema ya Nuru Katika Nyakati za Kisasa

6. Ni jambo gani hakika linalojitokeza sana kuhusu kufunuliwa kwa kweli hatua kwa hatua?

6 Jambo moja linalotokeza sana kuhusu wale ambao Yehova alitumia kuleta nuru hii ya kiroho yenye kuongezeka hatua kwa hatua ni kwamba wao hawakujisifu. Mtazamo wa C. T. Russell, msimamizi wa kwanza wa Watch Tower Society, ulikuwa kwamba Bwana alifurahi kutumia vipawa vyao vya kawaida. Kuhusu maneno ya kukejeli ambayo maadui wake walipenda kutumia, Ndugu Russell alisisitiza sana kwamba hajapata kamwe kukutana na “Mruseli” na kwamba hakukuwa na “Uruseli” wowote. Sifa zote zilimwendea Mungu.

7. Ndugu Russell na wafanyakazi wenzake walitoa uthibitisho gani kwamba kwa kweli wao walishirikiana na mtumwa mwaminifu mwenye akili?

7 Kwa kutazama matokeo, hakuna shaka kwamba roho takatifu ya Yehova ilikuwa ikielekeza jitihada za Ndugu Russell na wale walioshirikiana naye. Walionyesha uthibitisho wa kushirikishwa na mtumwa mwaminifu mwenye akili. Ingawa makasisi wengi wa wakati huo walidai waliamini kwamba Biblia ilikuwa Neno la Mungu iliyopuliziwa na kwamba Yesu alikuwa Mwana wa Mungu, wao walikubali mafundisho bandia ya Kibabiloni, kama vile Utatu, kutokufa kwa nafsi ya binadamu, na mateso ya milele. Kwa kupatana na ahadi ya Yesu, kwa kweli ni kupitia roho takatifu kwamba jitihada za unyenyekevu za Ndugu Russell na washiriki wake zilisababisha kweli kuangaza kuliko wakati mwingine wowote. (Yohana 16:13) Hawa Wanafunzi wa Biblia watiwa-mafuta walithibitisha kwamba kwa kweli wao walikuwa sehemu ya jamii ya mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambayo utume wayo ni kuandaa chakula cha kiroho kwa watumishi wa nyumbani wa Bwana-Mkubwa. Jitihada zao zilikuwa msaada mkubwa katika kukusanya watiwa-mafuta.

8. Ni mambo gani ya hakika yaliyo ya msingi kuhusu Yehova, Biblia, Yesu Kristo, na roho takatifu ambayo Wanafunzi wa Biblia walielewa wazi?

8 Ni jambo la kutokeza sana kuona jinsi Yehova, kwa kupitia roho takatifu, aliwapendelea sana hawa Wanafunzi wa Biblia wa mapema kwa kuwapa mimweko ya nuru. Kwanza, walithibitisha kabisa kwamba Muumba yupo na kwamba yeye ana jina la kipekee Yehova. (Zaburi 83:18; Warumi 1:20) Walitambua kwamba Yehova ana sifa kubwa nne—uwezo, haki, hekima, na upendo. (Mwanzo 17:1; Kumbukumbu la Torati 32:4; Warumi 11:33; 1 Yohana 4:8) Wakristo hawa watiwa-mafuta walithibitisha wazi kwamba Biblia ni Neno la Mungu lililopuliziwa na ndiyo kweli. (Yohana 17:17; 2 Timotheo 3:16, 17) Zaidi, wao walisisitiza kwamba Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, aliumbwa na kwamba alitoa uhai wake ukiwa fidia kwa ajili ya wanadamu wote. (Mathayo 20:28; Wakolosai 1:15) Roho takatifu, mbali na kuwa mtu wa tatu wa ule Utatu, ilionwa kuwa kani ya utendaji ya Mungu.—Matendo 2:17.

9. (a) Ni kweli zipi ambazo Wanafunzi wa Biblia walielewa kabisa kuhusu asili ya mwanadamu na hali za wakati ujao zinazotajwa katika Biblia? (b) Ni kweli zipi nyingine ambazo watumishi wa Yehova waliona wazi?

9 Wanafunzi wa Biblia walitambua wazi kwamba mwanadamu hana nafsi isiyoweza kufa bali yeye ni nafsi iwezayo kufa. Wao walitambua kwamba “mshahara wa dhambi ni mauti,” bali si mateso ya milele, huku kukiwa hakuna kabisa helo yenye kuwaka moto. (Warumi 5:12; 6:23; Mwanzo 2:7; Ezekieli 18:4) Isitoshe, wao walitambua wazi kwamba nadharia ya mageuzi si ya kimaandiko na pia haina msingi wowote wa mambo ya hakika. (Mwanzo, sura 1 na 2) Walitambua pia kwamba Biblia inataja mahali pawili—mbinguni kwa wale watiwa-mafuta 144,000 wafuatao hatua za Kristo na dunia paradiso kwa “umati mkubwa” usiohesabika wa “kondoo wengine.” (Ufunuo 7:9, NW; 14:1; Yohana 10:16) Hao Wanafunzi wa Biblia wa mapema walitambua kwamba dunia hudumu milele nayo haitachomwa, kama vile dini nyingi hufundisha. (Mhubiri 1:4; Luka 23:43) Walijifunza pia kwamba kurudi kwa Kristo kungekuwa kusikoonekana na kwamba angetekeleza hukumu kwa mataifa na kuleta paradiso ya kidunia.—Matendo 10:42; Warumi 8:19-21; 1 Petro 3:18.

10. Ni kweli ipi Wanafunzi wa Biblia walijifunza kuhusu ubatizo, mgawanyo wa makasisi na watu wa kawaida, na Ukumbusho wa kifo cha Kristo?

10 Wanafunzi wa Biblia walijifunza kwamba ubatizo wa Kimaandiko si kunyunyizia vitoto vichanga maji bali kwamba kwa kufuata amri ya Yesu kwenye Mathayo 28:19, 20, ni kuzamisha waamini ambao wamefundishwa. Walikuja kutambua kwamba hakuna msingi wowote wa Kimaandiko wa kuunga mkono mgawanyo kati ya makasisi na watu wa kawaida. (Mathayo 23:8-10) Kinyume cha hilo, Wakristo wote wanapaswa kuwa wahubiri wa habari njema. (Matendo 1:8) Wanafunzi wa Biblia walitambua kwamba Ukumbusho wa kifo cha Kristo wapaswa kuadhimishwa mara moja tu kila mwaka, katika Nisani 14. Na zaidi, wao walitambua kwamba Ista ni sikukuu ya kipagani. Kwa kuongezea, wale watiwa-mafuta walikuwa na hakika sana kwamba Mungu alikuwa akiunga mkono kazi yao hata hawakuwa wakikusanya michango. (Mathayo 10:8) Kutoka nyakati za mapema zaidi, wao walielewa kwamba ni lazima Wakristo waishi kwa kupatana na kanuni za Biblia, jambo linalotia ndani kusitawisha matunda ya roho takatifu ya Mungu.—Wagalatia 5:22, 23.

Mimweko Yenye Kuongezeka ya Nuru

11. Ni nuru gani iliyoangaza kwenye utume wa Wakristo na kwenye mfano wa Yesu juu ya kondoo na mbuzi?

11 Hasa tangu 1919 watumishi wa Yehova wamebarikiwa na mimweko yenye kuongezeka ya nuru. Ni mmweko mwangavu kama nini wa nuru ulioangaza katika mkusanyiko wa Cedar Point wa 1922 wakati J. F. Rutherford, msimamizi wa pili wa Watch Tower Society, alipokazia kwamba wajibu mkubwa wa watumishi wa Yehova ni ‘kutangaza, kutangaza, kutangaza, Mfalme na ufalme wake’! Mwaka uliofuata tu, nuru nyangavu iliangaza kwenye mfano wa kondoo na mbuzi. Ilitambuliwa kwamba unabii huu ulikuwa utimizwe katika siku ya Bwana ya wakati huu, si wakati ujao katika Mileani kama ilivyofikiriwa awali. Katika kipindi cha Mileani, ndugu wa Kristo hawangekuwa wagonjwa, wala hawangefungwa gerezani. Na zaidi ya hayo, mwishoni mwa Mileani, ni Yehova Mungu, na si Yesu Kristo, atakayehukumu.—Mathayo 25:31-46.

12. Ni mmweko gani wa nuru uliotokea kuhusu Har–Magedoni?

12 Katika 1926 mmweko mwingine mwangavu wa nuru ulifunua kwamba vita ya Har–Magedoni haingekuwa mapinduzi ya kijamii, kama vile Wanafunzi wa Biblia walivyodhani wakati fulani. Badala ya hivyo, ingekuwa vita ambayo Yehova ataonyesha uwezo wake kwa njia ya wazi sana hivi kwamba watu wote watasadiki kwamba yeye ni Mungu.—Ufunuo 16:14-16; 19:17-21.

Krismasi—Sikukuu ya Kipagani

13. (a) Ni nuru gani iliyoangazwa juu ya sherehe za Krismasi? (b) Kwa nini siku za kuzaliwa zilikoma kusherehekewa? (Tia ndani kielezi-chini.)

13 Muda mfupi baadaye, mmweko wa nuru ulifanya Wanafunzi wa Biblia waache kusherehekea Krismasi. Kabla ya wakati huo Krismasi ilikuwa imesherehekewa sikuzote na Wanafunzi wa Biblia ulimwenguni pote, na sherehe yayo katika makao makuu ya Brooklyn ilikuwa pindi yenye furaha sana. Lakini ikaja kutambuliwa kwamba mwadhimisho wa Desemba 25 ulikuwa hasa wa kipagani nao ulichaguliwa na Jumuiya ya Wakristo yenye uasi-imani ili kufanya iwe rahisi kugeuza wapagani. Isitoshe, ilipatikana kwamba Yesu hangeweza kuzaliwa katika majira ya kipupwe, kwa kuwa wakati wa kuzaliwa kwake, wachungaji walikuwa wakilisha makundi yao ya kondoo mashambani—jambo ambalo hawangefanya wakati wa usiku katika mwishoni-mwishoni mwa Desemba. (Luka 2:8) Badala ya hivyo, Maandiko yaonyesha kwamba Yesu alizaliwa karibu Oktoba 1. Wanafunzi wa Biblia pia walitambua kwamba wale waitwao eti wanaume wenye hekima waliomtembelea Yesu karibu miaka miwili baada ya kuzaliwa kwake walikuwa wanajimu wa kipagani.b

Jina Jipya

14. Kwa nini jina Wanafunzi wa Biblia halikuwakilisha vizuri watu wa Yehova?

14 Katika 1931 mmweko mwangavu wa kweli ulifunulia hao Wanafunzi wa Biblia jina la Kimaandiko lenye kufaa. Watu wa Yehova walikuwa wameelewa kwamba hawangekubali lolote kati ya majina waliobandikwa na wengine, kama vile Waruseli, Millennial Dawnists, na “wapinga-helo.”c Lakini wao pia walianza kutambua kwamba jina ambalo wao wenyewe walikuwa wamechukua—Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa—halikuwawakilisha vizuri. Wao walikuwa zaidi ya wanafunzi wa Biblia tu. Zaidi ya hayo, kulikuwa na wengine wengi waliokuwa wanafunzi wa Biblia lakini ambao hawakuhusika hata kidogo na Wanafunzi wa Biblia.

15. Wanafunzi wa Biblia walichukua jina jipi katika 1931, na kwa nini lafaa?

15 Wanafunzi wa Biblia walikuja kupataje jina jipya? Kwa miaka mingi The Watch Tower imekuwa ikitokeza sana jina la Yehova. Kwa hiyo, ilifaa sana kwamba Wanafunzi wa Biblia wachukue jina lipatikanalo kwenye Isaya 43:10: “Ninyi ni Mashahidi wangu, asema BWANA, na mtumishi niliyemchagua; mpate kujua, na kuniamini, na kufahamu ya kuwa mimi ndiye; kabla yangu hakuumbwa Mungu awaye yote, wala baada yangu mimi hatakuwapo mwingine.”

Utetezi na “Umati Mkubwa”

16. Kwa nini unabii mbalimbali wa urudisho haukuhusu kurudi kwa Wayahudi wa asili Palestina, bali unahusu nani?

16 Katika buku la pili la Vindication, lililotangazwa na Watch Tower Society katika 1932, mmweko wa nuru ulifunua kwamba unabii mbalimbali wa urudisho uliorekodiwa na Isaya, Yeremia, Ezekieli, na manabii wengine haukuhusu (kama ilivyofikiriwa wakati fulani) Wayahudi wa asili, ambao walikuwa wakirudi Palestina wakiwa hawana imani na wakiwa na madhumuni ya kisiasa. Badala ya hivyo, unabii mbalimbali wa urudisho, ambao ulikuwa na utimizo mdogo wakati Wayahudi walirudi kutoka utekwa wa Babiloni katika 537 K.W.K., ulikuwa na utimizo mkubwa katika kuokolewa na kurudishwa kwa Israeli la kiroho kuanzia 1919 na ule ufanisi uliofuata katika paradiso ya kiroho inayofurahiwa na watumishi wa kweli wa Yehova leo.

17, 18. (a) Baada ya muda, kupitia mmweko wa nuru, nini lilionyeshwa kuwa kusudi kubwa la Yehova? (b) Ni mmweko gani wa nuru kuhusu Ufunuo 7:9-17 uliotokea katika 1935?

17 Baada ya muda, mimweko ya nuru ilifunua kwamba kusudi kubwa la Yehova halikuwa wokovu wa viumbe vyake, bali kutetewa kwa enzi yake kuu. Kichwa kikubwa cha Biblia kilicho muhimu zaidi kilionwa kuwa, si ile fidia, bali ule Ufalme, kwa kuwa huo ungetetea enzi kuu ya Yehova. Huo ulikuwa mmweko wa nuru ulioje! Wakristo waliojiweka wakfu sasa hawakuhangaikia hasa kwenda kwao mbinguni.

18 Katika 1935 mmweko mwangavu wa nuru ulifunua kwamba umati mkubwa uliotajwa kwenye Ufunuo 7:9-17 haukuwa jamii ya pili ya kimbingu. Ilikuwa imefikiriwa kwamba wale wanaotajwa katika mistari hiyo walikuwa baadhi ya watiwa-mafuta ambao hawakuwa wamekuwa waaminifu vya kutosha na kwa hiyo walikuwa wamesimama mbele ya kiti cha enzi badala ya kuketi katika viti vya enzi wakitawala wakiwa wafalme na makuhani pamoja na Yesu Kristo. Lakini hakuna jambo lolote kamwe la kuwa nusu mwaminifu. Ama mtu ni mwaminifu ama yeye si mwaminifu. Kwa hiyo ilionwa kwamba unabii ulirejezea umati mkubwa usioweza kuhesabika kutoka kwa mataifa yote unaokusanywa sasa na ambao tumaini lao ni la kidunia. Wao ni “kondoo” wa Mathayo 25:31-46 na “kondoo wengine” wa Yohana 10:16.

Msalaba—Si Ishara ya Kikristo

19, 20. Kwa nini msalaba hauwezi kuwa ishara ya Ukristo wa kweli?

19 Kwa miaka mingi Wanafunzi wa Biblia walifanya msalaba utokeze sana ukiwa ishara ya Ukristo. Hata walikuwa na “pini zenye msalaba na taji.” Kulingana na King James Version, Yesu aliwaomba wafuasi wake kuchukua “msalaba,” na wengi wakaja kuamini kwamba aliuawa kwenye msalaba. (Mathayo 16:24; 27:32) Kwa miongo mingi ishara hiyo ilikuwa ikitokea pia katika jalada la gazeti la Watch Tower.

20 Kitabu Riches, kilichotangazwa na Sosaiti katika 1936, kilielewesha wazi kwamba Yesu Kristo hakuuawa kwenye msalaba bali kwenye mti uliosimama wima. Kulingana na mamlaka moja, neno la Kigiriki (stau·rosʹ) lililotafsiriwa “msalaba” katika King James Version “laonyesha, hasa, mti uliosimama wima. [Wa]tofautiana na msalaba wa kidini wenye boriti mbili. . . . [Msalaba] huu ulianzia Kaldayo ya kale, nao ulitumiwa ukiwa ishara ya mungu Tamuzi.” Badala ya kufanywa kiabudiwa, kitu ambacho Yesu alitundikiwa chapasa kuchukiwa.

21. Ni nini litakalozungumzwa katika makala ifuatayo?

21 Kuna vielelezo vingine zaidi vya mimweko mikubwa na ile iwezayo kuonwa kuwa midogo. Kwa mazungumzo ya hayo, tafadhali ona makala ifuatayo.

[Maelezo ya chini]

a Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

b Baada ya muda, ilionwa kwamba ikiwa uzaliwa wenye umaana zaidi uliopata kutokea haungesherehekewa, hatupaswi kusherehekea siku yoyote ya kuzaliwa. Zaidi ya hayo, wala Waisraeli wala Wakristo wa mapema hawakusherehekea siku za kuzaliwa. Biblia yataja siku mbili tu za kuzaliwa, moja ya Farao na nyingine ya Herode Antipa. Kila sherehe ilikuwa na uuaji. Mashahidi wa Yehova hawasherehekei siku za kuzaliwa kwa sababu miadhimisho hiyo ina vyanzo vya kipagani nayo huelekea kukweza wenye kusherehekea siku ya kuzaliwa.—Mwanzo 40:20-22; Marko 6:21-28.

c Hilo ni kosa lililofanywa na madhehebu kadhaa ya Jumuiya ya Wakristo. Lutheri lilikuwa jina ambalo maadui wa Martin Luther walibandika wafuasi wake, ambao nao walilikubali. Vivyo hivyo, Wabaptisti walikubali jina walilokuwa wamebandikwa na watu wa nje kwa sababu walihubiri ubatizo wa kuzamisha. Kwa njia ambayo karibu ifanane na hiyo, Wamethodisti walikubali jina walilobandikwa na mtu wa nje. Kuhusu jinsi Society of Friends ilivyokuja kuitwa Quakers (watetemeshaji), The World Book Encyclopedia chasema hivi: “Neno Quaker awali lilikusudiwa kudhihaki Fox [mwanzilishi], aliyemwambia hakimu mmoja Mwingereza ‘atetemekee Neno la Bwana.’ Hakimu huyo akamwita Fox ‘quaker.’”

Je, Wakumbuka?

◻ Ni nani aliye “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” na ni nani walio ‘watumishi wa nyumbani’?

◻ Ni ipi baadhi ya mimweko ya mapema ya nuru katika nyakati za kisasa?

◻ Kwa nini jina jipya, Mashahidi wa Yehova, lilifaa?

◻ Ni kweli zipi zenye kutokeza zilizofunuliwa katika 1935?

[Picha katika ukurasa wa17]

C. T. Russell na washiriki wake walieneza nuru ya kiroho, lakini sifa zote zilimwendea Yehova

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki