Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • it kur. 310-312
  • Mtu wa Uasi Sheria

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mtu wa Uasi Sheria
  • Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Habari Zinazolingana
  • Uasi Juu ya Mungu Unafunuka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • Kutambulisha “Mtu wa Kuasi [Sheria]”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Kifo cha Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1975
  • ‘Kuingiza Kisiri-siri Madhehebu Zenye Kuharibu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
Pata Habari Zaidi
Ufahamu wa Kina wa Maandiko
it kur. 310-312

MTU WA UASI SHERIA

Maneno hayo yanatumiwa na mtume Paulo katika 2 Wathesalonike 2:2, 3 kuonya kuhusu uasi-imani mkubwa ambao ungetokea katika Ukristo kabla ya “siku ya Yehova.” Neno la Kigiriki a·po·sta·siʹa, linalotumiwa kumaanisha “uasi imani,” halimaanishi tu kuanguka, au kuacha bila kujali. Linamaanisha uasi uliopangwa kufanywa kimakusudi. Katika hati za kale za mafunjo neno a·po·sta·siʹa, lilitumiwa kuhusiana na waasi wa kisiasa.

Uasi wa Kidini. Uasi huu si wa kisiasa. Ni uasi wa kidini, uasi dhidi ya Yehova Mungu na Yesu Kristo na hivyo ni dhidi ya kutaniko la Kikristo.

Ulitabiriwa. Mtume Paulo na Petro walitabiri kuhusu uasi huo kwa maneno na maandishi, na Bwana Yesu Kristo mwenyewe alionya kuhusu kutokea kwa uasi huo. Katika mfano wake wa ngano na magugu (Mt 13), Yesu alisema kwamba Ibilisi angepanda “magugu,” Wakristo wa uwongo, “wana wa yule mwovu,” katikati ya “ngano,” yaani, “wana wa ufalme.” Magugu yangeachwa yakue mpaka umalizio wa mfumo wa mambo, wakati ambapo yangekusanywa na ‘kuteketezwa motoni.’

Paulo aliwaonya waangalizi Wakristo huko Efeso kwamba baada ya yeye kuondoka “mbwamwitu wenye kukandamiza” wangeingia katikati ya Wakristo wa kweli na hawangelitendea kundi kwa wororo bali wangejaribu kuwavuta “wanafunzi“ wawafuate wao wenyewe (hawangetafuta wanafunzi wao bali wangejaribu kuwavuta wanafunzi wa Kristo). (Mdo 20:29, 30) Aliandika hivi katika 1 Timotheo 4:1-3: “Hata hivyo, neno lililoongozwa na roho linasema wazi kwamba wakati ujao watu fulani wataiacha imani, wakisikiliza maneno ya uwongo yaliyoongozwa na roho waovu na mafundisho ya roho waovu, kupitia unafiki wa watu wanaosema uwongo, ambao dhamiri zao zimetiwa alama kama kwa chuma cha moto [hawana hisia, ni wagumu, hivi kwamba hawasumbuliwi na dhamiri kwa sababu ya unafiki na kusema uwongo]. Wanakataza watu kufunga ndoa na kuwaamuru wasile vyakula ambavyo Mungu aliumba viliwe kwa shukrani na watu wenye imani na wanaoijua kweli kwa usahihi.”

Baadaye Paulo alimwandikia Timotheo kwamba “kutakuwa na wakati ambapo hawatalivumilia fundisho lenye manufaa, bali, kulingana na tamaa zao, watajikusanyia walimu ili masikio yao yafurahishwe. Wataacha kuisikiliza ile kweli, nao watageukia hadithi za uwongo.”​—2Ti 4:3, 4.

Mtume Petro alilinganisha uasi imani wa Kikristo na uasi uliotokea katika taifa la Waisraeli wa asili. Alisema hivi: “Hata hivyo, kulikuwa pia na manabii wa uwongo miongoni mwa watu, kama vile pia kutakavyokuwa na walimu wa uwongo miongoni mwenu. Hawa wataingiza kimyakimya madhehebu yenye kuharibu, na hata watamkana bwana aliyewanunua, na kujiletea maangamizi ya haraka. Zaidi ya hayo, wengi watafuata mwenendo wao mpotovu, na kwa sababu yao ile njia ya kweli itatukanwa.” Petro aliendelea kusema kwamba wangetumia kutaniko vibaya lakini “maangamizi yao hayalali.”​—2Pe 2:1-3.

Kikundi cha watu. “Mtu” anayetajwa katika 2 Wathesalonike 2:1-12 si mtu mmoja, bali ni kikundi cha watu, kama vile maandiko yaliyotajwa hapo juu yanavyoonyesha, na “mtu” huyo angeendelea kuwapo baada ya kifo cha mitume hadi wakati wa kuwapo kwa Bwana.

Uhaini dhidi ya Mungu. “Uasi sheria” anaofanya “mtu” huyo mwasi-imani ni uasi sheria dhidi ya Yehova Mungu Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. “Mtu” huyo ana hatia ya uhaini. Anaitwa “mwana wa maangamizi,” kama Yuda Iskariote, aliyemsaliti Bwana Yesu Kristo na kusababisha Yesu auawe. Kama Yuda, yeye pia ataangamizwa kabisa kwa umilele. “Mtu” huyo si “Babiloni Mkubwa,” ambaye pia anapigana na Mungu, kwa kuwa Babiloni Mkubwa ni mwanamke, kahaba. Hata hivyo, kwa kuwa anaendeleza uasi wa kidini dhidi ya Mungu, ni wazi kwamba yeye ni sehemu ya Babiloni.​—Yoh 17:12; Ufu 17:3, 5.

“Yule mtu wa uasi sheria” anampinga Mungu hivyo yeye ni “shetani” yaani, “mpinzani.” Na, kwa kweli, kuwapo kwake “ni kupitia kazi ya Shetani.” (2Th 2:9) Katika siku za mtume Paulo, kulikuwa na “fumbo,” au siri ya kidini, kuhusu utambulisho wa huyo “mtu wa uasi sheria.” Leo, bado utambulisho wake ni fumbo katika akili za watu wengi kwa sababu anatenda uovu huku akijifanya ana ujitoaji kimungu. (2Th 2:7) Kupitia mafundisho yake ya uwongo yaliyo kinyume na, au yanayochukua mahali pa, sheria ya Mungu, “mtu wa uasi sheria” amejiinua juu ya Yehova Mungu na ‘miungu’ mingine, yaani, watu wenye nguvu wa dunia, na pia dhidi ya watakatifu wa Mungu, ndugu wa kiroho wa Yesu Kristo. (Linganisha na 2Pe 2:10-13.) Kwa kuwa ni mnafiki, mwalimu wa uwongo anayedai kuwa Mkristo, yeye “huketi katika hekalu la Mungu,” yaani, kile ambacho walimu hao wa uwongo hudai kuwa hekalu.—2Th 2:4.

Kizuizi. Paulo alizungumza kuhusu kitu “kinachomzuia” mtu huyo. (2Th 2:6) Inaonekana mitume ndio waliokuwa kizuizi hicho. Paulo alikuwa amewaambia waangalizi Waefeso kwamba baada ya yeye kuondoka watu walio kama mbwamwitu wangeingia. (Mdo 20:29) Aliandika mara nyingi kuhusu uasi imani huo, si katika kitabu cha Pili cha Wathesalonike tu bali pia kupitia himizo kwa Timotheo. Na alimshauri Timotheo kwamba mambo aliyosikia kutoka kwa Paulo awakabidhi watu waaminifu ambao wangestahili kuwafundisha wengine. Alisema kwamba kutaniko la Mungu aliye hai ndilo “nguzo na tegemezo la ile kweli.” Alitaka liimarishwe kabisa kabla uasi imani mkubwa haujatokea.​—2Ti 2:2; 1Ti 3:15.

Baadaye, mtume Yohana aliagizwa na Kristo aandike onyo dhidi ya madhehebu, akataja hasa madhehebu ya Nikolao na manabii wa uwongo kama vile Balaamu na mwanamke Yezebeli ambaye alijiita nabii.​—Ufu 2:6, 14, 15, 20.

Fumbo lilifanya kazi katika siku za mitume. Mtume Paulo alisema kwamba fumbo hilo “tayari linafanya kazi.” (2Th 2:7) Kuna watu waliokuwa wakijaribu kufundisha mafundisho ya uwongo, wengine wao hata walivuruga kutaniko la Thesalonike, na hilo likafanya awaandikie barua yake ya pili. Kulikuwa na wapinga-Kristo Yohana alipoandika barua zake, na hata kabla ya hapo. Yohana alizungumzia “saa ya mwisho” ya kipindi cha mitume, naye alisema: “Kama vile mlivyosikia kwamba mpinga-Kristo anakuja, hata sasa wapinga-Kristo wengi wametokea . . . Waliondoka miongoni mwetu, lakini hawakuwa wa namna yetu; kwa maana kama wangekuwa wa namna yetu, wangebaki pamoja nasi. Lakini waliondoka ili ionekane kwamba si wote walio wa namna yetu.”​—1Yo 2:18, 19; ona MPINGA-KRISTO.

Anatambulishwa. Baada ya kifo cha mitume, “yule mtu wa uasi sheria” alionekana wazi kupitia unafiki wake wa kidini na mafundisho ya uwongo. (2Th 2:3, 6, 8) Kulingana na maneno ya Paulo, “mtu” huyo angepata nguvu nyingi, akiongozwa na Shetani, na kufanya “kila tendo lenye nguvu na ishara za uwongo na mambo ya ajabu.” Watu wanaopotoshwa na matendo ya “yule mtu wa uasi sheria” wanaitwa “wale wanaoangamia [kihalisi, “wanaojiangamiza wenyewe”], kama malipo kwa sababu hawakukubali kuipenda kweli ili waokolewe.” Mtume huyo anaonyesha kwamba ‘wanaamini uwongo’ na wote ‘watahukumiwa kwa sababu hawakuiamini kweli bali walipenda ukosefu wa uadilifu.’ (2The 2:9-12; ona Int.) Basi wanahukumiwa kuwa na hatia.​—Ona UFUFUO (Dhambi dhidi ya roho takatifu).

Anaangamizwa. Kikundi hicho cha kinafiki cha “mtu wa uasi sheria,” kitaangamizwa “kwa roho ya kinywa” chake Bwana Yesu na atakiharibu “kupitia ufunuo wa kuwapo kwake.” Kuharibiwa kwa huyo mpinzani mwovu wa Mungu kutaonekana wazi, na kuthibitisha wazi kwamba Bwana Yesu Kristo anatenda akiwa Hakimu. Hatahukumu kulingana na viwango vyake mwenyewe, hivyo basi kuangamizwa “kwa roho ya kinywa chake” kunamaanisha hukumu ya Yehova dhidi ya kikundi hicho kiovu.​—2Th 2:8; linganisha Ufu 19:21, kuhusu ‘upanga mrefu unaochomoza kinywani mwake.’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki