Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 2/15 kur. 5-9
  • Dini Inawezaje Kupunguza Mikazo?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Dini Inawezaje Kupunguza Mikazo?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Njia Iliyo Bora Zaidi ya Kusaidia
  • Je! Hii Inatosha?
  • Makanisa Yanajiingiza
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Je, Dini Inapaswa Kujihusisha Katika Siasa?
    Habari Zaidi
  • Je, Makasisi Wanapaswa Kujiingiza Katika Siasa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Manabii Wawongo Leo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 2/15 kur. 5-9

Dini Inawezaje Kupunguza Mikazo?

UONEZI, njaa, kuharibika kwa viwango vya adili,matumizi mabaya ya dawa za kulevya,mwelekeo wa kutokea kwa vita ya nyukilia​—hayo ni mengine ya matatizo yanayosemwa-semwa na wahudumu wengine wa dini walioagizwa rasmi ambao wanajitia sana siasani. Ni wazi kwamba Wakristo wote wanahangaikia mambo kama hayo. Lakini je! kujiingiza katika siasa ndiyo njia ya kupunguza mikazo ya ulimwengu?

Viongozi wa kidini wanajitia katika siasa kwa sababu wanataka kuwekea watu “kielelezo cha adili” au kutoa onyo wakati serikali zinapofuata “njia isiyofaa.” Lakini ikoje wakati wao wenyewe wanapofuata njia isiyofaa? Kwa mfano, hivi majuzi wakati wa utukuzaji-taifa wa Serbia, padri wa Serbia alirushia kombora makao ya afisa (balozi) mwenye kutunza mambo ya raia wa Yugoslavia katika United States (Amerika). Kwa uhakika, tendo hilo la uharamia ni kosa, hasa linapofanywa na mtu anayeitwa padri! Hata padri huyo awe alikuwa na sababu gani za kufanya hivyo, yeye anadai kwamba anawakilisha Mungu. Lakini Neno la Mungu linawaonya waziwazi wote wanaomwamini Yeye wawe na busara kwa kuwaambia: “Msijilipize kisasi, . . . maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena Bwana.” (Warumi 12:19) Matendo kama ya padri huyo yanadhoofisha uongozi wa maadili ambao dini fulani zinajaribu kuwapa watu.

Tena, hata katika Kanisa Katoliki, watu wengi wana mashaka makubwa juu ya mapadri na watawa wa kike wanaohusika katika mambo ya kimapinduzi. Myeswiti wa Kolombia alisema: “Watu wa kwanza kuumia katika uasi wa kutumia silaha wangekuwa ni maskini wenyewe, si viongozi wa kidini wala maaskofu. Tunawezaje kuunga mkono hali ya namna hiyo?” Papa mwenyewe amejaribu kukatiza utendaji fulani wa kisiasa, akisema kwamba ni wajibu wa padri au mtawa wa kike kuhudumia mahitaji ya kiroho ya kundi, badala ya kuliongoza kundi lifanye uasi.

Usaidizi wa Baraza ya Ulimwengu ya Makanisa kwa vikundi vya kimapinduzi ulitokeza mabishano pia, hasa ilipoonekana kwamba vingine vya vikundi vyenye kupokea misaada vilikuwa vimefanya matendo ya kuwatesa wamisionari! Jeshi la Wokofu lilijiondoa lisishiriki katika Baraza hiyo kuhusiana na suala hilo.

Hata vikundi vya Kiprotestanti vyenye kutia mkazo katika jambo hilo katika United States vimelaumiwa. Mhariri wa gazeti moja alitoa maoni haya: “Katika utendaji mbalimbali wa haki ambayo Ukristo unao, Yesu anatajwa-tajwa kwa jina tu lakini matendo mengine yote si ya Kikristo.” Ni wazi kwamba mhariri huyo aliona kwamba kwa kujiingiza katika siasa, watu hao walikuwa wakitenda kama wanasiasa wasiofuata kanuni badala ya kuwa kama wahudumu wa dini. Jambo hilo linatukumbusha onyo la upole la Yakobo mwandikaji wa Biblia, kwamba Mkristo wa kweli ajiweke katika hali ya kuwa “bila doa kutoka kwa ulimwengu.”​—Yakobo 1:27, NW.

Kwa hiyo, utendaji wa kidini katika mambo ya kilimwengu unatokeza maulizo magumu katika akili za watu wenye kufikiri. Lakini namna gani viongozi wa kidini wakipunguza utendaji wao, wawe wakitoa maoni ‘ya busara’ tu juu ya mashauri ya kiserikali yanayojulikana wazi? Hata kufanya hivyo kunaleta matatizo, kwa sababu viongozi hao wanatoa maoni yenye kupingana. Hilo halisaidii hata kidogo kupunguza mikazo.

Kwa mfano, katika United States wana dini fulani wanatoa kipa-moyo cha kwamba mataifa yaache kuwa na silaha. Walakini, wengine wanataka kuona nchi yao ikiwa na “jeshi lenye nguvu zaidi ya lo lote lililopata kuwako tangu wakati wa Uumbaji.” Kile kikundi kinachoitwa “Moral Majority” kinajitahidi ili “Amerika iokoke,” pamoja na mfumo wayo wa ubepari. Walakini, afisa wa Baraza ya Ulimwengu ya Makanisa aliandika hivi: “Mapinduzi ya ulimwengu mzima yanahitajiwa ili kukomboa wanadamu katika maangamizi, hali ya kuharibika kwa mali, katika hali ya kutumia watu ili wengine wajifaidi wenyewe na katika uonezi, hayo yakiwa ni mambo yaliyoletwa na mfumo wa kibepari.” Aliendelea kusifu maoni ya Cuba juu ya njia ya kuleta hayo “mapinduzi ya ulimwengu mzima.”

Hata katika mambo yanayohusu adili za mambo ya ngono, viongozi wa kidini wanatoa maoni yenye kutofautiana. Sasa basi mtu wa nje atajuaje ni kipi kilicho kiwango ‘cha adili’ kinachopasa kufuatwa na ni ipi iliyo “njia mbaya” inayopasa kuepukwa? Je! njia ‘inayofaa’ au ‘isiyofaa’ inategemea taifa ambamo mtu amezaliwa, chama cha kisiasa ambacho yeye ni mshiriki, rangi ya ngozi yake au cheo chake katika mambo ya kipesa? Au Mungu ameweka kiwango kinachohusu kila mtu kila mahali?

Kwa njia nyingi, kujiingiza kwa dini katika siasa kumeleta mvurugo badala ya kuleta hali ‘ya kimungu’ ndani ya mambo ya ulimwengu. Je! maana yake ni kwamba dini haina sehemu ya kutimiza? Je! Haina usaidizi wa kutoa ili kupunguza mikazo katika ulimwengu?

Njia Iliyo Bora Zaidi ya Kusaidia

Jambo la uhakika ni kwamba dini ya kweli inaweza kusaidia sana. Lakini ili tuone ni msaada gani itakaoutoa, lazima tufahamu mambo fulani ya uhakika yaliyo ya msingi.

Kwanza, ili iwe na msaada, ni lazima dini iseme kwa mamlaka ya Mungu, si ya mwanadamu? Inaweza kufanya hivyo namna gani? Biblia inasema: “Kila andiko limepewa kwa maongozi ya Mungu, na linafaa kwa mafundisho, na kwa kuonya watu juu ya makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa mafundisho katika haki; ili mutu wa Mungu awe mukamilifu, ametegemezwa kabisa kwa kila tendo jema.” (2 Timotheo 3:16, 17, ZSB) Ikiwa mhudumu wa kidini anatoa maoni yake mwenyewe, hata ikiwa ameshika Biblia mkononi, maoni hayo ni sawa tu na ya mtu mwingine ye yote. Hayana faida. Walakini, ikiwa anayosema yametajwa kweli katika Biblia, au ‘Andiko,’ yanapatana na mawazo ya Mungu.

Pili, Yesu alisema: “Ufalme wangu sio wa ulimwengu huu.” (Yohana 18:36) Kwa hiyo, dini ya kweli yenye kutegemea Biblia kama msingi wake inakuwa haimo katika siasa za ulimwengu. Haiungi mkono wala haipingi taifa lo lote, jamii ya watu, mfumo wa kisiasa wala mpango wo wote wa kiuchumi. Wakristo wanaendeleza mbele ufalme wa Mungu, si “ufalme” fulani wa ulimwengu huu. Mkristo hapaswi kujiunga upande wo wote wa magomvi ya kisiasa ya ulimwengu huu kama vile Yesu hakujiunga na mabishano yaliyokuwa yakizidi kuharibika kati ya Wayahudi na Warumi wa siku zake.​—Marko 12:17.

Kama Wakristo leo, Yesu aliwapa msaada wa kimwili wagonjwa na wenye mahitaji wakati alipoweza kufanya hivyo. Lakini yeye hakujiingiza katika siasa. Kazi yake kubwa ilikuwa kuhubiri “habari njema ya ufalme.” (Mathayo 9:35) Kuhubiri hizi hizi “habari njema” ndiyo njia bora zaidi ambayo Mkristo anaweza kusaidia jirani yake kwa sababu ya hali zenye magumu leo za ulimwengu.

Kwa sababu gani kufanya hivyo ni bora kuliko kuingia katika siasa? Kwa sababu, kama atakavyokubali mtu ye yote anayefuata mambo kama yalivyo kikweli, matatizo ya wanadamu hayatatatuliwa kikamili hata siku moja kwa kuchukua hatua ya kisiasa, hata wanasiasa fulani wafanye jitihada gani zenye bidii na unyofu wa moyo. Mamlaka yenye nguvu zipitazo za kibinadamu ndiyo inayoweza kumaliza umaskini, magonjwa, ufisadi na mabaya mengine yote yanayotusumbua. Nayo Biblia inaeleza kwamba jambo hilo litaweza kutimizwa na Mungu peke yake kupitia ufalme wake, serikali yake ya kimbingu ambayo mfalme wake ni Yesu Kristo.​—Yeremia 10:23; Danieli 2:44.

Kwa hiyo, agizo ambalo Yesu aliwapa wafuasi wake halikuwa la kujaribu kuvuta wanasiasa wa ulimwengu kwa maoni yao, bali kufanya wanafunzi, nao wanafanya hivyo leo kwa kuhubiri “habari njema hizi za ufalme” katika dunia yote inayokaliwa na watu. (Mathayo 24:14, NW) Wanapaswa kujulisha wanadamu sababu itakayofanya ufalme huo uondoe mikazo, na namna tunajua jambo hilo liko karibu sana sasa. Kazi yao ni kueleza wengine habari za baraka zitakazomiminika kutokana na ufalme huo sasa na wakati ujao, na wanapaswa kusaidia watu wawe wanafunzi wa Yesu Kristo. Watu wakiwa wanafunzi wataweza kuzishiriki baraka hizo.​—Mathayo 28:19, 20; 1 Timotheo 4:8; Ufunuo 21:3, 4.

Ujumbe huu ndio wenye thamani kubwa zaidi kwa wale wanaoukubali. Unajibu maulizo yao yanayowafadhaisha zaidi. Unaondoa mashaka yao, unawasaidia waiweze mikazo inayowazunguka kwa sasa na kwa hiyo inawaonyesha namna ya kupata “amani ya Mungu, ipitayo akili zote.”​—Wafilipi 4:6, 7.

Je! Hii Inatosha?

Wengine wanaelekea kuwa na maoni ya kwamba hiyo haitoshi. Mhudumu wa kidini mwenye bidii katika siasa katika nchi moja ya Magharibi inayozidi kuwa na maoni ya kutokutaka maoni ya kidini na kuzidiwa na uasherati alisema: “Lazima Wakristo wawe na nia ya kuwa wakali kwa kujaribu kuingilia mambo ya ulimwengu . . . au sivyo tumekwisha.” Lakini je! Ukristo utashindwa nguvu wenye kujiita Wakristo wasipojiingiza katika mambo ya kisiasa?

Wamisionari wengine katika nchi maskini wanaona kwamba kuhubiri “habari njema” hakutoshi. Wanaamini kwamba watu wanahitaji kupewa msaada sasa. Kwa hiyo, wao wanashiriki katika jitihada za kimapinduzi. Lakini kwa uhakika jitihada zo zote za kujaribu kupindua serikali zilizosimamishwa ni kwenda kinyume cha shauri hili la Biblia: “Kila mtu na aitii mamlaka iliyo kuu.” (Warumi 13:1) Vilevile ni kinyume kabisa cha mwenendo wa Yesu na wafuasi wake wa kwanza kabisa, ambao ‘hawakuwa wa ulimwengu.’ (Yohana 17:16) Kufanya hivyo kunaongeza mikazo tu.

Yesu aliwaahidi hivi wafuasi wake wa kweli: “Tazama! mimi nipo pamoja na ninyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 28:20, NW) Wakati wa karne ya kwanza baada ya kifo cha Yesu, wenye kujiita Wakristo waliiamini ahadi hiyo. Walijitenga na siasa. Na, ingawa waliteswa na kuzungukwa na watu wasioamini, imani ya Kikristo iliokoka ikaendelea kuwapo.

Leo, Yesu yungali pamoja na wafuasi wake. Yeye bado anaweza kuhifadhi Ukristo wa kweli bila ya Wakristo kujiingiza katika siasa. Naye atatimiza kusudi la Mungu la kugeuza dunia iwe paradiso yenye kujawa na watu wenye furaha, wasio na mikazo, ijapokuwa leo watu wengi wanaona kwamba wao ndio wanaopaswa kuubadili ulimwengu.​—Danieli 2:44; Ufunuo 21:4.

Lakini je! “habari njema” zinawatosha watu maskini wa ulimwengu? Mmoja wa Mashahidi wa Yehova aliyekuwa misionari miaka kadha katika Mashariki ya Mbali alisema:

“Ni kweli kwamba mara nyingi tulihuzunishwa na umaskini tuliouona. Lakini kungalikuwa na msaada gani kama tungaliwatia maskini moyo wafanye uasi? Ni nani angaliweza kuhakikishia watu kabisa kwamba serikali ambayo ingalifuata ingalifanya mambo yawe nafuu?

“Kwa hiyo sisi tulivuta fikira za watu kuzielekeza kwenye serikali ambayo tulijua ingeleta nafuu, yaani, ufalme wa Mungu. Na wakati maskini hao walipozikubali habari njema juu ya ufalme huo, walijihisi wakiwa na uhusiano mpya pamoja na Mungu. Walijisikia kwamba yeye aliwajali kweli kweli na wakaona namna alivyowasaidia nyakati za hatari kubwa-kubwa katika maisha zao. Jambo hilo lilifanya wajiheshimu na wakapata uhakika juu ya wakati ujao.”

Mwingine wa Mashahidi wa Yehova, aliyetumia miaka mingi akizihubiri ‘habari njema za ufalme’ katika Amerika ya Kati, alikubaliana na maoni hayo. Aliongezea hivi: “Maskini waliozikubali ‘habari njema’ waliacha mambo ya ushirikina na maovu yao ya zamani, kama vile kuvuta tumbako, kucheza kamari, kulewa na kutafuna tambuu; na mara nyingi hali zao za kimwili zilipata maendeleo kwa sababu walitumia mali zao vizuri zaidi. Na walipoendelea kuweka mambo ya kiroho kwanza katika maisha zao, umaskini wao wa kimwili ulizidi kuacha kuwalemea. Hawakuonea matajiri wivu tena, kwa sababu walijua walikuwa na kitu wasichokuwa nacho matajiri wengi.”

Ndiyo, ni jambo la asili ya mwanadamu kuhangaika kwa sababu ya ukosefu wa kumcha Mungu, kwa sababu ya uonezi unaoenea na mabaya mengine ya huu mfumo wa mambo. Kuendelea kuwapo kwa matatizo haya kunaonyesha wanadamu wanahitaji kwa haraka ufalme wa Mungu. Huo tu ndilo tumaini ambalo mtu ye yote analo la kuweza kuona wakati ujao wenye furaha, na dini ya Kikristo iliyo ya kweli tu, ambayo msingi wake ni Biblia, ndiyo inayosaidia watu kuuamini ufalme huo. Kwa kufanya hivyo, inawapa watu msaada bora zaidi uwezao kupatikana katika kupunguza mikazo ya kisasa.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Wanadini fulani wanataka kuona nchi yao ikiwa na “jeshi lenye nguvu zaidi ya lo lote lililopata kuwako tangu wakati wa Uumbaji”

[Blabu katika ukurasa wa 9]

“Sisi tulivuta fikira za watu kuzielekeza kwenye serikali ambayo tulijua ingeleta nafuu, yaani, ufalme wa Mungu”​—MISIONARI

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yesu alifundisha wafuasi wake wafanye wanafunzi, si kujaribu kuvuta watu katika mambo ya kisiasa

[Picha katika ukurasa wa 8]

Ujumbe wa Biblia unasaidia watu waweze kushinda hatari kubwa-kubwa zinazotukia katika maisha zao

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki