Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 7/1 kur. 19-24
  • Njia ya Wenye Haki Inaendelea Kung’aa Zaidi na Zaidi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Njia ya Wenye Haki Inaendelea Kung’aa Zaidi na Zaidi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UKOMBOZI NA JINA LA YEHOVA
  • MWENENDO NA KUHUBIRI
  • KUJITIISHA KWA “MAMLAKA ILIYO KUU”
  • NI NANI MAMINISTA?
  • Twende Kwa Nani Isipokuwa Kwa Yesu Kristo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Kuongezeka kwa Nuru Katika Nyakati za Kisasa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Mungu na Kaisari
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Kukua Katika Ujuzi Sahihi Juu ya Kweli
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 7/1 kur. 19-24

Njia ya Wenye Haki Inaendelea Kung’aa Zaidi na Zaidi

“Wakati mtu anayewatawala wanadamu ni mwenye haki, . . . Ndipo inapokuwa kama nuru ya asubuhi, wakati jua linapoangaza.”​—2 Samweli 23:3, 4, NW.

1. 2 Samweli 23:3, 4 linatuongoza tutazamie nini, na je! Jambo hilo limetimia?

NURU juu ya njia ya watumishi wa Yehova tangu nyakati za mapema sana mpaka sasa imeendelea kuongezeka. Hiyo imekuwa hata zaidi tangu ule mwaka wenye kutokeza wa 1914 wakati ‘ufalme wa dunia ulipokuwa ufalme wa Bwana wetu [Yehova] na wa Kristo wake,’ kama ilivyoonyeshwa na matukio hapa duniani. (Ufunuo 11:15) Nuru kutoka Neno la Mungu imemeta, kama mwanga wa jua wakati wa “asubuhi isiyo na mawingu” ili kuangaza kwa uzuri zaidi njia ambayo lazima watumishi wa Yehova waipitie.​—2 Samweli 23:3, 4, NW.

2. Tunaweza kuonaje marekebisho ya pindi kwa pindi juu ya maoni?

2 Hata hivyo, huenda ikawa imeonekana kwa wengine kama kwamba njia hiyo sikuzote haijakwenda mbele moja kwa moja. Nyakati nyingine imeonekana maelezo yaliyotolewa na tengenezo lionekanalo la Yehova yamekuwa na marekebisho, tofauti na maoni ya kwanza. Lakini kwa kweli hivyo sivyo imekuwa. Jambo hilo linaweza kulinganishwa na lile linaloitwa na mabaharia kuwa “kukisi matanga.” Kwa kusogeza matanga mabaharia wanaweza kuifanya meli (merikebu) itoke kulia iende kushoto, iende huku na huku, lakini wakati wote wakiwa wanafanya maendeleo kuelekea mahali wanakokwenda zijapokuwa pepo zenye kutofautiana. Mradi unaoweza kufananishwa na mahali ambako merikebu hiyo inaelekea kwa upande wa watumishi wa Yehova ni “mbingu mpya na dunia mpya” zilizoahidiwa na Mungu.​—2 Petro 3:13, NW.

3. Kuna ushuhuda gani kwamba Yehova anaendelea kuwabariki mashahidi wake?

3 Hakuna shaka kwamba Yehova Mungu anaendelea kubariki utendaji wa duniani pote wa mashahidi wake, kufuata uongozi wa “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” Matunda (matokeo) yanaonyesha jambo hilo. Kumbuka, Yesu alisema hivi: “Kila mti mwema huzaa matunda mazuri.” Na matunda hayo mazuri yanaonekana katika mataifa yote leo katika kikundi kimoja tu cha watu—jamii yenye umoja ya duniani pote ya Mashahidi wa Yehova.​—Mathayo 7:17.

4, 5. Kuongezea Neno lake lililoongozwa kwa roho, Yehova Mungu ametumia chombo gani kingine kuwaongoza watu wake?

4 Hata tuwe tunaishi wapi duniani, Neno la Mungu linaendelea kuwa nuru kwenye njia yetu na taa kwenye barabara yetu kwa habari ya mwenendo na masadikisho yetu. (Zaburi 119:105) Lakini pia Yehova Mungu ametoa tengenezo lake lionekanalo, “mtumwa mwaminifu mwenye akili” wake, ambaye washiriki wake ni wale waliotiwa mafuta kwa roho, ili kuwasaidia Wakristo wote katika mataifa yote kufahamu na kutumia inavyofaa Biblia maishani mwao. Tusiposhirikiana na njia hiyo ya kupasha habari ambayo Mungu anatumia, hatutafanya maendeleo kwenye njia inayoongoza kwenye uzima, hata tusome Biblia kadiri gani.​—Linganisha Matendo 8:30-40.

5 Kuhusu njia ya Mungu ya kupasha habari, Yesu alisema kwamba “mtumwa mwaminifu mwenye akili” angetoa chakula cha kiroho kwa wakati wake kwa wafuasi wake wote na kwamba angemweka “mtumwa” huyo juu ya vitu vyake vyote. (Mathayo 24:45-47) Vilevile ni jambo la kuangaliwa kwamba mtume Paulo, katika Waefeso 4:11-16, alionyesha kwamba kundi la Kikristo lilihitaji si vyombo vyenye kuongozwa na Mungu kama mitume na manabii tu bali pia waeneza injili, wachungaji na walimu ili kuwasaidia Wakristo waufikie umoja wa imani na maarifa sahihi ya Mwana wa Mungu, na kufikia kukomaa kamili kwa kiroho.​—Ona pia 1 Wakorintho 1:10; Wafilipi 1:9-11.

6. Imekuwa lazima kuchanganua upya maoni kwa sababu ya mambo gani?

6 Huyu “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” anayeshirikiana na Mashahidi wa Yehova, hakika ametumiwa na Yehova Mungu kuongoza, kutia nguvu na kuwapa mwongozo watu wake. Ni kweli kwamba Wakristo hao wamelazimika kuchanganua upya maoni na mafundisho yao uhitaji unapotokea, kwa kuwa nuru inang’aa hatua kwa hatua, na kwa sababu kumekuwako makosa kwa ajili ya kutokukamilika na udhaifu wa kibinadamu. Walakini je! hiyo haikuleta kusafika, kwa faida yao? Ebu fikiria baadhi ya mifano.

UKOMBOZI NA JINA LA YEHOVA

7. Ni kwa sababu gani na ni kwa msingi wa nini fundisho la ukombozi lilifanywa kuwa jambo la maana sana na Wanafunzi wa Biblia?

7 Katika mwaka 1878, Charles T. Russell, ambaye baadaye akawa msimamizi wa kwanza wa Sosaiti, alikata uhusiano wake na mhariri mwenzi wa The Herald of the Morning, N. H. Barbour, kwa ajili ya suala la ukombozi. Bw. Barbour alikana uwezo wa dhabihu ya Yesu kuondoa dhambi. Miaka mingi baada ya hayo Wanafunzi wa Biblia, kama ambavyo mashahidi hao wa Yehova walivyokuwa wakijiita wakati huo, walikuwa na maoni kwamba dhabihu ndiyo fundisho kuu la Biblia. Na bila shaka wokovu kupitia imani katika ukombozi wa Kristo unakaziwa katika Neno la Mungu. (Yohana 3:16; Matendo 4:12; Waebrania 5:9; Ufunuo 7:10) Dhabihu ya Yesu ya ukombozi ilitangulia kufananishwa na unabii wa Ibrahimu kumtoa Isaka na dhabihu zilizotolewa chini ya torati ya Musa. Vilevile ilitabiriwa na manabii. Kwa hiyo hao Wanafunzi wa Biblia waliweka mkazo mkubwa juu ya yale ambayo Yesu Kristo aliwafanyia wanadamu.​—Luka 24:25-27, 44.

8. (a) Halafu ni nini kilichoonekana kuwa cha maana kubwa zaidi? (b) Jambo hilo liliongoza kwenye nini, walakini ni rekebisho gani lililofanywa katika miongo ya miaka iliyofuata?

8 Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba kuna kitu cha maana zaidi ya wokovu wetu wa kibinafsi. Hilo ni suala kuu linalohusu enzi kuu ya ulimwengu wote ya Yehova, ambayo Shetani alitilia shaka wakati wa uasi katika Edeni. (Mwanzo 3:15; 1 Wakorintho 15:24, 25; Ufunuo 11:15; 12:10) Hiyo inataka jina la Yehova liondolewe lawama. Kweli kweli, kichwa kikuu cha Biblia, tangu Mwanzo mpaka Ufunuo, ni ufalme wa Kimasihi, ambao kupitia huo Jina hilo tukufu litaondolewa lawama kwa umilele wote! Mara 75 katika Biblia tunasoma juu ya tangazo la Mungu mwenyewe: ‘Watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.’a Mashahidi wake walikuja kufahamu baada ya wakati kwamba viumbe wangeweza kumwitia Yehova Mungu kwa msingi wa kwamba jina lake linahusika na kwamba “kila mtu aliitaye jina la Yehova ataokolewa.” (Warumi 10:13, NW; Yoeli 2:32; Sefania 3:19) Kwa hiyo kwa miaka fulani jina la Yehova na kuondolewa lawama kwa jina hilo yalifanywa yakawa mambo ya maana sana hata kwamba walaumu wa Mashahidi hao wakawashtaki kuwa hawamwamini Yesu Kristo. Hata hivyo, jambo hilo halikukaziwa kupita kiasi. Kama ambavyo wasomaji wa Mnara wa Mlinzi katika miongo ya miaka ya karibuni wanavyofahamu vizuri, mashahidi Wakristo wa Yehova kwa hakika wamekuwa wakitoa sifa inayostahili kwa sehemu ya Yesu katika utimizo wa makusudi ya Mungu. Kwa kweli Neno la Yehova la kiunabii linakaza fikira juu ya Yesu kuwa ‘Wakili Mkuu wa wokovu’ wa Mungu.​—Waebrania 2:10; 12:2, NW; Ufunuo 19:10.

9. Ni kanuni gani inayoongoza ukuzi wa mambo ya kisayansi inayoelekea kuhusu hapa?

9 Huenda ikasemekana marekebisho hayo yanafuata kanuni ya uongozi ambayo imekuwa ikiongoza ukuzi wa kweli za kisayansi. Kwa ufupi, marekebisho hayo yanafanywa kwa njia hii: Kwanza jambo fulani linapendekezwa na kuachwa wazi liweze kujadiliwa (kuzungumzwa) lionekane kama linafaa au halifai. Jambo hilo linaonyesha dalili nyingi za kwamba ni lenye kuelimisha watu au linaweza kuwaletea mafaa likianza kutumiwa. Lakini baada ya muda fulani jambo hilo linaonekana kuwa lenye makosa na hitilafu fulani-fulani. Kwa hiyo sasa kunakuwa na maelekeo ya kutafuta jawabu upande mwingine ulio tofauti kabisa na pendekezo lile la kwanza. Baadaye inakuja kuonekana kwamba hata jambo hilo la pili halina ukweli kamili, na kwa hiyo mawazo yenye kufaa kutoka pande zote mbili yanaunganishwa ili yatumike yakiwa jambo moja lenye mafaa. Hivyo ndivyo kanuni hiyo imetumika mara nyingi katika njia ambayo Mithali 4:18 imetimizwa.

MWENENDO NA KUHUBIRI

10, 11. Halafu, ni misimamo gani miwili iliyokaziwa, lakini matokeo ya mwisho yakawa nini?

10 Fikiria mfano mwingine wa ufahamu unaokuja hatua kwa hatua: Kwa miaka 40 Wanafunzi wa Biblia walikazia umaana wa kusitawisha utu mwema wa Kikristo, na usitawishaji huo waliuita “ukuzi wa utu.” Ulikaziwa sana kwa sababu ulikuwa umepuzwa katika Jumuiya ya Wakristo. Ni kweli Wakristo vilevile walipaswa kutoa ushuhuda kwa kuzungumza na wengine juu ya makusudi ya Mungu, walakini hilo lilikuwa jambo la pili. Baadaye, wakati watu wa Mungu walipothamini umaana wa jina la Yehova na kwamba walipaswa kuwa mashahidi wa jina lake na ufalme, jambo hilo lilikaziwa, na matokeo yakawa kwamba fikira chache zaidi zilikazwa juu ya kusitawisha utu kama wa Kristo. Hoja ilitolewa kwamba zaidi ya yote Yesu alikuja kutoa ushuhuda, na kwamba jambo la maana zaidi ni kuhubiri. Ikawa lazima kutafuta usawa kati ya misimamo hiyo miwili.​—Warumi 10:10; Wagalatia 5:22, 23.

11 Baada ya wakati, usawa huo wenye kuleta furaha ulifikiwa. Wakristo wanahitaji kusitawisha tunda la roho ya Mungu na kutoa ushuhuda bila woga na kwa uaminifu juu ya Yehova. Matakwa hayo mawili ni ya maana. Hatuwezi kupuza mojalapo na kudai tunafanya lile jingine. Mtume Paulo alisema hivi: “Ole wangu kama sikutangaza zile habari njema!” Lakini vilevile alisema hivi: “Mimi naupiga-piga ngumi mwili wangu na kuufanya kama mtumwa, ili, nikiisha kuhubiri wengine, mimi mwenyewe nisije nikakataliwa kwa njia fulani.”​—1 Wakorintho 9:16, 27, NW.

KUJITIISHA KWA “MAMLAKA ILIYO KUU”

12, 13. (a) Ni nini yaliyokuwa maoni ya kwanza kuhusu “mamlaka za juu” za Warumi 13:1? (b) Jambo hilo liliongoza kwenye kinyume gani, lakini kwa wazi kukawa faida gani?

12 Bado mfano mwingine wa kuendesha merikebu hiyo ya mfano kuelekea maoni yanayofaa ni kupata ufahamu unaofaa wa Warumi 13:1-7. Kwa kufaa Wanafunzi wa Biblia wa kwanza walifahamu kwamba “mamlaka za juu,” au “mamlaka iliyo kuu,” zilikuwa watawala wa kiserikali wa ulimwengu huu. (Linganisha Authorized, Version na Union Version.) Kwa msingi wa ufahamu huo walikata maneno kwamba Mkristo akiingizwa jeshini wakati wa vita ilikuwa ni lazima atumike katika jeshi, angevaa mavazi na kuondoka aende vitani. Lakini ilikubaliwa kwamba, ulipofika wakati wa kuua mwanadamu mwenzake angefyatua risasi hewani.

13 Hata hivyo, ilikuwa wazi kabisa kwamba mtume Paulo hakuwa akitetea mwenendo kama huo. Ulizo hili lilitokezwa: Basi, je! “mamlaka zilizo juu,” zaweza kuwa ni Yehova Mungu na Yesu Kristo? Kwa wakati fulani, watu wa Mungu walikuwa na maoni hayo. Na wakati wa miaka ya msukosuko ya Vita ya Ulimwengu ya Pili jambo hilo liliwaimarisha ‘wamtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu,’ kwa kuwa waliacha kumbukumbu nzuri sana duniani pote ya kutokuwamo kwa Kikristo kusiko na woga. (Matendo 5:28, 29, NW) Hakujapata kuwako shaka lo lote kwamba Wakristo wanapaswa kutoa utii wao mwingi kwa Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova na mfalme wake wa Kimasihi, Yesu Kristo. Walakini je! wakati uo huo wao ndio “mamlaka iliyo kuu” ambayo twapaswa ‘kuipa kodi, ushuru na heshima’?​—Warumi 13:7.

14. Ni kwa njia gani kujitiisha kwa mamlaka za kiserikali za ulimwengu mwishowe kulionwa inavyofaa?

14 Kwa furaha, katika mwaka 1962, Yehova aliwaongoza watu wake wakapata ufahamu wa kanuni ya utii wa kadiri. Ilionekana kwamba Wakristo waliojiweka wakf wanapaswa kutii watawala wa kidunia wakiwa ndiyo “mamlaka iliyo kuu,’ kuwatambua hao kwa furaha kuwa “mtumishi wa Mungu,” au mhudumu, kwa faida yao. (Warumi 13:4) Hata hivyo, “mamlaka” hizo zikiwauliza wavunje sheria za Mungu, basi iweje? Kufikia hatua hiyo Wakristo wametii amri katika Warumi 13:1: “Kila mtu na aitii mamlaka iliyo kuu.” Lakini jambo hilo linaelezwa kikamilifu na maneno ya Yesu, yaliyoandikwa katika Mathayo 22:21: “Mlipeni Kaisari yaliyo ya Kaisari, na Mungu yaliyo ya Mungu.” Kwa hiyo wakati wo wote “Kaisari” anapowauliza Wakristo wafanye mambo yanayopingana na mapenzi ya Mungu, lazima waweke sheria ya Yehova mbele ya ile ya “Kaisari.” Hiyo ni tofauti na yale yanayofanywa katika Jumuiya ya Wakristo kwa ujumla. Wengi wanaoitwa Wakristo wanapinga kidogo tu juu ya kuvunja sheria za Mungu wanapoamriwa wafanye hivyo na Kaisari. Mzalendo mmoja hata alilisema jambo hilo kwa njia hii: “Nchi yetu! . . . sikuzote na iwe ndiyo yenye haki; lakini ni nchi yetu, iwe ni yenye haki au ni yenye kosa.” Walakini sivyo ilivyo kwa mashahidi Wakristo wa Yehova! Wanapoamriwa watende kinyume cha mapenzi ya Mungu, wanavumisha maneno ya mitume wa Yesu, na kusema: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”​—Matendo 5:29, NW.

NI NANI MAMINISTA?

15, 16. (a) Kwa muda mrefu ufahamu ulikuwa nini juu ya ni nani walio maminista wa Mungu? (b) Ni rekebisho gani lililofanywa, na kwa sababu gani? (c) Walakini rekebisho hilo lilikuwa na kasoro gani?

15 Tukitaja mfano mwingine mmoja wa kupewa maarifa hatua kwa hatua, kuna lile ulizo la kama Wakristo wote waliojiweka wakf kwa unyofu wa moyo ni maminista, hata wawe ni wa umri gani, wawe ni wanaume au wanawake. Kwa miaka mingi Mashahidi wa Yehova walikuwa wameshikilia kwamba wote ambao wametubu, wakaongolewa, na kuonyesha imani katika Mungu na Kristo, walijiweka wakf kwa Yehova wafanye mapenzi yake kama yalivyofunuliwa na Kristo, kisha wakabatizwa, kwa kweli walikuwa maminista. Lakini ndipo wengine walipotokeza vipingamizi. Mamlaka za kiserikali mara nyingi hazikuthamini msimamo huo. Vilevile ilibishwa kwamba lugha nyingi hazikuwa na neno hilo (la Kiingereza) “minista” na kwa hiyo halikupasa kutumiwa kwa njia ya kidini na wale ambao lugha zao zilikuwa na neno hilo. Vilevile, ilibishwa kwamba ilionekana ubatizo si sherehe ya kutosha kuteuliwa kuwa minista. Walakini, je! hizo zilikuwa sababu zinazofaa za kufanya jina hilo ‘minista’ lisitumiwe kwa wale waliowekwa katika vyeo kundini, wazee na “mashemasi,” au watumishi wa huduma?

16 Uhakika ni kwamba sheria ya nchi mara nyingi inalipa kila tengenezo la kidini haki ya kuamua ni nini kinachomfanya mtu awe mmoja wa maminista walo. Si kitu kama wengine hawathamini wala kukubali msimamo wao. Wala si kitu kama lugha nyingi hazina neno linalofanana na neno hilo (la Kiingereza) ‘minista’ (katika Kiswahili hatuna neno hilo; tunatumia neno ‘mhudumu’). Hilo halipasi kuwazuia wale ambao lugha zao zina neno hilo—Kiingereza, Kiitalia, Kispania na nyingine—wasilitumie ikiwa linatimiza kusudi linalofaa.

17, 18. Kwa kweli ni nani wanaoweza kuitwa “maminista,” nao wanapaswa kuuonaje “uminista” wao?

17 Neno ‘minista’ linafaa, kwa kuwa linamhusu “mtumishi” wa aina ya pekee, mwenye mgawo wa utumishi uliokwezwa, wa pekee. Ye yote, bila kujali umri au ni mwanamume au mwanamke, kama anaweza kuonyesha kwamba yeye ana ufahamu mzuri wa mapenzi na makusudi ya Mungu kwa wanadamu, na ambaye amepatanisha maisha yake na kanuni za Biblia, na ambaye vilevile amejiweka wakf na kubatizwa kwa kufuata amri ya Yesu katika Mathayo 28:19, 20, kweli kweli yeye ni mmoja wa maminista wa Mungu. Kwa kweli, yaweza kusemwa kwamba yeye anastahili zaidi kusema kwa niaba ya Mungu kushinda wo wote kati ya wale ambao wamehudhuria seminari za kidini lakini wasiofahamu makusudi ya Mungu na ambao huenda wakawa hawajapatanisha maisha zao na matakwa ya haki ya Mungu. Wale wanaomtumikia Mungu kikweli wanaweza kusema hivi pamoja na mtume Paulo: “Ninautukuza uminista wangu.”​—Warumi 11:13, NW.

18 Lazima ikaziwe kwamba neno “minista” si cheo bali ni kitambulisho. (Linganisha Mathayo 20:28, NW.) Haitoshi mtu akichukua hatua zinazomstahilisha abatizwe awe mtumishi wa Yehova Mungu. Lazima mtu huyo afanye uminista wake, “utumishi mtakatifu” wake, kwa Yehova Mungu, uwe ndilo jambo kuu maishani mwake. Kama sivyo, hata atumie wakati wa kadiri gani katika uminista wake kwa sababu ya hali asizoweza kuziongoza, kwa kufaa hawezi kujiita minista au kuonwa na wengine kuwa mmoja wa maminista wa Mungu.​—Warumi 12:1, NW; 2 Timotheo 4:5.

19. (a) Ukuzi huo wa ufahamu umetokeza nini, walakini washikamanifu wanabarikiwaje? (b) Ni nini mpango wa Yehova wa kutawanya chakula cha kiroho na kwa sababu gani sikuzote unapasa kuwa uchaguzi wetu?

19 Bila shaka, ukuzi huo wa ufahamu, unaotia “kukisi matanga,” mara nyingi umekuwa jaribu la ushikamanifu kwa wale wanaoshirikiana na “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” Hata hivyo, wakati wote maendeleo yanafanywa kuelekea kuthamini kikamilifu “habari njema” na yote zinayomaanisha. Wale ambao wanakaa karibu na tengenezo la Mungu wamejionea kwamba maulizo na mambo yaliyo magumu kufahamu yanajibiwa sikuzote baada ya wakati kupita. Na nuru inapong’aa kwa uangavu zaidi, njia hiyo inachangamsha na kuridhisha kama nini! Ni kama Petro alivyosema wakati baadhi ya wanafunzi walipokwazwa na fundisho la Yesu: “Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele.” (Yohana 6:68) Bwana Yesu Kristo yungali na “maneno” hayo, na anayatawanya kupitia tengenezo moja la “mtumwa mwaminifu mwenye akili” analolitumia leo duniani. Ni kama ule “mti mwema” ambao Yesu alisimulia kuwa unazaa “matunda mema.” (Mathayo 7:17) Kando ya hilo, ule uchaguzi mwingine mmoja uliobaki ni kushirikiana na “mnyama” wa kisiasa wa Shetani na “Babeli Mkuu,” milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. (Ufunuo 13:1; 17:5) Hakuna Mkristo aliyejiweka wakf angependa kurudia ushirika huo!—2 Petro 2:22; Yohana 14:6.

20. (a) Kwa sababu gani sasa tunaweza kuwa na hakika kupita wakati mwingineo wo wote juu ya ‘nuru inayong’aa’? (b) Ni wakati gani ujao wenye furaha uliotaraja kwa wale wote wanaochagua njia ya nuru inayoongezeka?

20 Kwa kweli, “nuru yenyewe imemeta kwa mwenye haki.” (Zaburi 97:11, NW) Mithali 4:18 inatimizwa, kwa kuwa “njia ya wenye haki” ni kama mwangaza unaong’aa zaidi na zaidi. Ikiwa nyakati nyingine kuna kadiri fulani ya marekebisho, sikuzote matokeo yake ni kutokeza msimamo bora zaidi. Kusafika huko hakuwi kwa bure. Sasa Kristo akiwa anatawala, hali ya kupewa maarifa waliyopewa watu wa Yehova ni “nuru ya asubuhi, wakati jua linapoangaza.” (2 Samweli 23:3, 4, NW; Mathayo 25:31) Wale wote wanaotumikia kwa ushikamanifu na tengenezo la “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” wakili wa Yehova anayeonekana wa kupasha habari, wana pendeleo kweli kweli! Uchaguzi wao ndio wa hekima, kwa maana njia yao inaelekea kwenye mradi wenye thamani kubwa wa uzima wa milele katika taratibu mpya ambayo Yehova anaendelea kutayarisha.​—Isaya 65:17, 18; 66:22.—Kutoka The Watchtower, December 1, 1981.

[Maelezo ya Chini]

a Mara 60 hivi katika kitabu cha Ezekieli peke yake; pia katika Kutoka 6:7; Kumbukumbu 29:6, NW: Isaya 49 : 23, NW; Yoeli 3:17, NW, na maandiko mengine.

[Sanduku katika ukurasa wa 24]

Kupitia funzo na mambo yaliyowapata watumishi wa Yehova sasa wanaona kwa usawa unaofaa:

Kwamba kuondolewa lawama kwa jina la Yehova ni kwa maana kuliko wokovu wa viumbe.

Kwamba kuonyesha juhudi katika utoaji wa ushuhuda na kusitawisha matunda ya roho ni mambo yanayolingana kwa ubora.

Kwamba kujitiisha kwa Mkristo kwa mamlaka za kidunia ni utii wa kadiri.

Msimamo wao wenye heshima wakiwa maminista, wenye kumwakilisha Yehova kikweli, hata kama wengine wanawaona namna gani.

[Mchoro/​Picha katika ukurasa wa 20]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Kukisi Matanga kwenye Upepo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki