Kristo Aliuchukia Ukosefu wa Kufuata Sheria —Je! Wewe Wauchukia?
“Umependa haki [uadilifu, “NW”], umechukia maasi [ukosefu wa kufuata sheria, “NW”]; kwa hiyo Mungu, Mungu wako, amekutia mafuta, mafuta ya shangwe kupita wenzio.”—WAEBRANIA 1:9.
1. Zaidi ya kupenda uadilifu, ni jambo gani jingine linalohitajiwa kutoka kwa watumishi wote wa kweli wa Yehova Mungu?
WATUMISHI wa Yehova wa kweli humpenda kwa moyo, nafsi, akili, na nguvu zao zote. (Marko 12:30) Wanataka kuufurahisha moyo wa Yehova kwa kudumisha uaminifu-maadili. (Mithali 27:11) Ili kufanya hivyo, si lazima wapende uadilifu tu bali pia ni lazima wachukie ukosefu wa kufuata sheria. Kielelezo chao, Yesu Kristo, alifanya hivyo kwa hakika. Ilisemwa hivi juu yake: “Umependa haki [uadilifu, NW], umechukia maasi [ukosefu wa kufuata sheria, NW].”—Waebrania 1:9.
2. Ukosefu wa kufuata sheria unatia ndani nini?
2 Ukosefu wa kufuata sheria ni nini? Ni dhambi, kama vile mtume Yohana alivyoonyesha alipoandika hivi: “Kila atendaye dhambi, afanya uasi [ukosefu wa kufuata sheria, NW]; kwa kuwa dhambi ni uasi [ukosefu wa kufuata sheria, NW].” (1 Yohana 3:4) Mtu asiyefuata sheria “hazuiwi wala hadhibitiwi na sheria.” (Webster’s Ninth New Collegiate Dictionary) Ukosefu wa kufuata sheria hutia ndani yote yaliyo mabaya, maovu, yasiyo ya kiadili, yenye ufisadi, na yasiyofuata haki. Kutazama ulimwengu kwaonyesha kwamba ukosefu wa kufuata sheria umeenea sana leo kupita wakati wowote mwingine. Hakuna shaka kwamba tunaishi katika “nyakati za hatari” ambazo mtume Paulo alitabiri kwenye 2 Timotheo 3:1-5. Kwa sababu ya ukosefu wa kufuata sheria huo wote, ni vema kama nini kwamba tunaamriwa tuuchukie ubaya wote! Kwa mfano, tunaambiwa hivi: “Enyi mmpendao BWANA [Yehova, NW], uchukieni uovu.” (Zaburi 97:10) Vilevile, twasoma hivi: “Yachukieni mabaya; yapendeni mema.”—Amosi 5:15.
Aina Tatu za Chuki
3-5. Neno “chuki” linatumiwa katika njia gani tatu katika Neno la Mungu?
3 Inamaanisha nini kuchukia? Katika Neno la Mungu, “chuki” hutumiwa katika njia tatu tofauti. Kuna ile chuki inayochochewa na kijicho na inayojaribu kudhuru kile kitu inayochukia. Ni lazima Wakristo waepuke chuki ya aina hiyo. Chuki ya aina hiyo ndiyo ilimchochea Kaini amwue Abeli ndugu yake mwadilifu. (1 Yohana 3:12) Pia viongozi wa kidini walikuwa na chuki ya aina hiyo kuelekea Yesu Kristo.—Mathayo 26:3, 4.
4 Zaidi ya hayo, neno “chuki” hutumiwa katika Maandiko kwa maana ya kupenda kidogo zaidi. Kwa mfano, Yesu alisema: “Kama mtu akija kwangu naye hamchukii baba yake, na mama yake, na mke wake, na wanawe, na ndugu zake waume na wake; naam, na hata nafsi yake mwenyewe, hawezi kuwa mwanafunzi wangu.” (Luka 14:26) Kwa wazi, Yesu alimaanisha tu kuwapenda hao kidogo zaidi ya tumpendavyo. Yakobo ‘alimchukia Lea,’ lakini kwa kweli alimpenda kidogo zaidi ya alivyompenda Raheli.—Mwanzo 29:30, 31, NW.
5 Halafu kuna ile maana ya neno “chuki” ambayo twahangaikia hasa hapa. Ina wazo la kuwa na hisia nyingi ya kutofurahia au kuwa na karaha yenye nguvu kuelekea mtu au jambo hivi kwamba twaepuka kuwa na uhusiano wowote na mtu au jambo hilo. Katika Zaburi 139 hilo lasemwa kuwa “ukomo wa chuki.” Hapo Daudi alisema hivi: “Je! BWANA [Yehova, NW], nisiwachukie wanaokuchukia? Nisikirihike nao wakuasio? Nawachukia kwa ukomo wa chuki, wamekuwa adui kwangu.”—Zaburi 139:21, 22.
Sababu kwa Nini Twapaswa Kuchukia Ukosefu wa Kufuata Sheria
6, 7. (a) Ni kwa nini hasa, tunapaswa kuchukia ukosefu wa kufuata sheria? (b) Ni nini sababu ya pili yenye nguvu ya kuchukia ukosefu wa kufuata sheria?
6 Kwa nini twapaswa kuchukia ukosefu wa kufuata sheria? Sababu moja ni ili tuweze kujistahi na kuwa na dhamiri nzuri. Ni kwa njia hiyo pekee tuwezayo kuwa na uhusiano mzuri na Baba yetu wa kimbingu mwadilifu, mwenye upendo, Yehova. Daudi alituwekea mfano mzuri kwa habari hiyo, kama vile iwezavyo kuonwa na usomaji wa Zaburi 26. Kwa mfano alisema: “Nimelichukia kusanyiko la watenda mabaya, wala sitaketi pamoja na watu waovu.” (Zaburi 26:5) Kupenda kwetu Mungu na uadilifu kutatuchochea tuwe na hasira yenye uadilifu—naam, chuki—kwa kila jambo lisilofuata sheria kulingana na maoni yake, kutia na vitendo visivyofuata sheria vya wale wasiotii na wanaomchukia Yehova. Zaidi ya hayo, twapaswa kuchukia ukosefu wa kufuata sheria kwa sababu ya suto unaloletea jina la Mungu.
7 Sababu nyingine kwa nini watu wa Yehova wanapaswa kuchukia ukosefu wa kufuata sheria ni kwamba ni wa hatari sana na unadhuru. Kupanda kulingana na mnofu, kunakomaanisha kupanda ukosefu wa kufuata sheria, kutakuwa na tokeo gani? Paulo alionya hivi: “Msidanganyike, Mungu hadhihakiwi; kwa kuwa cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna. Maana yeye apandaye kwa mwili wake, katika mwili wake atavuna uharibifu; bali yeye apandaye kwa Roho, katika Roho atavuna uzima wa milele.” (Wagalatia 6:7, 8) Kwa hiyo twataka kutohusika hata kidogo na ukosefu wa kufuata sheria. Kwa kweli, twahitaji kuchukia ukosefu wote wa kufuata sheria kwa ajili ya hali njema na amani ya akili yetu wenyewe.
Wale Wachukiao Ukosefu wa Kufuata Sheria
8. Ni nani ambaye ameweka mfano mkamilifu katika kuchukia ukosefu wa kufuata sheria, kama ilivyoonyeshwa na maandiko gani?
8 Kwa kuchukia ukosefu wa kufuata sheria, Mungu huwekea viumbe vyote vyenye akili mfano mkamilifu. Yeye huwa na hasira yenye uadilifu kuelekea ukosefu wa kufuata sheria, na Neno lake husema hivi: “Kuna vitu sita anavyovichukia BWANA [Yehova, NW]; naam, viko saba vilivyo chukizo kwake. Macho ya kiburi, ulimi wa uongo, na mikono imwagayo damu isiyo na hatia; moyo uwazao mawazo mabaya; miguu iliyo myepesi kukimbilia maovu; shahidi wa uongo asemaye uongo; naye apandaye mbegu za fitina kati ya ndugu.” Twasoma hivi pia: “Kumcha BWANA [Yehova, NW] ni kuchukia uovu; kiburi na majivuno, na njia mbovu, na kinywa cha ukaidi pia nakichukia.” (Mithali 6:16-19; 8:13) Isitoshe, tunaambiwa hivi: “Mimi, BWANA [Yehova, NW], naipenda hukumu ya haki, nauchukia wivu na uovu.”—Isaya 61:8.
9, 10. Yesu alionyeshaje kwamba alichukia ukosefu wa kufuata sheria?
9 Yesu Kristo alimwiga Baba yake katika kuchukia ukosefu wa kufuata sheria. Hivyo, twasoma hivi: “Umependa haki [uadilifu, NW], umechukia maasi [ukosefu wa kufuata sheria, NW]; kwa hiyo Mungu, Mungu wako, amekutia mafuta, mafuta ya shangwe kupita wenzio.” (Waebrania 1:9) Yesu alituwekea sisi mfano wa chuki ya aina hiyo. Alionyesha kuchukia kwake ukosefu wa kufuata sheria kwa kufunua wale waliouzoea kimakusudi—viongozi wa kidini bandia. Tena na tena, aliwashutumu kuwa wanafiki. (Mathayo, sura 23) Kwenye pindi nyingine Yesu aliwaambia hivi: “Ninyi ni wa baba yenu, Ibilisi, na tamaa za baba yenu ndizo mpendazo kuzitenda.” (Yohana 8:44) Yesu alionyesha kuchukia kwake ukosefu wa kufuata sheria hata kwa kadiri ya kutumia nguvu za kimwili, kwenye pindi mbili akisafisha hekalu kwa kuondolea mbali wanafiki wa kidini wenye pupa.—Mathayo 21:12, 13; Yohana 2:13-17.
10 Yesu alionyesha kuchukia kwake ukosefu wa kufuata sheria na dhambi kwa kujiweka huru kabisa navyo. Kwa hiyo, angeweza kwa kufaa kuwauliza wapinzani wake hivi: “Ni nani miongoni mwenu anishuhudiaye ya kuwa nina dhambi?” (Yohana 8:46) Yesu alikuwa “mtakatifu, asiyekuwa na uovu, asiyekuwa na waa lo lote, aliyetengwa na wakosaji.” (Waebrania 7:26) Akihakikisha hilo, Petro aliandika kwamba Yesu “hakutenda dhambi, wala hila haikuonekana kinywani mwake.”—1 Petro 2:22.
11. Tuna mifano gani ya Kimaandiko ya wanadamu wasio wakamilifu waliochukia ukosefu wa kufuata sheria?
11 Hata hivyo, Yesu alikuwa mwanamume mkamilifu. Je! tunayo mifano ya Kimaandiko ya wanadamu wasio wakamilifu ambao kwa kweli walichukia ukosefu wa kufuata sheria? Kwa kweli tunayo! Kwa mfano, Musa na Walawi wenzake walionyesha kuchukia sana ibada ya sanamu kwa kuwaua waabudu sanamu 3,000 kwa amri ya Yehova. (Kutoka 32:27, 28) Finehasi alionyesha kuchukia sana ukosefu wa kufuata sheria alipowaua waasherati wawili kwa fumo.—Hesabu 25:7, 8.
Kuonyesha Chuki ya Ukosefu wa Kufuata Sheria
12. (a) Tunaweza kuonyeshaje kuchukia kwetu ukosefu wa kufuata sheria? (b) Ni njia zipi zifaazo za kuepuka mawazo yasiyofuata sheria?
12 Kufikia wakati wetu, twaweza kuonyeshaje kuchukia kwetu ukosefu wa kufuata sheria? Kwa kudhibiti mawazo, maneno, na matendo yetu. Twahitaji kusitawisha zoea la kufikiri juu ya mambo yanayojenga wakati akili zetu hazishughuliki na kazi fulani. Iwapo tuko macho kitandani usiku, huenda kukawa na mwelekeo wa kufikiria mambo hasi (mabaya), kama vile kufikiria masikitiko au kujifurahisha kwa fantasia za kingono. Usiyape nafasi kamwe mambo ya jinsi hiyo, lakini uwe na zoea la kushiriki katika kufikiri kunakonufaisha. Kwa mfano, jaribu kutia akilini maandiko, yale mambo tisa yaletayo furaha, na yale matunda tisa ya roho. (Mathayo 5:3-12; Wagalatia 5:22, 23) Je! wewe waweza kutaja wale mitume 12 kwa jina? Je! wazijua zile Amri Kumi? Yale makundi saba yanayozungumziwa katika Ufunuo ni yapi? Kutia akilini nyimbo za Ufalme husaidia pia kukazia akili zetu mambo ya kweli, yanayohusu kwa uzito, yaliyo ya uadilifu, yaliyo safi, yenye kupendeka, yenye kusemewa vizuri, yaliyo mema, yanayostahili sifa.—Wafilipi 4:8, NW.
13. Kuchukia ukosefu wa kufuata sheria kutatusababisha tuchukie aina gani ya usemi?
13 Zaidi ya hayo, tunaonyesha kwamba twachukia ukosefu wa kufuata sheria kwa kuepuka usemi wote mchafu. Watu wengi wa kilimwengu hufurahia kuongea na kusikiliza ucheshi mchafu, lakini ni lazima Wakristo wasiwe hata na mwelekeo wa kuusikiliza. Badala yake, twapaswa kuondoka na kuepuka kushiriki katika mazungumzo yoyote yanayoelekea kwenye viwango hivyo vya chini. Ikiwa hatuwezi kuondoka, twaweza angalau kuonyesha kwa uso wetu kwamba tunachukia maongezi ya jinsi hiyo. Twapaswa kutii shauri hili zuri: “Neno lo lote lililo ovu lisitoke vinywani mwenu, bali lililo jema la kumfaa mwenye kuhitaji, ili liwape neema wanaosikia.” (Waefeso 4:29) Hatupaswi kujichafua wenyewe kwa kusema au kusikiliza mambo machafu.
14. Kuchukia ukosefu wa kufuata sheria kunaandaa ulinzi gani kuhusu mazoea ya biashara na kazi ya kuajiriwa?
14 Ni lazima kuchukia kwetu ukosefu wa kufuata sheria kuelekezwe dhidi ya mazoea yote ya dhambi. Kuchukia ukosefu wa kufuata sheria kutatusaidia tuepuke mtego wa kuridhiana kwa habari hiyo. Wakristo wa kweli hawazoei dhambi. (Linganisha 1 Yohana 5:18.) Kwa mfano, ni lazima tuchukie mazoea yote ya biashara yasiyofuatia haki. Leo, Mashahidi wa Yehova walio wengi wamewekwa chini ya mbano wa kuwafanyia waajiri wao mambo yasiyofuatia haki lakini wamekataa kufanya hivyo. Wakristo hata wamekuwa na nia ya kupoteza kazi zao badala ya kufanya jambo linaloharibu dhamiri zao zenye kuzoezwa kwa Biblia. Isitoshe, twataka pia kuonyesha kuchukia kwetu ukosefu wa kufuata sheria kwa kutovunja sheria za uendeshaji magari na kwa kutodanganya tunapopaswa kulipa kodi au ushuru wa forodha.—Matendo 23:1; Waebrania 13:18.
Kuchukia Uchafu wa Kingono
15. Kuwaumba wanadamu na silika zenye nguvu za kuwa na mwenzi kulitumikia makusudi gani mazuri?
15 Tukiwa Wakristo, ni lazima hasa tuchukie uchafu wote unaohusu mambo ya kingono. Kwa kuwaumba wanadamu na silika zenye nguvu za kuwa na mwenzi, Mungu alitimiza makusudi mawili. Alihakikisha kwamba jamii ya kibinadamu isingetoweka, na yeye alifanya pia uandalizi wenye upendo sana wa kuleta furaha. Hata watu walio maskini, wasiojua kusoma, au waliopungukiwa kwa njia nyingine wanaweza kupata furaha nyingi katika uhusiano wa ndoa. Hata hivyo, Yehova ameweka mipaka ambayo katika hiyo uhusiano huo waweza kufurahiwa. Ni lazima mipaka hiyo iliyowekwa kimungu istahiwe.—Mwanzo 2:24; Waebrania 13:4.
16. Mtazamo wetu wapaswa kuwa nini kuelekea vitumbuizo na mazoea yaliyo machafu kingono?
16 Ikiwa tunachukia ukosefu wa kufuata sheria, tutaepuka kwa bidii mazoea yote machafu ya kingono na vitumbuizo vyote visivyo vya kiadili. Kwa hiyo tutaepuka vitabu, magazeti, na nyusipepa zote zenye kutiliwa shaka kiadili. Vilevile, tukichukia ukosefu wa kufuata sheria, hatutayatazama maonyesho yoyote machafu, iwe kwenye televisheni, katika sinema, au katika michezo ya kuigiza. Tukipata programu fulani kuwa isiyo ya kiadili, twapaswa tusukumwe kuizima televisheni mara moja au twapaswa kuwa na ujasiri wa kuondoka katika jumba hilo la wonyesho. Vivyo hivyo, kuchukia ukosefu wa kufuata sheria kutatulinda dhidi ya muziki wowote unaoamsha ashiki katika maneno yayo au mwendo wayo. Hatutajaribu kupata habari juu ya mambo yasiyo ya kiadili bali tutakuwa ‘watoto wachanga katika uovu, bali watu wazima katika akili.’—1 Wakorintho 14:20.
17. Wakolosai 3:5 linatupa sisi shauri gani liwezalo kutusaidia tubaki safi kiadili?
17 Kwa kufaa zaidi, tunashauriwa hivi: “Basi, vifisheni viungo vyenu vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya.” (Wakolosai 3:5) Hakuna shaka kwamba hatua zenye nguvu zinahitajiwa kwa upande wetu ikiwa tutapiga moyo konde kubaki safi kiadili. Kuhusu kitenzi cha Kigiriki kinachofasiriwa “vifisheni” kwenye Wakolosai 3:5, The Expositor’s Bible Commentary hutaarifu hivi: “Inadokeza kwamba hatupaswi kuzuia au kudhibiti tu vitendo na mitazamo miovu. Twapaswa kuyafutilia mbali, kuangamiza kabisa njia ya maisha ya zamani. ‘Kuchinja kabisa’ huenda ikaonyesha nguvu yacho. . . . Maana ya kitenzi hicho na nguvu ya njeo [hali] yacho hudokeza kitendo cha azimio la kibinafsi chenye juhudi, kinachoumiza.” Kwa hiyo tunapaswa kuepuka pornografia kana kwamba ni ugonjwa wa hatari, wenye kuambukiza, unaosababisha kifo, kwani hivyo ndivyo ilivyo kiadili na kiroho. Kristo alionyesha wazo kama hilo aliposema kukatalia mbali mkono, mguu, au hata jicho ikiwa linatusababisha tukwazwe.—Marko 9:43-48.
Kuchukia Dini Bandia na Uasi-Imani
18. Tunaweza kuonyeshaje kuchukia kwetu ukosefu wa kufuata sheria wa kidini?
18 Halafu pia, sawa na vile Yesu alivyoonyesha kuchukia kwake ukosefu wa kufuata sheria kwa kufunua wanadini wanafiki, Mashahidi wa Yehova leo vilevile wanaonyesha kuchukia kwao ukosefu wote wa kufuata sheria wa kidini wenye unafiki. Kwa jinsi gani? Kwa kugawanya fasihi ya Biblia inayofunua wazi Babuloni Mkubwa jinsi alivyo hasa, kahaba wa kidini. Ikiwa tunachukia kwa kweli unafiki wa kidini usiofuata haki, tutakuwa wenye uwazi katika kuifunua Babuloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini bandia. Tutafanya hivyo kwa ajili ya watu wenye mioyo yenye kufuatia haki ambao amewapofusha na kuwafunga katika utumwa wa kiroho. Kwa kadiri ambayo tunachukia kwa kweli ukosefu wa kufuata sheria wa Babuloni Mkubwa, ndivyo kwa kadiri hiyo tutakavyokuwa wenye bidii katika kushiriki katika sehemu zote za huduma ya Ufalme.—Mathayo 15:1-3, 7-9; Tito 2:13, 14; Ufunuo 18:1-5.
19. Twapaswa kuonaje waasi-imani, na kwa nini?
19 Wajibu wa kuchukia ukosefu wa kufuata sheria watumika pia kwa utendaji wote wa waasi-imani. Mtazamo wetu kuelekea waasi-imani wapaswa kuwa ule wa Daudi, aliyejulisha rasmi hivi: “Je! BWANA [Yehova, NW], nisiwachukie wanaokuchukia? Nisikirihike nao wakuasio? Nawachukia kwa ukomo wa chuki, wamekuwa adui kwangu.” (Zaburi 139:21, 22) Waasi-imani wa ki-siku-hizi wameshirikiana pamoja na “yule mtu wa kuasi,” makasisi wa Jumuiya ya Wakristo. (2 Wathesalonike 2:3) Kwa hiyo tukiwa Mashahidi wa Yehova waaminifu-washikamanifu, hatushiriki lolote pamoja nao. Tukiwa wasio wakamilifu, mioyo yetu ingeweza kwa urahisi kuwa na mwelekeo wa kuchambua-chambua ndugu zetu. Wakiwa watu mmoja mmoja, wale wa “mtumwa mwaminifu mwenye akili” ni wanadamu wasio wakamilifu. (Mathayo 24:45-47) Lakini jamii hiyo ni yenye uaminifu na yenye akili. Waasi-imani hukazia kasoro au yale yaonekanayo kuwa makosa yanayofanywa na ndugu wanaoongoza. Tuko salama tukiepuka propaganda ya uasi-imani kana kwamba ni sumu, ambayo kwa kweli ni sumu.—Warumi 16:17, 18.
20, 21. Sababu za kuchukia ukosefu wa kufuata sheria zaweza kutolewaje muhtasari?
20 Tumeona kwamba ulimwengu umejaa ukosefu wa kufuata sheria, ambao ni sawasawa na dhambi. Haitoshi kwetu kupenda uadilifu tu; ni lazima pia tuchukie ukosefu wa kufuata sheria. Baadhi ya wale ambao wametengwa na ushirika wa kundi la Kikristo huenda ikawa walifikiria kwamba walipenda uadilifu, lakini hawakuchukia ukosefu wa kufuata sheria vya kutosha. Tumeona pia ni kwa nini twapaswa kuchukia ukosefu wa kufuata sheria. Hatuwezi kuwa na dhamiri nzuri na kujistahi tusipofanya hivyo. Zaidi ya hayo, ukosefu wa kufuata sheria humaanisha kutokuwa mwaminifu-mshikamanifu kwa Yehova Mungu. Na ukosefu wa kufuata sheria unatusababisha tuvune matunda machungu sana—majonzi, ufisadi, na kifo.
21 Tumeona pia jinsi tunavyoonyesha kwamba tunachukia ukosefu wa kufuata sheria. Twafanya hivyo kwa kutohusika hata kidogo na aina yoyote ya kutofuatia haki, ukosefu wa maadili katika ngono, au uasi-imani. Kwa kuwa tunataka kushiriki katika utetezi wa Yehova na tunatamani kufurahisha moyo wake, ni lazima tupende si uadilifu tu na kuendelea kuwa wenye shughuli katika utumishi wake bali pia tuchukie ukosefu wa kufuata sheria, kama vile Kiongozi na Kamanda wetu, Yesu Kristo alivyofanya.
Ungejibuje?
◻ Maandiko hutumiaje neno “chuki”?
◻ Ni zipi baadhi ya sababu nzuri za kuchukia kwetu ukosefu wa kufuata sheria?
◻ Tuna mifano gani mizuri ya wale waliochukia ukosefu wa kufuata sheria?
◻ Tunaweza kuonyeshaje kuchukia kwetu ukosefu wa kufuata sheria?
[Picha katika ukurasa wa 8]
Yesu alisafisha hekalu kwa sababu alichukia ukosefu wa kufuata sheria
[Picha katika ukurasa wa 10]
Ikiwa tunachukia ukosefu wa kufuata sheria, tutaepuka vitumbuizo visivyo vya kiadili kingono