Kifo cha Mungu
Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi
1. “Mungu” ni nini?
MUNGU ni nini? Neno hili “mungu” linamaanisha “mwenye nguvu.” Neno hili limetumiwa mara nyingi juu ya cho chote kinachoabudiwa kama chenye nguvu au kiwezacho kutendea waabudu wacho mema au mabaya. Mungu angeweza kuwa kitu, au mtu, kikundi cha wanadamu au tengenezo.
2, 3. Mungu anayezungumzwa ni nini, na mtume Paulo anamsimuliaje?
2 Mungu anayezungumzwa hapa ni kikundi au jamii ya wanadamu. Ndicho Biblia inaita “yule mtu wa kuasi.” Mtume Paulo alitusimulia juu ya mungu huyo, hivi:
3 “Yule mpingamizi [wa Mungu Mwenye Nguvu Zote], ajiinuaye nafsi yake juu ya kila kiitwacho Mungu ama kuabudiwa; hata yeye mwenyewe kuketi katika hekalu la Mungu, akijionyesha nafsi yake kana kwamba yeye ndiye Mungu.”—2 The. 2:3, 4.
4, 5. Eleza namna mapadre wa Jumuiya ya Wakristo ndio wanaofaa kusimuliwa hivyo na mtume kama “yule mtu wa kuasi.”
4 Ni nani ambao simulio hili la “mtu wa kuasi” lawafaa? Labda tujibu kwa kuuliza hivi: Ni akina nani wamejitwalia wenyewe majina ya heshima kama “Reverend,” “Right Reverend,” “Father,” “Holy Father” (“Baba Mtakatifu”), na mengine kama hayo, yanayopingana kabisa na maneno ya Yesu katika Mathayo 23:8-12? (Linganisha Ayubu 32:21, 22.) Je! mapadre, wa Kikatoliki na wa Kiprotestanti, hawakufanya hivyo? Je! hawadai lile “kundi la Mungu” kama kundi lao, na katika mahali pengi wamejaribu sana kuzuia wengine wasiseme na watu katika mitaa yao juu ya Neno la Mungu, ikiwa mambo ambayo watu hawa wanasema hayapatani na mafundisho ya mapadre? (1 Pet. 5:2) Hii ndiyo nia hasa na hatua ambayo viongozi wa kidini wa Kiyahudi walionyesha juu ya mahubiri ya Yesu. (Luka 11:52) Linganisha pia mwendo wa viongozi wa Kiyahudi wa nyakati za kale.—Eze. 34:1-6; Mik. 3:5.
5 Mapadre wametumia uongozi wao kufanya serikali zipige marufuku au kuzuia vikali na kuonea wale wanaojaribu kuwafundisha watu kweli ya Biblia. Wengi wao wamekana kuongozwa kwa Biblia na Mungu na kuiita “hadithi,” “iliyochakaa” na isiyohusu maisha ya kisasa, kwa njia hiyo wakiweka neno lao juu ya neno la Mungu na kujionyesha wenyewe kuwa wenye kumwasi Mungu.
6. Ni mambo gani mengine yasiyo ya kimungu ambayo mapadre wa Jumuiya ya Wakristo wamefanya?
6 Ijapokuwa mapadre wa Jumuiya ya Wakristo wametafuta kujikweza wenyewe kwenye cheo kama kile cha mungu, mambo mengi ambayo wamefanya ni yale yasiyo ya kimungu kabisa. Wamejifanya wenyewe rafiki za ulimwengu, kwa njia hiyo wakijifanya adui za Mungu wa kweli, kama Yakobo ndugu mzazi mmoja na Yesu, alivyoandika. (Yak. 4:4) Wamekuwa wasiri na washauri wa wanasiasa wa ulimwengu na watu wa Biashara Kuu, nao wametumikia kama mtumishi wa wafanya vita na wa majeshi. Tunawaona wakitumikia kama makasisi wa kijeshi, wakizibariki silaha zenye kufisha za majeshi, na kuombea pande zote mbili za vita kati ya mataifa yaitwayo ya “Kikristo” ushindi.
7. Mapadre wa Jumuiya ya Wakristo ni sehemu ya nini?
7 Kwa njia hiyo mapadre wamejifanya wenyewe kuwa sehemu yenye nguvu ya ‘Babeli Mkuu,’ ile milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. Anasemekana kwa mfano kuwa “mji ule mkubwa, wenye ufalme juu ya wafalme wa nchi.” (Ufu. 17:18) Yeye ndiye “kahaba mkuu” wa kidini, “ambaye wafalme wa nchi wamezini naye, nao wakaao katika nchi wamelevywa kwa mvinyo ya uasherati wake.”—Ufu. 17:1, 2.
LAZIMA AHUKUMIWE NA MUNGU MWENYE NGUVU ZOTE
8, 9. Maneno ya mtunga Zaburi juu ya viongozi wa kibinadamu kama “miungu” yanapatanaje na jamii ya “yule mtu wa kuasi”?
8 Ni lazima “yule mtu wa kuasi” ahukumiwe na Yehova Mungu Mwenye Nguvu Zote kwa sababu ya kujiinua mwenyewe juu kama mungu. Yesu Kristo alielekeza kwenye Zaburi, zilizosema juu ya wanadamu wenye nguvu waliokuwa na cheo kama “miungu.” Wanadamu hawa, waliokuwa viongozi na mahakimu, walikuwa wanadamu wasio haki, na zaburi, ikiwataja kama “miungu,” inaendelea kusema hivi: “Lakini mtakufa kama wanadamu, mtaanguka kama mmoja wa wakuu.”—Zab. 82:1-7; Yohana 10:34-36.
9 Ile jamii ya mapadre, “yule mtu wa kuasi,” ‘anayejionyesha nafsi yake kana kwamba yeye ni mungu,’ si isiyoweza kufa, bali itakufa kama mwanadamu wa kawaida. Anaweza kulinganishwa na Yuda Iskariote mwenye kusaliti, aliyeitwa “mwana wa upotevu.” (Yohana 17:12; 2 The. 2:3) Ijapokuwa kujiinua nafsi yake juu ya “kila kiitwacho Mungu ama kuabudiwa,” “yule mtu wa kuasi” mkuu ataanguka, atauawa na Masihi wa Yehova.
10, 11. Ni katika utendaji gani wa ‘Babeli Mkuu’ wanamoishiriki sasa mapadre wa Jumuiya ya Wakristo, nao unafunuaje kwamba kweli wanashiriki katika kumpanda yule “mnyama” mwekundu sana?
10 “Yule mtu wa kuasi” anapataje uharibifu? Kujibu hilo, na tuiangalie hali na mwisho wa ‘Babeli Mkuu,’ kwa maana “yule mtu wa kuasi,” akiwa sehemu iliyo kuu ya hii milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, atashiriki hukumu yake. Biblia afananisha ‘Babeli Mkuu’ kama amepanda mgongoni mwa “mnyama” mwekundu sana. Mnyama huyu anafananisha tengenezo la ulimwengu la amani na usalama ambalo sasa lajulikana kama Umoja wa Mataifa. Anaitwa mfalme “wa nane,” Serikali ya Nane ya unabii wa Biblia.—Ufu. 17:1-11.
11 Mapadre wa Jumuiya ya Wakristo amependekeza na kusifu sana tengenezo hilo la amani na usalama, hata kulipa tengenezo hilo lisilo la Kikristo daraka la Kimasihi. Lile lililotangulia, Ushirika wa Mataifa, waliliita “wonyesho wa kisiasa wa Ufalme wa Mungu duniani.” Kutaka kwa “yule mtu wa kuasi” ni kwamba tengenezo hilo la mataifa yote liuokoe ulimwengu katika vita ya tatu ya dunia yote, vita yenye silaha za atomiki.
12. “Yule mtu wa kuasi” atapokeaje adhabu?
12 Lakini Biblia inatabiri kwamba zile “pembe” kumi za mfano za kiserikali ‘zitamchukia yule kahaba, nazo zitamfanya kuwa mkiwa na uchi, zitamla nyama yake, zitamteketeza kabisa kwa moto.’ (Ufu. 17:16) Wakati udanganyifu, unafiki, pupa, uchafu na uasi wa ‘Babeli Mkuu’ utakapokuwa wenye kuchukiza sana kwa watawala wa ulimwengu, “yule mtu wa kuasi” atashiriki adhabu atakayotolewa. Ile jamii ya mapadre itaonwa na watu wote kuwa imefundisha fundisho la uongo, imeshiriki katika siasa za kilimwengu, katika vita na mapinduzi ya serikali, na utajiri ambao matengenezo yao yamepata kwa kuwanyonya watu utachukuliwa kutoka kwao.
13. Je! kweli ni kukufuru kusema kwamba majengo ya kanisa na mapadre wa Jumuiya ya Wakristo wataharibiwa?
13 Kwa wengine inaonekana kukufuru kusema kwamba majengo ya kanisa, ambayo katika hayo mapadre wanaketi na kupokea heshima kama mungu, yataharibiwa, na kwamba “watu wenye kanzu” wenye kujidai utakatifu wataharibiwa pamoja na ‘Babeli Mkuu.’ Viongozi wa kidini wa Kiyahudi wa karne ya kwanza vile vile walishtuka kwa matabiri ya uharibifu wa Yerusalemu na hekalu lake. Hata hivyo uharibifu ulikuja katika mwaka wa 70 C.E. (Mt. 24:1, 2) Kitabu cha Ufunuo chaonyesha kwamba, vile vile, watakuwako waombolezaji wa kuanguka kwa ‘Babeli Mkuu,’ yaani, wale waliopata faida ya kimwili kwa kushughulika kwao naye.—Ufu. 18:9-19.
14. Onyesha aliye na daraka kweli la kuleta hukumu juu ya “yule mtu wa kuasi.”
14 Kufikiliza huku kwa hukumu juu ya “yule mtu wa kuasi,” kujapokuja kupitia kwa mkono wa watawala wa kisiasa, hakika kunatoka kwa Mungu kupitia kwa Mwana wake aliyetawazwa Yesu Kristo. Biblia inampa Mungu sifa kwa uharibifu wa ‘Babeli Mkuu’ na inatoa mwito wa kumsifu yeye kwa kumwangusha kabisa.—Ufu. 18:5, 8, 20; 19:1-3.
15. Bwana Yesu anamharibuje “yule mtu wa kuasi” “kwa pumzi ya kinywa chake”?
15 Katika njia hii maneno ya mtume Paulo yanatimizwa juu ya “yule mtu wa kuasi,” “ambaye,” Paulo aliandika, “Bwana Yesu atamwua kwa pumzi ya kinywa chake, na kumwangamiza kwa ufunuo wa kuwapo kwake.” (2 The. 2:8) Karibuni sasa Bwana Yesu Kristo, ambaye kuwapo kwake kusikoonekana katika mamlaka ya Ufalme kulianza katika mwaka wa 1914, atauleta uharibifu huo kwa ghafula. Ijapo wafalme wa kidunia ndivyo vyombo vinavyotumiwa, ni “pumzi” (roho), ile nguvu yenye kuendesha kutoka kinywa chake, inayoamuru uharibifu huo.
EPUKA KUFUATA ‘MADANGANYO YA UDHALIMU’
16. Maneno ya mtume Paulo yaonyeshaje kwamba kuna hatari kuu kwa wote wanaofuata mapadre?
16 Kuna hatari kuu inayowakaribia wote wanaofuata mapadre. Mtume alisema juu ya hili hivi: “[Kuwapo] kwake ni kwa . . . madanganyo yote ya udhalimu kwa hao wanaopotea; kwa sababu hawakukubali kuipenda ile kweli, wapate kuokolewa. Kwa hiyo Mungu awaletea nguvu ya upotevu, wauamini uongo; ili wahukumiwe wote ambao hawakuiamini kweli, bali walikuwa wakijifurahisha katika udhalimu.”—2 The. 2:9-12.
17. Sababu gani sasa ndio wakati wa kuchunguza jambo hili la “yule mtu wa kuasi”?
17 Sasa kuna ushuhuda mwingi wa kumtambulisha “yule mtu wa kuasi” bila kukosea. Katika siku zetu ule ukengeufu (kuacha imani ya kweli) umefikia upeo wake. Tunda lake baya limekomaa kabisa na limefunuliwa kama ovu, ili wote wanaotaka sana kweli waweze kuiona. Watu waipendao ile kweli’ lazima wachunguze sana ili waepuke kufuata ‘madanganyo ya udhalimu.’ Kutafuta na kukubali kweli ni kwa maana zaidi na kwa lazima zaidi kwa ye yote kuliko kufuata sana madanganyo, hata ikiwa sisi na babu zetu tumetegwa nayo kwa vizazi vingi. Hili laweza kumaanisha uzima au mauti, kwa maana Mungu ameruhusu “nguvu ya upotevu” iwaendee wale wanaoamini uongo, wanaomtumaini “yule mtu wa kuasi” kama mwenye kumwakilisha Mungu, ndiyo, hata zaidi, kama akiwa “Mungu,” wakikubali maneno yake kuliko yale ya Mungu Mwenye Nguvu Zote kama yalivyoandikwa katika Biblia.
18. “Nguvu ya upotevu” inawaendeaje wale wanaoamini uongo, na kwa kusudi gani?
18 Mungu haitumi moja kwa moja hii “nguvu ya upotevu,” bali anairuhusu iwaendee wenye kudanganywa ili kuonyesha kwamba ndivyo wanavyotaka kweli. (Linganisha Waebrania 4:12) Katika njia hii watu wote wenye mioyo minyofu wanaweza kuona kwamba Mungu ni mwenye haki katika hukumu yake. (Ufu. 19:2; 2 The. 1:6-8) Wale ‘wanaoamini uongo’ kwa sababu ya ‘kutokukubali kuipenda ile kweli,’ watajikuta wenyewe wamo kati ya “hao wanaopotea” wakati wa kifo cha “Mungu” wao, “yule mtu wa kuasi.”
19. Katika kuchunguza ushuhuda unaotambulisha “yule mtu wa kuasi,” mtafutaji ataona nini?
19 Kwa sababu hii ikiwa mtu anatumia wakati sasa ili auchunguze ule ushuhuda unaotambulisha na kumfunua “yule mtu wa kuasi,” anafuata mwendo wenye hekima. Atakuwa mwenye furaha sana kuona kwamba kuna ahadi tukufu za Mungu ambazo zimefichwa na mafundisho ya uongo ya mapadre wa Jumuiya ya Wakristo. Katika ‘kuketi katika hekalu la Mungu, akijionyesha nafsi yake kana kwamba yeye ndiye mungu,’ “yule mtu wa kuasi” amezuia watu wasijifunze juu ya na kupata kumjua Mungu wa kweli Yehova na sifa zake za upendo na makusudi yake kwa wanadamu.
20. Zaidi ya kutambulisha tu “yule mtu wa kuasi,” ni nini la maana kuu zaidi ambalo mchunguzi atajifunza?
20 Zaidi ya hayo, katika kutazama mbele kuliko kutambulishwa kwa “yule mtu wa kuasi,” mtafutaji mnyofu wa kweli ataona kwamba kusudi bora la Mungu kwa wanadamu sasa lakaribia kutimizwa kwalo. Uharibifu wa wale ambao wamemsingizia Mungu utafuatana na uharibifu kamili wa taratibu hii ya mambo. Kutakuwako kuokoka kwa wale ‘wanaokubali kuipenda ile kweli, wapate kuokolewa’ na nafasi ya uzima katika dunia safi. Mambo haya yatazungumzwa katika toleo litakalofuata la Mnara wa Mlinzi.—Ufu. 19:19-21; 7:9-17; 21:1-4; Sef. 2:3.
—Kutoka Kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached.