Maswali Kutoka kwa Wasomaji
◼ Inafaa kundi litende namna gani ikiwa mtu fulani anaiacha imani ya kweli ya Kikristo na kujiunga na dini nyingine?
Jambo kama hilo lilitukia nyakati nyingine katika karne ya kwanza. Hivyo, ni jambo lenye kueleweka kwamba leo kunaweza kuwa na tukio kama hilo pindi kwa pindi. Inapokuwa hivyo, kundi linachukua hatua kwa kufaa ili kulinda usafi wa kiroho wa Wakristo washikamanifu walio humo.
Kamusi moja inaeleza uasi-imani kuwa ni “mtu kukana dini yake, kanuni, chama cha kisiasa, n.k.” Nyingine inasema hivi: “Uasi-imani . . . 1 : kukana imani ya kidini 2 : kuacha ushikamanifu wa hapo kwanza.” Kwa hiyo, Yuda Iskariote alikuwa na hatia ya namna fulani ya uasi-imani wakati alipoacha ibada ya Yehova Mungu kwa kumsaliti Yesu. Baadaye, wengine wakawa waasi-imani kwa kuacha imani ya kweli hata wakati ule ambao mtume Yohana na wanafunzi wengine wa kwanza walipokuwa wangali hai. Yohana aliandika hivi: “Walitoka kwetu, lakini hawakuwa wa kwetu. Maana kama wangalikuwa wa kwetu, wangalikaa pamoja nasi.”—1 Yohana 2:19
Ni jambo gani linalopasa kufanywa kukiwa na tukio la namna hiyo leo? Wazee, au wachungaji, wa kundi huenda wakapata habari juu ya Mkristo aliyebatizwa ambaye ameacha kushirikiana na watu wa Yehova na ambaye inaonekana wazi amekuwa mwenye kushirikiana na dini nyingine. Kupatana na maneno ya Yesu juu ya kuhangaikia kondoo ye yote aliyepotea njia, wachungaji wa kiroho wanapasa wapendezwe kusaidia mtu huyo. (Mathayo 18:12-14; linganisha 1 Yohana 5:16.) Lakini namna gani wachungaji waliochaguliwa wachunguze jambo hilo wakiamua kwamba mtu huyo hataki tena kuwa na uhusiano wo wote na watu wa Yehova na ameamua kubaki katika dini ya uwongo?
Jambo tu ambalo wangefanya ni kutangazia kundi kwamba mtu huyo amejitenga na ushirika na hivyo si mmoja tena wa Mashahidi wa Yehova. Mtu huyo angekuwa ‘ameacha ushikamanifu wake wa hapo kwanza,’ lakini si lazima hatua yo yote rasmi ya kutenga na ushirika ichukuliwe. Kwa sababu gani? Kwa sababu tayari yeye amekwisha kujitenga mwenyewe na kundi. Inaelekea kwamba yeye hajaribu kudumisha njia ya kuwasiliana na wale waliokuwa ndugu zake ili awabembeleze wamfuate yeye. Kwa upande wao, ndugu washikamanifu hawatafuti ushirika pamoja naye, kwa kuwa ‘alitoka kwao, kwa sababu hakuwa wa kwao.’ (1 Yohana 2:19) Mtu huyo aliyejitenga na ushirika ambaye ‘ametoka kwetu’ huenda akaanza kupeleka barua au vitabu vya kuendeleza dini ya uwongo au uasi-imani. Jambo hilo lingekazia kwamba mtu huyo kwa uhakika ‘si wa kwetu.’
Ingawa hivyo, Maandiko yanaonya kwamba wengine wangejaribu kubaki kati ya watu wa Mungu na wakiwa hapo wajaribu kupoteza wengine. Mtume Paulo alishauri hivi: “Katika ninyi wenyewe watainuka watu, wakisema mapotovu, wawavute hao wanafunzi wawaandamie wao.” (Matendo 20:30) Yeye aliwaonya Wakristo kwa kutoboa mambo wazi kwamba ‘wawaangalie wale wafanyao fitina na mambo ya kukwaza kinyume cha mafundisho waliojifunza; wakajiepushe nao.’—Warumi 16:17, 18.
Kwa hiyo ikiwa mtu alipata kuwa mwalimu wa uwongo kati ya Wakristo wa kweli, kama walivyofanya Himenayo na Fileto katika siku za Paulo, wachungaji wa kundi wangelazimika kuchukua hatua za ulinzi. Kama mtu yule angekataa onyo lao la upole linalotolewa kwa upendo na azidi kuendeleza madhehebu, haImashauri fulani ya wazee ingeweza kumtenga na ushirika au kumwondosha nje, kwa sababu ya uasi-imani. (2 Timotheo 2:17; Tito 3:10, 11) Ndugu na dada mmoja mmoja katika kundi wangefuata mwelekezo wa Paulo ‘kuepuka’ yule mwenye kujaribu ‘kufanya fitina’ (‘kusababisha migawanyiko,’ NW) Yohana alishauri kwa njia inayofanana na hiyo: “Ikiwa mtu ye yote anakuja kwenu na haleti fundisho hilo, msimpokee kamwe ndani ya nyumba zenu wala kumpa salamu.”—2 Yohana 10, NW.