Endeleeni “Kuwa Imara katika Imani’
“Usemi ulioongozwa kwa roho wasema kwa hakika kwamba katika vipindi vya baadaye vya wakati wengine watakengeuka waiache imani.”—1 Tim. 4:1, NW.
1. Je! tunapaswa kushtuka isivyofaa mtu fulani akikengeuka aiache imani?
JE! UNASHTUKA sana na kufadhaika isivyofaa unapoona au kusikia juu ya Mkristo unayemjua akishindwa na mashaka, akipoa na pengine hata kuwa mwasi kufikia hatua ya kuliacha kundi la Kikristo na kujaribu kuvuta wengine pamoja naye? Ikiwa ndivyo, unaweza kufarijiwa kujua kwamba, ingawa matukio hayo yanakuwa yenye kusikitisha, Maandiko yanatangulia kutuonya kwamba yatatokea.
2, 3. (a) Neno ‘‘ukafiri’’ linamaanisha nini, naye kafiri wa kwanza alikuwa nani?(b) Mwendo wa ukafiri ulileta jambo gani juu ya Israeli na Yuda?
2 Neno “ukafiri” latokana na neno la Kigiriki linalomaanisha “kusimama mbali na,” “kukengeuka, kupotoka,” “uasi, kuacha dini.” Wa kwanza kuasi ibada ya kweli ya Yehova alikuwa Shetani Ibilisi. Kwa hiyo ndiye aliyekuwa kafiri wa kwanza. (Yohana 8:44) Aliwafanya wanadamu wawili wa kwanza wawe makafiri. (Mwanzo, sura 3) Mwanzoni kabisa katika historia ya Israeli kulikuwako “ukengeufu” au ‘kupotoka’ katika ibada ya kweli. Twasoma hivi:
“Lakini hawakusikiliza hao waamuzi wao, maana walifanya uasherati kwa kuifuata miungu mingine, wakajiinamisha mbele yao; wakageuka upesi, na kuiacha njia ile waliyoiendea baba zao, waliozitii amri za [Yehova].”—Amu. 2:17.
3 Baadaye, wafalme wengi wa Israeli na Yuda walipata kuwa waasi nao wakayaongoza mataifa ambayo walikuwa wanayatawala kwenye mwendo wa ukafiri. Kwanza Mungu aliadhibu ufalme wa kaskazini wa Israeli, akasema hivi: “Nitatuma [Ashuru] juu ya taifa [la Israeli] lenye kukufuru.” (Isa. 10:6) Na muda mfupi tu kabla ya kuharibiwa kwa Yerusalemu, mji mkuu wa Yuda, na Wababeli, Yehova alisema hivi: “Kutoka kwa manabii hao wa Yerusalemu kukufuru kumeingia katika nchi yote.” (Yer. 23:15) Ukafiri au kukengeuka kutoka kwa imani ya kweli kwa hakika hakukuleta baraka zo zote juu ya Israeli na Yuda.
Ukafiri Kati ya Wakristo wa Kwanza
4. Yesu alitoa onyo gani kwa makafiri?
4 Mapema zaidi wakati wa huduma yake ya kidunia, Yesu aliwaonya wafuasi wake juu ya makafiri. Katika Mahubiri yake ya Mlimani, alisema hivi:
“Ingieni kwa kupitia mlango ulio mwembamba; maana mlango ni mpana, na njia ni pana iendayo upotevuni, nao ni wengi waingiao kwa mlango huo. Bali mlango ni mwembamba, na njia imesonga iendayo uzimani, nao waionao ni wachache. Jihadharini na manabii wa uongo, watu wanaowajia wamevaa mavazi ya kondoo, walakini kwa ndani ni mbwa-mwitu wakali. Mtawatambua kwa matunda yao.”—Mt. 7:13-16.
5. Paulo alisema jambo gani juu ya makafiri?
5 Miaka ishirini na mitano baadaye, Paulo aliwaonya wazee Wakristo wa Efeso hivi: “Najua mimi ya kuwa baada ya kuondoka kwangu mbwa-mwitu wakali wataingia kwenu, wasilihurumie kundi; tena katika ninyi wenyewe watainuka watu, wakisema mapotovu, wawavute hao wanafunzi wawaandamie wao.” (Matendo 20:29, 30) Katika maandishi yake ya mwisho yaliyoongozwa na Mungu Paulo aliwataja wachache kati ya waasi hao wa karne ya kwanza. Alimwonya Timotheo hivi: “Jiepushe na maneno yasiyo na maana, ambayo si ya dini; kwa kuwa wataendelea zaidi katika maovu, na neno lao litaenea kama donda-ndugu. Miongoni mwa hao wamo Himenayo na Fileto, walioikosa ile kweli, . . . hata kuipindua imani ya watu kadha wa kadha.” “Iskanda, mfua shaba, alionyesha ubaya mwingi kwangu . . . jihadhari na huyo, kwa sababu aliyapinga sana maneno yetu.”—2 Tim. 2:16-18; 4:14, 15.
6. Ni baadhi ya mambo gani yenye kutambulisha makafiri wa kawaida?
6 Tukichanganua maonyo hayo yaliyotolewa na Yesu na Paulo, mambo yafuatayo yenye kutambulisha waasi wa kawaida yanajitokeza:
(1) Kuachana na kweli
(2) Mazungumzo yaliyopotoka, ya upuzi
(3) Jitihada za kuharibu imani ya wengine na kuvuta wanafunzi wawafuate
(4) Unafiki (‘mbwa-mwitu katika mavazi ya kondoo’)
(5) Wanaweza kutambuliwa kwa matunda yao; ‘wanaendelea zaidi katika kukosa utawa’
Ishara hizo zenye kuwafunua zilikusudiwa ziwawezeshe Wakristo wa kwanza watambue upesi waasi na ‘kujihadhari nao.’
Ukafiri “katika Vipindi vya Baadaye vya Wakati”
7. Ukafiri wa watu wengi ulitokea wakati gani, kama ilivyotabiriwa na andiko gani?
7 Ukafiri ambao tayari ulikuwa ‘unatenda kazi’ wakati baadhi ya mitume wa Kristo walipokuwa wangali hai ulipata kuwa wazi zaidi “katika vipindi vya baadaye vya wakati,” yaani, baada ya kufa kwao. Ishara hizo tano zenye kuwafunua zilipata kuwa wazi zaidi tangu karne ya pili na kuendelea na kufikia upeo wake katika karne ya nne. Uasi huo mkubwa ungetokea kabla ya “kuwapo kwa Bwana yetu Yesu Kristo” na “siku ya Yehova.”—2 The. 2:1-12, NW.
8, 9. (a) Petro alitoa onyo gani kuhusu siku za mwisho? (b) Je! “wadhihaki” hao na “watu wenye kuhalifu sheria” wote wangekuwa nje ya kundi la Kikristo?
8 Walakini maandiko mengineyo yanaonyesha wazi kwamba hata wakati wa “siku za mwisho” za taratibu hii ya mambo, visa vya ukafiri vingetokea ndani ya kundi la kweli la Kikristo. Mtume Petro anaandika hivi:
“Katika siku za mwisho watakuja wadhihaki pamoja na dhihaka yao, wakiendelea kulingana na tamaa zao wenyewe na kusema: ‘Ku wapi huku kuwapo kwake kulikoahidiwa?’ . . . Kwa hiyo, ninyi wapendwa, mkiisha kutangulia kujua hayo, jihadharini msije mkapotezwa nao kwa lile kosa la watu wenye kuhalifu sheria na kuanguka mtoke katika imara yenu wenyewe.—2 Pet. 3:3, 4, 17, NW.
9 Petro hakuwa akiwaonya ndugu zake juu ya “wadhihaki”’ na “watu wenye kukaidi sheria” tu katika ulimwengu huu. Sikuzote Wakristo wamefahamu hatari inayotoka upande huo. Vilevile Petro alikuwa akizungumza juu ya hatari ya ‘kupotezwa na wengine ndani ya kundi la Kikristo ambao walipata kuwa “wadhihaki,” wakipunguza uzito wa utimizo wa unabii kuhusu “kuwapo” kwa Kristo na kuchukua maoni ya kukaidi sheria kuelekea “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” Baraza Yenye Kuongoza ya kundi la Kikristo na wazee waliowekwa.
Visababishaji na Matokeo ya Uasi
10, 11. (a) Kisababishaji kimoja cha maana cha ukafiri ni kipi? (b) Baadhi ya maana zenye kulingana za neno la Kigiriki linalotafsiriwa kuwa “kutia shaka” ni zipi, naye kafiri anajiwekaje kuwa hakimu?
10 Kati ya visababishaji mbalimbali vya uasi, bila shaka kimojawapo kilicho kikubwa zaidi ni kukosa imani kwa kuwa na mashaka. (Ebr. 3:12) Kwa kupendeza, kitabu The New International Dictionary of New Testament Theology kinatoa habari ifuatayo juu ya kiarifa cha Kigiriki ambacho mara nyingi tafsiri yake ni “kutia shaka”: “Diakrinō, kutofautisha, kutoa uamuzi, . . . ; kutia shaka, kutikisika. . . . Katika vifungu fulani vya maneno [vya Agano Jipya] kutia shaka kunaonekana kuwa kukosa imani na hivyo kama dhambi (Rum. 14: 23) . . . . Katika Rum. 4:20f. kutia shaka kunakaribia kuwa kutokuamini. . . . Hivyo kutia shaka ni kutotumaini tendo la Mungu ambalo angali atafanya na ambalo wanadamu wangojea. . . . Katika Agano Jipya mwenye kutia shaka anamfanyia Mungu dhambi na ahadi zake pia, kwa kuwa anamhukumu Mungu kwa uongo.”
11 Kwa hiyo, mtu anayetia mashaka kufikia hatua ya kuwa kafiri anajiweka mwenyewe kuwa hakimu. Anadhani anajua zaidi ya Wakristo wenzake, zaidi hata ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” ambaye ni kupitia kwake amejifunza sehemu kubwa, ikiwa si yote anayojua juu ya Yehova Mungu na makusudi yake. Anasitawisha roho ya kujitegemea, naye anakuwa ‘mwenye moyo wa kiburi jambo ambalo ni chukizo kwa Yehova.’ (Mit. 16:5) Makafiri wengine hufikiri hata kwamba wanajua mengi zaidi ya Mungu, kwa habari ya yeye kuamrisha matukio katika kutimiza makusudi yake. Kwa hiyo visababishaji vingine viwili vya ukafiri ni kukosa shukrani na kujitanguliza.—2 Pet. 2:10b-13a.
12. Ni nini baadhi ya matokeo ya uasi na ukafiri?
12 Kwa habari ya matokeo ya mwendo wa uasi, mtu hupoteza furaha mara moja. Kafiri anakuwa mzoelevu wa njia zake za kuasi. Jambo jingine ni kuwa anakosa kutwaa chakula cha kiroho kinachotolewa na “mtumwa mwaminifu mwenye akili” jambo hilo likiongoza kwenye udhaifu na kuvunjika kwa roho. Akitofautisha furaha ya watumishi wake washikamanifu na hali yenye kusikitisha ya makafiri, Yehova alisema hivi kwa njia ya unabii:
“Tazama, watumishi wangu watakula, lakini ninyi mutakuwa na njaa; tazama, watumishi wangu watakunywa, lakini ninyi mutaona kiu; tazama, watumishi wangu watafurahi, lakini ninyi mutapata haya; tazama, watumishi wangu wataimba kwa furaha ya moyo, lakini ninyi mutalia kwa huzuni ya moyo, na mutapiga kelele kwa sababu ya uchungu wa roho zenu.”—Isa. 65:13, 14, ZSB.
13. ‘Kudharau ubwana’ kwamaanisha nini, nalo jambo hilo linatokeza nini? (Yuda 8, 10)
13 Baada ya kushindwa na kazi za mwili kama vile “uadui, ugomvi, wivu, kufoka kwa hasira, mashindano, migawanyiko, madhehebu,” mara nyingi makafiri huangukia zile kazi nyinginezo za mwili kama vile “mashindano ya ulevi,” “ufisadi” na “uasherati.” (Gal. 5:19-21, NW) Petro anatuonya juu ya wale “wanaodharau ubwana” kwa kupuza mpango wa kitheokrasi, ‘wanaotukana’ wale waliopewa daraka ndani ya kundi la Kikristo, na kwa njia hiyo wanaiacha ‘njia iliyonyoka.’ Anasema kwamba ‘hali zao mwisho zimekuwa mbaya zaidi kwao kuliko za kwanza.’—Soma kwa uangalifu 2 Petro sura 2.
Jinsi ya Kuepuka ‘Kukengeuka Kuiacha Imani’
14, 15. Twaweza kuepukaje kujitanguliza?
14 Tumekwisha kuona kwamba kisababishaji kimojawapo cha ukafiri ni kukosa imani kupitia kwa mashaka yenye kuharibu, na kwamba neno linalotafsiriwa kuwa “shaka” vilevile lamaanisha “kutofautisha.” Kafiri hujifanya kuwa mwamuzi wa yaliyo kweli na yaliyo uongo, wa yaliyo “mema na mabaya” kwa habari ya chakula cha kiroho. Anajitanguliza.—Linganisha Mwanzo 2:17; 3:1-7.
15 Kwa hiyo ili kuepuka kukengeuka kuiacha imani, Mkristo anapaswa kujihadhari na kukosa imani, “dhambi ituzingayo kwa wepesi,” na “tupige mbio kwa saburi katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu.” (Ebr. 12:1; 3:12, 19) Paulo anatupa shauri hili: “Endeleeni kujijaribu kama mu katika imani, endeleeni kujithibitisha wenyewe mlivyo.” (2 Kor. 13:5, NW) Paulo hatualiki tuwe na mashaka juu ya “imani,” bali tujiulize maulizo, kama tunaishi kulingana na imani hiyo au hapana. Kujichunguza huko kwa kibinafsi kwa unyofu kwapaswa kutujaze kiasi na unyenyekevu, hivyo kutulinde na roho ya kujitegemea na kujitanguliza kwa kafiri.
16. (a) Twapaswa kuepuka mtego gani mwingine? (b) Twaweza kupata somo gani lenye sehemu mbili kwa Wayahudi wa Beroya?
16 Ili kuepuka kukengeuka kuiacha imani, vilevile twahitaji kujilinda na kukosa shukrani. Twapaswa kuwa wenye shukrani kwa ajili ya chakula kingi cha kiroho tunachopata kupitia kwa “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mt. 24:45) Hiyo haimaanishi kwamba hatupaswi kujisadikisha juu ya mambo kwa kadiri tunavyoendelea. Kwa habari hii, somo lenye sehemu mbili laweza kupatikana kwa Wayahudi wa Beroya. Ili wawe na hakika, ‘walichunguza maandiko kila siku, waone kwamba mambo hayo ndivyo yalivyo,’ walakini vilevile walikuwa na akili za ‘kiungwana’ kwa sababu “walilipokea lile neno [lililokuwa likihubiriwa kwao na Paulo na Sila] kwa uelekevu wa moyo.”—Matendo 17:11.
17, 18. Twapaswa kuweza kutofautisha nini, naye Paulo anatupa shauri gani juu ya jambo hilo?
17 Uelekevu wa shukrani kama huo wa kutaka kujifunza utatusaidia tusitawishe upendo na kutwaa maarifa sahihi, pamoja na ufahamu kamili. Sifa hizo za Kikristo nazo, zinatuwezesha kutofautisha kati ya mambo ya maana sana na yale yasiyo ya maana sana. Je! jambo fulani tunaloshindwa kufahamu ni la maana kweli kweli? Je! linapasa mambo yaliyo ya maana kweli kweli ambayo tumejifunza kwa msaada wa jamii ya “mtumwa?” Je! linastahilisha kujikwaza wenyewe na pengine wengine? Je! linatuzuia tusizae matunda ya Kikristo?
18 Paulo anatushauri hivi: “Hivi ndivyo ninavyoendelea kusali, kwamba upendo wenu uzidi zaidi na zaidi pamoja na maarifa sahihi ya ufahamu kamili; mpate kuhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi, ili mpate kuwa bila hitilafu na kutokuwa mkikwaza wengine mpaka siku ya Kristo, na mpate kujawa na matunda yenye haki, ambayo yanakuja kupitia kwa Yesu Kristo, na kumletea Mungu utukufu na sifa.”—Flp. 1:9-11, NW.
‘Kuwanyakua Wenye Mashaka kutoka Motoni’
19. (a) Ni jambo gani jingine linalopaswa kutofautishwa? (b) Yuda anatoa kitia-moyo gani kingine chenye kujenga?
19 Kwa kuwa tumekwisha kuonywa kwamba “wengine watakengeuka waiache imani,” twapaswa kuwa tayari ‘kupiga vita kwa bidii kwa ajili ya imani waliyokabidhiwa watakatifu mara moja kwa wakati wote.’ (1 Tim. 4:1, NW; Yuda 3, NW) Walakini tofauti yapaswa kufanywa kati ya makafiri wenye kuleta matata, wanaotajwa katika 2 Petro, sura ya 2, na Wakristo wanaodhoofika katika imani na kuwa na mashaka kupitia kwa kukosa maarifa sahihi. Yuda anatofautisha. Baada ya kuonya juu ya “wanung’unikaji, walalamikaji,” “wanaosifu mno watu mashuhuri,” na juu ya “wenye kudhihaki,” ambao “ndio wenye kuleta migawanyiko,” anasema hivi: “Dumuni katika upendo wa Mungu, huku mkiingojea rehema ya Bwana yetu Kristo kwa tumaini la uzima wa milele. Vilevile, endeleeni kuonyesha rehema wengine wenye mashaka; waokoeni kwa kuwanyakua kutoka motoni.”—Yuda 16-23, NW.
20. Wenye kutia mashaka wanapaswa kusaidiwaje, lakini namna gani wakikataa msaada na ‘kukengeuka kuiacha imani’?
20 Ndiyo, wenye mashaka kama hao wanapaswa kuonyeshwa kwamba wamo katika hatari ya kumezwa na mashaka yenye kuharibu. Ndugu zao wa Kikristo, na sana sana wazee, wanapaswa kujitahidi kuwasaidia, kuwanyakua, iwapo inawezekana, kutoka “motoni” ambao unaweza kuwaharibu kiroho. Kwa habari ya wale wanaokataa msaada huo wa saburi na wa upendo na ambao kweli kweli ‘wanakengeuka kuiacha imani,’ hatupaswi kufadhaika isivyofaa. Pamoja na mtume Yohana tutasema hivi: “Walitoka kwetu, lakini hawakuwa wa kwetu. Maana kama wangalikuwa wa kwetu, wangalikaa pamoja nasi,”—1 Yohana 2:19.
“Mkithibitika katika Imani” mpaka Mwisho Kabisa
21, 22. (a) Petro anatoa kitia-moyo gani cha kuendelea kuwa wenye nguvu katika imani? (b) Waisraeli wa kiroho na “mkutano mkubwa” wanapaswa kuendelea kufanya nini ili watimiziwe matumaini yao?
21 Hakuna shaka kwamba Shetani angependa kutuona sote ‘tukikengeuka kuiacha imani.’ Kwa hiyo Petro anatushauri hivi:
“Chukueni hatua ya kumpinga yeye, mkithibitika katika imani, mkijua kwamba mambo ayo hayo kwa namna ya mateso yanatimizwa katika ushirika mzima wa ndugu zenu ulimwenguni. Walakini, baada ya kuteswa kwa kitambo kidogo, Mungu wa fadhili zote zisizostahilika, aliyewaitia utukufu wake wa milele katika umoja na Kristo, yeye mwenyewe atamaliza mazoezi yenu, atawafanya mwe imara, atawafanya mwe na nguvu.”—1 Pet. 5:10, NW.
Ndiyo, wale walio Waisraeli wa kiroho, ambao wameitwa watawale pamoja na Kristo katika “utukufu wa milele,” wanapaswa kuendelea kuwa waaminifu katika “saa ya kujaribiwa,” iwapo hawataki ‘mtu atwae taji yao.’—2 Tim. 2:10; Ufu. 3:10, 11.
22 Wenzi wao, washiriki wa “mkutano mkubwa,” vilevile wanatambua kwamba wanapaswa kuendelea ‘kuthibitika katika imani’ iwapo wanataka ‘kutoka katika dhiki ile iliyo kuu.’ (Ufu. 7:9, 10, 14) Wakristo wale wenye tumaini la kimbinguni, na wenzi wao ambao tumaini lao ni kuishi milele katika paradiso iliyorudishwa duniani, wameazimia kuendelea kuhubiri kwa uaminifu “habari njema hizi za ufalme.” (Mt. 24:14, NW) Mpanuko mkubwa katika sehemu nyingi za ulimwengu, kufikia mwaka huu wa 1981, unawathibitishia kwamba baraka ya Yehova i juu ya tengenezo lake, na kwamba kungali kuna kazi ya kufanywa. Kwa hiyo wanatii shauri la Paulo: “Tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho?—Gal. 6:8, 9.
23. Ni nini kinachotupa sisi sote “kitia-moyo chenye nguvu” tupate kuendelea ‘kuthibitika katika imani?
23 Tunapoyaona mambo yaliyotabiriwa kuwa katika “siku za mwisho” yalitokea mbele ya macho yetu, tuna uhakika sana kwamba “dhiki kubwa” na kupambazuka kwa taratibu mpya ya Mungu yenye haki kumekaribia sana. Baraka za ajabu ambazo zi karibu sana mbele yetu, ama mbinguni ama katika paradiso ya kidunia, zinatupa “kitia-moyo chenye nguvu tuendelee ‘kuthibitika katika imani’ mpaka mwisho kabisa, ili ‘tulishike tumaini lililowekwa mbele yetu.’—Ebr. 6:17-19.
“Lakini ninyi, wapendwa, kwa kujijenga wenyewe juu ya imani yenu iliyo takatifu zaidi sana, na kusali kwa roho takatifu, dumuni katika upendo wa Mungu, huku mkiingojea rehema ya Bwana yetu Yesu Kristo kwa tumaini la uzima wa milele.”—Yuda 20, 21, NW.
—Kutoka The Watchtower Aug. 1, 1980
[Sanduku katika ukurasa wa 14]
VISABABISHAJI
Kukosa imani
Roho ya kujitegemea
Kukosa shukrani
Kujitanguliza
[Sanduku katika ukurasa wa 14]
MATOKEO
Kupoteza furaha
Uasi
Kukosa chakula cha kiroho
Kazi za mwili
[Picha katika ukurasa wa 17]
“Waokoeni kwa kuwanyakua kutoka motoni”