Uasi-Imani
Maana: Uasi-imani ni kuacha ibada na utumishi wa Mungu, hasa ni kumwasi Yehova Mungu. Waasi-imani fulani hudai kwamba wanamjua na kumtumikia Mungu lakini hukataa mafundisho au matakwa yaliyoandikwa katika Neno lake. Wengine hudai kwamba wanaiamini Biblia lakini hulikataa tengenezo la Yehova.
Je, tutarajie kwamba waasi-imani watatokea katika kutaniko la Kikristo?
1 Tim. 4:1: “Neno lililoongozwa na roho linasema kwa hakika kwamba katika vipindi vya nyakati za mwisho wengine wataanguka kutoka kwenye imani, wakisikiliza maneno yaliyoongozwa kwa roho yenye kupotosha na mafundisho ya roho waovu.”
2 The. 2:3: “Msiache mtu yeyote awashawishi ninyi kwa namna yoyote, kwa sababu hiyo haitakuja isipokuwa uasi-imani uje kwanza na yule mtu wa uasi-sheria afunuliwe, mwana wa maangamizi.”
Baadhi ya mambo yanayowatambulisha waasi-imani—
Hutaka kuwafanya wengine wawe wafuasi wao, hivyo wakisababisha mafarakano
Mdo. 20:30: “Kutoka katikati yenu ninyi wenyewe watu watasimama na kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.”
2 Pet. 2:1, 3: ‘Pia kutakuwa na walimu wa uwongo katikati yenu. Hawa wataingiza ndani kimya-kimya madhehebu yenye kuharibu nao watamkana hata yule bwana aliyewanunua. Pia, kwa tamaa watawatumia ninyi vibaya kwa maneno yasiyo ya kweli.’
Huenda wakadai wanamwamini Kristo lakini wanapuuza kazi ya kuhubiri na kufundisha ambayo aliwapa wafuasi wake
Luka 6:46: “Kwa nini, basi, mnaniita ‘Bwana! Bwana!’ lakini hamfanyi mambo ninayosema?”
Mt. 28:19, 20: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza . . . na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”
Mt. 24:14: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”
Huenda wakadai kwamba wanamtumikia Mungu lakini wanawakataa wawakilishi wake, tengenezo lake linaloonekana
Yuda 8, 11: “Watu hawa, pia, wakijitia mno katika ndoto, wanautia mwili unajisi na kupuuza mamlaka na kuwatukana watukufu. Ole wao, kwa sababu . . . wameangamia katika maneno ya uasi ya Kora!”
Hes. 16:1-3, 11, 19-21: “Kora . . . akaondoka, pamoja na . . . watu 250 kati ya wana wa Israeli, wakuu wa kusanyiko . . . Basi wakakutana dhidi ya Musa na Haruni na kuwaambia: ‘Imetosha, kwa sababu kusanyiko lote, wote hao ni watakatifu na Yehova yuko katikati yao. Kwa nini, basi, mjiinue wenyewe juu ya kutaniko la Yehova?’ . . . [Musa akasema:] ‘Wewe na kusanyiko lako lote wanaokusanyika pamoja mnampinga Yehova. Na Haruni, yeye ni nani hata mnung’unike juu yake?’ Kora alipokuwa amekusanya kusanyiko lote pamoja dhidi yao kwenye mwingilio wa hema la mkutano, ndipo utukufu wa Yehova ukalitokea kusanyiko lote. Sasa Yehova akasema na Musa na Haruni, na kuwaambia: ‘Jitengeni wenyewe kutoka katikati ya kusanyiko hili, nipate kuwaangamiza wao mara moja.’”
Wao hawaiachi tu imani ya kweli bali pia ‘huwapiga’ washiriki wao wa zamani, wakiwachambua hadharani na kutumia njia nyingine za kuzuia kazi yao; jitihada za waasi-imani hao zinatumiwa ili kubomoa, wala si kujenga
Mt. 24:45-51: “Ni nani kwa kweli mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambaye bwana wake alimweka rasmi juu ya watumishi wake wa nyumbani, awape chakula chao kwa wakati unaofaa? . . . Lakini mtumwa huyo mwovu akisema moyoni mwake, ‘Bwana wangu anakawia,’ naye aanze kuwapiga watumwa wenzake na kula na kunywa pamoja na walevi wa kupindukia, bwana wa mtumwa huyo atakuja katika siku ambayo hatazamii na katika saa ambayo hajui, naye atamwadhibu kwa ukali mkubwa zaidi na kumgawia sehemu yake pamoja na wanafiki.”
2 Tim. 2:16-18: “Epuka kabisa maneno matupu ambayo huchafua mambo matakatifu; kwa maana wataendelea kwenye ukosefu wa kumwogopa Mungu ulio mwingi zaidi na zaidi, na neno lao litaenea kama kidonda chenye kuoza. Himenayo na Fileto ni kati ya hao. Watu hao wamegeuka kutoka kwenye kweli, wakisema kwamba ufufuo tayari umetukia; nao wanaipindua imani ya wengine.”
Je, Wakristo waaminifu wangewakaribisha waasi-imani, kibinafsi ama kwa kusoma vichapo vyao?
2 Yoh. 9, 10: “Kila mtu anayevuka mipaka naye hakai katika fundisho la Kristo hana Mungu. . . . Mtu yeyote akija kwenu naye haleti fundisho hili, msimpokee kamwe nyumbani mwenu wala kumsalimu.”
Rom. 16:17, 18: “Sasa nawahimiza ninyi, akina ndugu, waangalieni wale wanaosababisha migawanyiko na kusababisha kukwazika kinyume cha fundisho ambalo mmejifunza, nanyi mjiepushe nao. . . . Kwa maneno laini na maneno ya kusifusifu wao huishawishi mioyo ya wasio na lawama.”
Je, kutaka kujua maoni ya waasi-imani kunaweza kuwa na madhara yoyote mabaya?
Met. 11:9: “Mwasi-imani humletea mwenzake uharibifu kwa kinywa chake.”
Isa. 32:6: “Mtu asiye na akili atasema upumbavu mtupu, na moyo wake utatenda madhara, utatenda uasi-imani na kusema juu ya Yehova mambo mapotovu, utasababisha nafsi ya mwenye njaa kushinda bila kula, naye anasababisha hata mtu mwenye kiu ashinde bila maji ya kunywa.” (Linganisha na Isaya 65:13, 14.)
Uasi-imani ni mbaya kadiri gani?
2 Pet. 2:1: “Hawa wataingiza ndani kimya-kimya madhehebu yenye kuharibu nao watamkana hata yule bwana aliyewanunua, wakijiletea wenyewe maangamizi ya haraka.”
Ayu. 13:16: “Hakuna mwasi-imani yeyote atakayekuja mbele zake [Mungu].”
Ebr. 6:4-6: “Kwa maana haiwezekani kamwe kwa habari ya wale ambao wametiwa nuru mara moja kwa wakati wote, na ambao wameonja zawadi ya bure ya kimbingu, na ambao wamekuwa washiriki wa roho takatifu, na ambao wameonja neno zuri la Mungu na nguvu za mfumo wa mambo unaokuja, lakini ambao wameanguka [“kisha wakaiasi imani yao,” BHN] kuwarudisha tena kwenye toba, kwa sababu wanamtundika upya mtini Mwana wa Mungu kwa ajili yao wenyewe na kumfunua yeye kwenye aibu ya hadharani.”