Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 10/15 uku. 23
  • Maswali kutoka kwa Wasomaji

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maswali kutoka kwa Wasomaji
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Habari Zinazolingana
  • Kutenga na Ushirika—Jinsi Kunavyopasa Kuonwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • “Imewapasa Kuwasaidia Wanyonge”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Kudumisha Amani na Usafi wa Kutaniko
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 10/15 uku. 23

Maswali kutoka kwa Wasomaji

◼ Mwanangu, ambaye alibatizwa akiwa tineja (kijana), sasa ameoa na ana jamaa yake. Kwa sababu ya mikazo ya kujitafutia chakula amepoa kiroho naye hashirikiani na kundi. Je! anapaswa achukuliwe kuwa mtu ‘aliyejitenga na ushirika’?

Hakuna jambo lo lote katika maelezo yako linaloonyesha kwamba angepaswa kuchukuliwa hivyo. Labda ulizo hilo limetokea kwa sababu ya kutokufahamu vizuri maana ya kuchukuliwa (kuonwa) kuwa mtu ‘aliyejitenga na ushirika.’

Mnara wa Mlinzi wa Januari 1, 1982, kurasa 14 na 15, ulionyesha kwamba kuna tofauti kati ya (a) Mkristo anayekuwa dhaifu kiroho na asiye mtendaji, na (b) mtu anayetangaza waziwazi kwamba yeye si mmoja wa Mashahidi wa Yehova tena, kisha wazee wa kundi wanatangaza kwamba yeye ‘amejitenga mwenyewe na ushirika.’ Inaonekana kwamba mwana wako anahusika katika maelezo yale ya kwanza.

Huo Mnara wa Mlinzi ulitaja kwamba Wakristo wengine wanakuwa dhaifu katika imani na hali ya kiroho. Jambo hilo lilitukia katika karne ya kwanza pia. (Warumi 14:1, 2; 1 Wakriontho 11:30) Hiyo si kusema wameacha kuwa Wakristo. Hata wakiwa dhaifu sana kiasi cha kuacha kushiriki kueleza watu wale wengine “habari njema” na kuacha kuhudhuria mikutano, nao hawaleti lawama juu ya kundi la Kikristo, bado wanapaswa kuchukuliwa kuwa ndugu na dada zetu wa kiroho. Inatupasa tuwasaidie kwa upendo, kupatana na shauri hili la mtume Paulo: “Ndugu, twawasihi, waonyeni wale wasiokaa kwa utaratibu; watieni moyo walio dhaifu; watieni nguvu wanyonge; vumilieni na watu wote.” Ingawa mara nyingi wazee ndio wanaoongoza katika kufanya hivyo, inapasa kuangaliwa kwamba shauri hili lilielekezwa kwa ‘kundi lote la Wathesalonike.’ (1 Wathesalonike 1:1; 5:14) Kwa hiyo wazee na watu wengine wanaweza kutoa msaada wenye upendo na kipa-moyo, wakiyakumbuka maoni haya yenye msaada: “Inyosheni mikono iliyolegea na magoti yaliyopooza, mkaifanyie miguu yenu njia za kunyoka, ili kitu kilicho kiwete kisipotoshwe, bali afadhali kiponywe.”​—Waebrania 12:12, 13; Ufunuo 3:1-3.

Hiyo ni tofauti sana na kisa cha mtu aliyekuwa Mkristo zamani ambaye ‘amejitenga na ushirika.’ Maneno hayo ya kujitenga na ushirika yanatumiwa hasa katika hali mbili:

Ingawa si tukio la kawaida, kwanza huenda mtu akaamua kwamba hataki kamwe kamwe kuwa Shahidi tena. Hatumaanishi mtu wa namna iliyotangulia kuelezwa, Mkristo dhaifu kiroho au aliyevunjika moyo na ambaye huenda akaonyesha mashaka fulani. Hapana, tunamaanisha mtu anayekata kauli kwa kujikaza akisema kwamba yeye si mmoja wa Mashahidi wa Yehova tena. Kwa kuwa hapo kwanza alijitolea mwenyewe awe mshiriki wa kundi, sasa ingemfaa alipashe kundi habari za kwamba yeye anamalizia hapo uhusiano wake na kundi. Ingefaa zaidi afanye hivyo kwa kuandikia wazee barua fupi, lakini hata akitumia mdomo kutangaza waziwazi kabisa kwamba anakomeshea hapo msimamo wake wa kuwa Shahidi, wazee wanaweza kushughulika na shauri hilo.​—1 Yohana 2:19.

Hali ile ya pili inahusu mtu anayekana msimamo wake kundini kwa kujiunga na tengenezo la kilimwengu lenye kusudi lililo kinyume cha shauri kama lile linalopatikana kwenye Isaya 2:4, ambako tunasoma hivi juu ya watumishi wa Mungu: “Watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.” Pia, kama vile inavyosemwa kwenye Yohana 17:16, NW “wao si sehemu ya ule ulimwengu, sawasawa na vile mimi [Yesu] nisivyo sehemu ya ule ulimwengu.”​—Linganisha Ufunuo 19:17-21.

Katika yo yote ya hali mbili hizo, mtu huyo kwa maneno na/au kwa matendo amekomesha waziwazi cheo chake cha kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, akajitenga mwenyewe na ushirika. Kwa hiyo, wazee watalitangazia kundi kwa ufupi kwamba mtu huyo amejitenga mwenyewe na ushirika. Wale waliomo kundini wataukubali uamuzi wa mtu huyo na baada ya hayo wamchukue yeye kuwa mtu ambaye zamani alikuwa ndugu, na sasa hawawezi kushirikiana naye, kupatana na yale tunayosoma kwenye 1 Wakorintho 5:11 na 2 Yohana 9-11.

Kama inavyofahamika, mwana aliye dhaifu kiroho, asiye mtendaji, ambaye ulizo hili limeulizwa kwa habari yake hajawa mtu ‘aliyejitenga mwenyewe na ushirika’ katika yo yote ya maana mbili hizo wala hakuna tangazo lililofanywa kundini. Kwa hiyo labda inawezekana bado kumsaidia kwa kuifuata roho ya Warumi 15:1: “Basi imetupasa sisi tulio na nguvu kuuchukua udhaifu wao wasio na nguvu.”​—Angalia pia Isaya 35:3.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki