Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 8/1 kur. 4-7
  • Je! Dini na Siasa—Zimo Katika Mwendo wa Kugongana?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Dini na Siasa—Zimo Katika Mwendo wa Kugongana?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ukristo wa Kweli—Ni Tofauti
  • Kuwa Rafiki wa Ulimwengu
  • Dini na Vita
  • Kuvuna Kimbunga
  • Je, Dini Inapaswa Kujihusisha Katika Siasa?
    Habari Zaidi
  • Sababu kwa Nini Dini ya Kilimwengu Itaisha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Je, Makasisi Wanapaswa Kujiingiza Katika Siasa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Mwisho Wa Dini Ya Uwongo Unakaribia!
    Mwisho Wa Dini Ya Uwongo Unakaribia!
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 8/1 kur. 4-7

Je! Dini na Siasa—Zimo Katika Mwendo wa Kugongana?

MWONGOZO wa kuunganisha mamlaka ya kisiasa na kidini katika mtu mmoja haukuanza na Henri wa Nane. Katika siku zake hiyo tayari ilikuwa shughuli ya kisiasa iliyokuwa imekusudiwa kuendeleza umoja wa kitaifa.

Kwa mfano, milki ya kale ya Misri ilikuwa na miungu mingi. “Farao mwenyewe alikuwa mmoja wa miungu hiyo, na mtu mashuhuri katika maisha za raia zake,” inasema The New Bible Dictionary. Vivyo hivyo Milki ya Kiroma ilikuwa na mahekalu yenye mchanganyiko wa miungu yote, kutia ndani watawala wenyewe wa milki hiyo. Mwanahistoria mmoja anaeleza ibada waliyopewa watawala kuwa “kani yenye nguvu zaidi katika dini ya ulimwengu wa Kiroma.”

Lakini ijapokuwa miungano ya Kanisa na Serikali imekuwapo muda wa karne nyingi, hatua ambazo Jumuiya ya Wakristo imechukua wakati wa kisasa kuingia katika siasa zimeiweka katika mwendo wa kugongana na wale ambao inawashawishi ili ipate upendeleo wao. Kwa nini? Ili kujibu ulizo hilo, acheni sasa tuangalie jinsi Jumuiya ya Wakristo ilivyohusika katika siasa hapo mwanzo.

Ukristo wa Kweli—Ni Tofauti

Yesu Kristo, mwanzilishi wa Ukristo, alikataa mamlaka yote ya kisiasa. Angalau pindi moja watu waliposisimuliwa na miujiza yake, walijaribu kumlazimisha awe mfalme lakini yeye “akajitenga, akaenda tena mlimani yeye peke yake.” (Yohana 6:15) Alipoulizwa na Gavana Mroma kama yeye ni mfalme, Yesu alijibu: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungalikuwa sehemu ya ulimwengu huu, wahudumu wangu wangalikuwa wamepiga vita kwamba nisitolewe nipewe kwa Wayahudi.”​—Yohana 18:36, Biblia ya New World Translation.

Halafu tena Kristo aliambia wanafunzi wake hivi: “Kwa sababu ninyi si sehemu ya ulimwengu, bali mimi nimewachagua katika ulimwengu, kwa sababu hii ulimwengu unawachukia ninyi.” (Yohana 15:19, Biblia ya New World Translation) Kwa hiyo, matatizo ya kijamii au ya kisiasa hayakukengeua Wakristo wa kwanza. Kwa mfano, wakati huo kulikuwa na tatizo kubwa la kufanya watu watumwa, lakini Wakristo hawakufanya shughuli ya kisiasa waukomeshe. Bali, watumwa Wakristo waliamriwa watii bwana zao.​—Wakolosai 3:22.

Badala ya kujiingiza-ingiza katika siasa, Wakristo hao wa kwanza walijitayarisha kuanza kufanya kazi ya kuhubiri juu ya “ufalme wa Mungu.” (Matendo 28:23) Katika muda wa makumi machache tu ya miaka, ujumbe wao ulifikia vikomo vya ulimwengu uliojulikana wakati huo. (Wakolosai 1:23) Nayo matokeo yakawa nini? Maelfu ya watu waliitikia wakawa ‘ndugu na dada’ za kiroho. (Mathayo 23:8, 9) Wayahudi na Mataifa ambao wakawa Wakristo waliacha hali zao za uadui. Kati ya Wayahudi na Wasamaria hata tofauti zilizokuwa kati yao zilimalizika kwa sababu ya “juhudi nyingi katika kupendana” kwa Wakristo.​—1 Petro 4:8.

Lakini, upendo wa Kikristo ulienea ukafikia hata adui zao. (Mathayo 5:44) Basi wao walikataa kujiunga na majeshi ya Kaisari. ‘Lakini,’ huenda wengine wakakataa wakisema, ‘je, Yesu hakusema “Mlipeni Kaisari yaliyo ya Kaisari?” ‘ Ni kweli. Lakini, je, Yesu alikuwa akiongea juu ya utumishi wa kijeshi? Hapana, alikuwa akiongea tu juu ya suala la kama inafaa au haifai ‘kumlipa Kaisari kodi.’ (Mathayo 22:15-21) Kwa hiyo Wakristo walilipa kodi zao. Lakini waliona maisha zao kuwa zinawekwa wakfu kwa Mungu na wakakataa kuumiza wanadamu wenzao.

Kuwa Rafiki wa Ulimwengu

‘Lakini ebu tazama Jumuiya ya Wakristo leo,’ huenda wengine wakasema. ‘Imegawanyika kwa njia isiyoweza kutengenezwa, washiriki wayo wanachinjana mara nyingi, viongozi wake wa kidini wamejihusisha sana na siasa. Ni jambo gani limepata Ukristo?’ Yesu alionya kwamba Wakristo wa uongo ‘wangepandwa’ kati ya Wakristo wa kweli. (Mathayo 13:24-30) Vivyo hivyo Paulo alitoa unabii huu: “Najua mimi ya kuwa . . . mbwa-mwitu wakali wataingia kwenu . . . [tena] watainuka watu, wakisema mapotovu, wawavute hao wanafunzi wawaandamie wao.”​—Matendo 20:29, 30.

Hata katika karne ya kwanza maelekeo hayo yalikuwa yameanza. Mwanafunzi Yakobo aliona uhitaji mkubwa kabisa wa kuandika maneno haya yenye mkazo: “Ninyi ni watu wasio waaminifu sawa na wake wazinzi; ninyi hamjui kwamba kufanya ulimwengu rafiki yenu ni kufanya Mungu adui yenu?” (Yakobo 4:4, The Jerusalem Bible; italiki ni zetu.) Watu wengi walichagua kupuuza shauri hilo la kimungu. Ndivyo ilivyokuwa sana hivi kwamba katika karne ya nne mbwa-mwitu akiwa katika mavazi ya kondoo, Mfalme Konstantino, akaweza kuzidi kuchafua “Ukristo” kwa kuufanya uwe dini rasmi ya Milki ya Kiroma. Lakini kwa kuwa ‘rafiki ya ulimwengu,’ Jumuiya ya Wakristo ikawa adui ya Mungu. Ikawa haiepukiki kuje kuwa na mgongano mwishowe.

Kufikia karne ya 13 Kanisa, lenye kutawalwa na “papa” wake, au “baba,” lilikuwa limeingia katika “kilele” cha mamlaka yalo,” hiyo ikatayarisha njia ya kuwa na ndoa ya karibu zaidi kati ya Kanisa na Serikali. Papa Innocent wa Tatu akasadiki kwamba “Bwana alimpa Petro utawala, si wa lile Kanisa Lenye Kuenea Kote tu, bali pia utawala wa ulimwengu mzima.” (Italiki ni zetu.) Profesa wa historia T. F. Tout, anaendelea kusema hivi katika kichapo The Empire and the Papacy: “Kazi ya Innocent ilikuwa ile ya mtawala wa taifa aliye mwanadini, . . . akiweka-weka na kuondoa-ondoa wafalme kulingana na mapenzi yake.” Lakini mwandikaji uyo huyo anaongezea hivi: “Kadiri mamlaka ya papa ilivyozidi kuwa ya kisiasa, ndivyo ilivyozidi kuwa vigumu kuunga mkono fahari ya mamlaka hiyo kuwa ndiyo chanzo cha sheria, cha maadili, cha dini.”

Dini na Vita

Vita ni siasa za kadiri iliyo na jeuri zaidi. Lakini Papa Innocent wa Tatu mwenyewe alipanga shughuli ya kijeshi ya kupinga Waalbigense wa kusini ya Ufaransa. Jambo hilo lilileta machinjo mabaya sana ya maelfu ya watu huko Beziers mwaka wa 1209, na kuteketezwa kwa watu wengi sana na lile Baraza Takatifu la Kukomesha Wazushi wa Kidini. Shughuli takatifu, ambayo hapo kwanza ilikusudiwa kwa Palestina, ilipotoshwa kwa ujanja wa kisiasa ikatia ndani Konstantinopo. Wakiwa huko, askari mashuhuri “wa Kikristo” walihusika katika “siku tatu zenye maovu za kuteka nyara, kuua, kuonyesha tamaa chafu, na kutenda mambo yasiyo matakatifu kwa njia mbaya sana.” Juu ya nani? Juu ya “Wakristo” wenzao! Mwanahistoria mmoja anasema: “Makanisa yenyewe yalinyang’anywa vitu vyayo bila huruma.”

Mwishowe njia zisizofuata mfano wa Kristo zenye kufuatwa na Kanisa zilifanya Martin Lutheri apigilie kwa misumari sababu zake za upinzani kwenye mlango wa kanisa la ngomeni huko Wittenberg mwaka wa 1517—na hapo ndipo ukaanza ule Urekebishaji wa Kidini. Lakini, anasema H. A. L. Fisher, katika kichapo History of Europe: “Imani mpya za kidini. . . zilitegemea sana upendeleo wa mfalme na serikali.” Ujeremani ukagawanyika ukawa na upande wa kisiasa na wa kidini.” Katika Ufaransa, wafuasi wa Kalvin walichangamana pia na viongozi wa kisiasa. Basi vita vya kidini vilivyofuata vilipigwa si kwa ajili ya uhuru wa kidini tu, bali pia kwa sababu ya “wakuu Waprotestanti na wa Katoliki ya Roma kushindania uongozi katika Kiti cha Kifalme.” Ndivyo historia ya dini katika Ulaya imeandikwa kwa damu!

Karne ya 20 ilipoanza Briton na Boer walikuwa waking’ang’ana mashindanoni katika Afrika ya Kusini. Viongozi wa kidini pande zote mbili walichochea moto kwa kutoa “vitia-moyo kwenye jukwaa la kanisa.” Anasema hivi mwanahistoria R. Kruger: “Ingawa ni maombi mengi yaliyopelekwa mbinguni na kila upande wakati wa vita, wingi huo ulikuwa sawa tu na uchochezi ambao kila dhehebu lilifanya.” “Wakristo” weupe walichinjana huku wakimwomba Mungu awasaidie kufanya hivyo!

Kiolezo hicho kilirudiwa kwa kadiri kubwa sana mwaka wa 1914 wakati askari Wajeremani walipoingia Ubelgiji wakiwa wamevaa mishipi iliyoandikwa maneno “Gott mit uns” (Mungu pamoja nasi). Pande zote mbili Kanisa lilitoa sala kwa wingi likiomba ushindi nalo likawa likitupia adui matukano makali.

Watu wengi waliona wazi unafiki wa dini kwa kujitia katika Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Wakiwa wanaiita dini “kasumba ya watu,” wasioamini kuwako kwa Mungu na wakomunisti waliongezeka. Hata hivyo, viongozi wa kidini waliendelea kuhusika katika siasa, wakiunga mkono watawala wa kimabavu wa ufashisti kama vile Mussolini na Franco. Mwaka wa 1933 Kanisa Katoliki la Roma hata lilifanya mapatano pamoja na Wanazi. Kardinali Faulhaber alimwandikia Hitler hivi: “Mapatano haya yaliyofanywa pamoja na makao ya Papa . . . ni tendo hodari la baraka zisizolinganika . . . Mungu na amhifadhi [Hitler] Kiongozi wa Serikali.”

Hata uwezekano wa kutokea vita nyingine ya ulimwengu haujavuta viongozi wa kidini waache siasa. Elekeo moja la makanisa wakati wa karibuni limekuwa ni kwenda upande wa kisiasa unaotaka mapinduzi. Mwandikaji mmoja anasema: “Kizazi cha karibuni zaidi cha walimu wa kidini kutoka Latini Amerika . . . kinasisitiza kwamba mawazo ya Marx ndiyo wonyesho wa kisiasa usioepukika wa Ukristo.” Lakini Biblia inaonya hivi: “Wanapanda upepo, watavuna kimbunga.”​—Hosea 8:7, JB.

Kuvuna Kimbunga

Ndiyo, Biblia inatoa onyo zito: Mgongano mbaya sana kati ya dini na siasa unakuja. Katika Ufunuo sura ya 17, Biblia inaonyesha milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo kuwa imetiwa madoa ya damu mfano wa “kahaba mkuu aketiye juu ya maji mengi.” “Maji” hayo yanafananisha ‘jamaa na mataifa.’ (Mistari 1, 15) Kahaba huyo anaitwa “BABELI MKUU, MAMA WA MAKAHABA NA MACHUKIZO YA NCHI,” naye “amelewa kwa damu ya watakatifu.” (Mistari 5, 6) “BABELI” ni jina linalofaa dini ya uwongo iliyo katika namna ya tengenezo, kwa kuwa mengi ya mafundisho yake yametokana na mji wa kale wa Babeli.a Imejipatia sifa ya uuaji wa kumwaga damu kwa kutesa Wakristo wa kweli muda wa karne zilizopita.

Milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo inaonyeshwa tena kuwa imepanda mnyama “mwenye vichwa saba na pembe kumi . . . [ambazo zinamaanisha] wafalme kumi.” (Mistari 3, 12) Makala zilizotangulia katika jarida hili zimetambulisha “mnyama” huyo kuwa chombo kile kilichokabidhiwa jukumu la kudumisha amani ya ulimwengu, yaani Umoja wa Mataifa. Makanisa yamejulikana kuwa yakiunga mkono tengenezo hilo. Katika mwezi Oktoba mwaka wa 1965, Papa Paul wa Sita alisimulia Umoja wa Mataifa kuwa “ndilo tumaini la mwisho la upatano na amani.” Mwaka wa 1979, Papa John Paul wa Pili alihutubia Kusanyiko Kuu la Umoja wa Mataifa. Bila kumtaja Kristo wala Ufalme wake hata safari moja, aliutaja Umoja wa Mataifa kuwa “baraza kuu zaidi la amani na haki.”

Lakini kwa nini muungano huo wa dini na Umoja wa Mataifa ni hatari sana? Kwa sababu “zile pembe kumi . . . na huyo mnyama, hao watamchukia yule kahaba, nao watamfanya kuwa mkiwa na uchi. . . na watamteketeza kabisa kwa moto.” (Mstari wa 16) Basi dini ya uwongo inaelekea kwenye mgongano wenye msiba pamoja na siasa. Kwa kufunuliwa uchi wake, na uchafu wake mwingi sana kufunuliwa, itaharibiwa kabisa kabisa.

Jambo hilo litaanzisha “dhiki kubwa” aliyoitaja Yesu, kisha ifikie upeo katika pigano la Har–Magedoni. Kwa kuungwa mkono na vikosi vya kimbingu visivyoshindika, Kristo ‘atauvunja vipande-vipande na kuuharibu’ mfumo wa ulimwenguni pote wa Shetani, aache ‘wapole tu wairithi dunia.’ Hao watakuwa ni Wakristo wa kweli ambao, kati ya mambo mengine mengi, wamejiepusha kabisa na siasa zenye kuleta migawanyiko.​—Mathayo 24:21; Danieli 2:44; Zaburi 37:10, 11; Mathayo 5:5; Ufunuo 6:2; 16:14-16.

Ikiwa wewe ni mmoja anayesumbuka sana moyoni kwa sababu ya taabu na malawama ambayo dini ya uwongo imeletea jina la Mungu, inakupasa ufanye nini sasa? Biblia inaamuru hivi: “Tokeni kwake [yaani, dini ya uwongo], enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake.” (Ufunuo 18:4) Ni Mashahidi wa Yehova peke yao wanaohimiza watu watii amri hiyo. Wao, kama Wakristo wa kwanza, wanajiepusha na vita na siasa na kwa hiyo hawatakuwa kati ya wenye kuelekea uharibifuni wakati dini itakapogongana na siasa. Kwa hiyo wafikie mzungumze. Watafurahi kukuonyesha jinsi ya kuuona ule ‘mlango mwembamba’ unaoongoza si kwenye uharibifu bali kwenye uzima wa milele.​—Mathayo 7:13, 14; Yohana 17:3.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa maelezo mengi, ona kitabu “Babylon the Great Has Fallen!” God’s Kingdom Rules!, kilichochapishwa na Sosaiti yetu.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Mwaka wa 1914, kwenye madhabahu moja ya ngoma katika ngazi za kanisa la Mt. Paulo, Askofu wa London alichochea roho ya uzalendo (kutukuza nchi) katika askari Waingereza

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki