Makanisa Yanajiingiza
“WAKATI umefika kwa watu wa Mungu kujiingiza katika serikali.” Hayo yalisemwa na mchungaji wa California. Je! unakubaliana naye, kwamba wanadini wanapaswa wahusike katika siasa? Wengi wanafanya hivyo, kwa maana wanakatishwa tamaa na kuharibika kwa viwango vya adili, kuongezeka kwa uhalifu, kuharibika kwa hali ya uchumi, misuko-suko ya kimataifa, umaskini na kufa njaa kwa watu na ukosefu wa imani unaoenea ulimwenguni kote.
Ni kweli kwamba mengi ya matatizo haya yameletwa na serikali. Hata hivyo mara nyingi serikali zinakuwa hazina la kufanya. Kuongezea hilo, nyingi zinakuwa na kasoro ya kuwa na matendo yenye sifa mbaya. Ripoti za ufisadi na udanganyifu zimefanya watu wapunguze matumaini yao katika serikali mpaka wengi wakafikia hatua ya kukubaliana na mama wa makamo aliyesema: “Mimi ninaanza kufikiri mfumo mzima wa kisiasa umekuwa mfisadi na usiofuata adili.”
Kwa hiyo, watu wengi wanyofu moyoni wanaona kwamba dini inapasa ijaribu kusaidia. Wanaona kwamba dini inawakilisha Mungu, na wanaamini—na hapo wanasema kweli—kwamba ujuzi unaozidi wa kibinadamu unahitaji kutatua matatizo ya mwanadamu. Wanasali kuomba msaada, lakini hawana uhakika Mungu atawasaidiaje. Wanaona kwamba labda ni juu yao kuchukua hatua. Kwa hiyo, wanataka kuona wale wanaoitwa “watu wa Mungu” wakijiingiza katika siasa ili kuingiza hali ya “uungu” ndani ya serikali. Wahudumu (maminista wa kidini), mapadri na watu mmoja mmoja wenye kufuata dini wanazidi kujitia kwa bidii katika siasa.
Je! hiyo ndiyo njia bora zaidi ambayo dini inaweza kusaidia hali ya mambo leo? Acha tuangalie mambo yanayofanywa na wengine wa wanadini, kisha tuone wanatumainia kutimiza nini.
Dini Katika Siasa
Katika United States (Amerika) dini fulani zinaweka kati ya mji mkuu wa taifa hilo watu wa kujaribu kuwavuta watunga-sheria wafuate mawazo yao. Wanatumainia kutimiza nini? Padri Mkatoliki alieleza hivi: “Tunajisikia kwamba tutaendelea kwa muda mrefu kuongoza maoni ya kiadili yanayoliwekea taifa mwendo wa kufuata katika siasa.” Mhudumu Mprotestanti aliongezea hivi: “Inatupasa tuweze kuiambia serikali hivi: ‘umekosea jambo fulani; umefuata njia isiyofaa.’”
Kwa muda mrefu hali hiyo ya kuvuta maamuzi ya wakuu wa kiserikali kwa busara imeendelea kuwapo. Hivi karibuni zaidi kumetokea vikundi visivyo na busara nyingi. Hivyo vimekuwa vikitetea mapendezi ya kipekee ya watu, navyo vimeanzishwa na Waprotestanti wenye kushikilia sana mawazo ya kidini wasiyotaka yabadilishwe. Vikundi hivyo, kama kile kinachoitwa “Moral Majority” katika United States, vimelaani vikali mambo kama kuungwa mkono kwa Israeli, kuruhusiwa kwa haki za wanaume wenye kulalana na wanaume wenzao na wanawake wa namna hiyo pia, kuungwa mkono kwa mkataba wa Mfereji Mkubwa wa Panama, usalama wa Taiwan na utoaji wa mimba. Wanasiasa wamepata somo la kutokudhani vikundi hivyo havina mavutano yenye nguvu. Maseneta waliounga mkono programu zisizopendwa na vikundi hivyo wamepigiwa kura za kuwaondoa katika vyeo vyao.
Baraza ya Ulimwengu ya Makanisa, ambayo makao makuu yake yako Ulaya, ilihusika katika siasa kwa njia nyingine. Tangu mwaka wa 1970, Baraza hiyo imeripotiwa kuwa imetoa msaada wa dola milioni tatu za Amerika kusaidia vyama mbalimbali vyenye kutaka mapinduzi ya kisiasa.
Tena, wahuduma wengine walioagizwa rasmi wanatafuta kuchaguliwa wapate cheo serikalini. Walakini, kichwa cha hivi majuzi kilichokuwa kwenye gazeti kilionyesha lile linaloweza kuwa ni lengo lao katika kujiingiza siasani: “Mapadri Wafilipino waziacha sehemu zao za uchungaji kujiunga na uasi.” Makala hiyo ilieleza habari za mapadri wanne Wakatoliki waliojiunga na chama cha waviziaji Wakomunisti wenye kufanya vita. Kuhusika kwa bidii hiyo katika vyama vyenye kutaka mapinduzi ni jambo lililoenea sana, bali hasara kubwa sana imepatikana. Katika Latini Amerika matokeo yamekuwa yenye mauaji, kutoroshwa au kuhamishwa kwa mapadri wanaokadiriwa kuwa 850, kutia ndani watawa wa kike na wanakanisa wa kawaida muda wa kumi moja la miaka iliyopita.
Wewe una maoni gani juu ya utendaji huo wa kisiasa wa viongozi wa kidini? Je! wewe ungeushangilia? Au una mashaka? Labda wewe huoni ubaya wa dini kutoa maoni yazo kwa busara juu ya masuala ya kisiasa lakini unajisikia vibaya kuona mapadri wakiunga mkono mambo ya mapinduzi.
Hata hivyo, tukikubaliana na hatua yo yote ya kujiingiza kwa dini katika siasa, ni vigumu kusema ni wapi zisipopaswa kuhusika. Ikiwa inakubalika wahudumu wengine walioagizwa rasmi wajaribu kufanya rasilmali ya taifa itumiwe kwa programu wanazoona ni nzuri, kwa sababu gani ni vibaya kwa Waprotestanti wenye kushikilia sana mawazo yao wasimamie vikundi vya taifa zima vya kukaza watu wafuate programu ambazo ni za maana kwa vikundi hivyo? Pia, ikiwa kile kikundi kinachoitwa “Moral Majority” kinaweza kutoa sauti ya kutetea Israeli, kwa sababu gani Baraza ya Ulimwengu ya Makanisa isiweze kuchanga pesa za matumizi ya kijeshi ambayo wao wanayapendelea? Na ikiwa hilo si kosa, kwa sababu gani mapadri Wakatoliki wakatazwe kupigana na kufa kwa ajili ya mambo wanayounga mkono katika Amerika ya Kusini na Asia, na badala yake isemwe ingewapasa kuwalipa watu wengine pesa za kujitia katika hatari hizo?
Je! unaona kwamba kuna jambo fulani lisilofaa katika namna hizo za kuwaza? Je! kweli hiyo ndiyo njia iliyo bora zaidi ya dini kuwasaidia wanadamu hizi siku zenye magumu?
Si jambo jipya kwa dini kujaribu kuongoza siasa. Katika orodha inayotangulia zimepangwa pindi zinazojulikana sana wakati dini na siasa zilipochangamana.
[Sanduku katika ukurasa wa 4]
◻ Mwaka wa 1095 Papa Urban wa Pili: alipeleka ombi la kuambia majeshi ya Magharibi ‘yaende yakasaidie ndugu zao katika Mashariki ya Kikristo’ kwa kupigana na Waturuki. Jambo hilo lilitokeza Vita ya Kidini ya kwanza na kundi la Wapigania imani. Kwa sababu hiyo damu nyingi sana ilimwagwa muda wa karne mbili.
◻ Katika karne ya 12 Papa Adrian wa Nne alimpa kwa njia rasmi Henry wa Pili, mfalme Mwingereza, nchi ya Irelandi. Kwa njia hiyo alihalalisha (kulingana na maoni ya waaminifu) kutekwa kwa nchi hiyo na Waingereza.
◻ Mwaka wa 1524 wakulima katika Ujeremani walifanya maasi. Kwa kadiri fulani walifanya hivyo kwa kuitikia mafundisho ya Martin Luther. Ingawa hapo kwanza Luther alipendelea shughuli ya wakulima hao, mwaka wa 1525 yeye alipendekeza kwamba wana-wafalme wo Ujeremani wasage-sage “Makundi ya Wakulima Wanyakuaji na Wauaji.” Wana-wafalme walifuata shauri lake kwa kufanya ukatili mkubwa.
◻ Mwaka wa 1618 jitihada za mfalme-mkusudiwa wa Bohemia za kulazimisha watu wafuate Ukatoliki katika eneo kubwa sana la Waprotestanti zilishiriki kutokeza ile Vita ya Miaka Thelathini.
◻ Mwaka wa 1918 makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yalitumia uvutano wayo kuunga mkono Ushirika wa Mataifa. Lakini hayakufanikiwa. Baada ya makumi mawili tu ya miaka ulimwengu uliingizwa katika vita iliyo mbaya kupita vita vyote vya historia ya kibinadamu. Sasa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yameunga mkono Umoja wa Mataifa, lakini sasa ndio wakati ambao mataifa yana silaha nyingi zaidi na yamekosa umoja zaidi ya wakati wo wote uliotangulia.