UASI IMANI
Neno hilo katika Kigiriki (a·po·sta·siʹa) linatokana na kitenzi a·phiʹste·mi ambacho kihalisi kinamaanisha “simama mbali na.” Nomino hiyo inamaanisha “kuondoka, kuacha au kuasi.” (Mdo 21:21) Katika Kigiriki cha zamani nomino hiyo ilitumiwa kurejelea kuhama kisiasa, na inaonekana kwamba kitenzi hicho kimetumiwa katika maana hiyo kwenye Matendo 5:37, kuhusiana na Yuda Mgalilaya ambaye ‘alipata wafuasi’ (a·peʹste·se, kutokana na kitenzi a·phiʹste·mi). Septuajinti ya Kigiriki inatumia neno hilo katika Mwanzo 14:4 kurejelea uasi wa aina hiyo. Hata hivyo, katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo neno hilo linatumiwa hasa kuhusiana na kuhama dini; kuondoka au kuacha njia au ibada ya kweli, na kuacha kumtumikia Mungu, na hivyo kuacha mambo ambayo mtu aliamini, kutofuata kanuni au imani. Viongozi wa kidini huko Yerusalemu walidai Paulo alikuwa ameasi kwa njia hiyo, kwa kuacha Sheria ya Musa.
Inaweza kusemwa kwamba Adui wa Mungu ndiye aliyekuwa mwasi imani wa kwanza, kama jina lake Shetani linavyoonyesha. Alifanya wanadamu wawili wa kwanza waasi imani. (Mwa 3:1-15; Yoh 8:44) Baada ya Gharika, watu waliasi maneno ambayo Mungu wa Noa alisema. (Mwa 11:1-9) Baadaye Ayubu alilazimika kujitetea wafariji watatu wa uwongo walipodai kwamba yeye ni mwasi imani. (Ayu 8:13; 15:34; 20:5, Maelezo ya Chini.) Ayubu alijitetea kwa kusema kwamba hakuna mwasi imani anayeweza kwenda mbele za Mungu (Ayu 13:16), na alionyesha pia kwamba mwasi imani anapoangamizwa hana tumaini lolote. (Ayu 27:8; linganisha pia na maneno ya Elihu katika 34:30; 36:13.) Maandiko hayo yanatumia nomino ya Kiebrania cha·nephʹ kumaanisha “[mtu] aliyetengwa mbali na Mungu,” yaani, mwasi imani. Kitenzi cha·nephʹ kinachohusiana na nomino hiyo kinamaanisha “kujitenga mbali na uhusiano unaofaa pamoja na Mungu,” au “kuchafua, kuongoza kwenye uasi imani.”— Lexicon in Veteris Testamenti Libros, ya L. Koehler na W. Baumgartner, Leiden, 1958, uku. 317.
Uasi Imani Katika Israeli. Amri mbili za kwanza katika Sheria zilikataza uasi imani wa aina yoyote. (Kut 20:3-6) Na kabla ya Waisraeli kuingia katika Nchi ya Ahadi, walionywa kuhusu hatari kubwa ya kuasi imani ambayo ingetokana na kufunga ndoa na watu wa nchi hiyo. (Kum 7:3, 4) Mtu aliyewachochea wengine kuasi imani alipaswa kuuawa hata ikiwa alikuwa mtu wa karibu wa ukoo au mwenzi wa ndoa kwa sababu ‘aliwachochea wengine kumwasi Yehova Mungu wao.’ (Kum 13:1-15) Watu wa makabila ya Rubeni, Gadi, na Manase walijitetea haraka waliposhtakiwa kwamba wameasi imani kwa sababu walikuwa wamejenga madhabahu.—Yos 22:21-29.
Wafalme wengi wa Israeli na Yuda waliasi imani—kwa mfano, Sauli (1Sa 15:11; 28:6, 7), Yeroboamu (1Fa 12:28-32), Ahabu (1Fa 16:30-33), Ahazia (1Fa 22:51-53), Yehoramu (2Nya 21:6-15), Ahazi (2Nya 28:1-4), na Amoni (2Nya 33:22, 23). Baada ya muda uasi imani ulienea katika taifa hilo kwa sababu watu waliwasikiliza makuhani na manabii waasi imani (Yer 23:11, 15) na watu wengine wasio na msimamo waliotumia maneno ya ujanja na ya uwongo kuwaongoza kwenye mwenendo mpotovu, uasherati, na kuwafanya wamwache Yehova, “chanzo cha maji yaliyo hai.” (Isa 10:6; 32:6, 7; Yer 3:1; 17:13) Kulingana na Isaya 24:5, nchi hiyo ‘ilichafuliwa [cha·nephahʹ] na wakaaji wake, kwa maana walikuwa wamezivunja sheria, wakabadili amri, na kuvunja agano linalodumu.’ Hawangeonyeshwa rehema wakati wa maangamizi yaliyotabiriwa.—Isa 9:17; 33:11-14; Sef 1:4-6.
Ni mambo gani yanayowatofautisha waasi imani na Wakristo wa kweli?
Katika 2 Wathesalonike 2:3, mtume Paulo alitabiri kwamba uasi imani ungetokea miongoni mwa Wakristo. Aliwataja kihususa baadhi ya waasi imani hao, kama vile Himenayo, Aleksanda, na Fileto. (1Ti 1:19, 20; 2Ti 2:16-19) Baadhi ya mambo yanayosababisha uasi imani yanayotajwa katika maonyo ya mitume ni: kukosa imani (Ebr 3:12), kukosa uvumilivu unapoteswa (Ebr 10:32-39), kuacha kanuni zinazofaa za maadili (2Pe 2:15-22), kusikiliza “maneno ya uwongo” ya walimu wa uwongo na “maneno ya uwongo yaliyoongozwa na roho waovu” (2Pe 2:1-3; 1Ti 4:1-3; 2Ti 2:16-19; linganisha na Met 11:9), na kujaribu “kutangazwa kuwa waadilifu kupitia sheria” (Ga 5:2-4). Huenda waasi imani wakaacha kumtumikia Mungu kwa kupuuza kazi ya kuhubiri na kufundisha aliyowapa wafuasi wa Yesu Kristo huku wakidai kwamba bado wanaamini Neno la Mungu. (Lu 6:46; Mt 24:14; 28:19, 20) Huenda pia wakadai kwamba wanamtumikia Mungu lakini wanawakataa wawakilishi wake, tengenezo lake linaloonekana. (Yuda 8, 11; Hes 16:19-21) Mara nyingi waasi imani hujaribu kuwafanya wengine wawe wafuasi wao. (Mdo 20:30; 2Pe 2:1, 3) Watu hao huacha kimakusudi kutaniko la Kikristo na hivyo wanakuwa sehemu ya “mpinga-Kristo.” (1Yo 2:18, 19) Kama ilivyotabiriwa kwamba Waisraeli waasi imani wangeangamizwa, vivyo hivyo imetabiriwa kwamba waasi imani katika kutaniko la Kikristo wataangamizwa.—2Pe 2:1; Ebr 6:4-8; angalia MARAFIKI.
Kutaniko la Kikristo la mapema lilipokuwa likiteswa na Milki ya Roma, nyakati nyingine wale waliodai kuwa Wakristo walishawishiwa wakane kuwa wanafunzi wa Kristo, na wale waliofanya hivyo walipaswa kuonyesha kwamba wameasi imani kwa kufukiza uvumba mbele ya mungu fulani wa kipagani au kwa kukufuru jina la Kristo hadharani.
Ni wazi kwamba kuna tofauti kati ya ‘kuanguka’ kwa sababu ya udhaifu na ‘kuacha’ ambako ni uasi imani. “Kuacha” ni kuamua kimakusudi kuondoka kwenye njia ya uadilifu. (1Yo 3:4-8; 5:16, 17) Kuamua kufanya hivyo kwa sababu yoyote ile, iwe ni kwa sababu linaonekana kuwa jambo la kiakili, linalofaa, au kwa sababu za kidini, ni uasi dhidi ya Mungu na kukataa Neno lake la kweli.—2Th 2:3, 4; angalia MTU WA UASI SHERIA.